Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w92 9/15 kur. 13-18
  • Roho ya Yehova Huwaongoza Watu Wake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Roho ya Yehova Huwaongoza Watu Wake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mwombe Mungu Akupe Roho Yake
  • Yehova Ana Nia ya Kusaidia
  • Jinsi Ambavyo Roho Husaidia
  • “Kwa Kuugua Kusikoweza Kutamkwa”
  • Usiihuzunishe Kamwe Roho
  • Endelea Kusali Ili Kupata Roho Takatifu
  • ‘Kwa Jina la Roho Takatifu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Tembea kwa Roho na Uishi Kulingana na Wakfu Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Je, Nimeifanya Roho Takatifu Kuwa Msaidizi Wangu wa Kibinafsi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
w92 9/15 kur. 13-18

Roho ya Yehova Huwaongoza Watu Wake

“Roho yako ni nzuri; na iniongoze mimi katika nchi ya unyoofu.”—ZABURI 143:10, NW.

1, 2. Ni nini kiwezacho kuwasababishia taabu watumishi waaminifu-washikamanifu wa Yehova?

‘NINAHISI nimeshuka moyo sana! Naweza kupata wapi faraja? Je! Mungu ameniacha?’ Je! wewe huhisi hivyo wakati wowote? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Ingawa watumishi waaminifu-washikamanifu wa Yehova hukaa katika paradiso ya kiroho yenye kusitawi, wao nyakati nyingine hukabili matatizo yenye kutaabisha, majaribu, na vishawishi vya kawaida kwa ainabinadamu.—1 Wakorintho 10:13.

2 Labda umepatwa na jaribu fulani lenye kudumu kwa muda mrefu au kisababishi cha mkazo mwingi. Huenda ikawa una huzuni juu ya kifo cha mpendwa na huenda ukahisi upweke mwingi. Au huenda ikawa moyo wako unahangaishwa na ugonjwa wa rafiki mpendwa. Hali za jinsi hiyo huenda zikawa zinakunyang’anya shangwe na amani na huenda hata zikawa zinatisha imani yako. Wapaswa kufanya nini?

Mwombe Mungu Akupe Roho Yake

3. Ikiwa jambo fulani linakunyang’anya sifa kama vile amani na shangwe, lingekuwa jambo la hekima kufanya nini?

3 Ikiwa jambo fulani linakunyang’anya amani, shangwe, au sifa nyingine ya kimungu lingekuwa jambo la hekima kusali ili kupata roho takatifu au kani ya utendaji ya Mungu. Kwa nini? Kwa sababu roho ya Yehova hutokeza matunda mazuri yanayomsaidia Mkristo akabili matatizo, majaribu, na vishawishi. Baada ya kuonya dhidi ya “kazi za mnofu,” mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa upande mwingine, tunda la roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti. Dhidi ya mambo hayo hakuna sheria.”—Wagalatia 5:19-23, NW.

4. Mtu anapokabiliwa na jaribu au kishawishi fulani, kwa nini kungefaa kudhihirisha hilo katika sala zake?

4 Kwa sababu ya aina ya jaribu unalokabili, huenda ukatambua kwamba umo katika hatari ya kupoteza upole, au hali pole yako. Kwa hiyo taja wazi jambo hilo kwa kumwomba Yehova Mungu akupe tunda la roho la upole. Ikiwa unakabili kishawishi fulani, unahitaji hasa tunda la kujidhibiti. Bila shaka, ingefaa pia kusali ili kupata msaada wa kimungu wa kushindana na kishawishi, kuokolewa kutoka kwa Shetani, na kupata hekima inayohitajiwa ili kuvumilia jaribu hilo.—Mathayo 6:13; Yakobo 1:5, 6.

5. Hali zikiwa zenye kutaabisha sana hivi kwamba hujui ni tunda gani la roho utakaloomba, ni jambo gani liwezalo kufanywa?

5 Hata hivyo, nyakati nyingine hali zaweza kuwa zenye kutaabisha au zenye kufadhaisha sana hivi kwamba hujui ni tunda gani la roho unalohitaji. Kwa hakika, shangwe, amani, upole, na sifa nyinginezo za kimungu huenda zote zikawa hatarini. Namna gani basi? Kwa nini usimwombe Mungu roho takatifu yenyewe na kuiacha ifanye yale matunda yanayohitajiwa yasitawi kwa habari yako? Matunda yanayohitajiwa yaweza kuwa upendo au shangwe au amani au mchanganyiko wa matunda ya roho. Sali pia kwamba Mungu akusaidie ufuate mwelekezo wa roho yake, kwani yeye huitumia kuwaongoza watu wake.

Yehova Ana Nia ya Kusaidia

6. Yesu alikaziaje kwa wafuasi wake uhitaji wa kusali bila kukoma?

6 Wanafunzi wa Yesu Kristo walipomwomba maagizo juu ya sala, kwa sehemu aliwahimiza wasali ili kupata roho ya Mungu. Yesu mwanzoni alitumia kielezi kilichobuniwa kuwasukuma wasali bila kukoma. Alisema hivi: “Ni nani kwenu aliye na rafiki, akamwendea usiku wa manane, na kumwambia, Rafiki yangu, nikopeshe mikate mitatu, kwa sababu rafiki yangu amefika kwangu, atoka safarini, nami sina kitu cha kuweka mbele yake; na yule wa ndani amjibu akisema, Usinitaabishe; mlango umekwisha fungwa, nasi tumelala kitandani mimi na watoto wangu; siwezi kuondoka nikupe? Nawaambia ya kwamba, ijapokuwa haondoki ampe kwa kuwa ni rafiki yake, lakini kwa vile asivyoacha kumwomba, ataondoka na kumpa kadiri ya haja yake.”—Luka 11:5-8.

7. Ni nini maana ya maneno ya Yesu kwenye Luka 11:11-13, na yanatupa sisi uhakikishio gani kuhusu Mungu na roho yake?

7 Yehova ana nia ya kusaidia kila mmoja wa watumishi wake waaminifu waliojiweka wakfu, na yeye huyasikiliza maombi yao. Lakini mtu huyo ‘akiendelea kuomba,’ kama vile Yesu alivyohimiza, hilo linaonyesha tamaa ya kuhisiwa moyoni na ni wonyesho wa imani. (Luka 11:9, 10) Kristo aliongeza hivi: “Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] hao wamwombao?” (Luka 11:11-13) Ikiwa mzazi wa kidunia, ajapokuwa mwovu kwa kadiri fulani kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa, humpa mtoto wake vitu vizuri, kwa hakika Baba yetu wa kimbingu ataendelea kutoa roho takatifu yake kwa yeyote kati ya watumishi wake waaminifu-washikamanifu anayeiomba kwa unyenyekevu.

8. Zaburi 143:10 hutumikaje kwa Daudi, Yesu, na watumishi wa Mungu wa ki-siku-hizi?

8 Ili tufaidike kutokana na roho ya Mungu, ni lazima tuwe na nia ya kufuata mwongozo wayo kama vile Daudi alivyofanya. Alisali hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu. Roho yako ni nzuri; na iniongoze mimi katika nchi ya unyoofu.” (Zaburi 143:10, NW) Daudi, aliyekuwa ametoroshwa na mfalme Mwisraeli Sauli, alitaka roho ya Mungu imwongoze ili ahakikishe kwamba mwendo wake ulikuwa mnyoofu. Baadaye Abiathari alikuja akiwa na efodi ya kuhani iliyotumiwa ili kuhakikisha mapenzi ya Mungu. Akiwa mwakilishi wa Mungu wa kikuhani, Abiathari alimwagiza Daudi juu ya njia ya kwenda ili kumpendeza Yehova. (1 Samweli 22:17–23:12; 30:6-8) Kama vile Daudi, Yesu aliongozwa na roho ya Yehova, na hiyo imekuwa kweli kwa habari ya wafuasi wa Kristo wapakwa-mafuta wakiwa jamii. Katika 1918-19, walionwa na jamii ya kibinadamu kuwa wahuni, na maadui wao wa kidini walifikiri wangeweza kuwaharibu. Wapakwa-mafuta walisali ili kupata njia ya kutoka katika hali yao ya kutotenda, na katika 1919, Mungu alijibu sala zao, akawakomboa, na kuwatendesha kazi tena katika utumishi wake. (Zaburi 143:7-9) Kwa hakika, roho ya Yehova ilikuwa ikisaidia na kuwaongoza watu wake wakati huo, kama ifanyavyo hadi siku hii ya leo.

Jinsi Ambavyo Roho Husaidia

9. (a) Roho takatifu hutumikaje ikiwa “msaidizi”? (b) Tunajuaje kwamba roho takatifu si mtu? (Ona kielezi-chini.)

9 Yesu Kristo aliiita roho takatifu “msaidizi.” Kwa mfano, aliwaambia wafuasi wake hivi: “Nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.” Miongoni mwa mambo mengine, “msaidizi” huyo angekuwa mwalimu, kwani Kristo aliahidi hivi: “Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW], ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.” Roho hiyo ingeshuhudia pia juu ya Kristo, na yeye aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Yawafaa ninyi mimi niondoke; kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu.”—Yohana 14:16, 17, 26; 15:26; 16:7.a

10. Roho takatifu imethibitika kuwa msaidizi katika njia zipi?

10 Kutoka mbinguni, Yesu aliwamwagia wafuasi wake katika siku ya Pentekoste 33 W.K., ile roho takatifu iliyokuwa imeahidiwa. (Matendo 1:4, 5; 2:1-11) Ikiwa msaidizi, roho iliwapa uelewevu wenye kuongezeka juu ya mapenzi na kusudi la Mungu na ikawafungulia Neno lake la kiunabii. (1 Wakorintho 2:10-16; Wakolosai 1:9, 10; Waebrania 9:8-10) Msaidizi huyo pia aliwasaidia wanafunzi wa Yesu wawe mashahidi katika dunia yote. (Luka 24:49; Matendo 1:8; Waefeso 3:5, 6) Leo, roho takatifu yaweza kumsaidia Mkristo aliyejiweka wakfu akue katika maarifa akijifaidi kutokana na maandalizi ya kiroho ambayo Mungu hutoa kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Roho ya Mungu yaweza kuandaa msaada kwa kutoa ujasiri na imara inayohitajiwa ili mtu aweze kutoa ushahidi akiwa mmoja wa watumishi wa Yehova. (Mathayo 10:19, 20; Matendo 4:29-31) Hata hivyo, roho takatifu pia husaidia watu wa Mungu katika njia nyinginezo.

“Kwa Kuugua Kusikoweza Kutamkwa”

11. Jaribu linapoonekana kuwa lenye kulemeza, Mkristo apaswa kufanya nini?

11 Ikiwa Mkristo amepatwa na jaribu linaloonekana kuwa lenye kulemeza sana, yeye apaswa kufanya nini? Kusali ili kupata roho takatifu, na kuiacha ifanye kazi yayo! “Roho naye hutusaidia udhaifu wetu,” akasema Paulo, “kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo; lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Na yeye aichunguzaye mioyo aijua nia ya Roho ilivyo, kwa kuwa huwaombea watakatifu kama apendavyo Mungu.”—Warumi 8:26, 27.

12, 13. (a) Warumi 8:26, 27 hutumikaje kwa sala zinazotolewa hasa katika hali zenye kujaribu? (b) Paulo na washiriki wake walifanya nini walipokuwa chini ya mbano mwingi katika wilaya ya Esia?

12 Wale watakatifu ambao roho ya Mungu huwaombea ni wafuasi wa Yesu wapakwa-mafuta, wenye tumaini la kimbingu. Lakini iwe una mwito wa kimbingu au tumaini la kidunia, ukiwa Mkristo wewe unaweza kupata msaada wa roho takatifu ya Mungu. Yehova nyakati nyingine hutolea sala mahususi jibu la moja kwa moja. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ukataabika sana hivi kwamba huwezi kueleza hisia zako kwa maneno na huenda tu ukaweza kumsihi Yehova kwa kuugua kusikoweza kutamkwa. Kwa kweli, huenda usijue lile likufaalo na huenda hata ukaomba jambo lisilofaa isipokuwa ukisali ili kupata roho takatifu. Mungu anajua kwamba unataka mapenzi yake yatendeke, naye atambua kile unachohitaji kwa kweli. Isitoshe, kupitia roho takatifu yake, alisababisha baadhi ya sala zirekodiwe katika Neno lake, na sala hizo hushughulikia hali zenye kujaribu. (2 Timotheo 3:16, 17; 2 Petro 1:21) Kwa hiyo, Yehova aweza kuyaona maoni hayo yanayoonyeshwa katika sala hizo zenye kupuliziwa roho kuwa ni maoni ambayo ungependa kueleza ukiwa mmoja wa watumishi wake, na yeye aweza kujibu sala hizo kwa ajili yako.

13 Paulo na washiriki wake huenda ikawa hawakujua lile la kusali walipopatwa na dhiki katika wilaya ya Esia. ‘Wakilemewa mno kuliko nguvu zao, walikata tamaa ya kuishi.’ Lakini waliwaomba wengine watoe sala kwa ajili yao na wakamtumaini Mungu, awezaye kuwafufua wafu, na yeye aliwakomboa. (2 Wakorintho 1:8-11) Inafariji kama nini kwamba Yehova Mungu husikia na kutenda kulingana na sala za watumishi wake waaminifu!

14. Kwaweza kuwako matokeo gani mazuri ikiwa Yehova anaruhusu jaribu liendelee kwa wakati fulani?

14 Watu wa Mungu mara nyingi hupatwa na majaribu wakiwa tengenezo. Kama ilivyoonyeshwa mapema zaidi, walinyanyaswa wakati wa Vita ya Ulimwengu 1. Ingawa wakati huo hawakuwa na uelewevu wa wazi juu ya hali yao na kwa hiyo hawakujua lile hasa la kusali, Neno la Yehova lilikuwa na sala za kiunabii ambazo alijibu kwa ajili yao. (Zaburi 69, 102, 126; Isaya, sura 12) Lakini namna gani ikiwa Yehova anaruhusu jaribu liendelee kwa wakati fulani? Hilo huenda likatokeza kutolewa kwa ushahidi, huenda likawasukuma wengine waikubali kweli, na huwatolea Wakristo nafasi ya kuonyesha upendo wa kidugu kwa kusali kwa ajili ya au kuwasaidia waamini wenzao. (Yohana 13:34, 35; 2 Wakorintho 1:11) Kumbuka kwamba Yehova huwaongoza watu wake kupitia roho takatifu yake, huwafanyia linalowafaa zaidi, na sikuzote husuluhisha mambo katika njia itakayoheshimu na kutakasa jina lake takatifu.—Kutoka 9:16; Mathayo 6:9.

Usiihuzunishe Kamwe Roho

15. Wakristo wanaweza kuitegemea roho takatifu ifanye nini kwa ajili yao?

15 Kwa hiyo, ikiwa wewe ni mtumishi wa Yehova, sali ili upate roho takatifu wakati wa majaribu na katika nyakati nyinginezo. Halafu hakikisha unafuata mwongozo wayo, kwani Paulo aliandika hivi: “Msimhuzunishe yule Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi.” (Waefeso 4:30) Roho ya Mungu ilikuwa na ndiyo muhuri, au ‘arbuni ya kitu ambacho kitakuja,’ kwa ajili ya Wakristo waaminifu wapakwa-mafuta—yaani, uhai wa kimbingu usioweza kufa. (2 Wakorintho 1:22, NW; Warumi 8:15; 1 Wakorintho 15:50-57; Ufunuo 2:10) Wakristo wapakwa-mafuta na wale wenye tumaini la kidunia pia wanaweza kuitegemea roho ya Yehova ifanye mengi kwa ajili yao. Inaweza kuwaelekeza katika maisha ya uaminifu na kuwasaidia waepuke kazi zenye dhambi zinazoongoza kwenye kukosa kwao kibali cha Mungu, kupoteza roho takatifu yake, na kushindwa kupata uhai wa milele.—Wagalatia 5:19-21.

16, 17. Mkristo anaweza kuihuzunishaje roho?

16 Mkristo awezaje, ama kwa kujua au bila kujua, kuihuzunisha roho? Yehova hutumia roho yake kuendeleza umoja na kuwaweka rasmi wanaume wenye daraka katika kundi. Kwa hiyo, ikiwa mshiriki wa kundi angenung’unika dhidi ya wazee waliowekwa rasmi, kueneza porojo zenye uchongezi, na kadhalika, asingekuwa akifuata miongozo ya roho ya Mungu kuelekea amani na umoja. Kwa ujumla, angekuwa akiihuzunisha roho.—1 Wakorintho 1:10; 3:1-4, 16, 17; 1 Wathesalonike 5:12, 13; Yuda 16.

17 Katika kuwaandikia Wakristo katika Efeso, Paulo alionya dhidi ya mielekeo ya kusema uwongo, hasira ya kuendelea, kuiba, usemi usiofaa, kupendezwa kwenye kuamsha ashiki na uasherati, mwenendo wa aibu, na ucheshi wa aibu. Ikiwa Mkristo angejiruhusu mwenyewe apeperuke kuelekea mambo ya jinsi hiyo, angekuwa akitenda dhidi ya shauri la Bibia lililopuliziwa roho. (Waefeso 4:17-29; 5:1-5) Naam, na hivyo angekuwa akiihuzunisha roho ya Mungu kwa kadiri fulani.

18. Ni jambo gani liwezalo kumpata Mkristo yeyote anayeanza kupuuza shauri la Neno la Mungu lililopuliziwa roho?

18 Kwa kweli, Mkristo yeyote anayeanza kupuuza shauri la Neno la Yehova lililopuliziwa roho huenda akaanza kukuza mitazamo au vitabia viwezavyo kutokeza dhambi ya kusudi na kupoteza kibali cha kimungu. Ingawa huenda ikawa hazoei dhambi sasa, aweza kuwa anaelekea hatua hiyo. Mkristo huyo anayefanya kinyume cha mwongozo wa roho angekuwa akiihuzunisha. Hivyo angekuwa pia akimpinga na kumhuzunisha Yehova, Chanzo cha roho takatifu. Ampendao Mungu asingetaka kamwe kufanya hivyo!

Endelea Kusali Ili Kupata Roho Takatifu

19. Kwa nini watu wa Yehova wanahitaji roho yake leo hasa?

19 Ikiwa wewe ni mtumishi wa Yehova, endelea kusali ili upate roho takatifu yake. Hasa katika “siku [hizi] za mwisho” zikiwa na nyakati zazo za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo, Wakristo wanahitaji msaada wa roho ya Mungu. (2 Timotheo 3:1-5) Ibilisi na roho waovu wake, walioondoshwa mbinguni na sasa wakiwa katika ujirani wa dunia, wana ghadhabu nyingi dhidi ya tengenezo la Yehova. Kwa hiyo, sasa kuliko wakati mwingine wowote, watu wa Mungu wanahitaji roho takatifu yake iwaongoze, au kuwaelekeza, na kuwawezesha wavumilie magumu na mnyanyaso.—Ufunuo 12:7-12.

20, 21. Kwa nini ufuate mwelekezo wa Neno la Yehova, wa roho, na wa tengenezo?

20 Sikuzote onyesha uthamini kwa ajili ya msaada ambao Yehova Mungu huandaa kupitia roho takatifu yake. Fuata mwelekezo wa Neno lake, Biblia, lililopuliziwa roho. Shirikiana kikamili na tengenezo la Mungu lililoongozwa kwa roho. Usijiruhusu kamwe ugeuke hadi kwenye mwendo usio wa kimaandiko ambao ungekuwa sawa na kuihuzunisha roho takatifu, kwani hilo laweza hatimaye kuongoza kwenye kuondolewa kwayo na hivyo kwenye msiba wa kiroho.—Zaburi 51:11.

21 Kuongozwa na roho ya Yehova ndiyo njia ya pekee ya kumpendeza na kuwa na maisha yenye amani, na yenye shangwe. Kumbuka pia, kwamba Yesu aliiita roho takatifu “msaidizi,” au “mfariji.” (Yohana 14:16, NW, kielezi-chini) Kupitia hiyo, Mungu huwafariji Wakristo na huwaimarisha ili waweze kukabili majaribu yao. (2 Wakorintho 1:3, 4) Roho huwatia nguvu watu wa Yehova wahubiri habari njema na huwasaidia wakumbuke mambo ya Kimaandiko yanayohitajiwa ili kutoa ushahidi mzuri. (Luka 12:11, 12; Yohana 14:25, 26; Matendo 1:4-8; 5:32) Kupitia sala na mwongozo wa roho, Wakristo wanaweza kukabili mitihani ya imani wakiwa na hekima ya kimbingu. Kwa hiyo, katika hali zote za maisha wanaendelea kusali ili kupata roho takatifu ya Mungu. Tokeo likiwa kwamba, roho ya Yehova huwaongoza watu wake.

[Maelezo ya Chini]

a Ingawa inapewa hali ya mtu kuwa “msaidizi,” roho takatifu si mtu, kwani kiwakilishi-nafsi cha Kigiriki cha jinsi kati (kinachofasiriwa “it”) hutumiwa kwa roho. Viwakilishi-nafsi vya Kiebrania vya jinsi kike hutumiwa vivyo hivyo kwa hekima inayopewa hali ya mtu. (Mithali 1:20-33; 8:1-36) Isitoshe, roho takatifu ‘ilimwagwa,’ jambo lisiloweza kufanywa kwa mtu.—Matendo 2:33.

Majibu Yako ni Nini?

◻ Kwa nini usali ili kupata roho takatifu ya Mungu?

◻ Roho takatifu ni msaidizi kwa jinsi gani?

◻ Kuihuzunisha roho kunamaanisha nini, na twaweza kuepukaje kufanya hivyo?

◻ Kwa nini uendelee kusali ili kupata roho takatifu na kufuata mwongozo wayo?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Sawa na vile baba mwenye upendo humpa mwana wake vitu vizuri, ndivyo Yehova huwapa roho takatifu watumishi wake wanaosali ili kuipata

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je! unajua jinsi ambavyo roho ya Mungu huwaombea Wakristo wanaosali?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki