Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 7/15 kur. 18-22
  • Fuatia Fadhili-Upendo Sikuzote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fuatia Fadhili-Upendo Sikuzote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fadhili Yatufanya Tusiwe Wenye Ubinafsi
  • Fadhili Yatufanya Tuwe Wenye Ufikirio
  • Fadhili Huimarisha Vifungo
  • Wanawake Wanapoonyesha Fadhili
  • Endelea Kufuatia Fadhili-Upendo
  • Waonyeshe Fadhili-upendo Wenye Uhitaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Acha “Sheria ya Fadhili Zenye Upendo” Ilinde Ulimi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kufaidika na Fadhili-upendo za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Pendeza Yehova kwa Kuonyesha Fadhili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 7/15 kur. 18-22

Fuatia Fadhili-Upendo Sikuzote

“Aandamaye [Afuatiaye, NW] haki na fadhili [fadhili-upendo, NW], ataona uhai na haki na heshima.”—Mithali 21:21.

1. Kwa nini tungetazamia wale wanaoongozwa na roho ya Mungu waonyeshe fadhili?

YEHOVA ni mwenye fadhili na mwenye huruma. Yeye ni “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema [fadhili-upendo, NW] na kweli.” (Kutoka 34:6, 7) Basi yaeleweka, tunda la roho takatifu yake latia ndani upendo na fadhili.—Wagalatia 5:22, 23.

2. Tutaangalia mifano ipi sasa?

2 Wale wanaoongozwa na roho takatifu au nguvu ya utendaji ya Yehova, huonyesha tunda layo la fadhili. Wanaonyesha fadhili-upendo katika mahusiano yao pamoja na wengine. Kwa kweli, wanafuata mfano wa mtume Paulo, wakijipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu “kwa fadhili” na katika njia nyinginezo. (2 Wakorintho 6:3-10, NW) Roho yao yenye fadhili, yenye huruma na yenye kusamehe inapatana na utu wa Yehova, ambaye ni “mwingi wa fadhili-upendo” na ambaye katika Neno lake mna mifano mingi ya fadhili. (Zaburi 86:15, NW; Waefeso 4:32) Twaweza kujifunza nini kutokana na baadhi yazo?

Fadhili Yatufanya Tusiwe Wenye Ubinafsi

Bali Tuwe Wakaribishaji-Wageni

3. Abrahamu alikuwaje mfano mzuri katika kuonyesha fadhili, na Paulo atoa kitia moyo gani katika jambo hilo?

3 Abrahamu (Abramu) mzee wa ukoo—“rafiki wa Mungu” na “baba yao wote waaminio”—aliweka mfano mzuri katika kuonye-sha fadhili. (Yakobo 2:23; Warumi 4:11) Yeye na familia yake, kutia na mpwa wake Lutu, waliondoka Uru jiji la Ukaldayo na kuingia Kanaani kwa amri ya Mungu. Ingawa Abrahamu ndiye aliyekuwa mwanamume mwenye umri mkubwa zaidi na kichwa cha familia, alikuwa mwenye fadhili na asiye na ubinafsi katika kumruhusu Lutu achague mabara mazuri zaidi ya kulisha, huku yeye mwenyewe akichukua yaliyobaki. (Mwanzo 13:5-18) Fadhili iyo hiyo huenda ikatusukuma kuruhusu wengine wapate faida kwa hasara yetu. Fadhili isiyo na ubinafsi kama hiyo inapatana na shauri la mtume Paulo: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.” Paulo mwenyewe ‘aliwapendeza watu wote katika mambo yote, asitake faida yake mwenyewe, ila faida yao walio wengi, wapate kuokolewa.’—1 Wakorintho 10:24, 33.

4. Abrahamu na Sara walipata thawabu jinsi gani kwa kuonyesha fadhili kwa namna ya ukaribishaji-wageni?

4 Nyakati nyingine fadhili huchukua namna ya ukaribishaji-wageni wa kutoka moyoni. Abrahamu na mke wake, Sara, walikuwa wenye fadhili na wakaribishaji-wageni kwa wageni watatu waliokuwa wakipitia siku moja. Abrahamu aliwashawishi wakae kwa muda fulani, wakati yeye na Sara walipotayarisha kwa haraka chakula kizuri kwa ajili ya wageni. Wageni hao walitokea kuwa malaika wa Yehova, mmoja wao ambaye ndiye aliyewasilisha ahadi kwamba Sara aliyezeeka na asiye na mtoto angepata mwana. (Mwanzo 18:1-15) Thawabu iliyoje kwa ukaribishaji-wageni wenye fadhili!

5. Gayo alionyesha fadhili kwa njia gani, nasi twaweza kufanyaje jambo ilo hilo?

5 Njia moja ambayo Wakristo wote waweza kuonyesha fadhili ni kwa kuwa wakaribishaji-wageni. (Warumi 12:13; 1 Timotheo 3:1, 2) Kulingana na hiyo, watumishi wa Yehova huwaonyesha kwa fadhili ukaribishaji-wageni waangalizi wasafirio. Hiyo yakumbusha fadhili iliyoonyeshwa na Gayo Mkristo wa karne ya kwanza. Alifanya ‘kazi ya uaminifu’ katika kukaribisha ndugu waliozuru kwa ukaribishaji-wageni—nao walikuwa “wageni” ambao hakuwajua kabla ya hapo. (3 Yohana 5-8) Kwa kawaida, tunajua wale tunaoweza kuwaonyesha ukaribishaji-wageni kwa fadhili. Labda tunaona kwamba dada wa kiroho ni mwenye huzuni. Mwenzi wake wa ndoa huenda ikawa ni asiyeamini au hata mtu aliyetengwa na ushirika. Ni nafasi iliyoje kuonyesha fadhili kwa kumkaribisha kuonea shangwe ushirika wa kiroho na mlo pamoja na familia yetu mara kwa mara! Ingawa huenda ikawa hatutaandaa chakula kingi, kwa uhakika familia yetu itapata shangwe katika kuonyesha fadhili kwa dada kama huyo. (Linganisha Mithali 15:17.) Naye bila shaka ataonyesha shukrani yake kwa ajili ya hilo kwa maneno au katika barua ya asante yenye fadhili.

6. Lidia alionyeshaje fadhili, na kwa nini ni muhimu kuonyesha uthamini kwa vitendo vya fadhili?

6 Baada ya mwanamke Lidia mwenye kumcha Mungu kubatizwa, “alisema [kwa kusihi, NW], Kama mmeniona [Paulo na washirika wake] kuwa mwaminifu kwa Bwana [Yehova, NW], ingieni nyumbani mwangu mkakae. Akatushurutisha [naye akatukaribisha tu, NW],” aongeza Luka. Bila shaka, fadhili ya Lidia ilithaminiwa. (Matendo 16:14, 15, 40) Lakini kushindwa kuonyesha uthamini kwaweza kudhuru. Pindi moja, dada mwenye umri wa miaka 80 aliye na nguvu na mali za kadiri alifanya kazi ngumu kwa fadhili kutayarisha mlo kwa ajili ya wageni wachache. Alitamaushwa (alikata tamaa) hasa wakati kijana mmoja mwanamume hata hakumjulisha kwamba hangeweza kuja. Pindi nyingine, dada wawili walikosa mlo ambao mwanamke mmoja kijana alitayarisha kwa ajili yao hasa. “Nilivunjika moyo,” alisema, “kwa kuwa hakuna mmoja wao aliyekuwa amesahau. . . . Ningependelea kusikia kwamba walikuwa wamesahau juu ya mlo, lakini badala ya hivyo hakuna yeyote wa dada hao aliyekuwa na fadhili au upendo wa kutosha ili kunipigia simu.” Je! tunda la roho takatifu la fadhili litakusukuma kuthamini na kuwa mwenye kufikiri chini ya hali izo hizo?

Fadhili Yatufanya Tuwe Wenye Ufikirio

7. Ni jambo gani kuhusu fadhili linatolewa kielezo na juhudi iliyofanywa kufuata matakwa ya mazishi ya Yakobo?

7 Fadhili yapasa kutufanya tuwe wenye ufikirio kwa wengine na kwa matakwa yao yanayofaa. Kutoa kielezo: Yakobo (Israeli) aliomba mwana wake Yusufu aonyeshe fadhili-upendo kwake kwa kutomzika Misri. Ingawa hiyo ilihitaji kwamba mwili wa Yakobo ubebwe mwendo mrefu, Yusufu na wana wale wengine wa Yakobo ‘walimchukua mpaka nchi ya Kanaani, nao wakamzika katika pango la shamba la Makpela, lililokuwa mbele ya Mamre, alilolinunua Ibrahimu pamoja na shamba kwa Efroni Mhiti, pawe milki yake pa kuzikia.’ (Mwanzo 47:29; 49:29-31; 50:12, 13) Kupatana na mfano huo, je, fadhili-upendo haipasi kutusukuma kufuata mipango ya mazishi inayokubalika Kimaandiko ambayo mshirika Mkristo wa familia anataka?

8. Kisa cha Rahabu kinatufunza nini juu ya kurudisha fadhili?

8 Wengine wanapotuonyesha fadhili-upendo, je, tusionyeshe uthamini au kurudisha hiyo kwa njia fulani? Kwa uhakika twapaswa kufanya hivyo. Rahabu yule kahaba alionyesha fadhili kwa kuwaficha wapelelezi Waisraeli. Hivyo, Waisraeli walionyesha fadhili-upendo kwa kuhifadhi yeye na familia yake walipoharibu jiji la Yeriko. (Yoshua 2:1-21; 6:20-23) Ni mfano mzuri kama nini kuonyesha kwamba tunapaswa kurudisha fadhili iliyofanywa kwetu kwa kuwa wenye ufikirio na wenye fadhili sisi wenyewe!

9. Kwa nini ungesema kwamba si vibaya kumwomba mtu atuonyeshe fadhili-upendo?

9 Kulingana na jambo hilo, si vibaya kumwomba mtu atuonyeshe fadhili-upendo. Hilo lilifanywa na Yonathani, mwana wa Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli. Yonathani alimwomba kijana Daudi mpendwa na rafiki yake aonyeshe fadhili-upendo kwake na kwa nyumba yake. (1 Samweli 20:14, 15; 2 Samweli 9:3-7) Daudi alikumbuka hilo alipolipia kisasi Wagibeoni waliotendewa vibaya na Sauli. Akikumbuka “kiapo cha Yehova” kati yake na Yonathani, Daudi alionyesha fadhili-upendo kwa kuhifadhi uhai wa Mefiboshethi mwana wa Yonathani. (2 Samweli 21:7, 8) Je! sisi vile vile huacha ‘ndiyo yetu iwe ndiyo’? (Yakobo 5:12) Na ikiwa sisi ni wazee wa kundi, je, sisi ni wenye huruma vivyo hivyo wakati waamini wenzetu wanapohitaji kuonyeshwa fadhili-upendo?

Fadhili Huimarisha Vifungo

10. Fadhili-upendo za Ruthu zilibarikiwaje?

10 Fadhili-upendo huimarisha vifungo vya familia na kuchochea furaha. Hiyo ilionyeshwa katika kisa cha Ruthu Mmoabi. Alifanya kazi ngumu akiwa mbugaji (mwokotaji) katika shamba la mzee Boazi karibu na Bethlehemu, akiandaa chakula kwa ajili yake na Naomi mama-mkwe wake aliyekuwa mjane na mwenye uhitaji. (Ruthu 2:14-18) Boazi alimwambia Ruthu baadaye: “Umezidi kuonyesha fadhili [fadhili-upendo, NW] zako mwisho kuliko mwanzo, kwa vile usivyowafuata vijana, kama ni maskini kama ni matajiri.” (Ruthu 3:10) Kwanza, Ruthu alionyesha fadhili-upendo kwa Naomi. “Mwisho,” Mmoabi huyo alionyesha fadhili-upendo kwa kuwa na nia ya kuolewa na mzee Boazi ili amwinulie uzao mume wake aliyekufa na Naomi aliyezeeka. Kupitia Boazi, Ruthu alikuwa mama wa Obedi babu ya Daudi. Mungu akampa “thawabu kamili” ya kuwa nyanya wa kale wa Yesu Kristo. (Ruthu 2:12; 4:13-17; Mathayo 1:3-6, 16; Luka 3:23, 31-33) Fadhili-upendo za Ruthu zilitokeza mibaraka iliyoje kwake na kwa familia yake! Leo, mibaraka, furaha, na kuimarishwa kwa vifungo vya familia hutokea pia wakati fadhili-upendo inapositawi katika nyumba za wenye kumhofu Mungu.

11. Fadhili ya Filemoni ilikuwa na matokeo gani?

11 Fadhili inaimarisha vifungo ndani ya makundi ya watu wa Yehova. Mwanamume Mkristo Filemoni alijulikana kwa ajili ya kuonyesha fadhili-upendo kwa waamini wenzi. Paulo alimwambia hivi: “Namshukuru Mungu wangu sikuzote, nikikukumbuka katika maombi yangu; nikisikia habari za upendo wako na imani uliyo nayo kwa Bwana Yesu na kwa watakatifu wote . . . nalikuwa na furaha nyingi na faraja kwa sababu ya upendo wako, kwa kuwa mioyo ya [shauku nyororo za, NW] watakatifu [z]imeburudishwa nawe, ndugu yangu.” (Filemoni 4-7) Maandiko hayasemi jinsi shauku nyororo za watakatifu zilivyoburudishwa kupitia Filemoni. Hata hivyo, ni lazima iwe alionyesha fadhili-upendo kwa wapakwa-mafuta wenzi katika njia mbalimbali zilizothibitika kuwa zenye kuburudisha kwao, na hilo bila shaka liliimarisha vifungo kati yao. Mambo ayo hayo hutukia wakati Wakristo wanapoonyesha fadhili-upendo leo.

12. Ni matokeo gani yaliyotokana na fadhili iliyoonyeshwa na Onesiforo?

12 Fadhili ya Onesiforo ilikuwa na matokeo mazuri pia. “Bwana awape rehema wale walio wa mlango wake Onesiforo,” Paulo alisema, “maana mara nyingi aliniburudisha, wala hakuuonea haya mnyororo wangu; bali, alipokuwapo hapa Rumi, alinitafuta kwa bidii akanipata. Bwana na ampe kuona rehema machoni pa Bwana [Yehova, NW] siku ile. Na jinsi alivyonihudumia kwa mengi huko Efeso, wewe unajua sana.” (2 Timotheo 1:16-18) Tukijibidiisha kuonyesha fadhili-upendo kwa waabudu wenzi, tutakuwa wenye furaha na tutakuwa tukiimarisha vifungo vya shauku ya kidugu ndani ya kundi la Kikristo.

13, 14. Kundi katika Filipi lilitoaje mfano mzuri, na Paulo aliitikiaje fadhili hiyo?

13 Wakati kundi zima lionyeshapo fadhili-upendo kuelekea waabudu wenzao, hiyo inaimarisha kifungo kati yao. Kifungo kama hicho kilikuwako kati ya Paulo na kundi katika jiji la Filipi. Kwa hakika, sababu moja ya kuandika kwake barua yake kwa Wafilipi ilikuwa kuonyesha shukrani kwa ajili ya fadhili yao na msaada wao wa kimwili. Aliandika hivi: “Katika mwanzo wa Injili [habari njema, NW], nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa [kundi, NW] lingine lililoshirikiana nami katika habari hii ya kutoa na kupokea, ila ninyi peke yenu. Kwa kuwa hata huko Thesalonike mliniletea msaada kwa mahitaji yangu, wala si mara moja. . . .  Lakini ninavyo vitu vyote na kuzidi, tena nimejaa tele; nimepokea kwa mkono wa Epafrodito vitu vile vilivyotoka kwenu, harufu ya manukato, sadaka yenye kibali, impendezayo Mungu.”—Wafilipi 4:15-18.

14 Haishangazi kwamba Wafilipi wenye fadhili walitiwa katika sala za Paulo! Alisema hivi: “Namshukuru Mungu wangu kila niwakumbukapo, sikuzote kila niwaombeapo ninyi nyote nikisema sala zangu kwa furaha, kwa sababu ya ushirika wenu katika kuieneza Injili [habari njema, NW], tangu siku ile ya kwanza hata leo hivi.” (Wafilipi 1:3-5) Utegemezo kama huo wenye fadhili za moyoni na wenye ukarimu wa kazi ya kuhubiri Ufalme haufanyi kamwe kundi kuwa maskini. Wafilipi walipofanya walivyoweza kufanya katika jambo hilo, Paulo aliwahakikishia hivi: “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:19) Naam, Mungu hulipa fadhili na ukarimu. Neno lake husema hivi: “Kila neno jema alitendalo mtu atapewa lilo hilo na Bwana [Yehova, NW].”—Waefeso 6:8.

Wanawake Wanapoonyesha Fadhili

15, 16. (a) Fadhili ya Dorkasi ilikumbukwaje, na ni nini kilichotokea alipokufa? (b) Wanawake Wakristo wenye mioyo yenye fadhili hujaaaje matendo mema leo?

15 Fadhili-upendo za mwanafunzi Dorkasi (Tabitha) wa Yafa hazikuenda bila kupata thawabu. “Alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa [zawadi za rehema, NW],” na ‘alipougua na kufa,’ wanafunzi walipeleka ujumbe huko Lida ili Petro aitwe. Alipowasili, “wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao.” Ebu wazia tamasha hiyo: Wajane wenye huzuni, wenye machozi walimwambia mtume jinsi Dorkasi alivyokuwa mwenye fadhili wakamwonyesha zile nguo kuwa ushuhuda wa upendo na fadhili zake. Akitoa kila mtu nje, Petro alipiga magoti katika sala na kuuelekea mwili. Sikiliza! Alisema hivi: “Tabitha, ondoka [inuka, NW].” Na tazama! “Akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai.” (Matendo 9:36-41) Ni baraka iliyoje kutoka kwa Mungu!

16 Huo ulikuwa ufufuo wa kwanza ulioandikwa uliofanywa na mtume wa Yesu Kristo. Na hali zilizoongoza kwenye muujiza huo wa ajabu zilitokana na fadhili. Ni nani aweza kusema kwamba Dorkasi angalifufuliwa kwenye uhai kama asingalijaa matendo mema na zawadi za rehema—kama asingalikuwa na wingi wa fadhili-upendo? Dorkasi na wajane wale wengine hawakubarikiwa tu lakini muujiza wa ufufuo wake ulitoa ushuhuda wa utukufu wa Mungu. Naam, “ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana.” (Matendo 9:42) Leo, wanawake Wakristo wenye mioyo yenye fadhili hujaa matendo mema pia—labda wakiwashonea nguo waamini wenzao, wakiwatayarishia chakula wale miongoni mwetu waliozeeka, wakiwaonyesha wengine ukaribishaji-wageni. (1 Timotheo 5:9, 10) Hiyo hutoa ushahidi ulioje kwa watazamaji! Zaidi ya yote, tunafurahia kama nini kwamba ujitoaji kimungu na fadhili-upendo husukuma hilo ‘jeshi kubwa la wanawake kutangaza habari njema’ kwa utukufu wa Mungu wetu, Yehova!—Zaburi 68:11.

Endelea Kufuatia Fadhili-Upendo

17. Ni nini kinachosemwa katika Mithali 21:21, na maneno hayo hutumikaje kwa watu mmoja mmoja wenye kumtii Mungu?

17 Ni lazima wote wanaotamani upendeleo wa Mungu wafuatie fadhili-upendo. “Aandamaye [Afuatiaye, NW] haki na fadhili [fadhili-upendo, NW], ataona uhai na haki na heshima,” yasema mithali yenye hekima. (Mithali 21:21) Mtu mwenye kumtii Mungu hufuatia kwa bidii-nyendelevu uadilifu wa Mungu, akiongozwa sikuzote na viwango vya kimungu. (Mathayo 6:33) Aonyesha daima upendo wenye ushikamanifu, au fadhili-upendo, kwa wengine katika njia za kimwili na hasa za kiroho. Hivyo, anapata uadilifu, kwa maana roho ya Yehova humsaidia kuishi katika njia ya uadilifu. Kwa hakika, ‘anajivika uadilifu’ kama vile Ayubu mwanamume mwenye kumtii Mungu alivyokuwa. (Ayubu 29:14, NW) Mtu kama huyo hatafuti fahari yake mwenyewe. (Mitahli 25:27) Badala ya hiyo, anapata fahari yoyote ambayo Yehova humruhusu kupata, labda kwa namna ya heshima kutoka kwa wanadamu wenzake wanaosukumwa na Mungu kushughulika kwa fadhili naye kwa sababu ya fadhili-upendo zake mwenyewe kuwaelekea. Tena, wale wanaofanya mapenzi ya Mungu kwa ushikamanifu watapata uhai—si kwa miaka michache tu inayopita upesi bali milele.

18. Kwa nini tufuatie fadhili-upendo?

18 Kwa hiyo, acheni wote wampendao Yehova Mungu waendelee kufuatia fadhili-upendo. Sifa hiyo inatupendekeza kwa Mungu na kwa wengine. Inachochea sifa ya ukaribishaji-wageni na inatufanya tuwe wenye ufikirio. Fadhili inaimarisha vifungo ndani ya familia na kundi la Kikristo. Wanawake wanaoonyesha fadhili-upendo huthaminiwa na kuheshimiwa sana. Na wote wanaofuatia sifa hiyo nzuri sana humletea utukufu Mungu wa fadhili-upendo, Yehova.

Ungejibuje?

◻ Abrahamu alikuwaje mfano mzuri katika kuonyesha fadhili?

◻ Kisa cha Rahabu kinatufunza nini juu ya kurudisha fadhili?

◻ Kundi la Filipi lilionyeshaje fadhili?

◻ Wanawake Wakristo wenye mioyo yenye fadhili hujaaaje matendo mema leo?

◻ Kwa nini tunapaswa kufuatia fadhili-upendo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki