Endelea Sambamba Pamoja na Gari la Yehova la Kimbingu
“Nawe utawaambia maneno yangu, kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia.”—EZEKIELI 2:7.
1, 2. Ni kibebeo gani cha kifalme ambacho Ezekieli aliona, naye aliambiwa nini?
GARI la Yehova la kimbingu sasa lasimama mbele ya watumishi wake. Kwa macho ya imani, wao wakiona kisafirio hicho cha kifalme cha Bwana wao Mwenye Enzi Kuu. Ni chenye utukufu, cha kutia hofu, chenye fahari.
2 Kibebeo icho hicho cha kifalme kilikuja mbele ya Ezekieli nabii wa Mungu katika njozi kama miaka 2,600 iliyopita. Kutoka kwenye gari hili lenye kuchukua kiti cha enzi—tengenezo la kimbingu la Mungu la viumbe roho—Yehova alimtolea Ezekieli amri hii ya kutazamisha: “Wana hao wana nyuso zisizo na haya, na mioyo yao ni migumu. Mimi nakutuma kwa hao; nawe utawaambia, Bwana MUNGU [Yehova, NW] asema hivi. Nao, kwamba watasikia, au kwamba hawataki kusikia, (maana ndio nyumba ya kuasi hao), hata hivyo watajua ya kuwa nabii amekuwako miongoni mwao.”—Ezekieli 2:4, 5.
3. Ezekieli ana mfanani gani wa ki-siku-hizi?
3 Ezekieli alitekeleza utume huo kwa kuazimia, akitumikia kuwa chombo kimoja tu kilichokuwa katika mkono wa kimungu. Vivyo hivyo, sasa Mungu ana chombo kimoja tu cha kitengenezo katika udhibiti wake. Jamii ya Ezekieli, mabaki wapakwa-mafuta, iko kwenye mstari wa mbele wa kazi ya kutoa ushahidi wa mwisho, “umati mkubwa” wa “kondoo wengine” wakiwa wamekusanyika kuwazunguka wawaunge mkono. (Ufunuo 7:9, 10; Yohana 10:16) Wakiwa pamoja wao ni “kundi moja,” huku yule Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, akiwaongoza chini ya enzi kuu ya yule Mpandaji Gari aliye mkuu, Yehova Mungu.
4, 5. Tengenezo la Mungu lionekanalo lilitokeaje, nalo limepatwa na nini kupatana na Isaya 60:22?
4 Chini ya mwelekezo wa Yehova, tengenezo hili la ulimwenguni pote limekua kutoka mianzo midogo likawa shirika lenye nguvu la kupiga mbiu ya amri ya “mcheni Mungu, na kumtukuza, kwa maana saa ya hukumu yake imekuja.” (Ufunuo 14:7) Kama vile Ezekieli hakujiinua wala kujiweka awe nabii, ndivyo tengenezo lionekanavyo la Mungu halikujiumba wala kujiweka lenyewe. Halikutokea kwa mapenzi wala jitihada ya kibinadamu. Mpandaji Gari aliye wa kimungu alisababisha tengenezo hili litokee. Kwa kutiwa nguvu na roho ya Mungu na kutegemezwa na malaika watakatifu, watu wa Yehova wamepata mpanuko wa kutazamisha hivi kwamba ‘mdogo amekuwa taifa hodari.’—Isaya 60:22.
5 Mashahidi zaidi ya 4,000,000 wa Yehova wanapiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme katika mabara 212. Wamepangwa vikundi-vikundi katika makundi zaidi ya 63,000 yenye kupangwa kitengenezo katika mizunguko na wilaya. Vifaa vikubwa vya ofisi ya tawi na vya uchapaji vinafanya kazi chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza likiwa kitovu cha tengenezo la makao makuu. Kana kwamba wao ni mtu mmoja, wote wanasonga mbele, wakihubiri habari njema, wakielimisha wale wenye kuitikia, wakijenga mahali pa mikutano. Ndiyo, tengenezo lionekanalo la Yehova linaenda sambamba pamoja na gari la kimbingu na Mpandaji walo.
6. Ni nini kihusikacho katika kuendelea sambamba pamoja na tengenezo lionekanalo la Yehova?
6 Ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, je! unaenda sambamba pamoja na tengenezo lionekanalo la Mungu? Kufanya hivyo si jambo la kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kutumia wakati tu katika huduma. Hasa, kwa msingi mwendo wa usambamba wahusiana na maendeleo na ukuzi wa kiroho. Watia ndani kuwa na matazamio chanya, kutanguliza yafaayo kuwekwa kwanza, na kupiga mwendo kulingana na mambo ya kisasa. Ikiwa sisi tunaenda sambamba na gari la kimbingu la Yehova, maisha zetu zinapatana na ule ujumbe ambao twaupigia mbiu.
7. Kwa nini kufikiria mwenendo wa Ezekieli akiwa nabii wa Mungu?
7 Katika lile jambo la kuendelea sambamba, watumishi wa Yehova wa ki-siku-hizi waweza kujifunza mengi kutokana na kielelezo cha Ezekieli. Ingawa aliwekwa na Yehova kwa njia maalumu awe nabii, bado Ezekieli alikuwa na maoni ya kihisia, mahangaiko, na mahitaji. Mathalani, akiwa mwanamume aliye mchanga katika ndoa kwa kulinganishwa, alipatwa na kihoro cha kufiwa na mke wake. Hata hivyo, yeye hakuacha kamwe kuona utume wake akiwa nabii wa Yehova. Kwa kufikiria jinsi Ezekieli alivyojiendesha katika mambo mengine pia, twaweza kujiimarisha tuendelee sambamba pamoja na tengenezo lionekanalo la Mungu. Hii itatuwezesha kuendelea sambamba pamoja na tengenezo lake lionekanalo.
Utume Wakubaliwa na Kutimizwa
8. Kwa habari ya utume wake, ni kielelezo gani ambacho Ezekieli aliweka?
8 Ezekieli aliweka kielelezo kizuri kwa kukubali utume wake na kuutimiza. Hata hivyo, utii na moyo mkuu vilihitajiwa ili kuu-tekeleza, kwa maana twasoma hivi: “Na wewe, mwanadamu, usiwaogope hao, wala usiyaogope maneno yao, ijapokuwa miiba na michongoma i pamoja nawe, nawe unakaa katikati ya nge; usiyaogope maneno yao, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba yenye kuasi. Nawe utawaambia maneno yangu kwamba watasika, au kwamba hawataki kusikia; maana hao wanaasi sana. Bali wewe, mwanadamu, sikia neno hili ninalokuambia; usiwe mwenye kuasi kama nyumba ile yenye kuasi.”—Ezekieli 2:6-8.
9. Ni kwa kufanya nini tu Ezekieli angekuwa bila hatia ya damu?
9 Ezekieli hakupaswa kuwa baridi-baridi wala mwenye hofu, akihitaji kuchochewa daima ili atimize utume wake. Yeye angekuwa bila hatia ya damu ikiwa tu angesema maneno ya Yehova kwa nia na ujasiri. Ezekieli aliambiwa hivi: “Kama ukionya mwovu, naye hageuki toka uovu wake, wala toka njia yake ya uovu, atakufa katika uovu wake; lakini umeponyesha nafsi yako.”—Ezekieli 3:19, ZSB.
10. Jamii ya Ezekieli imethibitikaje kuwa kama nabii huyo?
10 Kama katika kisa cha Ezekieli, jamii ya Ezekieli ya wapakwa-mafuta wamekubali utume wao waliopewa na Mungu nao wanautimiza. Ikiwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, twapaswa kukumbuka kwamba maisha yetu na maisha za wengine zategemea utii wetu. (1 Timotheo 4:15, 16) Kila Shahidi ahitaji kuendelea sambamba pamoja na tengenezo la Yehova. Mungu hatatufunga sisi kwenye gari lake na kutuvuta twende naye. Ubaridi-baridi na moyo wenye kugawanyika humshushia heshima Mpandaji wa Gari. Hivyo basi tengenezo lionekanalo la Yehova latuhimiza tuweke masilahi za kimungu kwenye kitovu cha maisha zetu. Itikio lenye upatani kwa himizo hilo latuweka sambamba pamoja na tengenezo la Mungu na kukweza huduma yetu takatifu isiwe ya kikawaida tu, ya kidesturi tu. Kwa uhakika, watu wa Yehova kwa ujumla huonyesha ujitoaji wa ajabu. Sehemu yetu mmoja mmoja ni kudumisha mwendo huo.
Maneno ya Mungu Yazingatiwa Moyoni
11. Ezekieli aliweka kielelezo gani kuhusu maneno ya Mungu?
11 Ezekieli pia aliweka kielelezo kizuri kwa kuzingatia maneno ya Mungu katika moyo wake. Alipoamrishwa, alikula kunjo, au hati-kunjo aliyopewa na Mungu. “Kinywani mwangu lilikuwa tamu, kama utamu wa asali,” akasema Ezekieli. Ingawa kunjo hilo lilijawa “maombolezo, na vilio, na ole,” lilikuwa tamu kwa Ezekieli kwa sababu aliithamini heshima ya kumwakilisha Yehova. Lilikuwa jambo tamu kwa nabii kutimiza mgawo wake aliopewa na Mungu. Mungu alimwambia hivi: “Mwanadamu, maneno yangu yote nitakayokuambia, yapokee moyoni mwako, na kuyasikia kwa masikio yako.” (Ezekieli 2:9–3:3, 10) Njozi hizo zilifanya Ezekieli ajue wazi sana ni mambo gani Mungu alimruhusu kushiriki na zikaimarisha uhusiano wake pamoja na Yehova.
12. Ezekieli alifanya nini kwa zaidi ya makumi mawili ya utumishi wa kiunabii?
12 Ezekieli alipewa njozi na ujumbe mbali-mbali kwa ajili ya makusudi na wasikilizaji tofauti-tofauti. Alipaswa kusikiliza kwa uangalifu halafu aseme na kutenda kama alivyoelekezwa. Habari mpya na taratibu zilifunuliwa kwake hatua kwa hatua wakati wa miaka kama 22 ya utumishi wake wa kiunabii. Nyakati fulani Ezekieli alisema ujumbe uliopangiwa maneno maalumu. Nyakati nyingine, aligeukia kuigiza maneno bila kuyatamka kwa sauti, kama kwa kulala mbele ya tofali lenye kufananisha Yerusalemu. (Ezekieli 4:1-8) Kielelezo chake katika mambo ya kibinafsi, kama vile itikio lake kwa kifo cha mke wake, kilikuwa na ujumbe fulani pia. (Ezekieli 24:15-19) Ilikuwa lazima ajue mambo ya kisasa, sikuzote akiwakilisha ujumbe ufaao na kufanya kitendo kifaacho wakati ufaao. Ezekieli alifungwa katika uhusiano wa karibu sana, wa kufanya kazi hatua kwa hatua pamoja na Yehova.
13. Twaweza kujengaje uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?
13 Vivyo hivyo, ili sisi tujenge na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova tukiwa wafanya kazi wenzake, ni lazima tuingize Neno la Mungu katika moyo wetu. (1 Wakorintho 3:9) Kuendelea sambamba na tengenezo la Mungu lionekanalo katika habari hii kwataka kwamba tupige mwendo mmoja na tiririko la chakula cha kiroho kama kitolewavyo kwa wakati ufaao. (Mathayo 24:45-47) “Lugha iliyo safi” inapanuka daima. (Sefania 3:9) Ni ikiwa tu sisi twaendelea na mambo ya kisasa kwamba twaweza kikweli kuitikia kwa utii mwelekezo wa Mpandaji wa Gari.
14, 15. Ni kawaida gani ambayo yahitajiwa ili kuendelea sambamba na mwendo uwekwao na tengenezo la Mungu?
14 Kwa kusudi hilo, twahitaji kawaida nzuri ya sala ya kibinafsi, funzo la kibinafsi, na kushiriki katika huduma takatifu ya habari njema. (Warumi 15:16) Kumbukeni kielelezo cha Ezekieli katika kula lile kunjo lenye ujumbe wa Mungu. Ezekieli alikula kunjo zima, si sehemu yalo. Hakuokota na kuchagua vitonge ambavyo vingaliweza kupendeza zaidi ladha yake ya kibinafsi. Vivyo hivyo, funzo letu la kibinafsi la Biblia na vichapo vya Kikristo lapasa kuratibishwa ili liendelee sambamba na tiririko la chakula cha kiroho, nasi twapaswa kushiriki yote yawekwayo juu ya ile meza ya kiroho, kutia na kweli zenye kina kirefu.
15 Je! sisi hufanya jitihada ya sala kupata maana ya kile chakula kigumu? Kuendelea sambamba kwataka kwamba maarifa na uelewevu wetu yasonge mbele kupita yaliyo ya msingi, kwa maana twasoma hivi: “Kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga. Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya.” (Waebrania 5:13, 14) Ndiyo, kufanya maendeleo ya kiroho ni sehemu muhimu ya kwenda sambamba na mwendo ambao tengenezo la Mungu laweka.
Hatuzuiliwi na Kutojali kwa Watu
16, 17. Ezekieli alishughulikaje na kutojali kwa watu, dhihaka, na ukosefu wa itikio?
16 Ezekieli pia aliweka kielelezo kizuri kwa kuwa mtii na kutojiruhusu azuiliwe na kutojali kwa watu au dhihaka. Vivyo hivyo, kwa kuendelea mwendo mmoja na ukuzi wa lugha iliyo safi, twaelekea kumoja na upande wenye kuendewa na Mpandaji Gari aliye wa kifalme. Hivyo twapewa vifaa vya kuitikia amri zake, kuimarishwa tusizuiliwe na kutojali kwa watu wala dhihaka ya wale tuwaambiao ujumbe wa hukumu ya Yehova. Kama kwa habari ya Ezekieli, Mungu ametangulia kutuonya kwamba watu fulani wangepinga kwa bidii, wakiwa na vichwa vigumu na mioyo migumu. Wengine hawangesikia kwa sababu hawataki kumsikiliza Yehova. (Ezekieli 3:7-9) Bado wengine wangekuwa wanafiki, kama vile Ezekieli 33:31, 32 isemavyo: “Nao huja kwako kama watu wajavyo, nao hukaa mbele yako kama watu wangu, nao husikia maneno yako, wasiyatende; maana kwa vinywa vyao hujifanya kuwa wenye upendo mwingi, lakini mioyo yao inatafuta faida yao. Na tazama, wewe umekuwa kwao kama wimbo mzuri sana, wa mtu mwenye sauti ipendezayo, awezaye kupiga kinanda vizuri; maana, wasikia maneno yako, lakini hawayatendi.”
17 Tokeo litakuwa nini? Mstari wa 33 waongezea hivi: “Na hayo yatakapokuwapo, (tazama, yanakuja), ndipo watakapojua ya kuwa nabii amekuwapo kati yao.” Maneno hayo yafunua kwamba Ezekieli hakuacha kwa sababu ya ukosefu wa itikio. Ubaridi wa wengine haukumfanya awe baridi-baridi. Watu wawe walisikiliza au sivyo, yeye alimtii Mungu na kutimiza utume wake.
18. Ni maswali gani ambayo ungeweza kujiuliza?
18 Tengenezo lionekanalo la Mungu sasa linazidisha mbiu ya kwamba wote wapaswa kumhofu Mungu na kumpa utukufu. Je! wewe huvumilia uchambuliwapo kwa kuchukua msimamo jasiri katika kutoa ushahidi wa Ufalme, kwa kufuata adili katika mtindo wa maisha yako? Je! unasimama imara unapokuwa shabaha ya kukazwa kwa sababu ya kutokubali damu, kutoabudu mifano ya kitaifa, kutosherehekea sikukuu za kilimwengu?—Mathayo 5:11, 12; 1 Petro 4:4, 5.
19. Kwa habari ya mwelekezo, sisi tutafanya nini ikiwa tunaendelea sambamba pamoja na gari la Yehova la kimbingu?
19 Mwendo huo si rahisi, lakini wale wenye kuvumilia hadi mwisho wataokolewa. (Mathayo 24:13) Kwa msaada wa Yehova, hatutaacha watu wa ulimwengu watufanye kama wao na hivyo watuondoe katika mwendo pamoja na gari la Yehova la kimbingu. (Ezekieli 2:8; Warumi 12:21) Ikiwa tunaendelea sambamba na tengenezo la kimalaika lililo kama gari, tutafuata upesi mwelekezo na maagizo yapokewayo kupitia tengenezo lionekanalo la Mungu. Yehova huandaa tuhitajiyo ili kukabili mashambulio ya imani yetu, kudumisha mshiko wetu juu ya Neno la uhai, na kuweka macho yetu yakiwa yamekazwa juu ya mambo halisi ya kiroho ambayo yahusu hasa Mpandaji wa Kifalme wa gari la kimbingu.
Twachochewa Kuendelea Sambamba
20. Ni nini mengine ya mambo yaliyoandikwa na Ezekieli ambayo yapasa kutuchochea tuendelee sambamba?
20 Njozi za Ezekieli zapasa kutuchochea tuendelee sambamba. Si kwamba tu alijulisha wazi hukumu za Mungu juu ya Israeli bali pia aliandika unabii mbalimbali wa kurudishwa. Ezekieli alielekeza kwa Mmoja ambaye angekuwa na haki ya kisheria kutawala akiwa juu ya kiti cha enzi cha Yehova kwenye wakati uliowekwa. (Ezekieli 21:27) Mtumishi huyo wa Kifalme, “Daudi,” angekusanya tena watu wa Mungu na kuwachunga. (Ezekieli 34:23, 24) Ingawa wangeshambuliwa na Gogu wa Magogu, Mungu angewakomboa, na adui Zake wangelazimishwa ‘kumjua Yehova’ wakati hasa wangekuwa wakiingia katika uharibifu. (Ezekieli 38:8-12; 39:4, 7) Ndipo watumishi wa Mungu wangeona shangwe ya uhai usio na mwisho katika mfumo wa ibada safi inayohusisha hekalu la kiroho. Maji ya uhai yanayotiririka kutoka patakatifu yangekuwa chanzo cha ulishaji na uponyaji, na urithi wa nchi ungegawanywa mafungu-mafungu kwa baraka yao.—Ezekieli 40:2; 47:9, 12, 21.
21. Kwa nini fungu la Mashahidi wa ki-siku-hizi wa Yehova ni kubwa kuliko lile la Ezekieli?
21 Ni lazima Ezekieli awe alisisimuka kama nini kuandika unabii huo mbalimbali! Hata hivyo, fungu la Mashahidi wa Yehova wa ki-siku-hizi ni kubwa zaidi. Tunaishi wakati ambapo baadhi ya unabii mbalimbali huo unatimizwa. Kwa uhakika, sisi ni washiriki watendaji katika matimizo fulani. Kwa njia ambayo twaishi, je! sisi mmoja mmoja huonyesha usadikisho wa kwamba Yesu sasa atawala akiwa Mmoja mwenye haki iliyo halali kisheria? Je! sisi binafsi twasadiki kwamba karibuni Yehova atajitakasa na kuwakomboa waingie katika ulimwengu mpya wake wale wanaoendelea sambamba na tengenezo lake? (2 Petro 3:13) Usadikisho huo, ukiandamana na kazi za imani, waonyesha kwamba kwa kweli sisi tunaendelea sambamba pamoja na gari la Yehova la kimbingu.
Endelea na Kufuata Mwendo Sambamba
22. Ni nini liwezalo kufanywa kuepuka vikengeusha-fikira ili kudumisha tazamio la kiroho la kuona mambo wazi?
22 Tukiisha ‘kutia mkono wetu kulima,’ ni lazima tusitazame nyuma kwa kutamani chochote chenye kutolewa na ulimwengu. (Luka 9:62; 17:32; Tito 2:11-13) Hivyo basi acheni tuzuie mbetuko wowote wa kuweka hazina duniani, na acheni tuendeleze jicho letu likiwa sahili (rahisi), likiwa limekazwa juu ya Ufalme. (Mathayo 6:19-22, 33) Kusahilisha maisha zetu, kubwaga chini vilemeaji vya kilimwengu, kutatusaidia tuendelee sambamba pamoja na tengenezo la Yehova. (Waebrania 12:1-3) Vikengeusha-fikira vyaweza kutia kiwi katika mwono wetu wa gari la kimbingu na Mpandaji walo. Lakini kwa msaada wake, twaweza kudumisha tazamio la kiroho lenye mwono wa wazi, kama Ezekieli alivyofanya.
23. Mashahidi waaminifu wahitaji kufanya nini kwa ajili ya wapya?
23 Sehemu ya daraka letu tukiwa Mashahidi wa Yehova latia ndani kusaidia wale wapya wengi waendelee sambamba pamoja na gari la Mungu la kimbingu. Katika 1990 karibu 10,000,000 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo. Ingawa wengi wa watu mmoja mmoja hao huenda wakawa wanahudhuria mikutano michache ya Kikristo, wao wahitaji kuona umaana wa kufanya maendeleo pamoja na tengenezo lionekanalo la Yehova. Sisi Mashahidi waaminifu, twaweza kuwasaidia kwa roho tuonyeshayo na kitia-moyo tutoacho.
24. Twapaswa kufanya nini katika nyakati hizi za upeo?
24 Hizi ni nyakati zenye kufikia upeo. Kwa macho ya imani, tumeliona gari la kimbingu likija mbele yetu. Mpandaji wa Gari aliye wa kifalme amelipa tengenezo lake lionekanalo utume wa kuyahubiria mataifa hivi kwamba, katika upeo kamili, wao watajua Yehova ni nani. (Ezekieli 39:7) Tumia kwa ubora kabisa fursa kubwa hii ya kushiriki katika kuondolewa malawama kwa enzi kuu ya Mungu na kutakaswa kwa jina lake takatifu kwa kuendelea sambamba pamoja na gari la Yehova la kimbingu.
Wewe Ungejibuje?
◻ Ezekieli aliweka kielelezo gani kwa kadiri utume wake ulivyohusika?
◻ Yamaanisha nini kuendelea sambamba pamoja na tengenezo la Mungu?
◻ Ezekieli aliyaonaje maneno ya Yehova?
◻ Sisi twaweza kufuataje kielelezo cha Ezekieli katika kushughulika na kutojali kwa watu?
◻ Ni nini chapasa kusukuma watumishi wa Yehova waendelee sambamba pamoja na gari lake la kimbingu?y
[Picha katika ukurasa wa 15]
Ni nini ambacho chatakwa ili kuendelea sambamba pamoja na gari la Yehova la kimbingu?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Ezekieli alithamini mapendeleo yake aliyopewa na Mungu. Wewe je?