Tumaini—Ulinzi Muhimu Katika Ulimwengu Usio na Tumaini
Mvulana mmoja mchanga kutoka Korea alitaka kumsaidia mama yake amsadikishe mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu aone jinsi lilivyo jambo la maana kuwa na tumaini kwa wakati ujao. Akikumbuka kielezi kimoja alichokuwa amesikia kwenye mkutano wa Kikristo, alimwuliza mwanafunzi huyo kama angemsaidia kutanzua kitendawili fulani. Mwanafunzi huyo alikubali. Mvulana huyo alisema hivi: “Kulikuwako familia mbili. Zote mbili zilikuwa maskini sana. Kulikuwa kukinyesha sana, na paa za nyumba zote mbili zilikuwa zikivuja. Familia moja ilihuzunika sana, na ililalamika sana kuhusu kuvuja huko. Lakini ile familia nyingine ilikuwa na furaha na yenye kupendeza ilipokuwa ikiziba mashimo ya paa yayo. Kwa nini kulikuwa tofauti kubwa hivyo kati ya familia hizo mbili?” Akiwa na hamu ya kujua, mwanamke huyo mchanga alijibu kwamba hakujua sababu. “Basi,” mvulana huyo akasema, “familia ya pili ilikuwa na furaha kwa sababu ilikuwa imetoka tu kupokea taarifa kutoka kwa serikali ya jiji hilo kwamba ingepewa nyumba mpya. Kwa hiyo ilikuwa na tumaini. Hiyo ndiyo iliyokuwa tofauti!”
KITENDAWILI cha mvulana huyo chatoa kielezi cha ukweli sahili: Tumaini hubadili jinsi tunavyohisi juu ya maisha, mara nyingi zijapokuwa hali zetu. Kama vile familia hizo mbili alizosimulia, wengi wetu tunalazimika kuvumilia majaribu maishani—matatizo ya afya, mahangaiko ya kiuchumi, mikazo ya familia, uhalifu, na majaribu na visa vingine vingi sana vya kutendwa vibaya. Mara nyingi, hatuwezi kuondolea mbali matatizo hayo kama vile tusivyoweza kuondolea mbali mvua na ngurumo kutoka kwa ujirani wetu. Kwa hiyo huenda tukahisi kuvurugika, tukiwa peke yetu—kwa ufupi, tukiwa hoi. Kufanya hali iwe mbaya zaidi, huenda ikawa tumefundishwa kanisani kwamba hakuna tumaini kwa wakati ujao kwa watenda dhambi wengi, kwamba huenda hiyo ikatia ndani kuadhibiwa milele.
Imesemwa kwamba mambo yanayosababisha kuvunjika moyo ni hali ya kuwa hoi na hali ya kukosa tumaini. Lakini kwa kweli tunaweza kuondolea mbali mojawapo mambo hayo; hakuna yeyote kati yetu anayelazimika kukosa tumaini. Na tumaini lenyewe linaweza kuwa silaha bora zaidi ya kugeuzia mbali lile jambo jingine, hisi za kuwa hoi. Ikiwa tuna tumaini, tunaweza kuvumilia majaribu maishani tukiwa na kadiri fulani ya utulivu na uradhi badala ya kung’ang’ana tuzidi kusonga mbele katika huzuni nyingi mno. Naam, tumaini ni ulinzi muhimu.
Je! dai hilo lakusababisha uwe mtia-shaka? Je! tumaini kwa kweli ni lenye nguvu sana hivi kwamba lasababisha tofauti hiyo kubwa? Na je, tumaini lenye kutegemeka lapatikana kwa kila mmoja wetu?
Kama Chapeo
Matabibu wameanza kutambua zile nguvu za ajabu za tumaini. Mwokokaji mmoja wa yale Machinjo Makubwa ya Nazi, mstadi wa mkazo wa akili, Dakt. Shlomo Breznitz, alitaarifu kwamba kwa habari ya matatizo mengi zaidi ya maisha, “mkazo wa akili hutokana na ufasiri wetu wa ugumu wayo, si kutokana na matatizo yenyewe. Tumaini hupunguza mkazo wayo.” Makala moja katika The Journal of the American Medical Association ilidai kwamba tumaini ni “dawa yenye nguvu.” Gazeti la American Health liliripoti hivi: “Kuna vielelezo vingi vya wagonjwa, hasa wagonjwa wa kansa, ambao hali yao inageuka kwa ghafula kuwa mbaya zaidi wakati jambo fulani linapowafanya wapoteze tumaini—au ambao hufanya maendeleo kwa ghafula wanapopata jambo jipya la kutumainia.”—Linganisha Mithali 17:22.
Wanafunzi wa Biblia wamejua kwa muda mrefu umaana wa tumaini. Kwenye 1 Wathesalonike 5:8, mtume Paulo aliwahimiza Wakristo hivi: “Tuwe na kiasi, hali tukijivika . . . chapeo yetu iwe tumaini la wokovu.” “Tumaini la wokovu” ni kama chapeo kwa jinsi gani?
Fikiria chapeo hufanya nini. Askari-jeshi wa nyakati za Biblia alivaa chapeo ya shaba nyekundu au ya chuma, iliyowekwa juu ya kofia ya tarbushi, sufu, au ngozi. Chapeo hiyo ililinda kichwa chake na mishale yenye kuruka, marungu yenye kuvurumishwa, na mapanga ya vita yenye kukatakata. Kwa hiyo, yaelekea, ni askari-jeshi wachache waliosita kuvaa chapeo ikiwa walikuwa na moja. Hata hivyo, kuvaa chapeo hakukumaanisha kwamba askari-jeshi huyo hakuweza kushindwa au kwamba hakuhisi chochote wakati kichwa chake kilipopigwa; badala ya hivyo, chapeo ilihakikisha tu kwamba mapigo mengi yalipita badala ya kufanya madhara yenye kusababisha kifo.
Kama vile chapeo inavyolinda kichwa, ndivyo tumaini linavyolinda akili. Huenda tumaini lisituwezeshe kuondoshea mbali kila tatizo au kizuizi kana kwambo si kitu. Lakini tumaini hupunguza mkazo wa matatizo hayo na lasaidia kuhakikisha kwamba hayathibitiki kuwa yenye kudhuru vibaya sana afya yetu ya kiakili, kihisiamoyo na kiroho.
Ni wazi kwamba yule mwanamume mwaminifu Abrahamu alijivika chapeo hiyo ya kitamathali. Yehova alimwomba amtoe mwana wake mpendwa, Isaka, kuwa dhabihu. (Mwanzo 22:1, 2) Lingalikuwa jambo rahisi kama nini kwa Abrahamu kutumbukia katika hali ya kukata tamaa, na katika hisi ambayo yaelekea ingalimwongoza asimtii Mungu. Ni nini kilicholinda moyo wake asiwe na hisi kama hizo? Tumaini lilikuwa jambo la msingi. Kulingana na Waebrania 11:19, “aliamini kwamba Mungu anaweza kuwafufua wafu.” (HNWW) Vivyo hivyo, tumaini la Ayubu katika ufufuo lilisaidia kulinda akili yake isiwe na uchungu, ambao ungemwongoza kumkufuru Mungu. (Ayubu 2:9, 10; 14:13-15) Yesu Kristo, akikabili kifo chenye uchungu mkali, alipata nguvu na faraja katika tumaini lake lenye shangwe kwa wakati ujao. (Waebrania 12:2) Uhakika wa kwamba Mungu hatafanya kamwe yasiyofaa, hatashindwa kamwe kutimiza neno lake, ndio msingi wa tumaini la kweli.—Waebrania 11:1.
Msingi wa Tumaini la Kweli
Kama vile imani, tumaini la kweli linategemea mambo ya hakika, uhalisi, ukweli. Hilo huenda likawashangaza baadhi ya watu. Kama vile mwandishi mmoja alivyosema, “watu wengi huonekana wakifikiri kwamba tumaini ni namna ya kipumbavu ya kukana ukweli.” Hata hivyo, tumaini la kweli si matazamio mazuri tu yaliyoahirishwa, imani dufu kwamba tutapata chochote tunachotaka au kwamba tutasuluhishiwa matatizo yetu yote madogo-madogo. Uhalisi hufutilia mbali madanganyo hayo ya kuwazia tu.
Tumaini la kweli ni tofauti. Latokana na ujuzi, si kutamani. Ebu fikiria familia ile ya pili katika kile kitendawili kilichotajwa mwanzoni. Ingalikuwa na tumaini gani ikiwa serikali yayo ilikuwa imekuwa na sifa mbaya ya kutotimiza ahadi zayo? Badala ya hivyo, ahadi hiyo pamoja na uthibitisho wa kutegemeka kwayo ingeweza kuipa familia hiyo msingi thabiti wa tumaini.
Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova leo wana tumaini linalohusika kwa ukaribu sana na serikali fulani—Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ndicho kiini hasa cha ujumbe wa Biblia. Kwa mileani mingi kimekuwa chanzo cha tumaini kwa wanawake na wanaume, kama vile Abrahamu. (Waebrania 11:10) Mungu aahidi kwamba kupitia Ufalme wake, yeye ataleta mwisho wa mfumo huu wa ulimwengu ulioharibika na kuleta mpya. (Warumi 8:20-22; 2 Petro 3:13) Tumaini hili la Ufalme ni la kweli, si ndoto. Chanzo chalo—Yehova Mungu, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima—hakitiliki shaka hata kidogo. Tunahitaji tu kuchunguza uumbaji wa Mungu wa vitu vionekanavyo ili kuona kwamba yeye yuko na ana nguvu za kutosha za kutimiza ahadi zake zote. (Warumi 1:20) Tunahitaji tu kuchunguza sana maandishi ya shughuli zake pamoja na ainabinadamu kuona kwamba neno lake halikosi kamwe kutimizwa.—Isaya 55:11.
Lakini kwa kusikitisha, wengi wanaodai kuwa Wakristo wamesahau tumaini la kweli. Mwanatheolojia Paul Tillich aliyekufa alisema hivi katika mahubiri yaliyotangazwa kwa chapa hivi majuzi: “Wakristo [wa mapema] walijifunza kuungojea mwisho. Lakini polepole waliacha kungojea. . . . Tazamio la hali mpya ya mambo duniani likaja kudhoofika, ingawa mtu alisali lije katika kila Sala ya Bwana—Mapenzi yako yatimizwe duniani kama yalivyo mbinguni!”
Huo ni msiba ulioje! Mamilioni, hata mabilioni, ya watu wenye uhitaji mkubwa sana wa tumaini hawana lolote, hata hivyo wanaweza kulipata kwa urahisi sana humohumo katika Biblia zao wenyewe. Ona matokeo yenye kuhuzunisha! Bila kuwa na tumaini la hakika lenye kulinda akili zao, je, ni jambo la ajabu hata kidogo kwamba “hali ya kiakili isiyokubaliwa” ya kukata tamaa imewaongoza wengi sana wauchafue ulimwengu kwa ukosefu wa maadili na jeuri yenye kuenea pote? (Warumi 1:28, NW) Ni muhimu sana tusitumbukie kamwe katika mtego uo huo. Badala ya kuipuuza chapeo ya tumaini, sikuzote tunahitaji kuiimarisha.
Namna ya Kujenga Tumaini Lako
Njia bora zaidi ya kujenga tumaini ni kufahamu chanzo chalo, Yehova Mungu. Jifunze Neno lake, Biblia, kwa bidii-nyendelevu. Warumi 15:4 lasema hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.”
Zaidi ya hayo, tunapaswa kuhakikisha kwamba tumaini letu kwa wakati ujao si jambo linalowaziwa tu. Tunahitaji kulifanya liwe kweli akilini mwetu. Je! unatumaini kuishi milele katika Paradiso duniani? Je! ungependa kukutana na wapendwa wako waliokufa wanapofufuliwa duniani? Ikiwa ndivyo, je unajiona mwenyewe huko wakati huo? Kwa mfano, Isaya 65:21, 22 husema juu ya kila mtu akijenga nyumba yake mwenyewe na kisha kuishi ndani yayo. Je! waweza kufunga macho yako na kujiwazia ukifanyia kazi paa ya nyumba yako mpya, ukipigilia msumari ubao wa mwisho wa paa? Ebu fikiria ukiangalia huku na huku na kuona matokeo ya mipango na kazi yako ya jasho. Mivumo michangamfu ya ujenzi yapungua; unachunguza mandhari huku vivuli vya alasiri vikinyooka juu yayo. Upepo wafanya miti iyumbeyumbe kwa uanana na kukutia baridi kukuondolea joto la kazi yako. Kicheko cha watoto, kilichochanganyika na wimbo wa ndege, chafikia masikio yako. Mazungumzo ya wapendwa wako yainuka kutoka ndani ya nyumba iliyo chini yako.
Kuona akilini wakati huo wenye furaha si kukisia bure; bali, ni kutafakari juu ya unabii utakaotimizwa kwa hakika. (2 Wakorintho 4:18) Kadiri taraja hilo lilivyo halisi zaidi kwako, ndivyo tumaini lako kwamba utakuwa huko litakavyokuwa imara zaidi. Tumaini hilo imara, lililo dhahiri litakulinda ‘usionee haya habari njema,’ jambo ambalo laweza kukufanya ujiepushe na ule mgawo wa kuzishiriki pamoja na wengine. (Warumi 1:16) Kinyume cha hilo, utataka ‘kuonea fahari tumaini’ kama mtume Paulo alivyofanya, kwa kulishiriki na wengine kwa uhakika.—Waebrania 3:6.
Kuna mengi zaidi ya wakati ujao wa milele unaotoa tumaini. Kuna vyanzo vya tumaini katika wakati wa sasa pia. Jinsi gani? Waziri wa serikali Mroma wa karne ya tano W.K. aliyeitwa Kassiodoro alisema hivi: “Yeye atambuaye faida ambayo tayari imepatikana, hupokea tumaini katika faida za wakati ujao.” Maneno yenye hekima kama nini! Tutapata faraja gani katika ahadi za baraka za wakati ujao ikiwa hatuwezi kuthamini baraka za wakati uliopo?
Sala pia hujenga tumaini wakati huu. Zaidi ya kusali kwa ajili ya wakati ujao ulio mbali, tunapaswa kusali kwa ajili ya mahitaji yetu ya sasa. Tunaweza kutumaini na kusali kwa ajili ya mahusiano bora zaidi pamoja na washiriki wa familia na Wakristo wenzetu, kusali kwa ajili ya mlo wa kiroho wetu ujao, hata kusali kwamba mahitaji yetu ya kimwili yatoshelezwe. (Zaburi 25:4; Mathayo 6:11) Kuweka matumaini hayo mikononi mwa Yehova kutatusaidia kuvumilia kila siku. (Zaburi 55:22) Tunapovumilia, uvumilivu wetu wenyewe utaimarisha pia ile chapeo ya tumaini.—Warumi 5:3-5.
Kuwa na Maoni Yenye Tumaini Kuelekea Watu
Kufikiri kusikofaa ni kama kutu juu ya chapeo ya tumaini. Inaozesha, na kidato kwa kidato huenda ikafanya chapeo kuwa isiyofaa kitu. Je! umejifunza kutambua kufikiri kusikofaa na kukushinda? Usidanganywe na lile wazo la kimakosa kwamba ule mtazamo wa kudharau-dharau, kuchambua-chambua, na kuwa na matazamio mabaya ni sawasawa na kuwa na akili nyingi. Kwa kweli, kufikiri kusikofaa kunahitaji akili kidogo sana.
Ni rahisi sana kuwa na mtazamo wa kukosa tumaini kuhusu wanadamu wenzetu. Wengine, kwa sababu ya maono machungu ya wakati uliopita, hukata tamaa wasitumaini kupokea msaada au faraja kutoka kwa watu tena. Huenda hata wakasita kuwaendea wazee wa Kikristo ili kusaidiwa na matatizo yao.
Biblia hutuambia tuwe na maoni yenye usawaziko zaidi juu ya watu. Ni kweli, si jambo la hekima kuweka matumaini yetu yote juu ya watu. (Zaburi 146:3, 4) Lakini katika kundi la Kikristo, wazee hutumikia wakiwa “zawadi katika watu” kutoka kwa Yehova. (Waefeso 4:8, 11, NW) Wao ni Wakristo wenye kudhamiria, walio na ujuzi wanaotaka kwa moyo mweupe kuwa “mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba.”—Isaya 32:2.
Wengine wengi katika kundi la Kikristo hujali sana pia juu ya kuwa chanzo cha tumaini. Ebu fikiria ni mamia ya maelfu mangapi yao wanaotenda sasa wakiwa akina mama, akina baba, akina dada, akina ndugu, na watoto kwa wale ambao wamepoteza familia zao wenyewe; fikiria ni wangapi wengine wanaotenda wakiwa rafiki “aambatanaye na mtu kuliko ndugu” kwa wale waliomo katika msononeko.—Mithali 18:24; Marko 10:30.
Ikiwa umemwomba Yehova msaada, usiache kutumaini. Huenda ikawa tayari amekujibu; huenda kukawa mzee au Mkristo mwingine mkomavu aliye tayari sasa hivi kukusaidia mara unapojulisha uhitaji wako. Tumaini lililosawazika katika watu linatulinda tusijiondoshe kutoka kwa kila mtu na kujitenga wenyewe, jambo ambalo laweza kuongoza kwenye mwenendo wenye ubinafsi, usiofaa.—Mithali 18:1.
Zaidi ya hayo, ikiwa tuna tatizo fulani pamoja na Mkristo mwenzetu, hatuhitaji kulikabili kwa mtazamo usio na tumaini, ambao haufai. Kwani, “upendo . . . hutumaini yote.” (1 Wakorintho 13:4-7) Jaribu kuwaona akina ndugu na dada wa Kikristo kama vile Yehova awaonavyo—kwa tumaini. Kazia sifa zao nzuri, watumaini, na kujitahidi kusuluhisha matatizo. Tumaini hilo hutulinda na uadui na ugomvi, ambao haumfaidi yeyote.
Usishindwe kamwe na hali ya kukosa tumaini ya ulimwengu huu wa kale unaopitilia mbali. Kuna tumaini—kwa wakati ujao wetu wa milele na pia kwa suluhisho la matatizo yetu mengi ya sasa. Je! utashikamana na tumaini? Akiwa amejivika tumaini la wokovu kama chapeo yenye kulinda, hakuna mtumishi yeyote wa Yehova aliye hoi kwelikweli—hata hali ziwe mbaya kama nini. Tusipoliacha sisi wenyewe, hakuna chochote mbinguni au duniani kiwezacho kutwalia mbali kwa nguvu tumaini ambalo Yehova ametupa sisi.—Linganisha Warumi 8:38, 39.