Furaha ya Milele Yawangoja Watoaji wa Kimungu
“Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee [mzaliwa-pekee, NW], ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—YOHANA 3:16.
1, 2. (a) Ni nani aliye Mtoaji mkubwa zaidi, na zawadi yake iliyo kubwa zaidi kwa ainabinadamu ni nini? (b) Katika kutoa zawadi yake iliyo kubwa zaidi, Mungu alionyesha sifa gani?
YEHOVA MUNGU ndiye Mtoaji mkubwa kushinda wote. Ni kuhusu yeye, Muumba wa mbingu na dunia, kwamba mwanafunzi Mkristo Yakobo aliandika: “Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.” (Yakobo 1:17) Yehova pia ndiye Mtoaji wa zawadi iliyo kubwa kupita zote zilizoweza kutolewa wakati wowote ule. Kuhusu zawadi yake iliyo kubwa kupita zote kwa ainabinadamu na kwa ajili yayo, ilisemwa hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee [mzaliwa-pekee, NW], ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
2 Msemaji wa maneno hayo hakuwa mwingine ila yule Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu mwenyewe. Kwa asili mwana mzaliwa-pekee wa baba angemthamini na kumpenda baba wa jinsi hiyo akiwa chanzo chake cha uhai na cha vitu vyote vizuri vinavyoandaliwa ili aonee shangwe uhai. Lakini upendo wa Mungu haukuzuiwa kwa Mwana wake huyo mmoja peke yake. Kueneza zawadi ya jinsi hiyo kwa wengine wa viumbe vyake kungeonyesha wazi upendo wa Mungu wa ajabu. (Linganisha Warumi 5:8-10.) Hiyo inadhihirika zaidi tunapochunguza maana hasa ya neno ‘-toa’ katika muktadha huo.
Zawadi ya Mungu Kumtoa “Mwana wa Pendo Lake”
3. Zaidi ya “Mwana wa pendo lake,” ni nani wengine waliouonea shangwe upendo wa Baba wa kimbingu?
3 Kwa kipindi cha wakati kisichodhahiri, Mungu alikuwa ameonea shangwe ushirika wa kibinafsi pamoja na Mwana mzaliwa-pekee wake—“Mwana wa pendo lake”—katika makao ya kimbingu. (Wakolosai 1:13) Muda wa wakati huo wote, Baba na Mwana walizidi sana katika upendo na shauku kuelekea mmoja na mwenzake hivi kwamba hakukuwa upendo mwingine kati ya watu wawili uliokuwa kama wao. Viumbe wale wengine waliopewa uhai na Mungu kupitia Mwana mzaliwa-pekee wake walipendwa pia wakiwa washiriki wa familia ya kimungu ya Yehova. Hivyo, upendo ulitawala juu ya familia yote ya Mungu. Inataarifiwa kwa usahihi katika Maandiko matakatifu kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo familia ya kimungu ingejumuika kuwa wale wapendwao na Baba, Yehova Mungu.
4. Kutoa kwa Mungu Mwana wake kulihusishaje zaidi ya kupoteza ushirika wa kibinafsi, na kwa ajili ya nani?
4 Vifungu kati ya Yehova na Mwana wake mzaliwa wa kwanza vilikuwa vya karibu sana hivi kwamba kule kujinyima tu wenyewe ushirika wa ukaribu kama huo kungekuwa hasara kubwa. (Wakolosai 1:15) Lakini ‘kutoa’ kwa Mwana mzaliwa-pekee huyo kulimaanisha zaidi ya kujinyima kwa Mungu mwenyewe ushirika wa kibinafsi pamoja na “Mwana wa pendo lake.” Kulifikia hata hatua ambayo Yehova alimruhusu Mwana wake afe na hivyo akome kuwapo kwa muda fulani akiwa mshiriki wa familia ya Mungu ya ulimwengu wote mzima. Hicho kilikuwa kifo kwa ajili ya wale ambao hawakupata kamwe kuwa washiriki wa familia ya Mungu. Yehova asingeweza kutoa kwa ajili ya aina ya kibinadamu yenye uhitaji, zawadi iliyo kubwa zaidi ya Mwana mzaliwa-pekee wake anayetambulishwa na Maandiko kuwa pia “mwanzo wa kuumba kwa Mungu.”—Ufunuo 3:14.
5. (a) Wazao wa Adamu walikuwa katika hali gani isiyopendeza, na haki ya Mungu ilitaka nini kwa upande wa mmoja wa wana Wake waaminifu? (b) Zawadi ya Mungu iliyo kubwa zaidi ingetaka nini kwa upande wake mwenyewe?
5 Wenzi wa ndoa wa kwanza, Adamu na Hawa, walishindwa kudumisha mahali pao wakiwa washiriki wa familia ya Mungu. Hiyo ndiyo hali ambamo walijipata wenyewe baada ya kuondoshwa katika shamba la Edeni kwa sababu ya kutenda dhambi dhidi ya Mungu. Hawakuacha tu kuwa washiriki wa familia ya Mungu bali pia walikuwa chini ya hukumu ya kifo. Kwa hiyo, tatizo halikuwa lile tu la kurudisha wazao wao kwenye pendeleo la Mungu wakiwa washiriki wa familia yake bali pia lilikuwa lile la kuwaondolea hukumu ya kimungu ya kifo. Kulingana na utendaji wa haki ya kimungu, hilo lingehitaji kwamba mmoja wa wana waaminifu wa Yehova Mungu afe akiwa badala au fidia. Kwa hiyo, swali kuu lilikuwa: Je! yule ambaye angechaguliwa angekuwa na nia ya kufa kifo cha badala kama hicho kwa ajili ya wanadamu watenda dhambi? Isitoshe, kufanya hivyo kungehitaji muujiza kwa upande wa Mungu Mweza Yote. Kungehitaji pia wonyesho wa upendo wa kimungu kwa kadiri isiyo na kifani.—Warumi 8:32.
6. Mwana wa Mungu aliweza kupatanaje na mahitaji ya hali iliyohusisha ainabinadamu yenye dhambi, na alisema nini kuhusu hilo?
6 Ni Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu tu aliyeweza kupatana na mahitaji ya pekee ya hali iliyohusisha ainabinadamu yenye dhambi. Yeye afanana sana na Baba yake katika kuonyesha shauku kwa washiriki wa familia iliyotokezwa kimungu hivi kwamba hana kifani chochote miongoni mwa wana wa Mungu. Kwa kuwa viumbe wote wengine wenye akili waliumbwa kupitia yeye, shauku yake kwao hakika ingekuwa nyingi. Zaidi ya hayo, upendo ni sifa kuu ya Yesu Kristo, Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, kwa sababu “yeye . . . ni mn’gao wa utukufu [wa Mungu] na chapa ya nafsi yake.” (Waebrania 1:3) Akionyesha nia yake ya kuonyesha upendo huo kwa kadiri kubwa zaidi kwa kutoa uhai wake kwa ajili ya ainabinadamu yenye dhambi, Yesu aliwaambia mitume wake 12: “Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”—Marko 10:45; ona pia Yohana 15:13.
7, 8. (a) Kusudi la Yehova la kumtuma Yesu Kristo katika ulimwengu wa ainabinadamu lilikuwa nini? (b) Mungu alimtuma Mwana mzaliwa-pekee wake kwenye utume wa aina gani?
7 Yehova Mungu alikuwa na sababu ya pekee ya kumtuma Yesu ndani ya ulimwengu huu wenye umaskini wa ainabinadamu. Upendo wa kimungu ndio uliochochea hilo, kwani Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee [mzaliwa-pekee, NW], ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.”—Yohana 3:16, 17.
8 Kwa upendo Yehova alimtuma Mwana mzaliwa-pekee wake kwenye utume wa wokovu. Mungu hakumtuma Mwana wake hapa ili auhukumu ulimwengu. Ikiwa Mwana wa Mungu alikuwa ametumwa kwenye utume wa kihukumu wa jinsi hiyo, tazamio la ainabinadamu yote lingekuwa baya kabisa. Adhabu ya hukumu kali ambayo ingalitamkwa na Yesu Kristo juu ya familia ya kibinadamu ingalikuwa lawama la kifo. (Warumi 5:12) Hivyo, kwa wonyesho huo wa kipekee wa upendo wa kimungu, Mungu alisawazisha ile hukumu ya kifo ambayo haki tupu ingalihitaji.
9. Mtunga zaburi Daudi alihisije juu ya utoaji wa Yehova?
9 Katika mambo yote, Yehova Mungu hudhihirisha na kuonyesha upendo ukiwa sehemu bora zaidi ya utu wake. Na yaweza kusemwa kwa usahihi kwamba kwa habari ya vitu vizuri, Mungu huwatolea waabudu wake waaminifu duniani zaidi ya vinavyotosha. Mtunga zaburi Daudi alihisi hivyo juu ya jambo hilo alipomwambia Mungu hivi: “Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako ulizowawekea wakuchao; ulizowatendea wakukimbiliao mbele ya wanadamu!” (Zaburi 31:19) Katika utawala wa Daudi juu ya taifa la Israeli—naam, muda wote wa maisha yake akiwa mshiriki wa taifa hilo lililoteuliwa kipekee na Mungu—aliona wema wa Yehova mara nyingi. Na Daudi aliuona kuwa mwingi.
Kupoteza kwa Israeli Zawadi Kubwa Kutoka kwa Mungu
10. Ni kwa nini Israeli la kale lilikuwa tofauti na taifa jingine lolote duniani?
10 Likiwa na Yehova akiwa Mungu walo, Israeli la kale lilikuwa tofauti na taifa jingine lolote duniani. Kupitia nabii Musa akiwa mpatanishi, Yehova aliwaingiza wazao wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo katika uhusiano wa agano pamoja na yeye mwenyewe. Hakuwa ameshughulika na taifa jingine lolote kwa njia hiyo. Kwa hiyo, mtunga zaburi aliyepuliziwa roho angeweza kusema kwa mshangao: “Humjulisha Yakobo ujumbe wake, na Israeli maongozi na maagizo yake. Lakini watu wengine hakuwafanyia hayo; watu wengine hawayajui maagizo yake. Asifiwe Mwenyezi-Mungu! Haleluya!”—Zaburi 147:19, 20, HNWW.
11. Israeli lilionea shangwe msimamo walo wenye upendeleo pamoja na Mungu hadi wakati gani, na Yesu alionyeshaje badiliko katika uhusiano walo?
11 Taifa la Israeli la asili liliendelea katika uhusiano huo wenye upendeleo pamoja na Mungu mpaka lilipomkataa Yesu Kristo akiwa Mesiya katika mwaka wa 33 wa Wakati wa Kawaida wetu. Kwa kweli ilikuwa siku yenye kuhuzunisha kwa Israeli wakati Yesu alipotoa mshangao huu wenye majonzi: “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Maneno ya Yesu yalionyesha kwamba taifa la Israeli, ingawa lilipendelewa na Yehova mbeleni, lilikuwa limekosa kupata zawadi ya pekee kutoka kwa Mungu. Jinsi gani?
12. ‘Watoto wa Yerusalemu’ walikuwa nani, na Yesu kuwakusanya pamoja kungemaanisha nini?
12 Kwa kutumia neno “watoto,” Yesu alirejezea tu wale Wayahudi wa asili waliotahiriwa ambao waliishi Yerusalemu na waliowakilisha taifa lote la Kiyahudi. Ili Yesu aweze kukusanya pamoja ‘watoto wa Yerusalemu’ angalihitaji kuwaingiza “watoto” hao katika agano jipya pamoja na Mungu, yeye mwenyewe akitumikia akiwa Mpatanishi kati ya Yehova na hao Wayahudi wa asili. (Yeremia 31:31-34) Hilo lingalitokeza msamaha wa dhambi, kwani hiyo ndiyo ilikuwa ndiyo kadiri ya upendo wa Mungu. (Linganisha Malaki 1:2.) Kwa kweli hiyo ingalikuwa zawadi kubwa.
13. Kukataa kwa Israeli Mwana wa Mungu kulitokeza hasara gani, lakini ni kwa nini shangwe ya Yehova haikufifia?
13 Kwa kupatana na Neno lake la kiunabii, Yehova alingoja kwa muda mrefu wa kutosha kabla ya kuwaenezea wasio Wayahudi zawadi ya kuwa washiriki wa agano jipya. Lakini kwa kumkataa Mwana wa Mungu mwenyewe, Mesiya, taifa la Israeli la asili lilikosa kupata zawadi hiyo kubwa. Kwa hiyo Yehova alisawazisha kukataliwa huko kwa Mwana wake kwa kufikisha zawadi hiyo kwa watu wasio wa taifa la Kiyahudi. Kwa njia hiyo, shangwe ya Yehova akiwa Mtoaji Mkuu iliendelea bila kufifia.
Furaha ya Kutoa
14. Kwa nini Yesu Kristo ni kiumbe mwenye furaha nyingi zaidi katika ulimwengu wote mzima?
14 Yehova ndiye “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11, NW) Kutolea wengine ni jambo linalomfurahisha. Na katika karne ya kwanza W.K., Mwana mzaliwa-pekee wake alisema hivi: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Kwa kupatana na kanuni hiyo, Yesu amekuwa kiumbe mwenye furaha nyingi zaidi wa Muumba wa ulimwengu wote mzima. Jinsi gani? Akiwa wa pili kutoka Yehova Mungu mwenyewe, Yesu Kristo ametoa zawadi iliyo kubwa zaidi ya zote kwa kuutoa uhai wake kwa faida ya ainabinadamu. Kwa kweli, yeye ndiye ‘Mfalme mwenye furaha.’ (1 Timotheo 6:15, NW) Hivyo Yesu hutoa mfano mwema wa lile alilosema juu ya furaha nyingi zaidi katika kutoa.
15. Yehova hataacha kamwe kuwa mfano gani, na viumbe wake wenye akili wanaweza kuonaje kadiri fulani ya furaha yake?
15 Kupitia Yesu Kristo, Yehova Mungu hatashindwa kamwe kuwa Mtoaji mkarimu kwa viumbe wake wote wenye akili na sikuzote atakuwa mfano wao ulio bora kabisa katika kutoa. Sawa na vile Mungu hupata raha katika kutoa zawadi nzuri kwa wengine, ndivyo ameweka roho ya ukarimu katika mioyo ya viumbe wake wenye akili duniani. Kwa njia hiyo wanaangaza na kuuiga utu wake na kuona kadiri fulani ya furaha yake. (Mwanzo 1:26; Waefeso 5:1) Kwa kufaa, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”—Luka 6:38.
16. Yesu alirejezea utoaji gani kwenye Luka 6:38?
16 Yesu aliweka mfano ulio bora sana katika kufanya zoea la kuwaandalia wafuasi wake mwendo wa kufuata. Alisema kwamba kungekuwa itikio zuri kwa utoaji wa jinsi hiyo kwa upande wa wapokeaji. Kwenye Luka 6:38, Yesu hakuwa akirejezea utoaji wa zawadi za kimwili tu. Hakuwa akiwaambia wanafunzi wake wafuatie mwendo ambao ungewafanya wawe maskini kimwili. Badala ya hilo, alikuwa akiwaelekeza kwenye mwendo ambao ungewapa hisia ya utimilifu wa kiroho.
Furaha ya Milele Yahakikishiwa
17. Mungu ametolea Mashahidi wake zawadi gani nzuri ajabu katika siku hizi za mwisho?
17 Yehova, Kichwa cha uumbaji wote, amewatolea Mashahidi wake zawadi nzuri ajabu kama nini katika siku hizi za mwisho! Ametupa sisi habari njema za Ufalme wake. Tuna pendeleo kubwa la kuwa wapiga mbiu wa Ufalme wa Mungu uliosimamishwa mikononi mwa Mwana wake anayetawala, Yesu Kristo. (Mathayo 24:14; Marko 13:10) Kufanywa kuwa Mashahidi wenye kusema kwa sauti wa Mungu Aliye Juu Zaidi ni zawadi isiyolinganika, na njia iliyo bora zaidi ambayo twaweza kuzoea kutoa katika kumwiga Mungu ni kushiriki ujumbe wa Ufalme pamoja na wengine kabla ya mwisho wa mfumo mwovu huu wa mambo kuja.
18. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, ni lazima tuwape wengine nini?
18 Mtume Paulo alirejezea magumu ambayo alikuwa ameona alipokuwa akiwatangazia wengine ujumbe wa Ufalme. (2 Wakorintho 11:23-27) Mashahidi wa Yehova wa ki-siku-hizi wanalazimika pia kupatwa na magumu na kuweka kando mapendeleo ya kibinafsi katika jitihada ya kuwatolea wengine tumaini la Ufalme. Huenda tusiwe na mwelekeo wa kwenda kwenye milango ya watu, hasa ikiwa sisi ni wenye haya. Lakini tukiwa wafuasi wa Kristo, hatuwezi kuepuka, au kukiuka, pendeleo hilo la kutolea wengine mambo ya kiroho kwa kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Tunahitaji kuwa na mwelekeo ule ule ambao Yesu alikuwa nao. Alipokabili kifo, alisali hivi: “Baba yangu, . . . si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.” (Mathayo 26:39) Katika jambo la kutolea wengine habari njema ya Ufalme, ni lazima watumishi wa Yehova wafanye mapenzi ya Mungu, si yao wenyewe—lile atakalo yeye, si lile ambalo huenda wakataka.
19. Ni nani Wanaomiliki “makao ya milele,” na tunaweza kufanyaje urafiki pamoja nao?
19 Utoaji wa jinsi hiyo utahusisha wakati na mali zetu, lakini tukiwa watoaji wa kimungu, tunahakikisha kwamba furaha yetu itakuwa ya milele. Kwa nini? Kwa sababu Yesu alisema hivi: “Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu [“utajiri wa kilimwengu,” New International Version], ili itakapokosekana wawakaribishe katika makao ya milele.” (Luka 16:9) Mradi wetu wapasa kuwa kutumia “mali ya udhalimu” kufanya urafiki pamoja na wale Wanaomiliki “makao ya milele.” Akiwa Muumba, Yehova amiliki kila kitu, na Mwana wake mzaliwa wa kwanza ashiriki katika umiliki huo akiwa Mrithi wa vitu vyote. (Zaburi 50:10-12; Waebrania 1:1, 2) Ili kufanya urafiki pamoja nao, ni lazima tutumie mali katika njia inayovuta kibali chao. Hiyo inatia ndani kuwa na mwelekeo unaofaa katika kutumia vitu vya kimwili kwa ajili ya faida ya wengine. (Linganisha Mathayo 6:3, 4; 2 Wakorintho 9:7.) Twaweza kutumia pesa kwa njia inayofaa ili tuimarishe urafiki wetu pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kwa mfano, tunafanya hivyo kwa kutumia kwa uchangamfu kile tulicho nacho ili kuwasaidia watu wenye uhitaji kweli kweli na kutumia mali zetu kuendeleza masilahi ya Ufalme wa Mungu.—Mithali 19:17; Mathayo 6:33.
20. (a) Ni kwa nini Yehova na Yesu Kristo waweza kutuingiza katika “makao ya milele,” na makao hayo yaweza kuwa wapi? (b) Ni pendeleo gani litakalokuwa letu katika muda wote wa umilele?
20 Kwa sababu ya hali yao ya kutoweza kufa, Yehova Mungu na Yesu Kristo wanaweza kuwa Rafiki zetu wa milele na wanaweza kutuingiza katika “makao ya milele.” Ndivyo ilivyo iwe ni mbinguni pamoja na malaika watakatifu wote au kwenye dunia hii katika Paradiso iliyorudishwa. (Luka 23:43) Zawadi yenye upendo kutoka kwa Mungu kwa kutupa Yesu Kristo ilifanya hayo yote yawezekane. (Yohana 3:16) Na Yehova Mungu atamtumia Yesu aendelee kutoa kwa uumbaji wote, kwa furaha Yake mwenyewe ya kipekee. Kwa kweli, katika muda wote wa umilele sisi wenyewe tutakuwa na pendeleo la kutoa chini ya enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova Mungu na umaliki wa Mwana mzaliwa-pekee wake, Bwana na Mwokozi wetu, Yesu Kristo. Hilo litatokeza furaha ya milele kwa watoaji wote wa kimungu.
Je! Unakumbuka?
◻ Zawadi ya Mungu iliyo kubwa zaidi ingetaka nini kwa upande wake?
◻ Mungu alimtuma Mwana wake kwenye utume wa aina gani?
◻ Ni nani aliye kiumbe mwenye furaha nyingi zaidi katika ulimwengu wote mzima, na kwa nini?
◻ Watoaji wa kimungu wataonaje furaha ya milele?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Je! wewe unaithamini zawadi kutoka kwa Mungu kwa kutoa Mwana wake akiwa dhabihu ya fidia?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Je! wewe unatafuta Ufalme wa Mungu kwanza kwa kuhubiri habari njema na kwa kutegemeza kazi hiyo kwa mali zako?