Tanguliza Mungu Katika Maisha Ya Familia Yako!
BOB na Jean—wenzi wa ndoa waliotangulizwa katika makala iliyopita—hawakupata talaka. Badala ya hiyo, walizungumza juu ya matatizo yao pamoja na mhudumu wa Kikristo. Upesi alifahamu kwamba magumu yao yalitokana na malezi yao tofauti.
Kwa mfano, kwa kuwa Bob alitoka kwa familia ya wafanya biashara na wenye kufanya kazi katika viwanda naye mwenyewe alifanya kazi za mkono, alitaka kiamusha-kinywa kikubwa kila asubuhi. Jean, ambaye alitoka kwa familia ya wafanya kazi za ofisini, alikuwa anampa kahawa na mkate-choma. Kwa hiyo, ugomvi juu ya kiamsha-kinywa ukawa vita kubwa!
Bob na Jean walihitaji kuendeleza uwasiliano wao. Hata hivyo, kisababishi cha kweli cha msononeko wao kilikuwa na kina kirefu zaidi. “Je! ninyi huonana kwa jinsi ya ufahamu wa 1 Wakorintho 13:4?” akauliza huyo mhudumu. Andiko hilo la Biblia lasomeka hivi: “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari; haujivuni.” Mstari unaofuata unasema upendo “haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya.” Jean na Bob pia walikubali kutumia maneno hayo katika uhusiano wao.
Matatizo ya wenzi hao wa ndoa yalihitaji hasa suluhisho la kiroho. Kwa kuwa Bob na Jean walitamani kudumisha uhusiano mzuri na Mungu, zaidi ya yote walihitaji kutumia kanuni za Biblia na kung’amua kwamba “BWANA [Yehova, NW] asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure.” (Zaburi 127:1) Mistari 3 hadi 5 inahusu kujenga familia. Na fanaka zaidi katika kuendeleza furaha ya kinyumbani inatokana na kumtanguliza Mungu katika maisha ya familia.—Waefeso 3:14, 15.
Yanayohusika Katika Kumtanguliza Mungu
Kutanguliza Mungu katika maisha ya familia yako huwa zaidi ya kusema tu, “Familia inayosali pamoja hukaa pamoja.” Kulingana na gazeti Family Relations, wengi huamini “kwamba dini inarahisisha uhusiano wa familia ulio chanya (mzuri) na wenye hali njema na inakuza uradhi wa uhai wa washiriki wayo.” Lakini kuzoeza dini tu si sawa na kutanguliza Mungu. Wengi hushikilia kidesturi kwa dini kwa sababu tu ya tabia, mapokeo ya familia, au faida ya kijamii. Mungu ana uvutano mdogo sana katika maisha yao ya kila siku. Yenye maana zaidi ni kwamba, si dini zote zilizo ‘safi, zisizo na taka mbele za Mungu Baba.’—Yakobo 1:27.
Kutanguliza Mungu katika maisha ya familia yetu, ni lazima sisi na wapendwa wetu tumwabudu Yehova, ‘Aliye juu, juu ya nchi yote,’ kulingana na matakwa yake. (Zaburi 83:18) Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alisema hivi: “Saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni Roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” (Yohana 4:23, 24) Kumwabudu Yehova Mungu “katika roho,” ni lazima utumishi wetu mtakatifu kwake uchochewe kwa moyo uliojaa upendo na imani. (Marko 12:28-31; Wagalatia 2:16) Kumwabudu Yehova katika “kweli” hutaka kwamba tukatae uwongo wa kidini na tupatane na mapenzi yake kabisa kama yalivyofunuliwa katika Biblia. Hatuwezi kutanguliza Yehova Mungu isipokuwa dini yetu inalingana na kanuni zake.a Baadhi yazo ni zipi? Na kuzitumia kunaweza kunufaishaje familia yako?
Kutanguliza Mungu Ukiwa Mume
Kwenye 1 Wakorintho 11:3, Biblia inasema hivi: “Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo, na kichwa cha mwanamke ni mwanamume, na kichwa cha Kristo ni Mungu.” Ikiwa wewe ni mume, una daraka ulilopewa na Mungu la kuwa mfanya-maamuzi mkuu katika familia yako. Lakini jambo hilo halimpi mume yeyote leseni ya kuwa mwonevu au mtawala mkali.
Biblia inawatia moyo waume wafikirie maoni ya wake zao wanapofanya maamuzi yanayowaathiri. (Linganisha Mwanzo 21:9-14.) Kwa kweli, Maandiko hutuhimiza sisi sote ‘tusiangalie mambo yetu wenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.’ (Wafilipi 2:2-4) Ambapo kanuni yoyote ya Biblia haihusiki, mara nyingi mume Mkristo atakubali pendezi la mke wake. Akiwa na upendezi wa kibinafsi kwake, atahakikisha pia kwamba mke halemewi zaidi na madaraka. Kwa mfano, huenda akamsaidia kazi za kinyumbani, hasa ikiwa mke ana kazi ya kimwili.
Mtume Paulo aliandika hivi: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa [kundi, NW].” (Waefeso 5:28, 29) Yesu Kristo hushughulika na washiriki wa kundi katika njia ya upendo.
Linalostahili kuangaliwa pia ni shauri la mtume Petro: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe.” (1 Petro 3:7) Je! si jambo zito kung’amua kwamba sala za mume zaweza kuzuiliwa ikiwa hamtendei mke wake kwa upendo? Naam, ni lazima mwanamume ashughulikie mke wake kwa njia ya upendo ikiwa Mungu atasikia na kujibu sala zake.
Kutanguliza Mungu kunaathiri pia uhusiano wa Baba pamoja na watoto wake. Anapaswa kuwa na ufikirio wenye kina kirefu juu ya hali yao njema ya kiroho. Hata hivyo, katika uchunguzi mkuu wa U.S., ni nusu tu ya wanaume ambao walisema kwamba “kushiriki katika vikundi vya mafunzo au mazungumzo ya Maandiko” kulikuwa kwa ‘maana zaidi katika ukuzi wa kiroho wa familia yao.’ Waliosalia walitaja mambo kama “kuangalia au kusikia ibada za kidini zinazoenezwa” au ‘kufikiria maana ya uhai.’
Hata hivyo, Biblia inawaambia akina baba hivi: “Msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana, [Yehova, NW].” (Waefeso 6:4) Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, akina baba wanatarajiwa kuongoza katika ibada ya familia. Kwa kawaida kuongoza mafunzo ya Biblia ya familia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kupatana na matakwa ya Kimaandiko, wanaume kama hao hutanguliza Mungu katika maisha ya familia.
Kutanguliza Mungu Ukiwa Mke
Ikiwa wewe ni mke, unaweza kutanguliza Mungu kwa kumwunga mkono mume wako katika daraka lake akiwa kichwa cha familia. Biblia husema hivi: “Ninyi wake, watiini waume zenu, kama ipendezavyo katika Bwana.” (Wakolosai 3:18) Hiyo huenda ikawa vigumu ikiwa mwanamume hawasiliani au ni mzembe katika kuongoza ibada ya familia. Kwa vyovyote, kukazia daima makosa yake au, vibaya zaidi, kuasi dhidi yake kutaongeza tu msononeko wa familia.
Mithali 14:1 yasema hivi: “Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.” Njia moja ambayo mwanamke mwenye hekima aliyeolewa aweza kutanguliza Mungu na ‘kuijenga nyumba yake’ ni kwa kujitiisha kwa mume wake. (1 Wakorintho 11:3) Akiwa na ‘sheria ya wema katika ulimi wake,’ yeye huepuka kumchambua mume wake isivyohitajiwa. (Mithali 31:26) Yeye pia hufanya kazi kwa bidii ili mipango ya mume wake ifanikiwe.
Njia nyingine ya mwanamke aliyeolewa kutanguliza Mungu ni kwa kuwa mke mwenye bidii ya kazi. Bila shaka, ikiwa ni lazima afanye kazi ya kimwili, huenda asiwe wala na wakati wala na nguvu inayohitajiwa kudumisha nyumba yake kama anavyotamani. Bado aweza kujitahidi kuwa kama “mke mwema” ambaye Biblia yasema hivi juu yake: “Huangalia sana njia za watu wa nyumbani mwake; wala hali chakula cha uvivu.”—Mithali 31:10, 27.
Zaidi ya hayo yote, mke anahitaji kutanguliza ibada ya Mungu maishani mwake. Wengi ambao huzuru Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova kwa wakati wa kwanza hueleza juu ya sura nadhifu za watoto. Kazi ya mke kuhusu jambo hili ina thamani isiyokadirika. Lakini ni lazima pia afanye kazi kudumisha hali yake ya kiroho kupitia sala, kujifunza, na utumishi kwa Mungu.
Kutanguliza Mungu Mkiwa Vijana
Makala katika Adolescent Counselor yataarifu hivi: “Watoto wameelekea kusitawisha mielekeo na falsafa ambazo zimewaruhusu kudhibiti wazazi wao. . . . Wakifunuliwa wazi kwa jamii inayokazia na kutukuza mapendezi ya mara iyo hiyo na utajiri wa kimwili, wabalehe [vijana] husitawisha mwelekeo wa ‘ninakitaka wakati huu huu.’” Ikiwa wewe ni kijana, je, huo ndio mwelekeo wako?
Wakolosai 3:20 lasema hivi: “Ninyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote; maana jambo hili lapendeza katika Bwana.” Kijana anayeona utii kama huo kuwa takwa la kimungu atashirikiana na wazazi wake. Kwa mfano, hataasi dhidi yao kisiri kwa kushiriki na wanashule wenzi ambao hawakubaliwi na wao; wala hatajaribu kuvuta kwa werevu mzazi yeyote ili apate haja yake. (Mithali 3:32) Badala ya hiyo, kijana yeyote anayetanguliza Mungu maishani mwake atajitiisha kwa mwongozo wenye upendo wa wazazi.
Endeleeni Kutanguliza Mungu!
Bila kujali mahali petu katika familia, tunahitaji kutanguliza Mungu maishani na kukuza uhusiano wenye ukaribu pamoja naye. Je! wewe na familia yako mnafanya hivyo?
Katika hizi “siku za mwisho,” sisi sote tunakabili “nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1-5) Hata hivyo, kusitawi kiroho kunawezekana na kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo. (Mathayo 24:3-14) Kwa kutenda kupatana na maarifa sahihi ya Biblia, wewe na familia yako mnaweza kuwa na tumaini la uhai wa milele katika dunia-paradiso. (Luka 23:43; Yohana 17:3; Ufunuo 21:3, 4) Naam, hiyo inawezekana ikiwa unatanguliza Mungu katika maisha ya familia yako.
[Maelezo ya Chini]
a Ona sura 22 ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichotangazwa kwa kuchapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Mke mwema huthaminiwa sana
[Picha katika ukurasa wa 7]
Biblia hutia moyo wanaume waongoze katika ibada ya familia