Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 4/1 kur. 26-29
  • Kuhesabu Gharama Ya Kuhamia Nchi Yenye Utajiri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhesabu Gharama Ya Kuhamia Nchi Yenye Utajiri
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mambo Halisi ya Maisha Ng’ambo
  • Misongo ya Kiadili
  • Wazazi Wasiokuwapo
  • Wenye Uhakika Katika Maandalizi ya Mungu
  • Je, Nikaishi Ng’ambo?
    Amkeni!—2000
  • ‘Kuandalia Watu wa Nyumbani mwa Mtu’—Kukabiliana na Huo Ugumu Katika Nchi Zinazositawi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Naweza Kufanikishaje Maisha Yangu Ng’ambo?
    Amkeni!—2000
  • Nifanyeje Ikiwa Sisi Ni Maskini?
    Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 4/1 kur. 26-29

Kuhesabu Gharama Ya Kuhamia Nchi Yenye Utajiri

NI TAMASHA ya kawaida kwenye ofisi za kibalozi kotekote katika ulimwengu unaositawi: chumba cha kungojea kikiwa kimejazana watu wanaotazamia mahoji yao kwa wasiwasi. Kwa msingi wa mazungumzo mafupi hayo yaliyo ya maana, itaamuliwa kama wao waweza kupata visa ya kwenda nchi ya Magharibi yenye maendeleo ya viwanda. Wengi huamini kwamba hii itakuwa ndiyo tikiti yao ya kupata ufanisi. “Mimi nimekuwa nikifanya kazi kwa bidii kwa miaka minne, na sijaweza kununua redio,” akalalamika kijana mmoja wa Afrika Magharibi. “Kama ningekuwa katika Uingereza au United States, kufikia sasa ningekuwa na gari na mahali pangu mwenyewe pa kuishi.”

Si vigumu kuelewa ni kwa nini wengi katika mataifa maskini, yanayositawi wana maoni hayo. Kwao, kazi ni ngumu kupatikana na mshahara ni wa chini. Inflesheni humomonyoa pesa za akiba. Nyumba ni haba na zenye kusongamana. Watu huvaa nguo ambazo zimetupwa na wale walio katika nchi zenye utajiri. Wengi huhisi wamenaswa katika uchumi ulio kama mchanga wa kutopeza ndani.

Nayo Magharibi yenye utajiri huwavutia kama nini! Alisema hivi kijana mwanamume mmoja katika Sierra Leone: “Watu fulani ambao wameenda ng’ambo hurudi na kutusimulia hadithi ambazo hutupa sisi moyo mkuu twende tukajionee wenyewe nchi zenye maendeleo ya viwanda. Wao husema utalazimika kufanya kazi kwa bidii, lakini utapata pesa nyingi ili uweze kujiruzuku na hata kupata anasa fulani-fulani, kama gari. Na ukirudi hapa ukiwa na dola karibu elfu mbili, waweza kuanzisha biashara na kufunga ndoa.”

Haishangazi kwamba, watumishi fulani wa Mungu husababu jinsi iyo hiyo. Dada mmoja Mwafrika alisema hivi: “Sisi wachanga katika tengenezo la Mungu husikiliza maongezi juu ya jinsi wengine wanavyoendelea vizuri ambao wameenda ng’ambo. Basi nyakati fulani mimi hujiuliza, ‘Namna gani mimi? Kwa nini mimi natesekea hapa? Niende au nibaki?’”

Ikiwa wewe waishi katika nchi maskini, huenda wewe vilevile ukajiuliza kama kuhama kungeleta maendeleo ya ubora wa maisha yako. Hata hivyo, kuhamia nchi ya kigeni ni jasirio kubwa sana, hatua ghali na nzito. Huenda ikahusisha kujifunza lugha mpya, kujipatia stadi mpya za kazi, kujirekebisha kulingana na utamaduni mpya, kuvumilia maoni ya ubaguzi ambayo wengi huonyesha kuelekea watu wa kigeni, na kujifunza njia mpya kabisa ya maisha. Hata hivyo, Wakristo wengi wamefanya hivyo kwa mafanikio na wakathibitika kuwa misaada halisi kwa makundi katika nchi za makao yao mapya, wakitumikia kama wahubiri, mapainia, wazee, na watumishi wa huduma walio vielelezo.

Ingawa hivyo, si wote ambao wameendelea vema sana. Mikazo na migogoro ya kuhamia huko imetokeza uangamivu wa kiroho kwa wengine. Kwa wazi, basi, mhamo huo wapasa kufanywa kwa fikira nzito, yenye sala. Biblia hushauri hivi kwenye Mithali 3:5, 6: “Mtumaini BWANA [Yehova, NW] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” Ndiyo, wewe wataka kuwa na uhakika kwamba unatenda kupatana na mapenzi ya Yehova. (Yakobo 4:13-15) Na Yesu alitoa ushauri fulani wenye kutumika ili kukusaidia ufanye hivi alipohimiza wasikilizaji wake “kuhesabu gharama.” (Luka 14:28) Hii yahusisha ndani mengi kuliko mafikirio ya kifedha. Yamaanisha kufikiria gharama za kiroho ambazo zawezekana kutokea kwa kuhamia huko.

Mambo Halisi ya Maisha Ng’ambo

Kabla ya kuhamia kwingineko, wapaswa kuwa na wazo zuri la kuona mambo kihalisi juu ya mambo ya kutazamia ufikapo huko. Ikiwezekana, fanya ziara ya utangulizi ujionee mwenyewe hali zilivyo. Ama sivyo, utalazimika kutegemea habari za kuambiwa. Yaonya hivi Biblia: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.”—Mithali 14:15.

Watu fulani wamepata habari zao zote juu ya maisha katika nchi za Magharibi kutokana na sinema na maonyesho ya televisheni. Hivyo wao huamini kwamba kila mtu huko ni tajiri, huendesha gari jipya, na huishi katika nyumba yenye vitu vya starehe. Ingawa hivyo, uhalisi ni tofauti kabisa. Nchi nyingi zenye utajiri zina kadiri kubwa ajabu za umaskini, ukosefu wa makao, na ukosefu wa kazi. Na wengi wa wakaaji walio maskini zaidi ni wale wahamiaji wapya. Aeleza hivi ofisa mmoja wa ofisi ya kibalozi kwenye ubalozi wa United States katika nchi maskini moja: “Watu hawatambui kamwe jinsi ilivyo vigumu kupata uthibitifu wa maisha katika Amerika. Wengine huandika barua wakieleza jinsi wanavyoendelea vema—jinsi wamenunua magari mawili na nyumba—lakini kwa ukweli wao huwa wakifanya jitihada ngumu kweli kweli.”

Ndivyo hali ilivyo mahali penginepo. Bw. Sahr Sorie ni mwelimishaji wa Afrika Magharibi ambaye ameishi na kusomea London. Alieleza hivi: “Si rahisi kuhama Afrika na kutulia katika Uingereza. Wahamiaji wengi huishi maisha ya umaskini sana. Mtu huona katika nyuso zao mikunjo ya kuonyesha magumu. Wengine huona ikiwa vigumu kukusanya-kusanya mapeni 20 ili wapige simu. Mara nyingi wao hushirikiana chumba kimoja pamoja na wengine wengi, kukiwa na chombo kidogo tu cha kuwapasha joto. Wao huweza kupata kazi za chini tu, na hata hapo huwa haziwatoshi kulipa gharama zao. Wale waondokao Afrika ili waepuke umaskini hujikuta mara nyingi wakiwa katika hali mbaya zaidi katika mitaa michafu ya Ulaya.”

Misongo ya kifedha ambayo huandamana na kupata uthibitifu wa maisha katika nchi mpya yaweza kusonga kwa urahisi hali ya kiroho ya mtu. (Mathayo 13:22) Ni kweli, kazi ngumu yasifiwa katika Biblia. (Mithali 10:4; 13:4) Lakini wengi waendao ng’ambo hulazimika kuchukua kazi mbili au tatu ili watimize miradi yao ya kifedha—au kuweza kujipatia riziki tu. Ni wakati kidogo sana ubakio kwa kufuatia ibada ya Mungu. Yenye kuachiliwa huwa ni mikutano ya Kikristo, funzo la Biblia, na kushiriki ukweli wa Biblia pamoja na wengine. Maneno ya Yesu Kristo huthibitika kuwa ya kweli kimsiba: “Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.”—Mathayo 6:24.

Misongo ya Kiadili

Pia wapaswa kufikiria hali ya kiadili ya ile utazamiayo kuwa nchi yako mpya. Biblia yatuambia kwamba Loti alichagua kuishi katika Wilaya ya Yordani. Kutokana na maoni ya kimwili, uamuzi wake ulionekana kuwa wa hekima, kwa maana ‘lilikuwa jimbo lenye kutiliwa maji vizuri, kama bustani ya Yehova.’ (Mwanzo 13:10, NW) Hata hivyo, majirani wapya wa Loti walikuwa “wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya BWANA [Yehova, NW]”—wapotosha-ngono. (Mwanzo 13:13) Tokeo ni kwamba, “mtu huyu mwenye haki akikaa kati yao, kwa kuona na kusikia, alijitesa roho yake yenye haki, siku baada ya siku, kwa matendo yao yasiyo na sheria.”—2 Petro 2:8.

Vivyo hivyo, mhamo wa kwenda Magharibi ungeweza kuweka wewe na familia yako wazi kwenye misongo ya kiadili na vishawishi vilivyo vikali kuliko katika nchi ya nyumbani kwenu. Zaidi ya hilo, huenda watu wenye umri mkubwa zaidi wasiheshimiwe kama walivyokuwa huko nyumbani. Staha kwa wazazi huenda isitiwe moyo. Huenda majirani wasipendezwe sana na mmoja na mwenzake. Misongo ya jinsi hiyo ingeweza kuathiri wewe na familia yako jinsi gani? Hilo ni jambo la kufikiria kwa sala.

Wazazi Wasiokuwapo

Wazazi fulani wamechagua kuacha familia zao nyuma na kusafiri ng’ambo peke yao. Mpango wao ni kutuma familia yao nzima ije mara wakiisha kutulia au labda warudi nyumbani wakiwa na pesa nyingi. Je! mpango wa jinsi hiyo ni wa hekima?

Maandiko yawapa wazazi wajibu wa kuandaa mahitaji ya kimwili ya familia zao, na katika visa fulani vya kupita kiasi, huenda mzazi asiwe sana na la kufanya isipokuwa kufanya kazi ng’ambo ili afanye uandalizi huo. (1 Timotheo 5:8) Na bado, wazazi wana wajibu pia wa kutunza mahitaji ya kiroho ya familia zao. Lasema hivi Neno la Mungu: “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.”—Waefeso 6:4.

Je! baba aweza kufanya hivyo kwa matokeo mazuri akiwa mbali na familia yake kwa miezi au miaka kadhaa kwa safari moja? Haielekei hivyo. Basi ni lazima wewe ufikirie kama faida zozote za kimwili zipatikanazo zastahili lile tokeo ambalo kutokuwapo kwako kungeweza kuwa nalo juu ya watoto wako. Zaidi ya hilo, mara nyingi wahamaji hukuta kwamba si rahisi hata kidogo kujipatia “donge la utajiri” kama walivyofikiri. Ikiwa mhamaji hawezi kulipa pesa za kuingia kwa familia, mtengano huo huenda ukajikokota kwa muda wa miaka. Hilo, nalo, huenda likafanyiza hatari nzito za kiadili. (Linganisha 1 Wakorintho 7:1-5.) Kwa kuhuzunisha, watu fulani katika hali zenye kujaribu wamejiacha wakashindwa na ukosefu wa adili katika ngono.

Wenye Uhakika Katika Maandalizi ya Mungu

Wakati hali za kiuchumi ulimwenguni zizorotapo, ni vema kukumbuka kwamba watumishi wa Mungu hawapaswi kuhofu kwamba wataachiliwa. Yesu alisema hivi: “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”—Mathayo 6:31-33.

Mashahidi wa Yehova leo hutumikia masilahi ya Ufalme wa Mungu kwa kupiga mbiu ya habari njema kwa bidii. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Katika mataifa maskini mengi, kuna uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Hasa kuna uhitaji wa wazee na watumishi wa huduma walio wakomavu. Badala ya kwenda kwenye nchi yenye ufanisi wa kiuchumi ambako uhitaji si mkubwa sana, wengi wamechagua kubaki katika nchi za kienyeji za kwao. Wengine wa hao wameendeleaje?

Alethia, Mwafrika wa Magharibi ambaye ametumikia katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 30 katika nchi ya kienyeji ya kwao, alisema hivi: “Mimi nilipata fursa ya kuishi ng’ambo. Sababu ambayo sikufanya hivyo ilikuwa kwamba napenda kuwa pamoja na watu wangu mwenyewe na watu wa ukoo. Naona shangwe ya kuwasaidia wajifunze ukweli ili sisi tuweze kumtumikia Yehova pamoja. Sijakosa hata kitu kimoja kwa kubaki hapa, nami sijutii lolote.”

Winifred vilevile huishi katika nchi fulani ya Kiafrika. Ubora wa maisha ya kimwili huko wakadiriwa kuwa ulio wa hali ya chini kabisa ulimwenguni. Lakini baada ya miaka 42 katika utumishi wa painia wa wakati wote, mwanamke huyo asema hivi: “Si rahisi sikuzote kuweza mambo kiuchumi. Shetani hujaribu kufanya mambo yawe magumu, lakini sikuzote Yehova ameniandalia mimi na kutunza mahitaji yangu.”

Nyakati za kale Abrahamu ‘alijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi.’ (Warumi 4:21) Je! wewe vilevile una uhakika kwamba Yehova aweza kutimiza ahadi yake na kukutunza ukiweka masilahi ya Ufalme kwanza katika maisha yako? Je! wakubaliana na mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Sheria ya kinywa [cha Mungu] ni njema kwangu, kuliko maelfu ya dhahabu na fedha”? (Zaburi 119:72) Au ingeweza kuwa kwamba wewe una uhitaji wa kutumia kikamili zaidi shauri la mtume Paulo? Kwenye 1 Timotheo 6:8, aliandika hivi: “Tukiwa na chakula na nguo tutaridhika na vitu hivyo.” Je! ingeweza kuwa kwamba jambo la hekima kufanya lingekuwa, si kutafuta mazingira mapya, bali kutumia kwa kadiri bora zaidi yale ya sasa?

Hali za kiuchumi katika nchi nyingi zaweza kusababisha magumu makali kwa Wakristo. Hivyo, baada ya kufikiria mambo yote yahusikayo, ikiwa familia yaamua kuhamia kwingineko, hakuna sababu ya wengine kuwa wachambuzi. (Wagalatia 6:5) Wale wanaobaki waweza kuendelea kuomba msaada wa Yehova katika kuvumilia magumu ambayo mfumo huu huleta, huku wakishangilia katika baraka za kiroho ambazo Mungu huwapa. Kumbuka, karibuni mambo yasiyo haki na madhalimu ya ulimwengu huu yatarekebishwa chini ya Ufalme wa Mungu. Ndipo itakapokuwa kama vile mtunga zaburi alivyoandika: “[Yehova] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”—Zaburi 145:16.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki