Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 9/15 kur. 8-13
  • Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Dhambi Nyingine Haziwezi Kusameheka
  • Dhambi Zao Zilikuwa Zisizosameheka
  • Walisamehewa Dhambi Zao
  • Sababu za Kuwa na Uhakika Katika Msamaha wa Mungu
  • Msaada Kutoka kwa Wazee
  • Mungu Hutoa Nguvu
  • Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Dhambi Isiyoweza Kusamehewa Ni Nini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Je, Kuna Dhambi Isiyosameheka?
    Amkeni!—2003
  • Mungu Aliye “Tayari Kusamehe”
    Mkaribie Yehova
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 9/15 kur. 8-13

Yehova Husamehe kwa Njia Kubwa

“Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA [Yehova, “NW”], . . . naye atamsamehe kabisa [kwa njia kubwa, “NW”].”—ISAYA 55:7.

1. Wapokezi wa msamaha wa Yehova wanabarikiwa na nini sasa?

YEHOVA huwasamehe wakosaji wanaotubu na sasa huwawezesha wafurahie amani ya akili katika paradiso ya kiroho. Ndivyo ilivyo kwa sababu wanapatana na matakwa haya: “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu; mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA [Yehova, NW], naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa [kwa njia kubwa, NW].”—Isaya 55:6, 7.

2. (a) Ni nini kinachomaanishwa na ‘kumtafuta Yehova’ na ‘kumrudia,’ kama ilivyotajwa kwenye Isaya 55:6, 7? (b) Kwa nini wahamishwa Wayahudi katika Babuloni walihitaji kumrudia Yehova, na ni nini kilichowapata baadhi yao?

2 Ili ‘kumtafuta Yehova’ na kumwita kwa kukubaliwa, mtu mwovu anahitaji kuacha njia yake mbaya na wazo lolote la kuwadhuru wengine. Uhitaji wa ‘kumrudia Yehova’ unaonyesha kwamba mkosaji huyo alimwacha Mungu, ambaye wakati mmoja alikuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja naye. Hali ilikuwa hivyo kwa habari ya wakazi wa Yuda, ambao ukosefu wao wa uaminifu kwa Mungu hatimaye uliongoza kwenye uhamisho katika Babuloni. Wahamishwa Wayahudi walihitaji kumrudia Yehova kwa kutubu makosa yaliyotokeza utumwa wao wa Kibabuloni na ule ukiwa wa nchi yao uliotabiriwa wa miaka 70. Katika 537 K.W.K., nchi hiyo ilikaliwa tena na mabaki ya Wayahudi wenye kumcha Mungu walioachiliwa huru kutoka Babuloni kwa amri ya kiserikali. (Ezra 1:1-8; Danieli 9:1-4) Matokeo ya kurudishwa huko yalikuwa makuu sana hivi kwamba nchi ya Yuda ililinganishwa na Paradiso ya Edeni.—Ezekieli 36:33-36.

3. Mabaki ya Israeli wa kiroho wamepatwaje na ono lile kama la wale wahamishwa wenye kumhofu Mungu waliorudi Yuda?

3 Waisraeli wa kiroho wamekuwa na ono kama hilo la wale Wayahudi wenye kumhofu Mungu waliorudi Yuda baada ya uhamisho wa Kibabuloni. (Wagalatia 6:16) Mabaki ya Israeli wa kiroho walibadili kwa kadiri fulani njia na mawazo yao baada tu ya Vita ya Ulimwengu 1. Mwaka 1919 ulikuwa mwisho wa uhamisho wao kutoka kibali kamili cha Mungu wakiwa katika milki ya Babuloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini bandia. Kwa sababu walitubu dhambi zao zilizohusu hofu ya mwanadamu na kutotenda katika utumishi wa Yehova, aliwaweka huru kutoka Babuloni Mkubwa, akawarudisha kwenye hali yao ya kiroho iliyo haki yao, na akaanza kuwatumia tena kuuhubiri ujumbe wa Ufalme. Paradiso ya kiroho imesitawi miongoni mwa watu wa Mungu tangu wakati huo, kwa heshima ya jina lake takatifu. (Isaya 55:8-13) Kwa hiyo, katika ule mfano wa kale na lile lililofananishwa la ki-siku-hizi, tuna ushuhuda wa wazi kwamba baraka zinafuata msamaha wa kimungu na kwamba Yehova kwa kweli husamehe wale wanaotubu kwa njia kubwa.

4. Baadhi ya watumishi wa Yehova wana hofu gani?

4 Kwa hiyo watumishi wa Yehova wa siku ya leo wanaweza kuutumaini msamaha wake. Hata hivyo, baadhi yao wamekuwa na majonzi kwa ajili ya makosa ya zamani, na hisia za hatia ziko karibu kuwashinda. Hawajioni wenyewe kuwa wenye kustahili kukaa katika paradiso ya kiroho. Kwa kweli, wengine huhofu kwamba wametenda dhambi isiyoweza kusameheka na hawatapokea kamwe msamaha wa Yehova. Je! hiyo yawezekana?

Dhambi Nyingine Haziwezi Kusameheka

5. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba baadhi ya dhambi haziwezi kusameheka?

5 Dhambi nyingine haziwezi kusameheka. Yesu Kristo alisema hivi: “Kila dhambi na kila neno la kufuru watasamehewa wanadamu, ila kwa kumkufuru Roho hawatasamehewa.” (Mathayo 12:31) Kwa hiyo, basi, ukufuru dhidi ya roho takatifu au kani ya utendaji ya Mungu, hautasamehewa. Mtume Paulo alitaja dhambi ya jinsi hiyo alipoandika hivi: “Hao waliokwisha kupewa nuru, . . . wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu, kwa kuwa wamsulibisha [wamtundika, NW] Mwana wa Mungu mara ya pili kwa nafsi zao, na kumfedhehi kwa dhahiri.”—Waebrania 6:4-6.

6. Ni nini kinachoamua kama dhambi yaweza kusameheka au la?

6 Ni Mungu peke yake ajuaye ikiwa mtu ametenda ile dhambi isiyoweza kusameheka. Hata hivyo, Paulo aliangaza nuru kwenye habari hiyo alipoandika hivi: “Kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; bali kuna kuitazamia hukumu.” (Waebrania 10:26, 27) Mtu mkaidi hutenda kimakusudi, au ni “mwasi kwa ushupavu na mara nyingi kwa upotovu.” (Webster’s New Collegiate Dictionary) Mtu yeyote anayeendelea kuzoea dhambi kimakusudi na kwa ushupavu baada ya yeye kujua kweli hasamehewi. Kwa hiyo, jambo linaloamua kama dhambi yaweza kusameheka au la, si dhambi yenyewe hasa bali hali ya moyo, kadiri ya ukaidi unaohusika. Kwa upande ule mwingine, hali yaelekea kuwa nini wakati Mkristo akosaye anaposumbuliwa sana juu ya kosa lake? Hangaiko lake kubwa labda huonyesha kwamba yeye kwa kweli hakutenda dhambi isiyoweza kusameheka.

Dhambi Zao Zilikuwa Zisizosameheka

7. Kwa nini twaweza kusema kwamba baadhi ya wapinzani wa kidini wa Yesu walitenda dhambi isiyoweza kusameheka?

7 Viongozi fulani wa kidini Wayahudi waliompinga Yesu walitenda dhambi ya kusudi, na hivyo isiyoweza kusameheka. Ingawa waliona roho takatifu ya Mungu ikitenda kazi kupitia Yesu alipofanya mema na kufanya miujiza, viongozi hao wa kidini walimhesabia Beelzebuli, au Shetani Ibilisi nguvu za Yesu. Walitenda dhambi wakiwa na ufahamu kamili wa utendaji wa roho ya Mungu usioweza kukanushwa. Hivyo, walitenda dhambi isiyoweza kusameheka, kwani Yesu alisema hivi: “Yeye atakayenena neno juu ya Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] hatasamehewa katika ulimwengu wa sasa, wala katika ule ujao.”—Mathayo 12:22-32.

8. Kwa nini dhambi ya Yuda Iskariote haikuweza kusameheka?

8 Dhambi ya Yuda Iskariote pia ilikuwa isiyoweza kusameheka. Kumsaliti kwake Yesu kulikuwa upeo wenye ukaidi, wa kimakusudi, wa mwendo wa unafiki na wa kutofuatia haki. Kwa mfano, Yuda alipomwona Mariamu akimpaka Yesu mafuta ya thamani nyingi, aliuliza hivi: “Mbona marhamu hii haikuuzwa kwa dinari mia tatu, wakapewa maskini?” Mtume Yohana aliongeza hivi: “[Yuda] aliyasema hayo, si kwa kuwahurumia maskini; bali kwa kuwa ni mwivi, naye ndiye aliyeshika mfuko, akavichukua vilivyotiwa humo.” Upesi baadaye, Yuda alimsaliti Yesu kwa vipande 30 vya fedha. (Yohana 12:1-6; Mathayo 26:6-16) Ni kweli, Yuda alihisi majuto na akajiua mwenyewe. (Mathayo 27:1-5) Lakini hakusamehewa, kwa kuwa mwendo wake wa kimakusudi, wenye kuendelea na tendo lake la usaliti lilionyesha dhambi yake dhidi ya roho takatifu. Ilifaa kama nini kwamba Yesu alimwita Yuda “mwana wa upotevu”!—Yohana 17:12; Marko 3:29; 14:21.

Walisamehewa Dhambi Zao

9. Kwa nini Mungu alisamehe dhambi za Daudi kwa habari ya Bath-sheba?

9 Dhambi za kusudi hutofautiana kabisa na makosa ya wale wanaosamehewa na Mungu. Chukua mfano wa Mfalme Daudi wa Israeli. Alifanya uzinzi na Bath-sheba, mke wa Uria, na baadaye alimwagiza Yoabu apange kwa hila kifo cha Uria vitani. (2 Samweli 11:1-27) Kwa nini Mungu alimwonyesha Daudi rehema? Hasa ni kwa sababu ya lile agano la Ufalme lakini pia ni kwa sababu ya rehema ya Daudi mwenyewe na toba yake ya kweli.—1 Samweli 24:4-7; 2 Samweli 7:12; 12:13.

10. Ingawa Petro alitenda dhambi nzito, ni kwa nini Mungu alimsamehe?

10 Fikiria pia, mtume Petro. Alitenda dhambi nzito kwa kumkana Yesu tena na tena. Kwa nini Mungu alimsamehe? Tofauti na Yuda Iskariote, Petro alikuwa amekuwa mnyoofu katika utumishi wa Mungu na Kristo. Dhambi ya mtume huyo ilikuwa kwa sababu ya udhaifu wa kimnofu, na yeye alitubu kweli kweli “akalia kwa majonzi.”—Mathayo 26:69-75.

11. Ungefafanuaje “toba,” na mtu apaswa kufanya nini ikiwa yeye ni mwenye kutubu kweli kweli?

11 Mifano inayotangulia inaonyesha kwamba hata mtu anayetenda dhambi nzito aweza kupata msamaha wa Yehova Mungu. Lakini ni mtazamo gani unaohitajiwa ili kusamehewa? Toba ya kweli ni ya muhimu ikiwa Mkristo akosaye atasamehewa na Mungu. Kutubu humaanisha “kugeuka kutoka kwa dhambi kwa sababu ya kujutia kosa la wakati uliopita” au “kuhisi majuto au masikitiko kwa ajili ya lile ambalo mtu amefanya au amekosa kufanya.” (Webster’s Third New International Dictionary) Mtu mwenye kutubu kweli kweli angeonyesha majuto juu ya suto, huzuni, au matatizo yoyote ambayo dhambi yake imeletea jina na tengenezo la Yehova. Mkosaji mwenye kutubu angetokeza pia matunda yanayolingana na hiyo, akitenda kazi zipasazo toba. (Mathayo 3:8; Matendo 26:20) Kwa mfano, ikiwa alimpunja mtu fulani, yeye angechukua hatua zifaazo ili kuilipia hasara. (Luka 19:8) Mkristo huyo mwenye kutubu ana sababu nzuri za Kimaandiko kuwa na uhakika kwamba Yehova atasamehe kwa njia kubwa. Hizo ni zipi?

Sababu za Kuwa na Uhakika Katika Msamaha wa Mungu

12. Zaburi 25:11 huonyesha kwa msingi gani kwamba mtu mwenye kutubu aweza kuomba msamaha?

12 Mkosaji mwenye kutubu aweza kuomba msamaha akiwa na uhakika kwa msingi wa jina la Yehova. Daudi aliomba hivi: “Ee BWANA [Yehova, NW], kwa ajili ya jina lako, unisamehe uovu wangu, maana ni mwingi.” (Zaburi 25:11) Sala ya jinsi hiyo, pamoja na kutubu suto lolote ambalo mkosaji ameletea jina la Mungu, yaweza pia kuzuia dhambi nzito katika wakati ujao.

13. Sala inatimiza nini katika msamaha wa kimungu?

13 Yehova Mungu hujibu sala za kuhisiwa moyoni za watumishi wake wakosao lakini wanaotubu. Kwa mfano, Yehova hakumpuuza Daudi, ambaye alisali kutoka moyoni baada ya kutambua ukubwa wa dhambi zake kwa habari ya Bath-sheba. Kwa kweli, maneno ya Daudi katika Zaburi 51 huonyesha maoni ya moyoni ya waombaji wengi. Aliomba hivi: “Ee Mungu, unirehemu, sawasawa na fadhili zako. Kiasi cha wingi wa rehema zako, uyafute makosa yangu. Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.”—Zaburi 51:1, 2, 17.

14. Maandiko yanaandaaje uhakikishio kwamba Mungu husamehe wale wanaozoea imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu?

14 Mungu huwasamehe wale wanaozoea imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Paulo aliandika hivi “Katika yeye huyo, kwa damu yake, tunao ukombozi wetu, masamaha ya dhambi.” (Waefeso 1:7) Akiwa na maana iyo hiyo, mtume Yohana aliandika hivi: “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”—1 Yohana 2:1, 2.

15. Ili aendelee kuonea shangwe rehema ya Mungu, ni lazima mtenda dhambi mwenye kutubu afanye nini?

15 Rehema ya Yehova humpa mkosaji mwenye kutubu msingi wa kuwa na uhakika kwamba aweza kusamehewa. Nehemia alisema hivi: “Wewe u Mungu, uliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, u mwingi wa rehema.” (Nehemia 9:17; linganisha Kutoka 34:6, 7.) Bila shaka, ili kuendelea kuonea shangwe rehema ya kimungu, ni lazima mtenda dhambi ajitahidi kufuata sheria ya Mungu. Kama vile mtunga zaburi alivyosema, “rehema zako zinijie nipate kuishi, maana sheria yako ni furaha yangu. Ee BWANA [Yehova, NW], rehema zako ni nyingi, unihuishe sawasawa na hukumu zako.”—Zaburi 119:77, 156.

16. Kuna faraja gani katika uhakika wa kwamba Yehova hukumbuka hali yetu yenye dhambi?

16 Uhakika wa kwamba Yehova hukumbuka hali yetu yenye dhambi pia humpa mkosaji mwenye kutubu faraja na sababu ya kusali kwa uhakika kwamba Mungu atamsamehe. (Zaburi 51:5; Warumi 5:12) Mtunga zaburi Daudi alitoa uhakikishio wenye kufariji alipotangaza rasmi hivi: “[Yehova Mungu] hakututenda sawasawa na hatia zetu, wala hukutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao. Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA [Yehova, NW] anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:10-14) Naam, Baba wetu wa kimbingu ni mwenye rehema na huruma zaidi ya mzazi wa kibinadamu.

17. Rekodi ya mtu ya utumishi wa zamani kwa Mungu inahusianaje na msamaha?

17 Mtenda dhambi mwenye kutubu aweza kuomba msamaha akiwa na uhakika wa kwamba Yehova hatapuuza rekodi yake ya zamani ya utumishi mwaminifu. Nehemia hakuwa akisihi kupata msamaha wa dhambi yake, hata hivyo alisema hivi: “Unikumbuke, Ee Mungu wangu, kwa mema.” (Nehemia 13:31, Zaire Swahili Bible) Mkristo mwenye kutubu aweza kupata faraja katika maneno haya: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.”—Waebrania 6:10.

Msaada Kutoka kwa Wazee

18. Ni nini kipaswacho kifanywe ikiwa dhambi ya Mkristo imemfanya awe mgonjwa kiroho?

18 Namna gani ikiwa Mkristo anahisi hafai kubaki ndani ya paradiso ya kiroho au hawezi kusali kwa sababu dhambi yake imemfanya awe mgonjwa kiroho? “Na awaite wazee wa kanisa [kundi, NW]; nao wamwombee na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana [Yehova, NW],” akaandika mwanafunzi Yakobo. “Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana [Yehova, NW] atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” Naam, wazee wa kundi wanaweza kusali kwa mafanikio wakiwa pamoja na au kwa ajili ya mwamini mwenzao mwenye kutubu wakitumaini kumrudisha kwenye afya njema ya kiroho.—Yakobo 5:14-16.

19. Ikiwa mtu ametengwa na ushirika, ni lazima afanye nini ili asamehewe na kurudishwa?

19 Hata kama halmashauri ya hukumu inamtenga na ushirika mtenda dhambi asiyetubu, haimaanishi kwamba alitenda ile dhambi isiyoweza kusameheka. Hata hivyo ili asamehewe na kurudishwa, ni lazima atii sheria za Mungu kwa unyenyekevu, atokeze matunda yapasayo toba, na awapelekee wazee ombi la kurudishwa. Baada ya mwasherati kutengwa na ushirika wa kundi katika Korintho ya kale, Paulo aliandika hivi: “Yamtosha mtu wa namna hii adabu ile aliyopewa na walio wengi; hata kinyume cha hayo, ni afadhali mmsamehe na kumfariji, mtu kama huyo asije akamezwa katika huzuni yake ipitayo kiasi. Kwa hiyo nawasihi kumthibitishia upendo wenu.”—2 Wakorintho 2:6-8; 1 Wakorintho 5:1-13.

Mungu Hutoa Nguvu

20, 21. Ni nini kiwezacho kumsaidia mtu mwenye hangaiko la kwamba labda ametenda dhambi isiyoweza kusameheka?

20 Ikiwa mambo kama vile afya mbaya au mkazo wa mawazo yanasababisha hangaiko la kwamba mtu ametenda dhambi isiyoweza kusameheka, kupata pumziko na usingizi wa kutosha huenda ukasaidia. Hata hivyo, wapaswa hasa kuyakumbuka maneno haya ya Petro: “Mwekeeni [Mungu] matatizo yenu yote, maana yeye anawatunzeni.” Na usiruhusu kamwe Shetani akuvunje moyo, kwani Petro aliongeza hivi: “Mwe macho; kesheni! Maana adui yenu, Ibilisi, huzungukazunguka kama simba angurumaye akitafuta mawindo. Mwe imara katika imani na kumpinga, mkijua kwamba ndugu zenu pote duniani wanapatwa na mateso hayohayo. Lakini mkisha teseka muda mfupi, Mungu aliye asili ya neema yote . . . atawakamilisheni na kuwapeni uthabiti, nguvu na msingi imara.”—1 Petro 5:6-10, Habari Njema kwa Watu Wote.

21 Kwa hiyo ikiwa wewe ni mwenye kutubu lakini umekuwa ukihofu kwamba una hatia ya dhambi isiyoweza kusameheka, kumbuka kwamba njia za Mungu ni zenye hekima, haki, na upendo. Kwa hiyo, sali kwake katika imani. Endelea kutwaa ndani chakula cha kiroho anachoandaa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Shirikiana na waamini wenzako na kushiriki kwa kawaida katika huduma ya Kikristo. Hilo litaimarisha imani yako na kukuweka huru na hofu yoyote ya kwamba huenda ikawa Mungu hakukusamehe dhambi yako.

22. Tutachunguza nini baadaye?

22 Wakazi wa paradiso ya kiroho wanaweza kufarijiwa na ufahamu wa kwamba Yehova husamehe katika njia kubwa. Hata hivyo, maisha yao hayakosi majaribu leo. Labda wameshuka moyo kwa sababu mpendwa amekufa au rafiki mpendwa ni mgonjwa mahututi. Kama tutakavyoona, katika hali hizo na nyinginezo, Yehova husaidia na huongoza watu wake kupitia roho takatifu yake.

Majibu Yako ni Nini?

◻ Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova ‘husamehe kwa njia kubwa’?

◻ Ni dhambi gani isiyoweza kusameheka?

◻ Mtu husamehewa dhambi zake chini ya hali zipi?

◻ Kwa nini wakosaji wenye kutubu wanaweza kuwa na uhakika katika msamaha wa Mungu?

◻ Ni msaada gani unaopatikana kwa wakosaji wenye kutubu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je! wajua ni kwa nini Daudi na Petro walisamehewa lakini Yuda Iskariote hakusamehewa?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Msaada wa wazee wa kundi waweza kumsaidia Mkristo sana kiroho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki