Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi
“Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.”—MATHAYO 16:16.
1, 2. (a) Ukuu wa mtu waweza kukadiriwaje? (b) Ni wanaume gani katika historia wameitwa Mkuu, na kwa nini?
WEWE wafikiri yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi ni nani? Wewe hukadiriaje ukuu wa mtu? Je! ni kwa ufundi wake wa kivita? je! ni kwa uwezo wake mwingi sana wa kiakili? Je! ni kwa nguvu zake za kimwili?
2 Watawala mbalimbali wameitwa Mkuu, kama vile Koreshi Mkuu, Aleksanda Mkuu, na Charlemagne aliyeitwa “Mkuu” hata wakati alipokuwa hai. Kwa kuwapo kwao kwenye kutia hofu, wanaume kama hao walitumia uvutano wenye nguvu juu ya wale waliotawala.
3. (a) Ni nini mtihani ambao katika huo ukuu wa mtu waweza kupimwa? (b) Kwa kutumia mtihani kama huo, ni nani aliye mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi?
3 Kwa kupendeza, mwanahistoria H. G. Wells alieleza mtihani wake wa kupima ukuu wa mtu. Zaidi ya miaka 50 iliyopita, aliandika hivi: “Mtihani wa mwanahistoria wa ukuu wa mtu ni ‘Aliacha nini kisitawi? Je! alifanya watu waanze kufikiri kwa njia mpya kwa nguvu zilizoendelea baada yake?’ “Kwa mtihani huu,” Wells alifikia mkataa huu, “Yesu ni wa kwanza.” Hata Napoléon Bonaparte alisema hivi: “Yesu Kristo amekuwa na uvutano na ametawala raia Zake bila ya Yeye kuwapo katika mwili wenye kuonekana.”
4. (a) Ni maoni gani yenye kutofautiana kuhusu Yesu yaliyoko? (b) Mwanahistoria asiye Mkristo ampa Yesu mahali gani katika historia?
4 Hata hivyo, watu fulani wamekataa wakisema kwamba Yesu hakupata kuishi kamwe, bali ni hadithi tu. Kwenye ule upande mwingine wenye kupita kiasi, wengi wamemfanya Yesu kuwa kiabudiwa kama kwamba ni Mungu, wakisema kwamba Mungu alikuja duniani akiwa Yesu. Lakini, akitegemeza mikataa yake juu ya uthibitisho wa kihistoria peke yake kuwa Yesu aliishi kikweli akiwa binadamu, Wells aliandika hivi: “Ni jambo la kupendeza tena la maana kwamba mwanahistoria, pasipo upendeleo wowote wa kitheolojia, apaswa kuona kwamba hawezi kuonyesha kwa unyofu maendeleo ya kibinadamu bila kumpa mahali pa kwanza kabisa mwalimu wa kutoka Nazareti ambaye hakuwa na mali. . . . Mwanahistoria kama mimi, ambaye hata hajiiti Mkristo, apata masimulizi yakitegemea sana maisha na sifa ya mtu huyo wa maana sana.”
Je! Kwa Kweli Yesu Alipata Kuishi?
5, 6. Wanahistoria H. G. Wells na Will Durant wanasema nini kuhusu kupata kuishi kwa Yesu?
5 Lakini namna gani ikiwa mtu fulani akwambia kwamba kwa kweli Yesu hakupata kuishi kamwe, kwamba kwa kweli yeye, alikuwa hadithi ya uwongo, kwamba yeye ni ubuni wa watu fulani wa karne ya kwanza? Wewe ungejibuje hoja hiyo? Ingawa Wells akubali kwamba “sisi hatujui mengi juu ya [Yesu] kama vile tungependa kujua,” hata hivyo yeye asema hivi: “Zile Gospeli nne . . . hupatana katika kutupatia masimulizi ya mtu ambaye ni halisi sana; zina usadikisho wa ukweli. Kudhania kwamba yeye hakuishi kamwe, kwamba masimulizi ya maisha yake ni ubuni, ni jambo gumu zaidi na hutokeza matatizo mengi zaidi kwa mwanahistoria kuliko kukubali ukweli wa masimulizi ya Gospeli kuwa [jambo la] hakika.”
6 Yule mwanahistoria Will Durant mwenye kuheshimiwa alitoa hoja kwa njia iyo hiyo, akieleza hivi: “Kwamba wanaume wachache wa kikawaida [waliojiita Wakristo] wangeweza katika kizazi kimoja kubuni mtu mwenye nguvu na mwenye uvutano mwingi kadiri hiyo, mwenye elimu ya maadili ya hali ya juu kadiri hiyo na njozi yenye kuchochea kadiri hiyo ya udugu wa kibinadamu, ungekuwa muujiza wenye kustaajabisha mno zaidi ya wowote ulioandikwa katika Gospeli.”
7, 8. Yesu alikuwa na uvutano wa kadiri gani kwenye historia ya kibinadamu?
7 Hivyo, ungeweza kumpa sababu hivi mtu huyo mwenye kutia shaka: “Je! mtu wa hadithi ya kubuniwa—ambaye hakupata kuishi kamwe—angeweza kuwa na uvutano juu ya historia ya kibinadamu kwa njia yenye kutokeza kadiri hiyo? Kitabu cha marejezo The Historian’s of the World kilionelea hivi: “Matokeo ya kihistoria ya utendaji [wa Yesu] yalikuwa ya maana sana, hata kwa maoni halisi ya kilimwengu, kuliko matendo ya mtu mwingine yeyote aliyepata kuishi kikweli. Muda mpya, wenye kutambuliwa na ustaarabu wote mkuu wa ulimwengu, hupewa tarehe kuanzia kuzaliwa kwake.” Ebu fikiria hilo. Hata kalenda fulani leo zinategemea mwaka ambao Yesu hudhaniwa kuwa ndio aliozaliwa. “Tarehe kabla ya mwaka huo zinaorodheshwa kuwa B.C., au kabla ya Kristo,” chaeleza kitabu The World Book Encyclopedia. “Tarehe baada ya mwaka huo zinaorodheshwa kuwa A.D., au anno Domini (katika mwaka wa Bwana wetu).”
8 Kwa mafundisho yake yenye nguvu ya kuchochea watu watende na kwa njia ambayo aliishi kupatana nayo, Yesu amekuwa na uvutano wenye nguvu nyingi juu ya maisha za watu wengi sana kwa karibu miaka elfu mbili. Kama vile mwandikaji mmoja alivyolisema jambo hilo kwa kufaa: “Majeshi yote yaliyopata kupiga miguu, na majeshi yote ya manowari yaliyopata kuundwa, na mabunge yote yaliyopata kuwa na kikao, wafalme wote waliopata kutawala, wakijumlishwa pamoja hawakupata kuwa na uvutano juu ya maisha ya wanadamu katika dunia hii kwa nguvu nyingi jinsi hiyo.” Lakini wachambuzi husema: ‘Kwa kweli yote tujuayo kuhusu Yesu yanapatikana katika Biblia. Hakuna maandishi mengine yanayohusu yeye ya wakati wake yanayopatikana.’ Lakini je! hiyo ni kweli?
9, 10. (a) Wanahistoria na waandikaji wa kilimwengu wa mapema walisema nini juu ya Yesu? (b) Ikitegemea ushuhuda wa wanahistoria wa mapema, ensaiklopedia yenye kuheshimiwa hufikia mkataa gani?
9 Ijapokuwa wanahistoria wa mapema wa kilimwengu wanarejezea Yesu Kristo mara chache, marejezeo hayo yako. Cornelius Tacitus, mwanahistoria Mroma mwenye kustahiwa wa karne ya kwanza, aliandika kwamba Nero, maliki Mroma ‘alihesabia Wakristo hatia ya kutetekeza Roma,’ kisha Tacitus akaeleza hivi: “Lile jina [Mkristo] hutokana na Kristo, ambaye prokureta Pontio Pilato alikuwa amemuua katika utawala wa Tiberio.” Suetonio na Pliny Mdogo, waandikaji wengine Waroma wa wakati huo, pia walimtaja Kristo. Kwa kuongezea, Flavio Yosefo, mwanahistoria Myahudi wa karne ya kwanza, aliandika katika kitabu chake Antiquities of the Jews juu ya kifo cha mwanafunzi Mkristo Yakobo. Katika kueleza, Yosefo alisema kwamba Yakobo alikuwa “ndugu ya Yesu, aliyeitwa Kristo.”
10 Hivyo The New Encyclopædia Britannica hufikia mkataa huu: “Masimulizi hayo ya watu tofauti-tofauti huthibitisha kwamba katika nyakati za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia shaka kamwe uhakika wa kuwako kwa Yesu, ambao ulikanushwa kwa mara ya kwanza na bila sababu za kutosha mwishoni mwa karne ya 18, wakati wa karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.”
Kwa Kweli Yesu Alikuwa Nani?
11. (a) Kwa msingi, ni nini kilicho chanzo cha pekee cha habari ya kihistoria juu ya Yesu? (b) Wafuasi wa Yesu mwenyewe walikuwa na swali gani juu ya utambulisho wake?
11 Hata hivyo, kwa msingi, yote yanayojulikana sasa juu ya Yesu yaliandikwa na wafuasi wake wa karne ya kwanza. Ripoti zao zimehifadhiwa katika zile Gospeli—vitabu vya Biblia vilivyoandikwa na wawili wa mitume wake, Mathayo na Yohana, na wanafunzi wake wawili, Marko na Luka. Masimulizi hayo ya wanaume hao yafunua nini kuhusu utambulisho wa Yesu? Kwa kweli yeye alikuwa nani? Washirika wa Yesu wa karne ya kwanza walitafakari juu ya swali hilo. Walipomwona Yesu akituliza kimuujiza bahari iliyochafuliwa na upepo kwa kuikemea, walistaajabu kwa kushangaa mno: “Ni nani huyu?” Katika pindi ya baadaye, Yesu aliuliza mitume wake: “Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?”—Marko 4:41; Mathayo 16:15.
12. Tunajuaje kwamba Yesu si Mungu?
12 Kama ungeulizwa swali hilo, wewe ungejibuje? Kwa kweli Yesu alikuwa nani? Bila shaka, wengi katika Jumuiya ya Wakristo wangesema kwamba yeye alikuwa Mungu Mweza Yote katika umbo la kibinadamu, Mungu aliyejivika mwili wa kibinadamu. Hata hivyo, walioshirikiana kibinafsi na Yesu hawakuamini kamwe kwamba yeye alikuwa Mungu. Mtume Petro alimwita “Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16) Na hata utafute-tafute kwa kadiri gani, wewe hutapata kusoma kamwe kwamba Yesu alidai kuwa Mungu. Badala ya hivyo, yeye aliwaambia Wayahudi, kwamba yeye alikuwa “Mwana wa Mungu,” si Mungu.—Yohana 10:36.
13. Yesu alitofautianaje na watu wote wengine?
13 Yesu alipotembea juu ya bahari iliyochafuliwa na upepo mkali, wanafunzi walivutiwa sana na uhakika wa kwamba yeye hakuwa mtu wa kawaida tu kama mtu mwingine yeyote. (Yohana 6:18-21) Yeye alikuwa mtu wa pekee sana. Hiyo ni kwa sababu wakati uliotangulia yeye alikuwa ameishi akiwa mtu wa roho pamoja na Mungu katika mbingu, ndiyo, akiwa malaika, anayetambulishwa katika Biblia kuwa malaika mkuu. (1 Wathesalonike 4:16; Yuda 9) Mungu alikuwa amemuumba kabla ya Yeye kuumba vitu vingine vyote. (Wakolosai 1:15) Hivyo, kwa vipindi virefu vya wakati visivyojulikana, kabla hata ulimwengu wote mzima uonekanao haujaumbwa, Yesu alionea shangwe ushirika wa karibu sana pamoja na Baba yake mbinguni, Yehova Mungu, yule Muumba Mkuu.—Mithali 8:22, 27-31; Mhubiri 12:1.
14. Yesu alikujaje kuwa mwanadamu?
14 Kisha, miaka elfu mbili hivi iliyopita, Mungu alihamisha uhai wa Mwana wake akautia ndani ya tumbo la uzazi la mwanamke mmoja. Hivyo Yesu akapata kuwa mwana wa kibinadamu wa Mungu, aliyezaliwa kwa njia ya kawaida kupitia mwanamke. (Wagalatia 4:4) Yesu alipokuwa akikua katika tumbo la Mariamu, mama yake, na baadaye alipokuwa akikua akiwa mvulana, aliwategemea wale ambao Mungu alikuwa amewateua wawe wazazi wake wa kidunia. Mwishowe Yesu akafikia hali ya kuwa mwanamume aliye mtu mzima, na kwa wazi ndipo akapewa uwezo wa kukumbuka kikamili ushirika wake wa wakati uliopita akiwa pamoja na Mungu katika mbingu. Hilo lilitukia ‘wakati mbingu zilipomfunukia’ kwenye ubatizo wake.—Mathayo 3:16; Yohana 8:23; 17:5.
15. Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa binadamu kamili wakati alipoishi duniani?
15 Kweli kweli, Yesu alikuwa mtu wa pekee sana. Hata hivyo, yeye alikuwa mwanadamu, aliyelingana na Adamu, yule mwanadamu ambaye aliumbwa na Mungu awali na kuwekwa katika bustani ya Edeni. Mtume Paulo alieleza hivi: “Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha.” Yesu aitwa “Adamu wa mwisho” kwa sababu, kama yule Adamu wa kwanza, Yesu alikuwa binadamu mkamilifu. Lakini baada ya Yesu kufa, alifufuliwa na kujiunga tena na Baba yake mbinguni akiwa mtu wa roho.—1 Wakorintho 15:45.
Jinsi ya Kujifunza Juu ya Mungu kwa Njia Iliyo Bora Zaidi
16. (a) Ni nini kilichofanya kushirikiana pamoja na Yesu kuwe pendeleo kubwa sana? (b) Kwa nini ingeweza kusemwa kwamba kumwona Yesu kulikuwa sawa na kumwona Mungu?
16 Ebu fikiria kidogo mapendeleo mazuri ajabu ambayo baadhi ya watu walionea shangwe wakishirikiana kibinafsi na Yesu wakati alipokuwa duniani! Wazia kumsikiliza, kumtazama, na hata kuongea na kufanya kazi pamoja na Yule ambaye alikuwa ametumia labda mabilioni ya miaka akiwa mwandamani wa karibu sana wa Yehova Mungu katika mbingu! Akiwa mwana mwaminifu, Yesu aliiga Baba yake wa kimbingu katika kila jambo alilofanya. Kwa kweli, yeye aliiga Baba yake kikamili sana hivi kwamba angeweza kuwaambia mitume wake hivi muda mfupi kabla ya kuuawa kwake: “Aliyeniona mimi amemwona Baba” pia. (Yohana 14:9, 10) Ndiyo, katika kila hali aliyokabili hapa duniani, Yesu alifanya sawasawa na vile Baba yake, Mungu Mweza Yote, angalifanya kama ni Yeye mwenyewe angalikuwa hapa. Hivyo tujifunzapo juu ya maisha na huduma ya Yesu Kristo, kwa kweli, sisi huwa tunajifunza Mungu ni mtu wa aina gani hasa.
17. Ni kusudi gani jema lililotimizwa na mfululizo katika Mnara wa Mlinzi wa “Maisha na Huduma ya Yesu”?
17 Kwa kusudi hilo, ule mfululizo wa makala “Maisha na Huduma ya Yesu,” uliokuwako katika matoleo yaliyofuatana ya Mnara wa Mlinzi tangu Agosti 1, 1985, hadi Juni 1991, haukuandaa maelezo mazuri tu juu ya mwanamume Yesu bali pia ulifundisha mambo mengi sana juu ya Baba yake wa kimbingu, Yehova Mungu. Baada ya visehemu vyao viwili vya kwanza, mhudumu mmoja painia aliandikia Sosaiti kwa uthamini, akisema: “Kuna njia gani bora zaidi ya kumkaribia zaidi Baba kuliko kupata kumjua vizuri zaidi Mwanaye!” Hiyo ni kweli kama nini! Utunzaji mwororo wa Baba kwa watu na moyo wake wa ukarimu hukuzwa katika maisha ya Mwana huyo.
18. Ni nani aliye Mwanzilishi wa ujumbe wa Ufalme, na Yesu alikirije hilo?
18 Upendo wa Yesu kwa Baba yake, kama ulivyodhihirishwa kwa unyenyekeo wake kamili kwa mapenzi ya Baba yake, kweli kweli ni jambo zuri kuona. “Sifanyi neno kwa nafsi yangu,” Yesu akawaambia Wayahudi waliotaka kumuua, “ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.” (Yohana 8:28) Hivyo, basi, Yesu siye aliyekuwa mwanzilishi wa ujumbe wa Ufalme aliohubiri. Alikuwa ni Yehova Mungu! Na kwa kurudia-rudia Yesu alionyesha kuwa Baba yake ndiye chanzo chao. “Kwa sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu,” akasema, “bali Baba aliyenipeleka, yeye mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. . . . Basi hayo ninenayo mimi, kama Baba alivyoniambia, ndivyo ninenavyo.”—Yohana 12:49, 50.
19. (a) Tunajuaje kwamba Yesu alifundisha katika njia ambayo Yehova hufundisha? (b) Ni kwa nini Yesu alikuwa yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi?
19 Hata hivyo, Yesu hakunena au kuyafundisha tu aliyoambiwa na Baba. Yeye alifanya zaidi ya hayo. Aliyanena au kufundisha katika njia ile Baba angaliyanena au kuyafundisha. Zaidi ya hilo, katika utendaji na mahusiano yake, alijiendesha na kutenda kama vile Baba angalijiendesha na kutenda chini ya hali zinazofanana na hizo. Yesu alieleza, “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile.” (Yohana 5:19) Katika kila njia, Yesu alikuwa mfano mkamilifu wa Baba yake, Yehova Mungu. Hivyo si ajabu kwamba Yesu alikuwa ndiye yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi! Hakika, basi, ni jambo lenye umaana muhimu kutafakari sana juu ya mtu huyu wa maana kuliko wote!
Upendo wa Mungu Waonwa Katika Yesu
20. Mtume Yohana angejuaje kwamba “Mungu ni upendo”?
20 Twajifunza nini hasa tufanyapo funzo lenye kina sana, la uangalifu juu ya maisha na huduma ya Yesu? Naam, mtume Yohana alikiri kwamba “hakuna mtu aliyemwona Mungu.” (Yohana 1:18) Hata hivyo, Yohana aliandika hivi kwenye 1 Yohana 4:8 akiwa na uhakika kamili: “Mungu ni upendo.” Yohana angeweza kusema hivyo kwa sababu alijua upendo wa Mungu kupitia yale aliyoona katika Yesu.
21. Ni nini kuhusu Yesu kilichomfanya awe yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi?
21 Kama vile Baba, Yesu alikuwa mwenye huruma, mwenye fadhili, mnyenyekevu, na mwenye kukaribika. Wale walio dhaifu na walioonewa walihisi wakistarehe wakiwa pamoja naye, hali moja na watu wa aina zote—wanaume, wanawake, watoto, matajiri, na maskini, wenye nguvu, na pia wenye kujulikana kuwa watenda dhambi. Kweli kweli, hasa kielelezo bora zaidi cha upendo wa Yesu, katika kumwiga Baba yake, ndicho kilichomfanya awe yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi. Hata Napoléon Bonaparte anaripotiwa kuwa alisema hivi: “Alexander, Kaisari, Charlemagne, na mimi mwenyewe tulianzisha milki mbalimbali, lakini kazi zetu kuu zilitegemea nini? Zilitegemea uwezo. Yesu peke yake ndiye aliyeanzisha ufalme wake juu ya upendo, na hadi siku ya leo mamilioni ya watu wangekufa kwa ajili yake.”
22. Ni nini kilichofanya mafundisho ya Yesu yawe yenye kuleta mabadiliko makubwa sana?
22 Mafundisho ya Yesu yalikuwa yenye kuleta mabadiliko makubwa sana. “Msishindane na mtu mwovu,” akahimiza Yesu, “lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili.” “Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi.” ‘Yo yote myatakayo mtendewe na wengine, watendeeni vivyo hivyo.’ (Mathayo 5:39, 44; 7:12) Ulimwengu ungekuwa tofauti kama nini kama kila mtu angetumia mafundisho hayo bora sana!
23. Yesu alifanya nini kugusa mioyo na kusukuma watu watende mema?
23 Mifano, au vielezi vya Yesu, viligusa mioyo, vikawasukuma watu watende mema na kuepuka mabaya. Huenda ukakumbuka ile hadithi yake ijulikanayo sana ya Msamaria mwenye kudharauliwa ambaye alisaidia mtu wa taifa jingine aliyejeruhiwa hali watu wenye kujionyesha kuwa wenye kufuata dini sana wa taifa lake mwenyewe hawakumsaidia. Au ule mfano wa baba mwenye huruma, mwenye kusamehe na mwana wake mpotevu. Na namna gani ile hadithi ya mfalme aliyesamehe mtumwa wake deni la dinari milioni 60, hali mtumwa huyo alimgeukia mtumwa mwenzake na kuagiza atupwe gerezani kwa kutoweza kulipa deni la dinari 100? Kwa mifano rahisi, Yesu alifanya matendo ya ubinafsi na pupa yachukize, na matendo ya upendo na rehema yavutie sana!—Mathayo 18:23-35; Luka 10:30-37; 15:11-32.
24. Ni kwa nini twaweza kusema kwamba Yesu pasipo shaka alikuwa ndiye yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi?
24 Hata hivyo, jambo lililovuta watu kwa Yesu hasa na kuwa na uvutano wenye mafaa kwao lilikuwa kwamba maisha yake mwenyewe yalilingana kikamilifu na yale aliyofundisha. Yeye alizoea aliyohubiri. Kwa subira yeye alivumilia makosa ya wengine. Wakati wanafunzi wake walipogombana juu ya ni nani aliyekuwa mkuu kupita wote, yeye aliwasahihisha kwa fadhili badala ya kuwakemea vikali. Alihudumia mahitaji yao kwa unyenyekevu, hata akaosha miguu yao. (Marko 9:30-37; 10:35-45; Luka 22:24-27; Yohana 13:5) Na, hatimaye, kwa kupenda kwake mwenyewe alipatwa na kifo chenye maumivu, si kwa ajili yao tu bali kwa ajili ya jamii yote ya kibinadamu! Pasipo shaka, Yesu alikuwa ndiye yule mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi.
Ungejibube?
◻ Kuna uthibitisho gani kwamba Yesu alikuwa mtu halisi katika historia?
◻ Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa mwanadamu, hata hivyo alitofautianaje na watu wote wengine?
◻ Ni kwa nini kujifunza juu ya maisha ya Yesu ni njia iliyo bora zaidi ya kujifunza juu ya Mungu?
◻ Twaweza kujifunza nini juu ya upendo wa Mungu kwa kujifunza juu ya Yesu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mitume wa Yesu walistaajabu kwa kushangaa mno: “Kwa kweli huyu ni nani?”