Kuithamini Ile Zawadi ya Uhai Yenye Thamani Kubwa
UHAI—ni mali yenye thamani kubwa kama nini! Bila uhai hatuwezi kufanya lolote. Unapopotezwa, hauwezi kurudishwa kwa njia yoyote ya kibinadamu. Uhai wetu ukiwa hatarini, tunafanya lolote tuwezalo kwa kufaa ili kuuhifadhi. Kwani, wengine hata wataomba msaada upitao uwezo wa kibinadamu wanapokuwa taabani!
Tunakumbushwa juu ya usimulizi wa Biblia wa merikebu iliyopatikana katika dhoruba yenye nguvu baharini. Ilipokuwa karibu kuvunjika, “mabaharia wakaogopa, kila mtu akamwomba mungu wake.” Baadaye, wao wote walimlilia Mungu wa kweli: “Twakuomba, Ee BWANA [Yehova, NW], twakuomba, tusiangamie.” Usimulizi huo wa Biblia husema hivi pia: “Nao wakatupa baharini shehena iliyokuwa merikebuni, ili kuupunguza uzito wake.”—Yona 1:4-6, 14; linganisha Matendo 27:18, 19.
Mabaharia hao walikuwa tayari hata kuzidhabihu mali za kimwili zenye kuthaminiwa katika jitihada ya kuhifadhi uhai wao. Tunaweza kurudisha upya mali za kimwili—lakini sio uhai. Na kwa sababu sisi huthamini uhai wetu kisilika, tunaepuka hatari. Tunakula, tunajivika nguo, na kuilisha miili yetu. Tunatafuta tiba tunapokuwa wagonjwa.
Hata hivyo, Mpaji wa uhai hutaka mengi zaidi kwetu kuliko kufuata kwetu tu silika za kujilinda wenyewe. Kwa vyovyote vile, uhai ni zawadi ya thamani kubwa, nayo hutoka kwa Mtu (Nafsi) aliye mashahuri zaidi katika ulimwengu wote mzima. Kwa sababu ya uthamini wa unyofu kwa ajili ya Mpaji na zawadi pia, je tusiuthamini uhai? Na je, hilo lisingetia ndani kuuthamini uhai wa watu wengine?
Basi, haipasi itushangaze kwamba Sheria ambayo Yehova Mungu alilipa taifa la Israeli lilitia ndani amri zilizobuniwa ili kulinda uhai na afya ya wengine. (Kutoka 21:29; Kumbukumbu la Torati 22:8) Wakristo leo wanapaswa vile vile wahangaikie usalama wa kimwili. Kwa mfano, ikiwa una watu wachanga nyumbani mwako, je, wewe huacha karibu-karibu shanga, pini, au vyombo vikali viwezavyo kusababisha madhara ma-baya sana kwa mtoto anayecheza navyo au kuvimeza bila kujua hatari yavyo? Je! kemikali na dawa za hatari huwekwa mahali pasipoweza kufikiwa na watoto? Maji inapomwagwa sakafuni, je, wewe huyapangusa upesi ili kuzuia aksidenti? Je! wewe huona kwamba vyombo vitumiavyo stima vyenye kasoro vinarekebishwa mara moja? Je! gari lako hudumishwa kwa kawaida? Je! wewe ni dereva wa salama? Ikiwa kwa kweli unathamini thamani kubwa ya uhai, utasukumwa kujihadhari ifaavyo katika mambo hayo na mengine kama hayo.
Lakini kwa huzuni, wengine hupuuza hata uhai wao wenyewe. Kwa mfano, ni nani leo asiyejua kwamba kuvuta sigareti huharibu afya? Hata hivyo, mamilioni ni watumwa wa zoea hilo, huku afya yao ikidhoofika kila wakati wanapovuta pumzi hiyo yenye sumu. Wengine hutumia vibaya dawa za kulevya, na wengine vile vile hutumia vibaya vileo, vyote kwa hasara yao wenyewe. UKIMWI ni ugonjwa wenye kuua usio na dawa ijulikanayo. Lakini wengi wangaliepuka kupatwa na ugonjwa huo ikiwa wangaliepukana na ukosefu wa maadili katika ngono, aina fulani za matumizi mabaya ya dawa za kulevya, na kutiwa damu mishipani. Ni ukosefu wa kuthamini uhai wenye kuhuzunisha kama nini!—Warumi 1:26, 27; 2 Wakorintho 7:1.
Badiliko Lawezekana!
Wale wamthaminio Muumba wao Mkuu, Yehova, wana sababu yenye nguvu ya kuona uhai kuwa wenye thamani kubwa. Uhai ni zawadi takatifu itokayo kwake. Kwa hiyo wao wana nia ya kufanya mabadiliko yoyote yanayohitajiwa ili kuitendea kama zawadi ya kimungu. Ona lile lililompata Kwaku, mwalimu mmoja katika Ghana. Akiwa mlevi asiyejali, alikuwa akitumia vibaya uhai wake.
Kwaku akumbuka hivi: “Nilijaribu kumlazimisha mke wangu anistahi, jambo ambalo mara nyingi liliongoza kwenye ugomvi mkali na mapigano, hasa nilipokuwa nimelewa. Kwa sababu ya kunywa vileo kupindukia, mara nyingi nilikuwa bila pesa, na mara nyingi nilikosa kuandaa pesa kwa ajili ya riziki ya familia. Kwa kueleweka, hilo lilimwudhi sana mke wangu. Wakati wowote nilipopungukiwa na fedha (na hilo lilitukia mara nyingi), nilifanya lolote nililoweza kufanya ili kulitegemeza zoea langu. Wakati mmoja nilifikia kadiri ya kutumia kibinafsi pesa nilizokuwa nimekusanya kutoka kwa wanafunzi wangu za kuwasajili kwa ajili ya mtihani wa watu wote. Nilikunywa kupindukia na pia nikawanunulia vinywaji marafiki wangu tuliokunywa pamoja. Upesi siku ya kutoa hesabu ikanifikia. Kama mwalimu wangu mkuu asingeingilia kwa wakati ufaao, ningalipoteza kazi yangu.
“Maisha yangu yalikuwa katika hali mbaya sana. Niliaibika, lakini upesi nikaacha kuhisi hivyo. Halafu nikaanza kuwa na mawazo ya kujiua mwenyewe kwa sababu nilihisi kwamba nilikuwa nimekosa kufaulu maishani. Bado, sikuweza kujiweka huru na uzoevu wa vileo. Lakini siku moja nilipohusika katika ugomvi wa kulewa nikachomwa na kisu, nilikuja kupata ufahamu usiopendeza wa kwamba kupenda kwangu vileo kungegharimu uhai wangu siku moja.
“Katika wakati huo, Mashahidi wa Yehova walikuwa wamezuru nyumba yetu mara kwa mara, wakijaribu kutufanya tupendezwa na Biblia. Mke wangu na mimi tuliwaepuka sikuzote kwa sababu tulifikiri kwamba walikuwa udhia. Lakini pindi moja, niliamua kuwasikiliza kwa kuwahurumia. Funzo la Biblia upesi lilinijulisha juu ya lile taraja zuri ajabu la kuishi milele katika mfumo mpya wa Mungu. Kadiri nilivyojifunza Biblia kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova, ndivyo kadiri kina cha uthamini wangu ulivyokua kwa ajili ya Yehova akiwa Mpaji-Uhai na kwa ajili ya zawadi ya uhai itokayo kwake, na ndivyo kadiri nilivyozidi kuvutiwa na manufaa ya shauri la Biblia. Hilo lilinitia moyo zaidi nisafishe maisha yangu. Hilo halikuwa rahisi, kwani nilihitaji daima kupinga kile kidogo [kileo] pamoja na marafiki wangu wa zamani. Yehova, yule Msikilizaji wa sala, aliona azimio la moyo wangu akanisikia.a
Mke wangu, ingawa si mmoja wa Mashahidi wa Yehova, hunistahi sana pamoja na dini yangu kwa sababu ya lile badiliko kubwa analoona maishani mwangu na katika uhusiano wetu wa kindoa. Majirani wetu hawahitaji tena kuingilia katika mapigano kati ya mke wangu na mimi. Ninathamini ile amani ya akili ninayoonea shangwe. Kwa hakika, kumthamini Yehova Mungu akiwa Mpaji-Uhai wetu, kufuata maoni yake juu ya thamani kubwa ya uhai, na kutii maagizo yake juu ya namna ya kuishi ni njia pekee ya uhai ifaayo.
Toleo la Mungu la Uhai wa Milele
Maelfu, kama Kwaku, wamesaidiwa na Mashahidi wa Yehova ‘wavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.’ (Waefeso 4:24) Wamekuja kuthamini si uhai wao wa sasa tu bali pia tumaini la uhai wa milele katika paradiso ya kidunia. Biblia huahidi kwamba katika Paradiso hiyo yenye kufanywa na Mungu, hakuna mwenyeji wa dunia atakayepatwa na maumivu ya njaa ya daima, kwani “BWANA [Yehova, NW] wa majeshi atwafanyia mataifa yote . . . karamu ya vinono vilivyojaa mafuta.”—Isaya 25:6.
Kwa sasa, uhai, ingawa ni zawadi nzuri ajabu, ni wa muda tu. Kila mtu akabili kifo, na kifo ni pigo liumizalo kama nini! Kumwona mtu unaompenda akitokomea kutoka miongoni mwa walio hai kuingia ule ukimya wa kaburi ni jambo lenye kutaabisha, bila kutia chumvi. Lakini chini ya Ufalme wa Mungu, utakaotawalwa na Kristo, ahadi ya Yehova itatimizwa: “Hakutakuwako tena na kifo, wala uchungu, wala kilio, wala maumivu; maana ile hali ya kale imepita.”—Ufunuo 21:4, Habari Njema kwa Watu Wote.
Wakati huo zawadi ya uhai itaenezwa katika njia nzuri ajabu. Waokokaji wa dhiki ya mwisho kwenye dunia hii watakuwa na nafasi ya kuingia katika ukamili wa uhai. Halafu, kwa njia ya ufufuo, kurudisha kwa uhai, Yehova Mungu atawarudishia wale waliolala usingizi katika kifo, ile zawadi itokayo kwake. (Yohana 5:24, 28, 29) Hilo litamaanisha kurudi kwa wapendwa waliokufa na watu wa zamani waliomcha Mungu!
Je! hayo yote si mambo halisi? La, kwani “hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”—Luka 1:37; linganisha Ayubu 42:2.
Zaidi ya hayo, Yehova Mungu mwenyewe ameipa ainabinadamu uthabiti wa kwamba hayo yote yatatukia. Jinsi gani? Kwa kumdhabihu yule aliyekuwa kipenzi cha moyo wake, Mwana wake mpendwa, Yesu Kristo, atufidi kutoka katika dhambi na kifo. Warumi 8:32 hutuhakikishia hivi: “Yeye [Yehova Mungu] asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?” Biblia hutuambia sisi kwamba hilo litatia ndani kuisafisha ainabinadamu na uchafu wa kiadili na kuondolea mbali namna zote za ukosefu wa haki, uhalifu, na jeuri. (Isaya 11:9) Uhai hautaonwa tena kamwe kuwa wenye kukosa thamani.
Hata sasa, chini ya hali zisizokamilifu, uhai waweza kuwa wenye kufurahisha sana. Ni nani asiyependezwa na harufu yenye kutamanisha ya chakula, kupapaswa na upepo mwanana kwenye siku yenye ujoto, kuona mlima mtukufu, machweo yenye kupendeza, kijito kinachotiririka kwa utulivu, maua yenye rangi za kustaajabisha, sauti ya muziki mtamu, au wimbo wa ndege? Ebu tua kidogo. Fikiri, ingekuwaje kuonea shangwe mambo kama hayo kwa umilele?
Basi je, kuna maana yoyote ya kutupilia mbali lile pendeleo lenye thamani kubwa la kuishi milele kwa sababu ya jambo lenye kufurahisha la muda tu liwezalo kutolewa na mwendo wa maisha la kipumbavu, wenye kujifurahisha na anasa? (Linganisha Waebrania 11:25.) Kwa hekima, Biblia hutuhimiza ‘tusiendelee kuishi katika tamaa za wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu.’ (1 Petro 4:2) Twakutia moyo kwa bidii, naam, twakusihi, ufanye hivyo kwa kujifunza Neno la Mungu, Biblia, na kuyazoea mambo unayojifunza. (Yohana 13:17) Hivyo utakuwa na uhusiano mzuri na Yehova, yule Mungu mwenye wema na rehema nyingi sana, awezaye kukuthawabisha na uhai wa milele!
[Maelezo ya Chini]
a Kupona kutokana na uzoevu wa vileo ni kazi ngumu, mara nyingi ikihitaji msaada wa kitiba. Ona gazeti letu jenzi, Amkeni! la Mei 22, 1992, (Kiingereza), ili kupata habari yenye kusaidia juu ya jambo hilo.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Je! mtindo-maisha wako unaonyesha uthamini kwa ajili ya uhai?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ulimwengu mpya wa Mungu utaturuhusu tuonee shangwe kwa umilele mambo ya uhai yenye kufurahisha