Utumaini Mkono wa Yehova Wenye Kuokoa
“Ee, BWANA [Yehova, NW], . . . uwe wewe mkono wetu kila asubuhi, na wokovu wetu pia wakati wa taabu.”—ISAYA 33:2.
1. Yehova ana mkono wenye nguvu katika maana gani?
YEHOVA ana mkono wenye nguvu. Bila shaka, kwa kuwa “Mungu ni roho,” huo si mkono wa mnofu. (Yohana 4:24) Katika Biblia, mkono wa ufananisho unawakilisha uwezo wa kutumia nguvu. Hivyo, Mungu hukomboa watu wake kwa mkono wake. Kwa kweli, ‘analilisha kundi lake kama mchungaji, awakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.’ (Isaya 40:11; Zaburi 23:1-4) Watu wa Yehova huhisi usalama kama nini wakiwa katika mkono wake wenye upendo!—Linganisha Kumbukumbu la Torati 3:24.
2. Ni maswali gani yaliyo hapa tunayostahili kufikiria?
2 Mkono wa Yehova umeokoaje watu wake, zamani na kwa wakati wa sasa? Yehova huwapa msaada gani wakiwa kundi? Na ni kwa nini watu wake waweza kutumaini mkono wake wenye kuokoa wakati wa taabu zao zote?
Mkono wa Mungu Wenye Kuokoa Katika Utendaji
3. Maandiko huhesabia nani ukombozi wa Israeli kutoka Misri?
3 Kabla ya kukomboa Waisraeli kutoka utumwa wa Misri miaka 3,500 iliyopita, Mungu alimwambia nabii wake Musa hivi: “Waambie wana wa Israeli, Mimi ni YEHOVA, nami nitawatoa ninyi mtoke chini ya mizigo ya Wamisri, nami nitawaokoa na utumwa wao, nami nitawakomboa kwa mkono ulionyoshwa, na kwa hukumu kubwa.” (Kutoka 6:6) Kulingana na mtume Paulo, Mungu aliwatoa Waisraeli kutoka Misri “kwa mkono ulioinuliwa.” (Matendo 13:17) Wana wa Kora walimpa Mungu sifa kwa ajili ya ushindi wa Bara Lililoahidiwa, wakisema hivi: “Maana si kwa upanga wao walivyoimiliki nchi, wala si mkono wao uliowaokoa; bali mkono wako wa kuume, naam, mkono wako, na nuru ya uso wako, kwa kuwa uliwaridhia.”—Zaburi 44:3.
4. Kutumaini mkono wa Yehova wenye kuokoa kulithawabishwaje katika siku za shambulio la Kiashuru?
4 Mkono wa Yehova uliwasaidia watu wake pia katika siku za shambulio la Kiashuru. Katika wakati huo nabii Isaya alisali hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], uturehemu; tumekungoja wewe, uwe wewe mkono wetu kila asubuhi, na wokovu wetu pia wakati wa taabu.” (Isaya 33:2) Sala hiyo ilijibiwa wakati malaika wa Mungu alipoua watu 185,000 katika kambi ya Kiashuru, akimfukuza Mfalme Senakeribu “mwenye haya ya uso” kutoka Yerusalemu uliozingirwa. (2 Mambo ya Nyakati 32:21; Isaya 37:33-37) Kutumaini mkono wa Yehova wenye kuokoa kunathawabishwa sikuzote.
5. Mkono wa Mungu wenye nguvu uliwafanyia nini Wakristo mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 1?
5 Mkono wa Mungu wenye nguvu uliokoa Wakristo wapakwa-mafuta walionyanyaswa mwishoni mwa Vita ya Ulimwengu 1. Katika 1918 makao makuu ya Baraza Linaloongoza yalishambuliwa kwa maneno yenye jeuri na adui zayo, na ndugu mashuhuri walifungwa gerezani. Wakihofu mamlaka za kilimwengu, wapakwa-mafuta walikuwa karibu kukomesha kazi yao ya kutoa ushahidi. Lakini walisali ili kazi ipate nguvu tena na ili wasafishwe dhambi ya kutotenda na uchafu wa hofu. Mungu aliitikia kwa kusababisha wale ndugu waliokuwa gerezani waachiliwe, na muda mfupi baadaye, kutangazwa kuwa bila hatia yoyote. Kwa sababu ya kweli zilizoelezwa kwenye mkusanyiko wao katika 1919 na kumiminwa kwa roho ya Mungu yenye kuwasukuma kwenye utendaji, wapakwa-mafuta walifufuliwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova usio wa woga kwa utimizo wa mwisho wa Yoeli 2:28-32.—Ufunuo 11:7-12.
Msaada Katika Kundi
6. Tunajuaje kwamba kuvumilia hali yenye kujaribu katika kundi kunawezekana?
6 Mungu ategemezapo tengenezo lake kwa ujumla, mkono wake huimarisha watu mmoja mmoja ndani yalo. Bila shaka, hali si kamilifu katika kundi lolote kwa sababu wanadamu wote ni wasiokamilika. (Warumi 5:12) Kwa hiyo huenda watumishi wengine wa Yehova wakapatwa nyakati nyingine na hali yenye kujaribu katika kundi. Kwa mfano, ingawa Gayo alifanya ‘kazi ya uaminifu’ katika kuwapokea ndugu waliozuru kwa ukaribishaji-wageni, Diotrefe hakuwapokea na hata akajaribu kuondoa kundini wale wenye ukaribishaji-wageni. (3 Yohana 5, 9, 10) Hata hivyo, Yehova alimsaidia Gayo na wengine waendelee kuonyesha ukaribishaji-wageni katika kutegemeza kazi ya kuhubiri Ufalme. Kumtegemea Yehova kwa sala kwapasa kutusaidia tuendelee kufanya kazi za uaminifu tunapomngoja asahihishe hali fulani ambayo huenda ikajaribu imani yetu.
7. Wakristo washikamanifu waliishi kulingana na wakfu wao kwa Mungu zijapokuwa hali zipi katika kundi la Korintho?
7 Tuseme ulikuwa ukishirikiana na kundi la Korintho la karne ya kwanza. Wakati mmoja, mafarakano yalitisha umoja walo, na kuachilia ukosefu wa maadili kulitisha roho yalo. (1 Wakorintho 1:10, 11; 5:1-5) Waamini walipelekana mahakamani ya kilimwengu, na wengine walizozana juu ya mambo mbalimbali. (1 Wakorintho 6:1-8; 8:1-13) Ugomvi, wivu, hasira, na mchafuko yalifanya maisha yawe magumu. Wengine hata walishuku mamlaka ya Paulo na kudharau uwezo wake wa kusema. (2 Wakorintho 10:10) Hata hivyo, washikamanifu walioshirikiana na kundi hilo walikuwa wanaishi kulingana na wakfu wao kwa Mungu katika wakati huo wenye kujaribu.
8, 9. Hali yenye kujaribu ikitukabili katika kundi twapaswa kufanya nini?
8 Hali yenye kujaribu ikitokea, tunahitaji kushikamana na watu wa Mungu. (Linganisha Yohana 6:66-69.) Acheni tuwe wenye saburi kwa mmoja na mwenzake, tukitambua kwamba watu fulani mmoja mmoja huchukua muda mrefu kuliko wengine kuvaa “utu mpya” na kujivika huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Kwa kuwa watumishi wa Mungu hutofautiana katika malezi pia, sisi sote twahitaji kuonyesha upendo na kuwa wenye kusamehe.—Wakolosai 3:10-14.
9 Baada ya miaka mingi ya utumishi kwa Yehova, ndugu mmoja alisema hivi: “Jambo moja ambalo limekuwa la maana zaidi kwangu, ni kule kuendelea kuwa karibu na tengenezo la Yehova lionekanalo. Maono yangu ya mapema yalinifunza jinsi kutegemea kufikiri kwa kibinadamu kunavyoharibu afya ya kiroho. Mara nilipotatua jambo hilo, nilipiga moyo konde nibaki karibu na tengenezo jaminifu. Mtu aweza kupata kibali na baraka ya Yehova kwa njia gani nyingine?” Je, wewe huthamini sana pendeleo lako la kumtumikia Yehova pamoja na watu wake wenye shangwe? (Zaburi 100:2) Ikiwa ndivyo, hutaruhusu jambo lolote likuvute mbali na tengenezo la Mungu au kuharibu uhusiano wako pamoja na Yule ambaye mikono yake huokoa wote wampendao.
Msaada Tunapokumbwa na Vishawishi
10. (a) Sala inasaidiaje watu wa Mungu kukabili kishawishi? (b) Paulo alitoa uhakikisho upi kwenye 1 Wakorintho 10:13?
10 Tukiwa watu mmoja mmoja waaminifu wanaoshiriki pamoja na tengenezo la Mungu, tuna msaada wake wakati wa jaribu. Kwa mfano, yeye hutusaidia tudumishe ukamilifu wetu kwake tunapokumbwa na kishawishi. Bila shaka, twapaswa kusali kupatana na maneno ya Yesu: “Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu,” Shetani Ibilisi. (Mathayo 6:9-13) Kwa uhalisi tunamwomba Mungu asituruhusu tushindwe tunaposhawishwa ili tusimtii. Pia yeye hujibu tusalipo tupate hekima ili tushinde majaribu. (Yakobo 1:5-8) Na watumishi wa Yehova waweza kuwa na hakika kwamba atawasaidia, kwa kuwa Paulo alisema hivi: “Jaribu [kishawishi, NW] halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu [kishawishi, NW] atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” (1 Wakorintho 10:13) Chanzo cha kishawishi hicho ni nini, na Mungu hufanyaje mlango wa kutokea?
11, 12. Waisraeli walishindwa na vishawishi vipi, nasi twaweza kufaidikaje na mambo waliyoona?
11 Kishawishi huja kutokana na hali ziwezazo kutufanya tukose kuwa waaminifu kwa Mungu. Paulo alisema hivi: “Mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya kama wale [Waisraeli] nao walivyotamani. Wala msiwe waabudu sa-namu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze. Wala tusifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu. Wala tusimjaribu Bwana [Yehova, NW], kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka. Wala msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.”—1 Wakorintho 10:6-10.
12 Waisraeli walitamani mabaya walipojiachilia washindwe na kishawishi cha kuwa wenye pupa kwa kukusanya na kula kware walioandaliwa na Mungu kimuujiza. (Hesabu 11:19, 20, 31-35) Mapema kidogo, walikuwa wameabudu sanamu wakati kutokuwapo kwa Musa kulipotokeza kishawishi cha kujiingiza katika ibada ya ndama. (Kutoka 32:1-6) Maelfu waliangamia kwa sababu walishindwa na kishawishi wakafanya uasherati na wanawake Wamoabi. (Hesabu 25:1-9) Waisraeli waliposhindwa na kishawishi na kunung’unika juu ya kuharibiwa kwa waasi, Kora, Dathani na Abiramu, na washirika wao, 14,700 waliangamia kwa tauni iliyopelekwa kwa njia ya kimungu. (Hesabu 16:41-49) Twaweza kunufaika kutokana na mambo hayo yaliyoonwa tuking’amua kwamba hakuna kimojawapo vishawishi hivyo kilichokuwa kikubwa mno hivi kwamba Waisraeli wasingaliweza kukishinda. Wangaliweza kufanya hivyo ikiwa wangalizoea imani, ikiwa wangalikuwa wenye shukrani kwa utunzaji wa Mungu wenye upendo, na ikiwa wangalithamini haki ya sheria yake. Kisha mkono wa Yehova ungaliwaokoa, kama vile unavyoweza kutuokoa.
13, 14. Yehova hufanyaje mlango wa kutokea watumishi wake wanapokabili kishawishi?
13 Tukiwa Wakristo, tunakabili vishawishi vilivyo kawaida kwa ainabinadamu. Hata hivyo, twaweza kuendelea kuwa waaminifu kwa Mungu kwa kumwomba msaada wake na kujitahidi kushinda kishawishi. Mungu ni mwaminifu, naye hatatuacha tushawishwe kupita tuwezavyo. Tukiwa washikamanifu kwa Yehova, hatutapata kamwe kwamba haiwezekani kufanya penzi lake. Yeye hufanya mlango wa kutokea kwa kutuimarisha ili tushinde kishawishi. Kwa mfano, tunaponyanyaswa, huenda tukashawishwa kuridhiana tukitumaini kuepuka mateso au kifo. Lakini tukitumaini mkono wa Yehova wenye nguvu, kishawishi hakifikii kamwe hatua ambapo yeye hawezi kuimarisha imani yetu na kutupa nguvu ya kutosha kudumisha ukamilifu. Kama alivyosema mtume Paulo: “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi.”—2 Wakorintho 4:8, 9.
14 Yehova hutegemeza watu wake pia kwa kutumia roho yake kuwa mkumbushaji na mwalimu. Inatusaidia tukumbuke mambo ya Kimaandiko na hutusaidia tutambue jinsi ya kuyatumia ili tukishinde kishawishi. (Yohana 14:26) Watumishi wa Yehova waaminifu huelewa masuala yanayohusika katika kishawishi na hawadanganywi kufuata mwendo wenye kosa. Mungu amefanya mlango wa kutokea kwa kuwawezesha wavumilie hata hadi kifo bila kushindwa na kishawishi. (Ufunuo 2:10) Zaidi ya kusaidia watumishi wake kupitia roho yake, Yehova hutumia malaika zake kwa ajili ya tengenezo lake.—Waebrania 1:14.
Msaada Katika Mambo ya Kibinafsi
15. Ni msaada upi wa kibinafsi tunaoweza kupata katika Wimbo Ulio Bora?
15 Wale wanaoshirikiana pamoja na tengenezo la Yehova wanapata msaada wake katika mambo ya kibinafsi. Kwa mfano, wengine huenda wakawa wanatafuta mwenzi wa ndoa Mkristo. (1 Wakorintho 7:39) Ikiwa kuna utamausho (kukata tamaa), huenda ikasaidia kufikiria mfalme wa Israeli Sulemani. Yeye alishindwa kupata kibali cha mwanamke Mshulami amwoe kwa sababu Mshulami alimpenda mchungaji mnyenyekevu. Maandishi ya mfalme kuhusu jambo hilo yaweza kuitwa Wimbo wa Upendo wa Sulemani Uliotamaushwa. Huenda tukalia machozi kama jitihada zetu za kimahaba hazipati matokeo katika hali fulani, lakini Sulemani alipona utamausho wake, nasi pia twaweza kupona. Roho ya Mungu yaweza kutusaidia tuonyeshe kujidhibiti na sifa nyingine za kimungu. Neno lake latusaidia tukubali lile jambo la hakika linaloumiza kwamba mtu hawezi kuwa na upendo wa kimahaba na mtu yeyote tu. (Wimbo Ulio Bora 2:7; 3:5) Hata hivyo, Wimbo Ulio Bora unaonyesha kwamba huenda ikawezekana kupata mwamini mwenzetu anayetupenda sana. Jambo la maana zaidi ni kwamba, huo “wimbo ulio bora” unatimizwa katika upendo wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, kwa “bibi-arusi” wake wale wafuasi wapakwa-mafuta 144,000.—Wimbo Ulio Bora 1:1; Ufunuo 14:1-4; 21:2, 9; Yohana 10:14.
16. “Dhiki katika mwili” inayopatwa na wenzi wa ndoa huenda ikatia ndani nini?
16 Hata wale wanaofunga ndoa na mwamini wana “dhiki katika mwili.” (1 Wakorintho 7:28) Kutakuwako wasiwasi na mambo ya kuhangaikia yanayohusisha mume na mke na watoto wao. (1 Wakorintho 7:32-35) Ugonjwa huenda ukaleta mizigo mizito na mkazo. Mnyanyaso au taabu ya kiuchumi huenda ukafanya iwe vigumu kwa baba Mkristo kuandalia familia yake mahitaji ya maisha. Wazazi na watoto huenda wakatenganishwa na kifungo cha gerezani, na wengine huenda wakateswa na hata kuuawa. Lakini katika hali zote kama hizo, tunaweza kushinda kishawishi cha kukana imani tukiutumaini kweli kweli mkono wa Yehova wenye kuokoa.—Zaburi 145:14.
17. Mungu aliwezesha Isaka na Rebeka wavumilie tatizo lipi la familia?
17 Huenda tukahitaji kuvumilia majaribu mengine kwa muda mrefu. Kwa mfano, huenda mwana akawasababishia wazazi wake wenye kumhofu Mungu taabu kwa kumwoa mtu asiyeamini. Jambo hilo lilitukia katika familia ya mzee wa ukoo Isaka na mkewe Rebeka. Mwana wao Esau mwenye umri wa miaka 40 aliwaoa wake wawili Wahiti waliofanya ‘roho zao Isaka na Rebeka zikajae uchungu.’ Kwa kweli, “Rebeka akamwambia Isaka, Rohoni mwangu sina raha kwa sababu ya hao binti za Hethi. Kama Yakobo [mwana wao mwingine] akitwaa mke katika binti za Hethi kama hawa binti za nchi, maisha yangu yatanifaidia nini?” (Mwanzo 26:34, 35; 27:46) Yaonekana kwamba, nafsi ya Rebeka yenye uadilifu iliteswa na tatizo hilo lenye kuendelea. (Linganisha 2 Petro 2:7, 8.) Hata hivyo, mkono wa Yehova uliwaimarisha Isaka na Rebeka, ukiwawezesha kuvumilia jaribu hilo walipokuwa wakidumisha uhusiano wenye nguvu pamoja Naye.
18. C. T. Russell alivumilia jaribu lipi kwa msaada wa Mungu?
18 Inataabisha wakati mshiriki wa familia aliyebatizwa anapopunguza utumishi wake kwa Mungu. (Linganisha 2 Timotheo 2:15.) Hata hivyo, wengine hata wamevumilia kupotea kiroho kwa mwenzi wa ndoa, kama vile Charles T. Russell, msimamizi wa kwanza wa Watch Tower Society. Mke wake alivunja uhusiano wake pamoja na Sosaiti na kumwacha katika 1897, baada ya karibu miaka 18 ya ndoa. Alichukua hatua ya kuachana na mume wake kisheria katika 1903, nayo ikatolewa katika 1908. Huzuni ya mume wake ilikuwa wazi alipomwambia mke wake hivi katika barua iliyoandikwa baada tu ya kuachana kwao: “Nimesali kwa Bwana kwa bidii kwa ajili yako. . . . Sitakulemeza na masimulizi ya huzuni yangu, wala sitajaribu kupata huruma yako kwa kueleza sana hisiamoyo zangu, kwa kuwa mara kwa mara mimi hupata nguo zako na vitu vingine vinavyonikumbusha waziwazi jinsi ulivyokuwa zamani—mwenye kujaa upendo na huruma na mwenye kusaidia sana—mwenye kuangaza roho ya Kristo. . . . Aa, fikiria kwa sala yale nitakayosema. Na ujue kwa hakika kwamba kile kinachoniumiza zaidi, chenye kuniathiri kihisiamoyo, si upweke wangu mwenyewe katika maisha yangu yanayobaki, bali ni kule kukosea kwako, mpenzi wangu, hasara yako ya milele, kadiri ninavyoweza kuona.” Ujapokuwa uchungu huo wa moyoni, Russell alikuwa na utegemezo wa Mungu hadi mwisho wa uhai wake wa kidunia. (Zaburi 116:12-15) Sikuzote Yehova huimarisha watumishi wake washikamanifu.
Kutoka Kwa Taabu Zote
19. Matatizo yenye kutaabisha yakidumu twapaswa kukumbuka nini?
19 Watu wa Yehova humjua kuwa “Mungu wa kuokoa,” Yeye ambaye “hutuchukulia mzigo wetu.” (Zaburi 68:19, 20) Kwa hiyo, tukiwa watu mmoja mmoja tuliojiweka wakfu wenye kushirikiana na tengenezo lake la kidunia, acheni tusikubali kamwe kukatishwa tamaa ikiwa matatizo yenye kutaabisha yanadumu. Kumbuka kwamba “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.” (Zaburi 46:1) Kumtumaini kwetu kunathawabishwa sikuzote. “Nalimtafuta BWANA [Yehova, NW] akanijibu,” akasema Daudi, “akaniponya na hofu zangu zote. . . . Maskini huyu aliita, BWANA [Yehova, NW] akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.”—Zaburi 34:4-6.
20. Ni swali lipi linalobaki kuzungumzwa?
20 Naam, Baba yetu wa kimbingu huokoa watu wake kutoka kwa taabu zote. Yeye hutegemeza tengenezo lake la kidunia, akiandaa msaada katika mambo ya kundi na mambo ya kibinafsi. Kwa kweli, “BWANA [Yehova, NW] hatawatupa watu wake.” (Zaburi 94:14) Lakini acheni sasa tuzungumzie njia nyingine ambazo katika hizo Yehova husaidia watu wake mmoja mmoja. Baba yetu wa kimbingu hutegemezaje watumishi wake walio wagonjwa, wenye mshuko wa akilini, wenye kulemewa na huzuni kwa sababu ya kufiwa, au wenye kutaabishwa na makosa yao? Kama tutakavyoona, katika mambo hayo pia, tuna sababu ya kutegemea mkono wa Yehova wenye nguvu.
Ungeitikiaje?
◻ Mkono wa Yehova umeletaje wokovu katika nyakati za zamani?
◻ Yehova husaidiaje watu wake katika kundi leo?
◻ Mungu huandaa msaada upi katika mambo ya kibinafsi?
◻ Matatizo yenye kutaabisha yakidumu twapaswa kufanya nini?
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Mungu aliwatoa Waisraeli kutoka Misri “kwa mkono ulioinuliwa.”