Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Kwenye Waebrania 11:26, je, Musa anasemwa kuwa “Kristo,” au badala ya hivyo alikuwa mfananishi wa Yesu Kristo?
Alipozungumzia imani ya Musa, mtume Paulo aliandika kwamba Musa ‘alihesabu kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri; kwa kuwa aliyatazamia hayo malipo.’ (Waebrania 11:26) Yaonekana kwamba Paulo alikuwa akimrejezea Musa kuwa “Kristo,” au mpakwa-mafuta, katika maana fulani.
Kwa kweli, Musa alimwekea kiolezo Mesiya aliyekuwa akija katika njia mbalimbali. Ingawa Musa mwenyewe alikuwa nabii, alitabiri juu ya kuja kwa nabii mkuu zaidi ‘kama yeye.’ Wayahudi wengi walihisi kwamba Yesu alikuwa ndiye “nabii yule,” jambo ambalo wafuasi wake walithibitisha. (Kumbukumbu la Torati 18:15-19; Yohana 1:21; 5:46; 6:14; 7:40; Matendo 3:22, 23; 7:37) Musa alikuwa pia mpatanishi wa agano la Sheria, lakini Yesu alipokea “huduma iliyo bora zaidi” akiwa “mjumbe [mpatanishi, NW] wa agano lililo bora,” lile agano jipya tukufu. (Waebrania 8:6; 9:15; 12:24; Wagalatia 3:19; 1 Timotheo 2:5) Kwa hiyo kwa njia fulani Musa angeweza kusemwa kuwa alikuwa mfananishi wa Mesiya aliyekuwa akija.
Hata hivyo, hiyo haionekani kuwa ndiyo maana ya msingi ya Waebrania 11:26. Hakuna wonyesho wowote wa kwamba Musa alijua mambo yote madogomadogo juu ya Mesiya, akiyahesabu kwa ufahamu yale yaliyompata Misri kuwa kwa ajili ya Mesiya au mwakilishi Wake.
Wengine wamedokeza kwamba maneno ya Paulo kwenye Waebrania 11:26 yalikuwa na maana sawasawa na maelezo yake ya kwamba Wakristo walipatwa na “mateso kwa ajili ya Kristo.” (2 Wakorintho 1:5, NW) Wakristo wapakwa-mafuta walijua kwamba Yesu Kristo alikuwa ameteseka na kwamba ikiwa ‘wangeteswa pamoja wangetukuzwa pamoja’ mbinguni. Lakini Musa hakujua yale ambayo Mesiya aliyekuwa akija angeteseka, wala Musa hakuwa na tumaini la kimbingu.—Warumi 8:17; Wakolosai 1:24.
Kuna uelewevu rahisi zaidi wa jinsi ambavyo Musa ‘alihesabu kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu.’
Paulo alipoandika “Kristo” kwenye Waebrania 11:26, alitumia neno la Kigiriki Khri·stouʹ, lililo sawa na neno la Kiebrania Ma·shiʹach, au Mesiya. “Mesiya” na “Kristo” pia humaanisha “mpakwa-mafuta.” Kwa hiyo Paulo alikuwa akiandika juu ya Musa ‘akihesabu kushutumiwa kwake mpakwa-mafuta.’ Je! Musa mwenyewe angeweza kuitwa “mpakwa-mafuta”?
Ndiyo. Katika nyakati za Biblia mtu angeweza kuthibitishwa katika cheo cha pekee kwa kumiminiwa mafuta kichwani pake. “Ndipo Samweli akatwaa kichupa cha mafuta, akayamimina kichwani pake [Sauli].” “Ndipo Samweli akaitwaa pembe yenye mafuta, akamtia mafuta [Daudi] kati ya ndugu zake; na roho ya BWANA [Yehova, NW] ikamjilia Daudi kwa nguvu.” (1 Samweli 10:1; 16:13; linganisha Kutoka 30:25, 20; Mambo ya Walawi 8:12; 2 Samweli 22:51; Zaburi 133:2.) Hata hivyo, wengine, kama vile nabii Elisha na Hazaeli mfalme wa Siria, walisemwa kuwa ‘wapakwa-mafuta’ hata ingawa hakukuwa uthibitisho wowote wa kwamba mafuta halisi yalikuwa yamemiminwa juu yao. (1 Wafalme 19:15, 16, NW; Zaburi 105:14, 15; Isaya 45:1) Kwa hiyo, mtu mmoja mmoja angeweza kuwa “mpakwa-mafuta” kwa kuwa alikuwa amechaguliwa au kupewa utume wa kipekee.
Katika maana hiyo Musa mwenyewe alikuwa mpakwa-mafuta wa Mungu, na Biblia nyinginezo hutoa fasiri kama vile “Mpakwa-Mafuta wa Mungu” au “Mpakwa-Mafuta” kwenye Waebrania 11:26. Musa alipewa utume kuwa mwakilishi wa Yehova na yule ambaye angeongoza Israeli kutoka Misri. (Kutoka 3:2-12, 15-17) Ingawa Musa alikuwa amelelewa miongoni mwa utajiri na utukufu wa Misri, alithamini zaidi utume wake, ambao alikubali na kutimiza. Kulingana na hilo, Paulo aliweza kuandika kwamba Musa ‘alihesabu kushutumiwa kwake Kristo ni utajiri mkuu kuliko hazina za Misri.’