Kukimbia Shindano La Mbio Kwa Uvumilivu
“Acheni sisi tukimbie kwa uvumilivu katika shindano la mbio ambalo limewekwa mbele yetu sisi.”—WAEBRANIA 12:1, NW.
1. (a) Tunapojiweka wakfu kwa Yehova Mungu ni nini kinachowekwa mbele yetu? (b) Ni lazima Mkristo ajitayarishe kwa ajili ya shindano la mbio la aina gani?
TULIPOJIWEKA wakfu kwa Yehova kupitia Yesu Kristo, Mungu aliweka shindano la mbio mbele yetu, kwa njia ya ufananisho. Mwishoni mwa shindano hilo la mbio, wote wanaomaliza kwa mafanikio watapewa zawadi. Zawadi gani? Uhai wa milele! Ili kushinda zawadi hiyo nzuri ajabu, mpiga mbio Mkristo anahitaji kuwa tayari, si kukimbia mbio za mwendo mfupi za upesi tu, bali kukimbia mbio za mwendo mrefu. Kwa hiyo atahitaji uvumilivu. Atalazimika kuvumilia muda mrefu wa kazi ngumu ya shindano la mbio lenyewe na pia vizuizi vinavyojitokeza katika muda wa shindano hilo la mbio.
2, 3. (a) Ni nini kitakachotusaidia katika kukimbia shindano la mbio la Kikristo hata mwisho? (b) Shangwe ilimsaidiaje Yesu alikimbie shindano la mbio kwa uvumilivu?
2 Ni nini kitakachotusaidia tukimbie shi-ndano la mbio kama hilo hadi mwisho? Ni nini kilichomsaidia Yesu avumilie alipokuwa mwanadamu duniani? Alitwaa nguvu ya ndani kutoka kwa sifa ya shangwe. Waebrania 12:1-3 husomwa hivi: “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba [mti wa mateso, NW] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”
3 Muda wote wa huduma yake ya peupe, Yesu aliweza kuendelea kukimbia shindano hilo la mbio kwa sababu ya shangwe ya Yehova. (Linganisha Nehemia 8:10.) Shangwe yake ilimsaidia hata avumilie kifo cha aibu kwenye mti wa mateso, baada ya hicho akaona shangwe isiyoelezeka ya kufufuka kutoka wafu na kupaa kwenye mkono wa kuume wa Baba yake, huko kuitimiliza kabisa kazi ya Mungu. Kwa uvumilivu wake akiwa mwanadamu aliye kwenye upande wa Mungu, alishikilia haki yake ya uhai wa milele. Naam, kama Luka 21:19 inavyosema: “Kwa subira yenu mtaziponya nafsi zenu.”
4. Yesu aliwawekea wapiga mbio wenzake mfano wa aina gani, na tunapaswa kuzingatia nini akilini?
4 Yesu Kristo aliwawekea wapiga mbio wenzake mfano bora kabisa, na mfano wake unatuhakikishia kwamba sisi pia twaweza kuwa washindi. (1 Petro 2:21) Lile ambalo Yesu atutaka tufanye, twaweza kulifanya. Kama alivyovumilia, sisi pia twaweza kuvumilia. Na tuendeleapo kumwiga kwa uthabiti, ni lazima tuzingatie akilini sababu zetu za kuwa wenye shangwe. (Yohana 15:11, 20, 21) Shangwe itatuimarisha kudumu katika kukimbia shindano la mbio katika utumishi wa Yehova hata zawadi tukufu ya uhai wa milele inapopatikana.—Wakolosai 1:10, 11.
5. Ni Jinsi gani tuwezavyo kuwa wenye shangwe na kuimarishwa kwa ajili ya shindano la mbio lililo mbele yetu?
5 Kutusaidia tudumu katika shindano hilo la mbio, Yehova huandaa uwezo unaopita ulio wa kawaida. Tunaponyanyaswa, uwezo huo na maarifa ya kujua ni kwa nini tumependelewa kupatwa na mnyanyaso hutuimarisha. (2 Wakorintho 4:7-9) Chochote kinachotupata kwa ajili ya kuliheshimu jina la Mungu na kuitetea enzi kuu yake ni sababu ya shangwe ambayo hakuna yeyote awezaye kutunyang’anya. (Yohana 16:22) Hiyo inaeleza ni kwa nini mitume, baada ya kupigwa kwa amri ya Sanhedrini ya Kiyahudi kwa sababu ya kutoa ushahidi kuhusu mambo mazuri ajabu ambayo Yehova Mungu alikuwa ametimiza kuhusiana na Yesu, walishangilia “kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo.” (Matendo 5:41, 42) Shangwe yao haikutokana na mnyanyaso wenyewe bali ilitokana na ile hali ya ndani ya kuridhika sana kwa kujua kwamba walikuwa wakimpendeza Yehova na Yesu.
6, 7. Mpiga mbio Mkristo aweza kufurahije hata ingawa ana dhiki, na tokeo likiwa nini?
6 Uwezo mwingine wenye kutegemeza katika maisha yetu ni lile tumaini ambalo Mungu ameweka mbele yetu. Kama Paulo alivyoeleza: “Basi tukiisha kuhesabiwa haki itokayo katika imani, na tuwe na amani kwa Mungu, kwa njia ya Bwana wetu Yesu Kristo. Ambaye kwa yeye tumepata kwa njia ya imani kuifikia neema hii ambayo tunasimama ndani yake; na kufurahi katika tumaini la utukufu wa Mungu. Wala si hivyo tu, ila na tufurahi katika dhiki pia; tukijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi [uvumilivu, NW]; na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo [hali inayokubalika, NW]; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; na tumaini halitahayarishi.”—Warumi 5:1-5.
7 Dhiki zenyewe hazifurahishi, hata hivyo matunda yenye amani yatokezwayo nazo baadaye hufurahisha. Matunda hayo ni uvumilivu, hali inayokubalika, tumaini, na utimilizo wa tumaini hilo. Kuvumilia kwetu kutaongoza kwenye kupokea kwetu kibali cha kimungu. Tunapokuwa na kibali cha Mungu, twaweza kutumainia kwa uhakika utimizo wa ahadi ambazo ametoa. Tumaini hilo hutudumisha katika mwendo unaofaa na hututia moyo chini ya dhiki hata tumaini litakapotimilizwa.—2 Wakorintho 4:16-18.
Wenye Furaha Ni Wale Wanaovumilia!
8. Kwa nini kipindi hiki cha kungoja si wakati wa bure kwetu?
8 Tungojapo ule wakati uliowekwa wa kugawa zawadi kwa wapiga mbio, tunapatwa na mabadiliko fulani. Hayo ni maendeleo ya kiroho ndani yetu ambayo ni tokeo la kukabiliana na majaribu kwa mafanikio, nayo hutupatia upendeleo mkubwa kwa Mungu. Yanathibitisha sisi tu watu wa aina gani na yanatupa nafasi ya kuzoea sifa nzuri kama zile ambazo watu waaminifu wa wakati wa zamani, hasa Mfano wetu Yesu Kristo, walionyesha. Mwanafunzi Yakobo asema hivi: “Ndugu zangu, mwe na furaha mnapopatwa na majaribu mbalimbali, kwani mwajua kwamba imani yenu ikisha stahimili, itawapatieni uvumilivu. Mwe na hakika kwamba uvumilivu wenu utawategemeza mpaka mwisho, mpate kuwa wakamilifu na watimilifu, bila kupungukiwa chochote.” (Yakobo 1:2-4, HNWW) Naam, twaweza kutazamia kupatwa na majaribu mbalimbali, lakini hayo yatatumika kutudumisha katika kusitawisha sifa zinazofaa. Hivyo tunaonyesha kwamba tutaendelea katika shindano la mbio hili hadi tujipatie zawadi, haidhuru ni vizuizi vipi tutakavyokabili.
9, 10. (a) Kwa nini wale wenye kuvumilia majaribu ni wenye furaha, na twapaswa kukabilianaje na majaribu? (b) Wale wenye furaha wa zamani walikuwa nani, na sisi twaweza kuhesabiwaje miongoni mwao?
9 Haishangazi basi, kwamba Yakobo alisema hivi: “Heri mtu astahimiliye majaribu; kwa sababu akiisha kukubaliwa ataipokea taji ya uzima, Bwana [Yehova, NW] aliyowaahidia wampendao”! (Yakobo 1:12) Acheni tukabiliane na majaribu bila ugeugeu, tukiwa na sifa za kimungu kama silaha zitakazotuimarisha kuyashinda majaribu hayo.—2 Petro 1:5-8.
10 Kumbuka kwamba njia ambayo Mungu anashughulika nasi si mpya au ya kigeni. Lile ‘wingu la mashahidi’ waaminifu wa nyakati za zamani walishughulikiwa kwa njia hiyo hiyo walipothibitisha uthabiti wao kwa Mungu. (Waebrania 12:1) Kibali cha Mungu kwao kimerekodiwa katika Neno lake, nasi tunawahesabu wao wote kuwa wenye furaha kwa sababu walivumilia chini ya jaribu. Yakobo asema hivi: “Ndugu, mkitaka kuona mfano wa subira na uvumilivu katika mateso fikirini juu ya manabii ambao walinena kwa jina la Bwana [Yehova, NW]. Tunawaita hao wenye heri kwa sababu walivumilia. Mmesikia habari za uvumilivu wa Yobu, na mnajua jinsi Bwana [Yehova, NW] alivyomtendea mwishoni. Maana Bwana [Yehova, NW] amejaa huruma na rehema.” (Yakobo 5:10, 11, HNWW) Ilitabiriwa kwamba muda wa siku za mwisho hizi, watu fulani wangetokea duniani ambao wangemtumikia Yehova kwa uaminifu wa kimaadili, kama vile manabii walivyofanya katika karne za kale. Je! sisi hatufurahi kuwa wale wanaofanya hivyo?—Danieli 12:3; Ufunuo 7:9.
Kupata Utegemezo Katika Neno la Yehova Lenye Kutia Moyo
11. Neno la Mungu laweza kutusaidiaje tuvumilie, na kwa nini tusiwe kama mahali penye miamba pa mfano wa Yesu?
11 Paulo alielekezea kwenye msaada mwingine katika kuvumilia aliposema kwamba “kupitia uvumilivu wenye saburi, na kupitia kitia moyo kinachopatikana katika Maandiko, twaweza kushikamana na tumaini letu.” (Warumi 15:4, The Twentieth Century New Testament) Kweli, Neno la Mungu, ni lazima iimarike sana ndani yetu ili sikuzote itokeze katika sisi itikio linalofaa. Hatunufaiki hata kidogo kwa kuwa kama ardhi yenye miamba iliyoelezwa katika mfano wa Yesu wa mpanzi: “Kadhalika na hawa ndio wapandwao penye miamba, ambao kwamba wakiisha kulisikia lile neno, mara hulipokea kwa furaha; ila hawana mizizi ndani yao, bali hudumu muda mchache; kisha ikitokea dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara hujikwaa.” (Marko 4:16, 17) Kweli katika Neno la Mungu haiimariki sana katika watu kama hao; kwa hiyo, katika nyakati za dhiki, haiwezi kuwategemeza ikiwa chanzo cha kweli cha nguvu na tumaini.
12. Tunapokubali habari njema hatupaswi kudanganyika kuhusu nini?
12 Yeyote anayekubali habari njema ya Ufalme hapaswi kujidanganya mwenyewe kuhusu kile kitakachofuata. Yeye anachagua mwendo wa maisha utakaompasisha dhiki au mnyanyaso. (2 Timotheo 3:12) Lakini apaswa aihesabu kuwa “ni furaha tupu” kuwa na pendeleo la kupatwa na majaribu mbalimbali kwa ajili ya kushikilia imara Neno la Mungu na kuambia wengine juu yalo.—Yakobo 1:2, 3.
13. Paulo alishangilia juu ya Wakristo katika Thesalonike, kwa njia gani na kwa nini?
13 Katika karne ya kwanza, wapinzani katika Thesalonike walifanya ghasia kwa sababu ya kuhubiri kwa Paulo. Paulo alipoenda Beroya, wanyanyasi hao walimfuata huko ili wasababishe matatizo zaidi. Kwa wale waaminifu waliobaki katika Thesalonike, mtume huyo aliyenyanyaswa alisema hivi: “Ndugu, imetupasa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, kama ilivyo wajibu, kwa kuwa imani yenu inazidi sana, na upendo wa kila mtu kwenu kwa mwenzake umekuwa mwingi. Hata na sisi wenyewe twaona fahari juu yenu katika makanisa ya Mungu kwa ajili ya saburi [uvumilivu, NW] yenu, na imani mliyo nayo katika adha zenu zote na dhiki mnazostahimili. Ndiyo ishara hasa ya hukumu iliyo haki ya Mungu, ili mhesabiwe kuwa mwastahili kuuingia ufalme wa Mungu, ambao kwa ajili yake mnateswa.” (2 Wathesalonike 1:3-5) Yajapokuwa mateso yao mikononi mwa adui zao, Wakristo Wathesalonike walizidi katika kufanana na Kristo na katika idadi. Hilo liliwezekanaje? Kwa sababu walitwaa nguvu katika Neno la Yehova lenye kutia moyo. Walitii maagizo ya Bwana na kukimbia shindano la mbio kwa uvumilivu.—2 Wathesalonike 2:13-17.
Kwa Ajili ya Wokovu wa Wengine
14. (a) Ni zipi baadhi ya sababu zinazotufanya tuendelee kwa shangwe katika huduma zijapokuwa taabu? (b) Tunaomba nini, na kwa nini?
14 Tunavumilia taabu na minyanyaso kwa uaminifu na bila kulalamika, hasa kwa ajili ya utetezi wa Mungu. Lakini kuna sababu nyingine isiyo ya ubinafsi kwa nini tunastahimili mambo kama hayo: ili tuweze kuwapitishia wengine habari za Ufalme ili wahubiri zaidi kwa ajili ya Ufalme wa Mungu waweze kutokezwa kufanya “tangazo la peupe la wokovu.” (Warumi 10:10, NW) Wale wafanyao kazi katika utumishi wa Mungu wapaswa wamwombe Bwana wa mavuno abariki kazi yao kwa kuandaa wahubiri zaidi wa Ufalme. (Mathayo 9:38) Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine. Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu.”—2 Timotheo 2:2, 3.
15. Kwa nini ni lazima tujichukue kama askari na washindani “katika machezo”?
15 Askari hujitenga na maisha ya raia wasio jeshini yasiyo na vizuizi vingi. Vilevile, ni lazima tusijitatanishe wenyewe na mambo ya wale wasio katika jeshi la Bwana bali ambalo kwa kweli, wako upande unaopinga. Hivyo, Paulo aliendelea kumwandikia Timotheo hivi: “Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari. Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali.” (2 Timotheo 2:4, 5) Kwa kujitahidi kupata ushindi katika shindano la mbio la “taji ya uzima,” ni lazima wapiga mbio wazoee kujidhibiti na kuepuka malemeo na matatanishi yasiyohitajiwa. Kwa njia hiyo wanaweza kukaza fikira katika kuwaletea wengine habari njema za wokovu.—Yakobo 1:12; linganisha 1 Wakorintho 9:24, 25.
16. Ni nini hakiwezi kufungwa, na tunavumilia kwa faida ya nani?
16 Kwa sababu twampenda Mungu na wale wenye mfano wa kondoo wanaomtafuta ili wampate, sisi huvumilia mengi kwa furaha ili kuwafikia wengine tukiwa na habari njema ya wokovu. Adui huenda wakatufunga kwa ajili ya kuhubiri Neno la Mungu. Lakini Neno la Mungu haliwezi kufungwa, na kusema juu yalo kwa ajili ya wokovu wa wengine hakuwezi kutiwa mnyororo. Paulo alimweleza Timotheo kwa nini yeye alikuwa na nia sana ya kukabili jaribu: “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao wa Daudi kama inenavyo injili yangu. Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi. Kwa ajili ya hilo nastahimili mambo yote, kwa ajili ya wateule, ili wao nao waupate wokovu ule ulio katika Kristo Yesu, pamoja na utukufu wa milele.” (2 Timotheo 2:8-10) Leo tunawafikiria si mabaki wachache tu wa wale watakaopokea Ufalme wa kimbingu bali pia na umati mkubwa wa kondoo wengine wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, umati mkubwa utakaopata Paradiso ya kidunia chini ya Ufalme wa Kristo.—Ufunuo 7:9-17.
17. Kwa nini tusiache shindano la mbio, na tokeo ni nini tukiendelea katika shindano la mbio hata mwisho?
17 Kama tungekuwa watu wenye kuacha mambo kabla ya kuyamaliza, tusingejisaidia wenyewe wala mtu mwingine yeyote kupata wokovu. Kwa kuvumilia katika shindano la mbio la Kikristo, vijapokuwa vizuizi tunavyokabili, tunajiweka tayari daima kupata zawadi na twaweza kusaidia wengine moja kwa moja wapate wokovu, hali tukiwa mfano wenye nguvu kwa wengine. Tumaini letu liwe vipi, la kimbingu au la kidunia, mwelekeo wa Paulo wa ‘kukaza mwendo, kuifikilia mede ya thawabu’ ni mzuri wa kuigwa.—Wafilipi 3:14, 15.
Kuendelea kwa Uthabiti Katika Shindano la Mbio
18. Kuishinda zawadi kunategemea nini, lakini ili kuvumilia hata mwisho, ni lazima nini kiepukwe?
18 Kuumaliza kwa ushindi mwendo wetu wa Kikristo kwa utetezi wa Yehova na kushinda zawadi anayotuwekea kwategemea kuendelea kwetu kwa uthabiti katika mwendo wote wa mbio za shindano hilo la mbio. Kwa hiyo, hatuwezi kuvumilia hata mwisho tukijilemeza na mambo ambayo hayatumikii kusudi la uadilifu. Hata tuondolewapo mambo hayo, matakwa bado ni mazito ya kutosha kuhitaji nguvu yote tuwezayo kuchochea. Kwa hiyo, Paulo ashauri hivi: “Na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi [uvumilivu, NW] katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.” (Waebrania 12:1) Kama Yesu hatupaswi kukaza fikira mno kwenye mateso yanayohitaji kuvumiliwa bali kuyaona kuwa bei ndogo ya kulipia zawadi ya shangwe.—Linganisha Warumi 8:18.
19. (a) Paulo alionyesha uhakikisho gani karibu na mwisho wa uhai wake? (b) Tukaribiapo mwisho wa shindano la mbio la uvumilivu, twapaswa kuwa na uhakika gani kuhusu thawabu iliyoahidiwa?
19 Karibu na mwisho wa uhai wake, Paulo aliweza kusema hivi: “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda; baada ya hayo nimewekewa taji ya haki.” (2 Timotheo 4:7, 8) Tumo katika shindano la mbio hili la uvumilivu ili kupokea zawadi ya uhai wa milele. Uvumilivu wetu ukikoma kwa sababu tu shindano la mbio limekuwa refu kuliko vile tulivyolitazamia kuwa tulipolianza, tutashindwa tunapokuwa karibu kuipata thawabu iliyoahidiwa. Usiwe na shaka yoyote. Hakika thawabu iko.
20. Twapaswa kuwa na nia gani hata ufike mwisho wa shindano la mbio?
20 Kwa hiyo macho yetu na yasichoke kutazama kuanza kwa dhiki kubwa, itakapoleta uharibifu kwanza kwa Babuloni Mkubwa na kisha kwa sehemu inayobaki ya tengenezo la Ibilisi. (2 Petro 3:11, 12) Kwa sababu ya ishara zote za waziwazi zinazotuzunguka, na tuangalie mbele kwa imani. Na tuvifunge viuno vya nguvu zetu za uvumilivu, na tuendelee kwa ujasiri katika shindano la mbio ambalo Yehova Mungu ameweka mbele yetu, hata mwisho ufikiwapo na zawadi ya shangwe kupatikana, kwa utetezi wa Yehova kupitia Yesu Kristo.
Ungejibuje?
◻ Ni lazima Wakristo wajitayarishe kwa ajili ya shindano la mbio la aina gani?
◻ Kwa nini shangwe ni ya maana sana katika kukimbia shindano hilo la mbio?
◻ Ni kwa sababu zipi kuu, tunaendelea katika huduma zijapokuwa taabu?
◻ Kwa nini hatupaswi kuliacha shindano la mbio ambalo Mungu ameweka mbele yetu?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kama vile katika shindano la mbio la mwendo mrefu, ni lazima Wakristo wavumilie
[Picha katika ukurasa wa 17]
Katika kujitahidi kupata “taji ya uzima,” ni lazima wapiga mbio wazoee kujidhibiti