Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 10/15 kur. 29-30
  • “Utakuwa Pamoja na Mimi Katika Paradiso”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Utakuwa Pamoja na Mimi Katika Paradiso”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Habari Zinazolingana
  • Paradiso
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • “Tutaonana Paradiso!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • “Utakuwa Pamoja Nami Katika Paradiso”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Tunajifunza Nini Kutoka kwa Mhalifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 10/15 kur. 29-30

“Utakuwa Pamoja na Mimi Katika Paradiso”

ALIPOKUWA akining’inia juu ya mti wa kuulia, akifa kwa maumivu sana, mhalifu alimwomba yule mtu aliyekuwa karibu naye hivi: “Yesu, unikumbuke mimi utakapoingia katika ufalme wako.” Hata ingawa Yesu alikuwa pia akifa kwa uchungu mkali sana, alijibu hivi: “Kweli kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:42, 43, NW) Ni tumaini lenye faraja kama nini kumpa mtu anayekufa!

Lakini, je, uliona kwamba, New World Translation—tafsiri iliyonukuliwa katika fungu linalotangulia—huweka alama ya kituo baada ya neno “leo” inapofasiri maneno hayo ya Yesu? Hilo huonyesha wazo kwamba hata siku ile ya kifo chake mwenyewe, Yesu aliweza kuahidi uhai katika Paradiso kwa yule mhalifu. Kwa upande mwingine, The New English Bible inaweka alama ya kituo katika maneno ya Yesu kwa njia hii: “Nakuambia hili: leo utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” Tafsiri nyinginezo nyingi hukubaliana na The New English Bible, zikionyesha wazo kwamba Yesu na yule mhalifu aliyekuwa anakufa walikuwa wanaenda Paradiso siku hiyo hiyo. Kwa nini kuna tofauti hiyo? Na ni njia gani ya kuweka alama ya kituo iliyo sahihi?

Kwa kweli, hakuna alama zozote za kituo katika hati za Kigiriki za Biblia za mapema zaidi. Kwa hiyo, alama za kituo zilipoingizwa, wanakili na watafsiri wa Biblia walihitaji kuziingiza kulingana na jinsi walivyoelewa kweli ya Biblia. Kwa hiyo, ile fasiri ya kimapokeo ni sahihi? Je, Yesu na yule mtenda maovu walienda Paradiso siku waliyokufa?

La, kulingana na Bibila, walienda mahali paitwapo Haʹdes katika Kigiriki na Sheʹol katika Kiebrania, mahali pote pawili pakirejezea kaburi la ujumla la ainabinadamu. (Luka 18:31-33; 24:46; Matendo 2:31) Kuhusu wale walio mle, Biblia husema hivi: “Wafu hawajui neno lo lote . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [Sheʹoli, NW, Haʹdes, Kigiriki] uendako wewe.” Si paradiso hata kidogo!—Mhubiri 9:5, 10.

Yesu hakufufuliwa kutoka Hadesi mpaka siku ya tatu. Kisha, katika muda wa karibu majuma sita akajitokeza mara kadhaa kwa wafuasi wake kotekote katika nchi ya Palestina. Pindi moja kati ya hizo, Yesu alimwambia Mariamu hivi: “Sijapaa kwenda kwa baba.” (Yohana 20:17) Kwa hiyo, hata wakati huo hakuwa bado amefika mahali popote ambapo pangeweza kuitwa paradiso.—Ufunuo 2:7.

Katika karne ya tatu W.K.—wakati mafundisho ya Kikristo na falsafa za Kigiriki zilipokuwa zikiunganishwa pamoja kwa mwendo wa kasi—Origeni alinukuu maneno ya Yesu kuwa akisema hivi: “Leo utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso ya Mungu.” Katika karne ya nne W.K., waandishi wa kanisa walibishana dhidi ya kuweka alama ya kituo baada ya “leo.” Hilo linaonyesha kwamba njia ya kimapokeo ya kusoma maneno ya Yesu ina historia ndefu. Lakini linaonyesha pia kwamba hata katika karne ya nne W.K., maneno ya Yesu yalisomwa na wengine kulingana na njia ambayo yanafasiriwa katika New World Translation.

Leo pia, ingawa watafsiri wengi huiwekea Luka 23:43 alama ya kituo kulingana na mapokeo ya kanisa, wengine huiwekea alama ya kituo kama New World Translation inavyoiweka. Kwa mfano, katika tafsiri ya Kijerumani ya Profesa Wilhelm Michaelis, maneno ya Yesu husomwa hivi: “Kweli kweli, ninakupa uhakikishio huu hata leo: Utakuwa pamoja na mimi (siku fulani) katika Paradiso.”

Basi, maneno ya Yesu kwa mtenda maovu huyo yalimaanisha nini? Huenda ikawa alikuwa amesikia juu ya madai kwamba Yesu alikuwa Mfalme aliyeahidiwa. Bila shaka, alijua kuhusu yale maneno “mfalme wa Wayahudi” ambayo Pilato alikuwa ameandika na kuangika juu ya kichwa cha Yesu. (Luka 23:35-38) Ingawa viongozi wa kidini walimkataa Yesu kwa uthabiti, mhalifu huyo mwenye kutubu alionyesha imani yake, kwa kusema hivi: “Yesu, unikumbuke mimi utakapoingia katika ufalme wako.” Yeye hakutazamia kutawala pamoja na Yesu, lakini alitaka kunufaika na utawala wa Yesu. Kwa hiyo, hata katika siku hiyo ngumu sana, Yesu aliahidi kwamba mtenda mabaya huyo angekuwa pamoja naye katika Paradiso.

Katika paradiso ipi? Katika Biblia, Paradiso ya kwanza ilikuwa lile bustani la Edeni iliyokuwa kama shamba la starehe ambalo wazazi wetu wa kwanza walipoteza. Biblia huahidi kwamba Paradiso hiyo ya kidunia itarudishwa chini ya Ufalme wa Mungu, ulio na Yesu akiwa Mfalme. (Zaburi 37:9-11; Mika 4:3, 4) Kwa hiyo, Yesu atakuwa pamoja na mtenda mabaya huyo na wafu wengine walio wengi wakati anapowafufua kutoka kaburi kwenye uhai katika dunia-paradiso na kwenye nafasi ya kujifunza kufanya mapenzi ya Mungu na kuishi milele.—Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-13; 21:3, 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki