Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 3/15 kur. 13-18
  • Yehova Hadharau Moyo Uliovunjika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Hadharau Moyo Uliovunjika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Moyo Safi Wahitajiwa
  • Roho Takatifu Ni ya Muhimu
  • Furaha ya Wokovu
  • Kuwafundisha Wakosaji Nini?
  • Dhabihu Zinazokubalika kwa Mungu
  • Hangaiko kwa Ajili ya Ibada Safi
  • Yehova Husikia Vilio Vyetu
  • Rehema ya Yehova Hutuokoa Kutoka Katika Hali ya Kukata Tamaa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Ungamo Liletalo Ponyo la Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Tegemea Roho ya Mungu Unaposhughulika na Mabadiliko ya Maisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 3/15 kur. 13-18

Yehova Hadharau Moyo Uliovunjika

“Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.”—ZABURI 51:17.

1. Yehova huwaonaje waabudu wake wanaotenda dhambi nzito lakini ambao ni wenye kutubu?

YEHOVA aweza ‘kujifunika nafsi yake kwa wingu, maombi yasipite.’ (Maombolezo 3:44) Lakini anataka watu wake wamkaribie. Hata ikiwa mmoja wa waabudu wake anakosea kwa uzito lakini ni mwenye kutubu, Baba yetu wa kimbingu hukumbuka mema yaliyofanywa na mtu huyo. Kwa hiyo, mtume Paulo aliweza kuwaambia Wakristo wenzake hivi: “Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake.”—Waebrania 6:10.

2, 3. Wazee wa Kikristo wanapaswa kufikiria nini katika kushughulika na waamini wenzao waliokosea?

2 Wazee wa Kikristo wanapaswa pia kufikiria miaka ya utumishi mwaminifu uliotolewa kwa Mungu na waamini wenzao. Hilo latia ndani utumishi mtakatifu kwa upande wa wale wenye kutubu ambao wamechukua hatua yenye kosa au ambao hata wametenda dhambi nzito. Wachungaji wa Kikristo hutafuta hali njema ya kiroho ya wote waliomo katika kundi la Mungu.—Wagalatia 6:1, 2.

3 Mkosaji mwenye kutubu ahitaji rehema ya Yehova. Hata hivyo, mengine zaidi yanahitajiwa. Hilo laeleweshwa wazi na maneno ya Daudi kwenye Zaburi 51:10-19.

Moyo Safi Wahitajiwa

4. Kwa nini Daudi alisali kupata moyo safi na roho mpya?

4 Ikiwa Mkristo aliyejiweka wakfu yumo katika hali mbaya ya kiroho kwa sababu ya dhambi, huenda akahitaji nini zaidi ya rehema na msamaha wa Yehova? Daudi alisihi hivi: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.” (Zaburi 51:10) Kwa wazi, Daudi aliomba jambo hilo kwa sababu alitambua kwamba mwelekeo wa kufanya dhambi mbaya sana ulikuwa ungali moyoni mwake. Huenda ikawa hatujahusika katika aina ya dhambi zilizomtega Daudi kuhusiana na Bath-sheba na Uria, lakini tunahitaji msaada wa Yehova ili kuepuka kushindwa na kishawishi cha kushiriki katika mwenendo wowote wa dhambi nzito. Na zaidi, huenda sisi binafsi tukahitaji msaada wa kimungu ili kuondolea mbali kutoka katika moyo wetu vitabia vya dhambi kama vile kutamani na chuki—uhalifu ulio sawa na kuiba na kuua kimakusudi.—Wakolosai 3:5, 6; 1 Yohana 3:15.

5. (a) Ni nini maana ya kuwa na moyo safi? (b) Daudi alitamani nini alipoomba kupata roho mpya?

5 Yehova ataka kwamba watumishi wake wawe na “moyo safi,” yaani, utakaso wa madhumuni au nia. Akitambua kwamba yeye hakuwa ameonyesha utakaso huo, Daudi alisali kwamba Mungu ausafishe moyo wake na kuupatanisha na viwango vya kimungu. Mtunga zaburi alitaka pia roho au mwelekeo wa kiakili mpya, wenye unyoofu. Alihitaji roho ambayo ingemsaidia akinze kishawishi na kushikamana imara na sheria na kanuni za Yehova.

Roho Takatifu Ni ya Muhimu

6. Kwa nini Daudi aliomba kwamba Yehova asimwondolee roho takatifu yake?

6 Tunapokuwa katika hali ya kukata tamaa kwa sababu ya makosa au utendaji kosa wetu, twaweza kuhisi kwamba Mungu yuko karibu kututupa kando na kutuondolea roho takatifu au kani yake ya utendaji. Daudi alihisi hivyo, kwani alimwomba Yehova hivi: “Usinitenge na uso wako, wala roho yako mtakatifu [takatifu, NW] usiniondolee.” (Zaburi 51:11) Daudi mwenye majuto na mnyenyekevu alihisi kwamba dhambi zake zilikuwa zimemfanya asistahili kumtumikia Yehova. Kutengwa na uso wa Mungu kungemaanisha kupoteza upendeleo, faraja, na baraka yake. Ikiwa Daudi angerudishwa kiroho, angehitaji roho takatifu ya Yehova. Akiwa na roho takatifu juu yake, mfalme huyo angeweza kutafuta mwelekezo wa kimungu kwa sala ili kumpendeza Yehova, ili aepuke dhambi, na ili aweze kutawala kwa hekima. Akitambua dhambi zake dhidi ya Mpaji wa roho takatifu, Daudi alisihi ifaavyo kwamba Yehova asimwondolee roho hiyo.

7. Kwa nini tusali kupata roho takatifu na tujilinde tusiihuzunishe?

7 Namna gani sisi? Twapaswa tusali ili kupata roho takatifu na ni lazima tujilinde dhidi ya kuihuzunisha kwa kushindwa kufuata mwelekezo wayo. (Luka 11:13; Waefeso 4:30) Kama sivyo, tungeweza kuipoteza roho hiyo na tusingeweza kuonyesha matunda yayo yenye kupewa na Mungu ya upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, na kujidhibiti. Yehova Mungu angetuondolea roho takatifu yake hasa ikiwa tungeendelea kutenda dhambi dhidi yake bila kutubu.

Furaha ya Wokovu

8. Tukitenda dhambi lakini twataka kuwa na shangwe ya wokovu, tunahitaji kufanya nini?

8 Mtenda dhambi mwenye kutubu anayepata kurudishwa kiroho aweza tena kushangilia katika uandalizi wa Yehova wa wokovu. Akitamani hilo, Daudi alimtolea Mungu ombi hili la bidii: “Unirudishie furaha ya wokovu wako; unitegemeze kwa roho ya wepesi.” (Zaburi 51:12) Lilikuwa jambo zuri ajabu kama nini kufurahia katika lile tumaini hakika la wokovu kupitia Yehova Mungu! (Zaburi 3:8) Baada ya kutenda dhambi dhidi ya Mungu, Daudi alijaribu kupata tena ile shangwe ya wokovu kupitia Yeye. Katika nyakati za baadaye, Yehova aliandaa wokovu kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo. Ikiwa sisi tukiwa watumishi wa Mungu walio wakfu twatenda dhambi nzito lakini twataka kupata tena ile shangwe ya wokovu, twahitaji kuwa na mtazamo wenye kutubu na ni lazima tusiendeleze dhambi yetu hadi hatua ya kutenda dhambi dhidi ya roho takatifu.—Mathayo 12:31, 32; Waebrania 6:4-6.

9. Daudi alikuwa akiomba nini alipomwomba Mungu amtegemeze “kwa roho ya wepesi”?

9 Daudi alimwomba Yehova amtegemeze “kwa roho ya wepesi.” Yaonekana, hilo halirejezei wepesi wa Mungu wa kuwa mwenye kutoa msaada wala halirejezei roho takatifu yake, bali larejezea mwelekeo wa kiakili wenye kushurutisha wa Daudi. Daudi alimtaka Mungu amtegemeze kwa kumtolea roho ya wepesi wa kufanya yafaayo na kutotumbukia katika dhambi mara nyingine tena. Yehova Mungu huwategemeza watumishi wake daima na huwainua wale waliolemewa na majaribu mbalimbali. (Zaburi 145:14) Ni jambo lenye kufariji kama nini kutambua hilo, hasa ikiwa tumekosea lakini tumetubu na twatamani kumtumikia Yehova kwa uaminifu daima milele!

Kuwafundisha Wakosaji Nini?

10, 11. (a) Daudi angeweza kuwafundisha wakosaji wa Israeli nini? (b) Daudi angeweza kuwafundisha watenda dhambi baada tu ya kufanya nini yeye mwenyewe?

10 Ikiwa Mungu angeruhusu, Daudi alitaka kufanya jambo fulani bila ubinafsi ambalo lingeonyesha uthamini wake kwa rehema ya Yehova na kuwasaidia wengine. Kwa maoni ya sala yaliyoelekezwa kwa Yehova, mfalme huyo mwenye kutubu aliendelea kutangaza hivi: “Nitawafundisha wakosaji njia zako, na wenye dhambi watarejea kwako.” (Zaburi 51:13) Daudi mwenye dhambi angeweza kuwafundishaje wakosaji Sheria ya Mungu? Angeweza kuwaambia nini? Na hilo lingeweza kuwa na faida gani?

11 Wakati ambapo angewaonyesha wakosaji wa Israeli njia za Yehova akitumaini kuwageuza kutoka katika kijia cha uovu, Daudi angeweza kuonyesha jinsi dhambi ilivyo ovu, maana ya toba, na namna ya kupokea rehema ya Mungu. Akiisha kuhisi uchungu mkali wa kutokuwa na pendeleo la Yehova na wa kuwa na dhamiri yenye hatia, bila shaka Daudi angekuwa mfunzi mwenye huruma wa watenda dhambi wenye kutubu, walio na mioyo iliyovunjika. Bila shaka, angeweza kutumia kielelezo chake ili kuwafundisha wengine baada tu ya yeye mwenyewe kukubali viwango vya Yehova na kupokea msamaha Wake, kwani wale wanaokataa kujitiisha kwa matakwa ya kimungu hawana haki ya ‘kuitangaza sheria yake.’—Zaburi 50:16, 17.

12. Daudi alifaidikaje kutokana na kujua kwake kwamba Mungu alikuwa amemkomboa kutoka katika hatia ya damu?

12 Akirudia nia zake kwa namna nyingine, Daudi alisema hivi: “Ee MUNGU [Yehova, NW], Mungu wa wokovu wangu, uniponye na damu za watu, na ulimi wangu utaiimba haki yako [uadilifu wako, NW].” (Zaburi 51:14) Hatia ya damu iliandamana na hukumu ya kifo. (Mwanzo 9:5, 6) Kwa hiyo kujua kwamba Mungu wa wokovu wake alikuwa amemkomboa kutoka katika hatia ya damu kwa habari ya Uria ungempa Daudi amani ya moyo na akili. Basi ulimi wake ungeweza kuimba kwa shangwe juu ya uadilifu wa Mungu, si wake mwenyewe. (Mhubiri 7:20; Warumi 3:10) Daudi asingeweza kutangua ukosefu wake wa adili wala kumrudisha Uria tena kutoka kaburini, sawa na vile mwanadamu wa siku hizi hawezi kurudisha usafi wa kiadili wa mtu ambaye ametongoza au kumfufua mtu ambaye amemwua. Je! hatupaswi kufikiria hilo tunaposhawishwa? Na twapaswa kuthamini kama nini rehema ambayo Yehova ameonyesha kwetu katika uadilifu! Kwa kweli, uthamini wapasa kutusukuma tuwaelekeze wengine kwenye Chanzo cha Chemichemi cha uadilifu na msamaha.

13. Ni chini ya hali zipi tu ambazo mtenda dhambi aweza kufunguliwa midomo yake ifaavyo ili kumsifu Yehova?

13 Hakuna mtenda dhambi awezaye kufungua midomo yake ifaavyo ili kumsifu Yehova isipokuwa kama Mungu aifungua kwa rehema, ili inene kweli Zake. Kwa hiyo Daudi aliimba hivi: “Ee Bwana [Yehova, NW], uifumbue midomo yangu, na kinywa changu kitazinena sifa zako.” (Zaburi 51:15) Dhamiri yake ikiwa imetulizwa kwa sababu ya msamaha wa Mungu, Daudi angesukumwa awafundishe wakosaji njia za Yehova naye angeweza kumsifu Yeye kwa hiari. Wote ambao wamesamehewa dhambi zao kama Daudi alivyosamehewa wanapaswa kuthamini fadhili isiyostahiliwa ya Mungu kuwaelekea, na wanapaswa kutumia kwa kujifaidi kila fursa ya kutangaza kweli ya Mungu na ‘kunena sifa zake.’—Zaburi 43:3.

Dhabihu Zinazokubalika kwa Mungu

14. (a) Ni dhabihu zipi zilizotakwa kulingana na agano la Sheria? (b) Kwa nini isingefaa kufikiri kwamba twaweza kulipia kosa la kuendelea kwa kufanya mambo mengine mazuri?

14 Daudi alikuwa amepata mwono-ndani wenye kina uliomsababisha aseme hivi: “Maana [Yehova] hupendezwi na dhabihu, au ningeitoa, wewe huridhii sadaka ya kuteketezwa.” (Zaburi 51:16) Agano la sheria lilihitaji kwamba dhabihu za wanyama zitolewe kwa Mungu. Lakini dhambi za Daudi za uzinzi na kuua kimakusudi, zilizoadhibika kwa kifo, zisingeweza kufunikwa kwa dhabihu hizo. Kama sivyo, angalilipa gharama yoyote ili kumtolea Yehova dhabihu za wanyama. Bila toba yenye kuhisiwa moyoni, dhabihu hazina thamani. Kwa hiyo isingefaa kufikiri kwamba tungeweza kulipia kosa lenye kuendelea kwa kufanya mambo mengine mazuri.

15. Ni nini mtazamo wa mtu ambaye amejiweka wakfu aliye na roho iliyovunjika?

15 Daudi aliongeza hivi: “Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu, hutaudharau.” (Zaburi 51:17) Kwa habari ya mtenda dhambi mwenye kutubu, “dhabihu za Mungu [zinazokubalika] ni roho iliyovunjika.” Mtu wa jinsi hiyo hana mtazamo wa kutaka vita. Moyo wa mtu aliyejiweka wakfu mwenye roho iliyovunjika unahuzunika sana kwa sababu ya dhambi yake, unanyenyekezwa kwa sababu ya kuhisi kutokubaliwa na Mungu, na una nia ya kufanya chochote ili kupata upendeleo wa kimungu tena. Hatuwezi kumtolea Mungu chochote chenye thamani mpaka tutubu dhambi zetu na kumpa mioyo yetu katika ujitoaji wa pekee.—Nahumu 1:2.

16. Mungu humwonaje mtu aliyevunjika moyo kwa sababu ya dhambi yake?

16 Mungu hakatalii mbali dhabihu kama vile moyo uliovunjika na kupondeka. Kwa hiyo ujapokuwa ugumu wowote tunaokabili tukiwa watu wake, acheni tusishindwe na hali ya kukata tamaa. Ikiwa tumekwazwa tukiwa kwenye njia ya uhai katika namna fulani inayofanya moyo wetu upaze kilio ili kupata rehema ya kimungu, bado kuna tumaini. Hata ikiwa tumetenda dhambi nzito lakini ni wenye kutubu, Yehova hatapuuza moyo wetu uliovunjika. Yeye atatusamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo na kuturudishia upendeleo Wake. (Isaya 57:15; Waebrania 4:16; 1 Yohana 2:1) Hata hivyo, kama vile Daudi, sala zetu zapasa kutolewa ili kurudishiwa upendeleo wa kimungu wala si ili kuponyoka karipio au kukosolewa kunakohitajiwa. Mungu alimsamehe Daudi, lakini alimsafisha kiadili pia.—2 Samweli 12:11-14.

Hangaiko kwa Ajili ya Ibada Safi

17. Zaidi ya kusihi kupata msamaha wa Mungu, watenda dhambi wanapaswa kufanya nini?

17 Ikiwa tumetenda dhambi fulani nzito, bila shaka hilo litatusumbua sana, na moyo wenye majuto utatusukuma tusihi kupata msamaha wa Mungu. Hata hivyo, acheni pia tutoe sala kwa ajili ya wengine. Ingawa Daudi alitazamia kutoa ibada inayokubalika kwa Mungu mara nyingine tena, zaburi yake haikuwaacha wengine nje kwa ubinafsi. Inatia ndani sihi hii kwa Yehova: “Uitendee mema Sayuni kwa radhi yako, uzijenge kuta za Yerusalemu.”—Zaburi 51:18.

18. Kwa nini Daudi mwenye kutubu alisali kwa ajili ya Sayuni?

18 Naam, Daudi alitazamia kupata tena upendeleo wa kimungu. Hata hivyo, sala ya mtunga zaburi huyo mnyenyekevu ilikuwa pia kwamba ‘Mungu angeitendea Sayuni kwa radhi yake,’ jiji kuu la Israeli, Yerusalemu, ambako Daudi alikuwa ametumaini kujenga hekalu la Mungu. Dhambi nzito za Daudi zilikuwa zimelitisha taifa nzima, kwani watu wote wangaliweza kuteseka kwa sababu ya utendaji kosa wa mfalme. (Linganisha 2 Samweli, sura 24.) Kwa kweli, dhambi zake zilidhoofisha “kuta za Yerusalemu,” hivi kwamba zilihitaji sasa kujengwa upya.

19. Ikiwa tumetenda dhambi lakini tukasamehewa, ingefaa tusali kwa ajili ya nini?

19 Ikiwa tumetenda dhambi nzito lakini tumepokea msamaha wa Mungu, ingefaa kusali kwamba arekebishe uharibifu wowote ambao mwenendo wetu umefanya. Huenda ikawa tumeleta suto juu ya jina lake takatifu, huenda ikawa tumelidhoofisha kundi, na huenda ikawa tumeletea familia yetu huzuni. Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo aweza kuondoa suto lolote ambalo limeletwa juu ya jina lake, aweza kulijenga kundi kupitia roho takatifu yake, na aweza kufariji mioyo ya wapendwa wetu wanaompenda na kumtumikia. Bila shaka, iwe dhambi yahusika au la, utakaso wa jina la Yehova na hali njema ya watu wake yapasa sikuzote liwe hangaiko letu.—Mathayo 6:9.

20. Yehova angefurahia dhabihu na matoleo ya Israeli chini ya hali zipi?

20 Ikiwa Yehova angejenga upya kuta za Sayuni, nini jingine lingetukia? Daudi aliimba hivi: “Ndipo utakapopendezwa na dhabihu za haki [uadilifu, NW], na sadaka [dhabihu, NW] za kuteketezwa, na kafara [toleo zima, NW]. Ndipo watakapotoa ng’ombe [mafahali, NW] juu ya madhabahu yako.” (Zaburi 51:19) Daudi alitamani sana kwamba yeye na taifa wangefurahia upendeleo wa Yehova ili waweze kumwabudu Yeye kwa njia inayokubalika. Kisha Mungu angependezwa na dhabihu za kuteketezwa na matoleo mazima. Hali ingekuwa hivyo kwa sababu hizo zingekuwa dhabihu za uadilifu zilizotolewa na watu waliojiweka wakfu, wenye mioyo myeupe, na wenye kutubu waliofurahia upendeleo wa Mungu. Kwa sababu ya shukrani kwa ajili ya rehema ya Yehova, wangetoa juu ya madhabahu yake mafahali—dhabihu zilizo bora zaidi na zenye gharama zaidi. Leo, tunamheshimu Yehova kwa kumletea yale tuliyo nayo yaliyo bora zaidi. Na matoleo yetu yanatia ndani “mafahali wachanga wa midomo yetu,” dhabihu za sifa kwa Mungu wetu mwenye rehema, Yehova.—Hosea 14:2, NW; Waebrania 13:15.

Yehova Husikia Vilio Vyetu

21, 22. Zaburi 51 ina masomo gani ya kutufaidi?

21 Sala ya Daudi ya kuhisiwa moyoni katika Zaburi 51 yatuonyesha kwamba twapaswa kuitikia dhambi yetu kwa roho yenye kutubu kikweli. Zaburi hiyo inatia ndani pia masomo yenye kutufaidi. Kwa mfano, tukitenda dhambi lakini ni wenye kutubu, twaweza kutumainia rehema ya Mungu. Hata hivyo, tuhangaikie hasa suto lolote ambalo huenda ikawa tumeleta juu ya jina la Yehova. (Mistari 1-4) Kama vile Daudi, twaweza kumsihi Baba yetu wa kimbingu aturehemu kwa msingi wa hali yetu yenye dhambi iliyorithiwa. (Mstari 5) Twapaswa kuwa wenye kusema kweli, na twahitaji kutafuta hekima kutoka kwa Mungu. (Mstari 6) Ikiwa tumetenda dhambi, twapaswa kumsihi Yehova atusafishe, atupe moyo safi, na roho iliyo imara.—Mistari 7-10.

22 Kutokana na Zaburi 51 twaweza kuona pia kwamba hatupaswi kamwe kujiruhusu kufanywa wagumu katika dhambi. Ikiwa tungefanya hivyo, Yehova angetuondolea roho takatifu au kani ya utendaji yake. Lakini, tukiwa na roho ya Mungu juu yetu, twaweza kwa mafanikio kuwafundisha wengine njia zake. (Mistari 11-13) Tukikosea lakini tutubu, Yehova ataturuhusu tuendelee kumsifu kwa sababu yeye hadharau kamwe moyo uliovunjika na kupondeka. (Mistari 14-17) Zaburi hiyo yaendelea kuonyesha kwamba sala zetu hazipasi kukazwa juu yetu tu. Bali, twapaswa kusali kwa ajili ya baraka na hali njema ya kiroho ya wale wote wanaoshiriki katika ibada safi ya Yehova.—Mistari 18, 19.

23. Kwa nini Zaburi 51 itusukume tuwe wenye moyo mkuu na wenye kutazamia mema?

23 Zaburi hiyo ya Daudi yenye kugusa moyo yapasa itusukume tuwe wenye moyo mkuu na wenye kutazamia mema. Yatusaidia tutambue kwamba hatuhitaji kufikiri kwamba hakuna tumaini lolote hata kama tumetumbukia katika dhambi. Kwa nini? Kwa sababu tukiwa wenye kutubu, rehema ya Yehova yaweza kutuokoa kutoka katika hali ya kukata tamaa. Tukiwa wenye majuto na wenye kujitoa kikamili kwa Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo, yeye husikia vilio vyetu vya kuomba rehema. Na inafariji kama nini kujua kwamba Yehova hadharau moyo uliovunjika!

Ungejibuje?

◻ Kwa nini Wakristo huhitaji moyo safi na roho takatifu ya Mungu?

◻ Mtu mwenye kutubu aweza kuwafundisha nini wakosaji wa sheria ya Yehova?

◻ Yehova huonaje moyo uliovunjika na kupondeka?

◻ Ni masomo gani yanayopatikana katika Zaburi 51?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Je! wewe husali ili kupata roho takatifu na kujilinda usiihuzunishe?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Onyesha uthamini kwa ajili ya fadhili isiyostahiliwa ya Yehova kwa kutangaza kweli yake

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki