Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 6/15 kur. 22-27
  • Kuvua Watu Katika Maji ya Tufe Lote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuvua Watu Katika Maji ya Tufe Lote
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuvua Watu, Kazi Ngumu ya Tufeni Pote
  • Maendeleo Katika Kazi ya Uvuvi ya Tufeni Pote
  • Wote Wana Sehemu
  • Mambo Yanayochangia Ukuzi
  • Je! Tunaweza Kufanya Maendeleo?
  • Kutumika Tukiwa Wavuvi wa Watu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Uvuvi Katika Bahari ya Galilaya
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Juya (Wavu) na Samaki Zinamaanisha Nini Kwako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 6/15 kur. 22-27

Kuvua Watu Katika Maji ya Tufe Lote

“Maana, ijapokuwa naihubiri Injili, sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!”—1 WAKORINTHO 9:16.

1, 2. (a) Ni nani ambao kwa kweli wamefanya kazi ngumu inayoonyeshwa kwenye 1 Wakorintho 9:16, na kwa nini unajibu hivyo? (b) Ni daraka gani ambalo Mashahidi wa Yehova wamekubali?

NI NANI katika karne hii ya 20 ambao kwa kweli wamefanya kazi ngumu inayoonyeshwa na maneno ya Paulo yaliyo juu? Ni nani wameenda kwenye ulimwengu kwa mamilioni ili kuvua wanaume na wanawake ambao “ni maskini wa roho”? (Mathayo 5:3) Ni nani ambao wamejasiria kufungwa na kufa, na wakapatwa na mambo hayo katika mabara mengi, kwa sababu ya kutimiza amri ya Kristo kwenye Mathayo 24:14?

2 Maandishi yanaonyesha: Ni Mashahidi wa Yehova. Mwaka jana pekee Mashahidi zaidi ya milioni nne walienda nyumba kwa nyumba ‘wakitangaza habari njema’ katika nchi na maeneo 211 na katika lugha zaidi ya 200. Hao hawakuwa tu kikundi kilichochaguliwa cha wamishonari waliozoezwa. La, Mashahidi wa Yehova wote wanahisi kuwa na daraka la kuhubiri na kufundisha kutoka nyumba kwa nyumba na katika kila pindi inayofaa. Kwa nini wao huhisi uhitaji huo wa kushiriki itikadi zao na wengine? Kwa sababu wanatambua kwamba maarifa huleta daraka—Ezekieli 33:8, 9; Warumi 10:14, 15; 1 Wakorintho 9:16, 17.

Kuvua Watu, Kazi Ngumu ya Tufeni Pote

3. Kazi ya uvuvi lazima ifikie kadiri gani?

3 Kazi hiyo kubwa ya uvuvi haifanywi kwenye mto fulani tu, au ziwa au hata kwenye bahari moja. La, kama Yesu alivyoamuru, ingepaswa ifanywe “katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Kabla ya kupaa kwenda kwa Baba yake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW]; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari.”—Mathayo 28:19, 20.

4. (a) Ni nini lazima kiwe kiliwashangaza wafuasi wa Yesu Wayahudi wa mapema? (b) Mashahidi wa Yehova huonaje kadiri ya kazi yao ya kuhubiri?

4 Kwa wafuasi wa Yesu Wayahudi, hilo lazima liwe lilikuwa agizo la kushangaza. Yeye alikuwa akiwaambia wanafunzi wake Wayahudi kwamba wangelazimika sasa kwenda kwa wasio Wayahudi “wasio safi” wa mataifa yote na kuwafundisha. Iliwabidi wafanye mabadiliko fulani ili waelewe maana na kutenda kupatana na mgawo huo. (Matendo 10:9-35, NW) Lakini hakukuwa na njia ya mkato; Yesu alikuwa amewaambia katika mfano kwamba “lile konde ni ulimwengu.” Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova leo huona ulimwengu mzima kuwa ndio mandhari ya haki zao za uvuvi. Hakuwezi kuwa na “mpaka wa maji wa kilometa 20” au “maji ya eneo la nchi” yanayozuia kazi waliyopewa na Mungu. Wakati mwingine utambuzi unahitajika mahali ambapo uhuru wa ibada haupo. Hata hivyo, wao huvua wakiwa na uharaka wa mambo. Kwa nini hivyo? Kwa sababu matukio ya ulimwengu na utimizo wa unabii wa Biblia yanaonyesha kwamba sisi tumo katika sehemu ya mwisho ya kazi ya uvuvi ya tufeni pote.—Mathayo 13:38; Luka 21:28-33.

Maendeleo Katika Kazi ya Uvuvi ya Tufeni Pote

5. Ni watu wa aina gani wanaoitikia kazi ya uvuvi ya ulimwenguni pote?

5 Wengi wa warithi wa Ufalme wapakwa-mafuta “walivuliwa” kutoka kwa mataifa kabla ya 1935, kwa hiyo idadi yao kamili imekamilishwa kwa msingi. Kwa hiyo, hasa tangu 1935, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitafuta watu hao wanyenyekevu wanaoweza kusemwa kuwa ‘wapole’ ambao ‘watairidhi nchi.’ (Zaburi 37:11, 29) Hao ni watu “wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanyika.” Wanachukua hatua kwa kupendelea utawala wa Ufalme wa Mungu kabla ya “dhiki kubwa” kufyatuka juu ya mfumo wa mambo wa Shetani ulio mpotovu na wenye ufisadi na waabudu wake kuamriwa kwenye “tanuru ya moto” ya uharibifu wa mwisho.—Ezekieli 9:4; Mathayo 13:47-50; 24:21.

6, 7. (a) Ni hatua gani zilizochukuliwa katika 1943 kuhusiana na kazi ya kuhubiri? (b) Matokeo yamekuwa nini?

6 Je! kazi ya uvuvi wa tufeni pote imefanikiwa kufikia sasa? Acha mambo ya hakika yajieleze yenyewe. Huko nyuma katika 1943, Vita ya Ulimwengu 2 bado ilikuwa inapiganwa, na bado ndugu waaminifu wapakwa-mafuta kwenye makao makuu ulimwenguni ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York, waliona kimbele kwamba utendaji mkubwa wa uvuvi wa tufeni pote ungepaswa ufanywe. Kwa hiyo, ni hatua zipi zilizochukuliwa?a—Ufunuo 12:16, 17.

7 Katika 1943 Watchtower Society ilianzisha shule ya wamishonari iitwayo Gileadi (Kiebrania, “Rundo la Shahidi”; Mwanzo 31:47, 48) iliyoanza kuzoeza wamishonari mia moja kila miezi sita ili waweze kutumwa nje wakiwa wavuvi wa ufananisho ulimwenguni pote. Wakati huo, kulikuwako Mashahidi 126,329 tu wakivua watu kwa bidii katika mabara 54. Kwa muda wa miaka kumi hesabu hizo zilikuwa kwa kweli zimeruka hadi kuwa Mashahidi 519,982 katika mabara 143! Kwa hakika, Shule ya Gileadi ilikuwa inatokeza wavuvi wanaume na wanawake walio hodari, waliotaka kwa hiari kwenda kwenye tamaduni za kigeni na kuzoeleana na maji mapya ya kuvulia. Kama tokeo, maelfu ya watu wenye mioyo minyofu waliitikia. Wamishonari hao, na Mashahidi wa mahali waliohubiri nao, waliweka msingi wa ongezeko zuri ajabu linalotukia sasa.

8, 9. (a) Ni mifano gani inayoweza kutajwa ya kazi ya umishonari yenye kutokeza? (b) Wamishonari wamepataje kuona ukuzi wenye kutokeza katika mashamba yao? (Ona pia Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1992.)

8 Wakongwe wengi waaminifu kutoka madarasa hayo ya mapema ya Gileadi bado wanatumikia katika migawo yao ya kigeni, hata ingawa sasa wana umri unaopita miaka 70 au hata 80. Mfano mmoja unaoonyesha hilo ni ule wa Eric Bitten mwenye umri wa miaka 82 na mke wake, Christina, waliohitimu darasa la 15 la Gileadi katika 1950 na bado wanatumikia katika Brazili. Walipoenda kutumikia katika Brazili, kulikuwako Mashahidi wanaopungua 3,000 katika nchi hiyo. Sasa kunao zaidi ya 300,000! Kwa kweli, ‘mdogo amekuwa taifa hodari’ katika Brazili kwa sababu kazi ya uvuvi imekuwa na mazao.—Isaya 60:22.

9 Na tunaweza kusema nini kuhusu wamishonari katika Afrika? Wengi wao wamefaana na tamaduni zilizo tofauti kabisa na wamekuja kuwapenda watu Waafrika. Mfano mmoja ni wale ndugu wa kimwili John na Eric Cooke na wake zao, Kathleen na Myrtle, wanaotumikia sasa katika Afrika Kusini. John na Eric walihitimu darasa la nane katika 1947. Nchi ambazo mmoja au mwingine kati yao ametumikia ni Angola, Zimbabwe, Msumbiji, na Afrika Kusini. Baadhi ya wamishonari walikufa katika Afrika kwa sababu ya ugonjwa, na wengine kwa sababu ya vita na mnyanyaso, kama vile Alan Battey na Arthur Lawson, waliokufa wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe vya hivi karibuni katika Liberia. Na bado, maji ya Afrika yamethibitika kuwa yenye mazao mengi. Sasa kuna Mashahidi zaidi ya 400,000 waliotawanyika kotekote katika bara hilo kubwa.

Wote Wana Sehemu

10. Kwa nini na ni kwa njia gani mapainia wanafanya kazi ya kustahili pongezi?

10 Hata hivyo, ni lazima itambuliwe kwamba ingawa wamishonari wa kigeni wamefikia kuwa maelfu kadhaa, wahubiri na mapainiab wa mahali wamefikia kuwa mamilioni. Wao wanafanya sehemu iliyo kubwa ya kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Katika 1991 kulikuwako na wastani wa mapainia na wahudumu wasafirio 550,000. Ni idadi yenye kutokeza kama nini tufikiripo juu ya Mashahidi waaminifu hao wote wanaofanya jitihada ya pekee kushiriki katika kazi kubwa ya uvuvi, wakifikia wastani wa kuanzia saa 60 hadi 140 za mahubiri kila mwezi. Wengi hufanya hivyo kwa kujidhabihu wao wenyewe na fedha zao. Kwa nini? Kwa sababu wao wanampenda Yehova Mungu wao kwa moyo wao wote, akili zao zote, nafsi zao zote, na nguvu zao zote, na wanapenda jirani zao kama wao wenyewe.—Mathayo 22:37-39.

11. Kuna ithibati gani hakika kwamba roho ya Yehova inatenda kazi miongoni mwa watu wake?

11 Tunaweza kusema nini kuhusu wale Mashahidi wengineo zaidi ya milioni tatu unusu ambao hawako katika utumishi wa wakati wote lakini ambao hujitoa kikamili katika utumishi wa Yehova, kulingana na hali zao? Wengine wao ni wake, hata akina mama wanaotunza watoto wadogo, ambao hata hivyo hutoa sehemu ya wakati wao wa thamani kwa kazi ya uvuvi ya tufeni pote. Wengi wao ni waume au akina baba wenye kazi za kimwili za wakati wote; na bado, wanaweka wakati kando kwenye miisho-juma na jioni kuwafunza kweli watu ambao ni wageni kwao. Halafu kuna umati mkubwa wa wanaume na wanawake waseja pamoja na wachanga wanaoshiriki kuhubiri na hupendekeza kweli kwa mwenendo wao. Ni kikundi kipi kingine cha kidini ambacho kina wenye kujitolea wasiolipwa wapatao kuwa zaidi ya milioni nne wanaohubiri habari njema za utawala wa Ufalme wa Mungu kila mwezi? Kwa kweli hilo laonyesha wazi roho ya Yehova ikitenda kazi!—Zaburi 68:11; Matendo 2:16-18; linganisha Zekaria 4:6.

Mambo Yanayochangia Ukuzi

12. Ni kwa nini watu wanaitikia kweli na ni kwa idadi gani?

12 Kazi hiyo kubwa ya kuhubiri inaleta matokeo ya kutokeza kila mwaka. Katika 1991 Mashahidi wapya zaidi ya 300,000 walibatizwa kwa kuzamishwa kabisa majini. Hilo linalingana na makundi zaidi ya 3,000 yenye Mashahidi 100 kila moja! Yote hayo yanatimizwaje? Ebu tukumbuke yale Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka . . . Imeandikwa katika manabii, Na wote watakuwa wamefundishwa na Mungu. Basi kila aliyesikia na kujifunza kwa Baba huja kwangu.” Kwa hiyo, si kwa jitihada za kibinadamu tu kwamba mtu huitikia uvuvi wa tufeni pote. Yehova huona hali ya moyoni na kuwavuta kwake wale wanaostahili.—Yohana 6:44, 45; Mathayo 10:11-13; Matendo 13:48.

13, 14. Ni mwelekeo gani unaofaa ambao Mashahidi wengi wameonyesha?

13 Hata hivyo, wavuvi wa kibinadamu ndio wajumbe ambao Yehova hutumia kuwavuta watu kwake. Kwa hiyo, mwelekeo wao kwa watu na eneo wanakovulia ni wa maana. Inatia moyo jinsi gani kuona kwamba walio wengi wanathamini kwa moyo maneno ya Paulo kwa Wagalatia: “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”—Wagalatia 6:9.

14 Mashahidi wengi waaminifu wamekuwa wakihubiri kwa miongo ya miaka, wakitazama kwa uangalifu matukio ya ulimwengu. Wameona Unazi, Ufashisti, na mifumo mingine ya kimabavu ikisitawi na kuangamia. Wengine wamejionea vita vingi ambavyo vimepiganwa tangu 1914. Wameona watawala wa ulimwengu wakiweka tumaini lao katika Ushirika wa Mataifa halafu katika Umoja wa Mataifa. Wameona kazi ya Yehova ikipigwa marufuku na baadaye ikahalalishwa kisheria katika mabara mengi. Katika yote hayo, Mashahidi wa Yehova hawajaacha kufanya yaliyo mema, kutia na kutumikia wakiwa wavuvi wa watu. Ni rekodi iliyoje ya kushika uadilifu wa kimaadili!—Mathayo 24:13.

15. (a) Ni misaada gani ambayo tumepata katika kufaana na mahitaji ya eneo letu la ulimwenguni pote? (b) Vichapo vimesaidiaje katika mgawo wako?

15 Kuna mambo mengine ambayo yamechangia ukuzi huo wa ulimwenguni pote. Moja ni mwelekeo wa kubadilikana wa wavuvi hao wa watu kuhusiana na mahitaji ya eneo. Kukiwa na kuhama kwa watu wa tamaduni, dini, na lugha tofauti, Mashahidi wa Yehova wamepanua uelewevu wao wa maoni hayo tofauti-tofauti. Na kundi la ulimwenguni pote limesaidia sana kwa kutayarisha Biblia na fasihi ya Biblia katika lugha zaidi ya 200. Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, ikiwa nzima au kwa sehemu, sasa inapatikana katika lugha 13, kutia na Kicheki na Kislovaki. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! sasa inapatikana katika lugha 198, kuanzia Kialbania hadi Kizulu, kukiwa na uchapishaji wa nakala milioni 72. Kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi tayari kimetafsiriwa katika lugha 69. Mankind’s Search for God, ambacho kimetafsiriwa katika lugha 29, hutoa mwono-ndani wa asili ya itikadi za mifumo mikuu ya kidini ya ulimwengu na kinathibitika kuwa msaada wa pekee katika uvuvi wa tufeni pote.

16. Wengine wameitikiaje uhitaji mbalimbali katika mabara mengine?

16 Ni nini kingine kimesogeza mbele kazi ya uvuvi ya tufeni pote? Maelfu wamekuwa wakiitikia ‘mwito wa Makedonia’ kwa moyo wa hiari. Kama vile ambavyo Paulo alikuwa tayari kuondoka Esia Ndogo hadi Makedonia katika Ulaya, kwa mwito wa Mungu, Mashahidi wengi wamehamia mabara na maeneo ambako kuna uhitaji zaidi wa wahubiri wa Ufalme, kutia na wazee na watumishi wa huduma. Wao wamekuwa kama wavuvi halisi wanaopata maji ya kwao yakiwa yamevuliwa kikamili na kuhamia kwenye maji ambamo kuna vyombo vichache zaidi na samaki ni wengi.—Matendo 16:9-12; Luka 5:4-10.

17. Ni mifano gani tuliyo nayo ya wale ambao wameitikia ‘mwito wa Makedonia’?

17 Madarasa ya shule ya wamishonari ya Gileadi ya hivi karibuni yametia ndani wanafunzi kutoka nchi mbalimbali za Ulaya ambao wamejifunza Kiingereza na hivyo wamejitoa wenyewe kwa utumishi katika mabara na tamaduni nyinginezo. Vivyo hivyo, kupitia Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, ndugu wengi waseja hupewa miezi miwili ya mazoezi ya bidii na kisha hutumwa kwenye mataifa mengine ili kuimarisha makundi na mizunguko. Sehemu nyingine za uvuvi zilizo za pekee zimo katika maeneo yanayopatikana sasa katika Ulaya ya Mashariki na jamhuri nyinginezo zilizokuwa za Urusi.—Linganisha Warumi 15:20, 21.

18. (a) Kwa nini mapainia mara nyingi huwa wahudumu wenye matokeo? (b) Wao wanaweza kusaidiaje wengine katika kundi?

18 Msaada wa ziada katika kazi ya uvuvi ya ulimwenguni pote ni Shule ya Utumishi wa Painia inayohudhuriwa na mapainia wa kawaida. Kupitia majuma mawili ya pitio la bidii la kichapo Kung’aa Kama Wamulikaji Katika Ulimwengu, kilichotayarishiwa mapainia kihususa, wao hufanyia maendeleo uwezo wao wa kihuduma wanapojifunza vichwa kama vile “Kuifuatia Njia ya Upendo,” “Fuata Yesu akiwa Kielelezo,” na “Kusitawisha Ufundi wa Kufundisha.” Jinsi makundi yote yalivyo na shukrani kuwa na vikundi hivyo vya wavuvi wa nyumba kwa nyumba wanaostahili ambao wanaweza kuwazoeza wengi katika kazi hii kubwa ya uvuvi!—Mathayo 5:14-16; Wafilipi 2:15; 2 Timotheo 2:1, 2.

Je! Tunaweza Kufanya Maendeleo?

19. Kama vile mtume Paulo, tunaweza kufanyaje maendeleo katika huduma yetu?

19 Kama vile Paulo, tunataka tuwe na mwelekeo chanya, wenye kutazama mbele. (Wafilipi 3:13, 14) Yeye alifaana na aina yote ya watu na hali. Alijua jinsi ya kupata mambo ya kukubaliana na jinsi ya kutoa sababu kwa kutegemea mielekeo na tamaduni za mahali. Tunaweza kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa kuwa chonjo kwa maitikio ya mwenye nyumba kwa ujumbe wa Ufalme halafu kugeuza utoaji wetu uweze kufaana na mahitaji ya mtu huyo. Tukiwa na misaada ya namna-namna ya kujifunzia Biblia, tunaweza kutoa ule unaofaa mtazamo wa mtu huyo binafsi. Mambo mengine ya maana pia ni kuwa wenye kubadilikana na walio chonjo katika uvuvi wenye mazao.—Matendo 17:1-4, 22-28, 34; 1 Wakorintho 9:19-23.

20. (a) Kwa nini kazi yetu ya uvuvi ni ya maana sana sasa? (b) Daraka letu sasa tukiwa mtu mmoja mmoja ni jipi?

20 Kwa nini kazi hii ya pekee ya uvuvi wa tufeni pote ni ya maana sana sasa? Kwa sababu kutokana na unabii mbalimbali wa Biblia unaoonyeshwa na mambo ambayo yametukia na yanayotukia, ni wazi kwamba mfumo wa ulimwengu wa Shetani unaelekea kwenye upeo wenye msiba. Kwa hiyo, sisi Mashahidi wa Yehova tunapaswa kuwa tukifanya nini? Makala tatu za funzo katika gazeti hili zimekazia daraka letu la kuwa wenye shughuli na bidii katika utendaji wetu wa uvuvi katika sehemu yetu ya maji ya tufeni pote. Tuna uhakikisho imara kutoka kwa Biblia kwamba Yehova hatasahau utendaji wetu wa uvuvi wenye bidii. Paulo alisema: “Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia. Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile, kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”—Waebrania 6:10-12.

[Maelezo ya Chini]

a Ona pia Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kurasa 185 na 186, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

b “Mhubiri painia . . . mfanyakazi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.”—Webster’s Third New International Dictionary.

Je! Wakumbuka?

◻ Kwa nini Mashahidi wa Yehova huona ulimwengu mzima kuwa ndio mandhari yao ya utendaji wa uvuvi?

◻ Shule ya mishonari ya Gileadi imekuwaje baraka kwa kazi ya uvuvi?

◻ Ni baadhi ya mambo gani ambayo yamechangia kufanikiwa kwa Mashahidi wa Yehova?

◻ Sisi tukiwa mtu mmoja mmoja tunaweza kufanyaje maendeleo katika huduma yetu ya Kikristo?

[Chati katika ukurasa wa 24]

MATOKEO YA UVUVI WA KIMATAIFA

Mwaka Mabara Mashahidi

1939 61 71,509

1943 54 126,329

1953 143 519,982

1973 208 1,758,429

1983 205 2,652,323

1991 211 4,278,820

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kazi ya kutoa ushahidi bado inafanywa miongoni mwa wavuvi Wagalilaya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki