Twaweza Kumlipaje Yehova?
YEHOVA MUNGU huonyesha mfano ulio mzuri zaidi wa kutoa. Aliipa ainabinadamu yote “uzima na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Mungu huwaangazia jua lake watu waovu na waadilifu pia. (Mathayo 5:45) Kwa kweli, ‘Yehova hutupa mvua kutoka mbinguni na nyakati za mavuno, akitushibisha mioyo yetu chakula na furaha.’ (Matendo 14:15-17) Kwani, “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga”!—Yakobo 1:17.
Kuongezea zawadi zote za Mungu za kimwili, yeye hutoa nuru na kweli ya kiroho. (Zaburi 43:3) Watumishi wa Yehova waaminifu-washikamanifu hubarikiwa sana na chakula cha kiroho ambacho yeye huandaa kwa wakati wake kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Twaweza kunufaika na maandalizi ya Mungu ya kiroho kwa sababu amewezesha wanadamu wenye dhambi na wenye kufa wapatanishwe naye. Kwa jinsi gani? Kupitia kifo cha Mwana wake, Yesu Kristo, aliyetoa uhai wake kuwa fidia kwa wengi. (Mathayo 20:28; Warumi 5:8-12) Ni zawadi nzuri iliyoje kutoka kwa Mungu mwenye upendo, Yehova!—Yohana 3:16.
Je! Twaweza Kumlipa kwa Njia Yoyote?
Karne nyingi kabla ya kuandaliwa kwa fidia, mtunga zaburi mwenye kupuliziwa roho alithamini sana rehema, ukombozi, na msaada wenye kutolewa na Mungu hivi kwamba alisema hivi: “Nimrudishie [nimlipe, NW] BWANA [Yehova, NW] nini kwa ukarimu wake wote alionitendea [fadhili zake zote kwangu, NW]? Nitakipokea kikombe cha wokovu; na kulitangaza jina la BWANA [Yehova, NW]; nitaziondoa nadhiri zangu kwa BWANA [Yehova, NW], naam, mbele ya watu wake wote.”—Zaburi 116:12-14.
Ikiwa tumejiweka wakfu kwa Yehova kwa moyo wote, tunaliita jina lake katika imani na kuzitimiza nadhiri zilizotolewa kwake. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, twaweza kumbariki Mungu kwa kusema vyema juu yake nyakati zote na kutangaza ujumbe wa Ufalme wake. (Zaburi 145:1, 2, 10-13; Mathayo 24:14) Lakini hatuwezi kumtajirisha Yehova, aliye na vitu vyote vikiwa mali yake, au kumlipa kwa fadhili zake zote kwetu.—1 Mambo ya Nyakati 29:14-17.
Kutoa michango ili kuendeleza masilahi ya Ufalme si njia ya kumlipa au kumtajirisha Yehova. Hata hivyo, kutoa huko hutupa nafasi za kuonyesha upendo wetu kwa Mungu. Michango isiyotolewa kwa kusudi la ubinafsi au kwa kuonwa na watu wote na kusifiwa, bali iliyotolewa kwa roho ya ukarimu na ili kuendeleza ibada ya kweli, humletea mpaji furaha na baraka ya Yehova. (Mathayo 6:1-4; Matendo 20:35) Mtu aweza kuhakikishiwa kushiriki katika kutoa huko na katika furaha inayotokea kwa kuweka kando kwa kawaida kitu fulani kutoka kwa mali zake za kimwili ili kutegemeza ibada ya kweli na kusaidia wale wanaostahili. (1 Wakorintho 16:1, 2) Je! hilo lapasa lifanywe kwa kulipa zaka?
Je! Wapaswa Kulipa Zaka?
Yehova alisema kupitia nabii wake Malaki: “Leteni zaka kamili ghalani, ili kiwemo chakula katika nyumba yangu, mkanijaribu kwa njia hiyo, . . . kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.” (Malaki 3:10) Tafsiri nyingine husomwa hivi: “Leteni zaka yote ndani ya nyumba ya kuweka akiba.”—An American Translation.
Zaka ni sehemu ya kumi ya kitu. Hiyo ni asilimia kumi inayotolewa au kulipwa kama ushuru. Kulipa zaka hufanywa hasa kwa makusudi ya kidini. Inamaanisha kutoa sehemu ya kumi ya mapato ya mtu ili kuendeleza ibada.
Mzee wa ukoo Abrahamu (Abramu) alimpa mfalme-kuhani Melkizedeki wa Salemu fungu la kumi la nyara za ushindi juu ya Kedorlaoma na waliojiunga naye. (Mwanzo 14:18-20; Waebrania 7:4-10) Baadaye, Yakobo aliweka nadhiri kumpa Mungu sehemu ya kumi ya mali zake za kimwili. (Mwanzo 28:20-22) Katika kila kisa, kutoa kwa sehemu ya kumi kulifanywa kwa hiari, kwani wale Waebrania wa mapema hawakuwa na sheria zilizowalazimisha kulipa zaka.
Kulipa Zaka Chini ya Sheria
Wakiwa watu wa Yehova, Waisraeli walipokea sheria za kulipa zaka. Hizo, yaonekana, zilihusisha kutumia sehemu mbili za kumi za mapato ya kila mwaka, ingawa wanachuo wengine hufikiri kulikuwako zaka moja tu ya kila mwaka. Hakuna zaka yoyote iliyolipwa wakati wa mwaka wa Sabato, kwa kuwa hakuna mapato yoyote yaliyotarajiwa wakati huo. (Mambo ya Walawi 25:1-12) Zaka zililipwa juu ya malimbuko yaliyotolewa kumpa Mungu.—Kutoka 23:19.
Sehemu moja ya kumi ya mazao ya nchi na ya matunda ya miti na yaonekana, ya ongezeko la mifugo na makundi ilipelekwa patakatifu na kupewa Walawi, ambao hawakupokea urithi wowote katika nchi. Kisha, wao walitoa sehemu ya kumi ya kile walichopokea ili kutegemeza ukuhani wa Kiharuni. Yaonekana nafaka ilipurwa na matunda ya mzabibu na mzeituni yaligeuzwa kuwa divai na mafuta kabla ya zaka kulipwa. Ikiwa Mwisraeli alitaka kulipa pesa badala ya mazao, angeweza kufanya hivyo, ikiwa angeongeza sehemu ya tano kwa thamani yayo.—Mambo ya Walawi 27:30-33; Hesabu 18:21-30.
Yaonekana zaka nyingine ilikuwa inawekwa kando. Kwa kawaida, ilikuwa inatumiwa na familia wakati watu walipokusanyika kwa ajili ya sikukuu mbalimbali. Lakini vipi ikiwa mwendo wa kwenda Yerusalemu ulikuwa mrefu sana kwa kusafirisha zaka hiyo kwa kufaa? Hapo, nafaka, divai mpya, mafuta na wanyama waliuzwa kupata pesa ambazo zingeweza kubebwa kwa urahisi. (Kumbukumbu la Torati 12:4-18; 14:22-27) Mwisho wa kila mwaka wa tatu na wa sita wa mfuatano wa miaka saba ya kisabato, zaka iliwekwa kando kwa ajili ya Walawi, wageni, wajane, na yatima.—Kumbukumbu la Torati 14:28, 29; 26:12.
Chini ya sheria, hakukuwako adhabu kwa ajili ya kukosa kulipa zaka. Bali, Yehova aliwaweka watu hao chini ya wajibu wa kiadili wenye nguvu wa kulipa zaka. Nyakati nyingine walihitaji kutangaza rasmi mbele zake kwamba zaka ilikuwa imelipwa kikamili. (Kumbukumbu la Torati 26:13-15) Chochote kilichonyimwa isivyofaa kilionwa kuwa kitu kilichoibiwa kutoka kwa Mungu.—Malaki 3:7-9.
Kulipa zaka hakukuwa mpango wenye kulemeza. Kwa kweli, Waisraeli walipofuata sheria hizo, walifanikiwa zaidi. Zaka iliendeleza ibada ya kweli bila kukazia isivyofaa jinsi ya kuitolea maandalizi ya kimwili. Kwa hiyo, mpango wa kulipa zaka ulikuwa kwa faida ya wote katika Israeli. Lakini je, kulipa zaka kwawapasa Wakristo?
Je! Ni Lazima Wakristo Walipe Zaka?
Kwa wakati fulani, kulipa zaka kulikuwa jambo la kawaida katika milki ya Jumuiya ya Wakristo. The Encyclopedia Americana hutaarifu hivi: “Hilo . . . lilikuja polepole kuwa jambo la kawaida kufikia karne ya 6. Baraza la Tours katika 567 na Baraza la Macon la pili katika 585 lilipendelea kulipa zaka. . . . Matumizi mabaya yakawa ya kawaida, hasa wakati haki ya kuchanga zaka mara nyingi ilipopewa au kuuzwa kwa watu wa kawaida. Kuanzia na Papa Gregory wa 7 zoea hilo lilitangazwa rasmi kuwa lisilo halali. Kisha watu wengi wa kawaida wakatoa haki zao za kulipa zaka kwa nyumba za watawa-waume na kwa wakuu wa kathedrali. Yale Marekebisho ya Kidini hayakuondolea mbali kulipa zaka, na zoea hilo likaendelea katika Kanisa Katoliki la Kiroma na katika nchi za Kiprotestanti.” Kulipa zaka kuliondolewa mbali au mahali pake pakachukuliwa polepole katika nchi mbalimbali, na sasa ni dini chache zinazofuata zoea hilo.
Kwa hiyo basi, Wakristo wanatakiwa walipe zaka? Katika konkodansi yake ya Biblia, Alexander Cruden alisema hivi: “Wala Mwokozi wetu, wala mitume wake hawatoi agizo lolote katika shughuli hii ya zaka.” Kwa kweli, Wakristo hawaagizwi kulipa zaka. Mungu mwenyewe ndiye aliyekomesha Sheria ya Musa, pamoja na mipango yayo ya kulipa zaka, akiigongomea kwenye mti wa mateso wa Yesu. (Warumi 6:14; Wakolosai 2:13, 14) Kwa hiyo, badala ya kutakiwa kutoa kiasi fulani kilichotajwa ili kulipia gharama za kundi, Wakristo hutoa michango ya hiari.
Mheshimu Yehova kwa Vitu Vyako Vinavyothamanika
Bila shaka ikiwa Mkristo achagua kwa hiari yake kutoa sehemu ya kumi ya mapato yake ili kuendeleza ibada ya kweli, kusingekuwako katazo lolote la Kimaandiko kwa yeye kufanya michango ya jinsi hiyo. Katika barua iliyoandamana na mchango wake, kijana mwenye umri wa miaka 15 katika Papua New Guinea aliandika hivi: “Nilipokuwa mdogo, baba yangu alikuwa akiniambia, ‘Unapoanza kufanya kazi, ni lazima umpe Yehova matunda ya kwanza ya mazao yako.’ Ninayakumbuka maneno ya Mithali 3:1, 9, yanayosema ni lazima tumpe Yehova malimbuko ya mazao yetu ili tumheshimu. Kwa hiyo niliahidi kufanya hivyo, na sasa ni lazima niitimize ahadi yangu. Ninafurahi sana kupeleka pesa hizi ili kusaidia kazi ya Ufalme.” Biblia haishurutishi Wakristo kufanya ahadi ya jinsi hiyo. Hata hivyo, kutoa kwa ukarimu ni njia nzuri ya kuonyesha upendezi wenye bidii katika kuendeleza ibada ya kweli.
Huenda Mkristo asichague kuweka mpaka hususa kwa upaji anaotoa ili kuendeleza ibada ya Yehova Mungu. Kutoa mfano: Walipokuwa kwenye kusanyiko la Mashahidi wa Yehova, dada wawili wazee-wazee walikuwa wakizungumza juu ya michango iwezayo kutolewa kwa kazi ya Ufalme. Kwa habari ya kupata chakula kwenye kusanyiko, mmoja wa dada hao, ambaye ni mwenye umri wa miaka 87, alitaka kujua gharama ya chakula ili aweze kuchanga kiasi hicho. Dada yule mwingine, ambaye ni mwenye umri wa miaka 90, akasema hivi: ‘Toa tu kiasi unachofikiri ni cha thamani yacho—na kuongeza zaidi kidogo.’ Huyo dada mwenye umri mkubwa zaidi alionyesha mwelekeo mzuri kama nini!
Kwa kuwa watu wa Yehova wameweka wakfu kwake vitu vyote walivyo navyo, wao hutoa kwa furaha michango ya kifedha na michango mingine ili kuitegemeza ibada ya kweli. (Linganisha 2 Wakorintho 8:12.) Kwa kweli, njia ya Kikristo ya kutoa huandaa nafasi za kuonyesha uthamini mwingi kwa ajili ya ibada ya Yehova. Kutoa huko hakuzuiwi kuwa zaka, au sehemu ya kumi tu, na huenda kukawa na hali ambamo mtu mmoja mmoja asukumwa kutoa zaidi ili kuendeleza masilahi ya Ufalme.—Mathayo 6:33.
Mtume Paulo alisema hivi: “Kila mmoja, basi, na atoe kadiri alivyoamua, kwa moyo na wala si kwa huzuni au kwa kulazimishwa, maana Mungu humpenda yule mwenye kutoa kwa furaha.” (2 Wakorintho 9:7, HNWW) Ukitoa kwa furaha na kwa ukarimu katika kuitegemeza ibada ya kweli, utafaidika, kwani mithali yenye hekima husema hivi: “Mheshimu BWANA [Yehova, NW] kwa mali yako, [vitu vyako vinavyothamanika, NW], na kwa malimbuko ya mazao yako yote. Ndipo ghala zako zitakapojazwa kwa wingi, na mashinikizo yako yatafurika divai mpya.”—Mithali 3:9, 10.
Hatuwezi kumtajirisha yule Aliye Juu Kabisa. Dhahabu na fedha, hayawani juu ya milima elfu, na vitu vinavyothamanika visivyo na hesabu, vyote ni mali zake. (Zaburi 50:10-12) Hatuwezi kamwe kumlipa Mungu kwa fadhili zake zote kwetu. Lakini twaweza kuonyesha uthamini wetu mwingi kwake na kwa pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu kwa sifa yake. Na twaweza kuhakikishiwa kwamba mibaraka mingi huwatiririkia wale wanaotoa kwa ukarimu ili kuendeleza ibada safi na kumheshimu Yehova, Mungu mwenye upendo na ukarimu.—2 Wakorintho 9:11.
[Sanduku katika ukurasa wa 29]
JINSI WENGINE WANAVYOCHANGIA KAZI YA UFALME
◻ MICHANGO KWA KAZI YA ULIMWENGUNI KOTE: Wengi huweka kando au hupangia kiasi cha fedha ambazo wanatia katika masanduku ya michango yaliyo na kibandiko hiki: “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Kote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi, makundi hupeleka kiasi hicho ama kwa makao makuu ya ulimwengu huko Brooklyn, New York, ama kwenye ofisi ya tawi iliyo karibu zaidi.
◻ ZAWADI: Michango ya hiari ya pesa inaweza kupelekwa moja kwa moja Watchtower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti iliyo karibu. Vito au mali nyingine zenye thamani zinaweza kupewa pia. Barua fupi yenye kutaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja inapasa iambatane na michango hiyo.
◻ MPANGO WA UPAJI WENYE MASHARTI: Pesa zinaweza kupewa kwa Watch Tower Society zishikiliwe zikiwa amana hadi kifo cha mwenye kuchanga, kukiwa na uandalizi wa kwamba kukitokea kisa cha uhitaji wa kibinafsi, zitarudishwa kwa mpaji.
◻ BIMA: Watch Tower Society inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mpango wa bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi/malipo ya uzeeni. Sosaiti inapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ AKIBA ZA PESA ZILIZO BENKI: Akiba za pesa zilizo benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja mmoja zinaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo. Sosaiti inapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
◻ HISA NA DHAMANA: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Society ama zikiwa zawadi ya moja kwa moja ama zikiwa chini ya mpango ambapo mapato yanaendelea kulipwa kwa mpaji.
◻ NYANJA NA MAJENGO: Nyanja na majengo zinazoweza kuuzwa zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower Society ama kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja ama kwa kuweka uwanja au jengo la maisha kwa ajili ya mpaji, ambaye aweza kuendelea kuishi huko muda wa maisha yake. Mtu anapaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kupa Sosaiti hati yoyote ya nyanja na majengo.
◻ MAWASIA NA AMANA: Mali au pesa zinaweza kupangiwa kuwa urithi wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini inaweza kuandaa faida fulani za kodi. Nakala ya wasia au mkataba wa amana inapasa kupelekwa kwa Sosaiti.
Kwa habari zaidi kuhusu mambo ya jinsi hiyo, andikia International Bible Students Association, P. O. Box 47788, Nairobi, Kenya.