Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kufuata Yaliyo ya Haki Hupendekeza Huduma Yetu
KUFUATA yaliyo ya haki ni takwa la msingi kwa Wakristo. Mtume Paulo aliandika hivi kwenye Waebrania 13:18: “Tunaamini kwamba tuna dhamiri njema, tukitaka kuwa na mwenendo mwema [kujiendesha wenyewe kwa kufuata yaliyo ya haki, NW] katika mambo yote.” Kuzoea kwetu kufuata yaliyo ya haki ‘kunayapamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’ (Tito 2:10) Kufuata yaliyo ya haki, pamoja na kuhubiri Ufalme, kwa Wakristo wawili katika ufalme wa Tonga wa Pasifiki Kusini kunatoa ushahidi wenye nguvu. Ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Samoa ya Magharibi yasimulia hivi:
“Kwa miaka kadhaa, wenzi wa ndoa Mashahidi walisema na watu katika vijiji vinne kwenye kisiwa chao juu ya Ufalme wa Mungu bila kuwa na matokeo ya wazi. Halafu, mume wake alipokuwa mgonjwa, mke huyo alilazimika kutunza shamba lao kubwa na kukata na kukausha mbata, chanzo chao pekee cha kupata mshahara. Wakati ulipofika wa mbata kuchunguzwa na wanunuzi, mfuko wa mtu mwingine ulikuwa umechanganyika na mifuko yake mitano. Wana-vijiji walimhimiza abaki na mfuko huo wa ziada na kuuona kama baraka kutoka kwa Mungu. Lakini, dada huyo alikataa na, hata alipolipwa kwa mifuko sita, alikubali tu kiasi kilichokuwa chake kikweli. Kufuata kwake yaliyo ya haki kulionwa.
“Baadaye, mume wake alipohitaji kusafiri hadi kisiwa kingine, mwenye duka alimwomba mume huyo amnunulie vifaa kadhaa. Shahidi huyo alifanya alivyoombwa akamrudishia mtu huyo fedha za ziada. Mtu huyo alistaajabu. Alisema kwamba hiyo ilikuwa ni mara ya kwanza mtu yeyote alipata kumrudishia fedha za ziada. Wengine aliokuwa amewaomba kununua vitu walibaki na fedha za ziada sikuzote. Wakati mwingine, Shahidi huyo alipohitaji kitu fulani kutoka kwa duka la mtu huyo, mtu huyo alimpa ufunguo wa duka, akimwagiza achukue alichohitaji na kuacha malipo dukani. Wengine waliokuwapo walimwuliza mwenye duka huyo kwa nini angeweza kumpa Shahidi huyo ufunguo wa duka na si wao. Mwenye duka huyo alieleza kwamba Shahidi huyo alikuwa ndiye mtu peke yake katika kijiji hicho ambaye aliweza kumtumaini.
“Mwenendo mwema wa wenzi hao unazungumziwa miongoni mwa wana-vijiji. Mashahidi wanajulikana kwa kufuata kwao yaliyo ya haki, msimamo wao wa kutokuwamo katika siasa, na kutoa kwao ushahidi juu ya Ufalme wa Mungu, ambako huonyesha tofauti kati ya imani za wana-vijiji na mafundisho ya Biblia. Sasa maswali yanapotokea kuhusu Biblia, mara nyingi watu huwaendea Mashahidi ili kupata majibu. Mume huyo hata ametoka kitandani usiku, akaende kwenye mkutano wa kijiji, na kujibu maswali ambayo yametokezwa juu ya habari ya Biblia. Anapohudhuria maziko kijijini, mara nyingi ameombwa aonyeshe yale ambayo Biblia husema kuhusu kifo, na maelezo yake yamekubaliwa.”
Kwa hiyo kufuata yaliyo ya haki kwa wenzi hao Mashahidi na kuhubiri kwao Ufalme kunatoa ushahidi mzuri kwenye kisiwa hiki chenye kupendeza cha Pasifiki Kusini. Wanatumaini kwamba wengine watajifunza Biblia na kuchukua msimamo wao kwa ajili ya kweli. Wakifanya hivyo, Yehova Mungu atawabariki kwa hakika.—Yohana 8:32.