Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 9/1 kur. 10-15
  • Familia ya Kikristo Hutanguliza Mambo ya Kiroho

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Familia ya Kikristo Hutanguliza Mambo ya Kiroho
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kristo—Kielelezo Kikamilifu cha Hali ya Kiroho
  • Hatari za Kuepukwa
  • Matendo Hupaaza Sauti Kuliko Maneno
  • Uwasiliano Wenye Maana Huendeleza Hali ya Kiroho
  • Hali ya Kiroho Ni Nini? Je, Ninaweza Kuwa Mtu wa Kiroho Bila Kuwa Mshiriki wa Dini?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Kutafuta Hali ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Je, Wewe Ni Mtu wa Kimwili au Mtu wa Kiroho?
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2019
  • Songa Mbele Ukiwa Mtu wa Kiroho!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 9/1 kur. 10-15

Familia ya Kikristo Hutanguliza Mambo ya Kiroho

“Mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitivu, wanyenyekevu.”—1 PETRO 3:8.

1. Sisi sote tuna chaguo jipi, na chaguo letu linaweza kuathirije wakati wetu ujao?

ANDIKO lililo juu linafaa vizuri kama nini katika mpango wa ainabinadamu ulio wa zamani zaidi—yaani familia! Na ni jambo la maana kama nini kwamba wazazi wawe kielelezo katika mambo hayo! Kwa kawaida sifa zao zifaazo na sifa zao zisizofaa zitaonekana katika watoto. Lakini, kila mshiriki wa familia aweza kujichagulia mambo. Tukiwa Wakristo, tunaweza kuchagua kuwa watu wa kiroho au watu wa kimwili. Tunaweza kuchagua kumpendeza Mungu au kutompendeza. Chaguo hilo laweza kutokeza ama baraka, uhai wa milele na amani—ama laana, kifo cha daima.—Mwanzo 4:1, 2; Warumi 8:5-8; Wagalatia 5:19-23.

2. (a) Petro alionyeshaje hangaiko lake juu ya familia? (b) Hali ya kiroho ni nini? (Ona kielezi-chini.)

2 Maneno ya mtume kwenye 1 Petro sura ya 3, mstari wa 8, yalifuata baada tu ya shauri zuri ambalo alikuwa amewapa wake na waume. Petro alipendezwa kikweli na hali njema ya familia za Kikristo. Alijua kwamba hali ya kiroho yenye nguvu ndio ufunguo wa nyumba yenye umoja, inayojali.a Hivyo, alidokeza katika mstari wa 7 kwamba ikiwa shauri lake kwa waume lingepuuzwa, tokeo lingekuwa kizuizi cha kiroho kati ya mume na Yehova. Sala za mume zingezuiliwa ikiwa angepuuza mahitaji ya mke wake au ikiwa angemkandamiza kwa kutenda mambo yasiyo ya fadhili.

Kristo—Kielelezo Kikamilifu cha Hali ya Kiroho

3. Paulo alikaziaje kielelezo cha Kristo kwa waume?

3 Hali ya kiroho ya familia hutegemea kielelezo chema. Mume akiwa ni Mkristo mtendaji, yeye huweka kielelezo katika kuonyesha sifa za kiroho. Ikiwa hakuna mume aliye mwamini, kwa kawaida mama hujaribu kuchukua daraka hilo. Katika hali zote mbili, Yesu Kristo huandaa mfano mkamilifu wa kufuata. Sikuzote mwenendo wake, maneno yake, na fikira zake zilikuwa zenye kujenga na zenye kuburudisha. Mara kwa mara, mtume Paulo amwelekeza msomaji kwenye kigezo cha Kristo chenye upendo. Kwa kielelezo, yeye asema hivi: “Mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa; akajitoa kwa ajili yake.”—Waefeso 5:23, 25, 29; Mathayo 11:28-30; Wakolosai 3:19.

4. Ni kielelezo kipi cha hali ya kiroho kilichowekwa na Yesu?

4 Yesu alikuwa ndiye kielelezo chenye kutokeza cha hali ya kiroho na ukichwa uliodhihirishwa kwa upendo, fadhili, na huruma. Alikuwa mwenye kujidhabihu, si mwenye kula raha. Sikuzote alimtukuza Baba yake akastahi ukichwa wake. Alifuata mwongozo wa Baba, hivi kwamba aliweza kusema hivi: “Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe; kama nisikiavyo ndivyo nihukumuvyo; na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” “Sifanyi neno kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo.”—Yohana 5:30; 8:28; 1 Wakorintho 11:3.

5. Alipokuwa akiwaandalia wafuasi wake, Yesu aliwawekea waume kielelezo kipi?

5 Hiyo inamaanisha nini kwa waume? Inamaanisha kwamba katika mambo yote wanapaswa kufuata mfano wa Kristo, aliyejitiisha mwenyewe kwa Baba yake sikuzote. Kwa mfano, kama vile Yehova alivyoandaa chakula kwa namna zote za uhai duniani, ndivyo Yesu alivyoandaa chakula kwa wafuasi wake. Yeye hakupuuza mahitaji yao ya kimwili yaliyo ya msingi. Miujiza yake ya kuwalisha wanaume 5,000 na wale 4,000 ni uthibitisho wa kujali kwake na kuchukua kwake madaraka. (Marko 6:35-44; 8:1-9) Leo vilevile, vichwa vya familia wenye kujali madaraka hutunza mahitaji ya kimwili ya watu wa nyumba zao. Lakini, je, daraka lao huishia hapo?—1 Timotheo 5:8.

6. (a) Ni mahitaji gani ya maana ya familia ambayo ni lazima yashughulikiwe? (b) Waume na akina baba wanaweza kuonyeshaje ufahamu?

6 Familia zina mahitaji mengine pia yaliyo ya maana zaidi, kama Yesu alivyoonyesha. Zina mahitaji ya kiroho na ya kihisiamoyo. (Kumbukumbu la Torati 8:3; Mathayo 4:4) Tuna uhusiano na wengine, katika familia na katika kutaniko. Tunahitaji mwongozo mzuri wa kutusukuma tuwe wenye kujenga. Kwa habari hiyo waume na akina baba wana daraka kuu—na ni hivyo hasa ikiwa wao ni wazee wa kutaniko au watumishi wa huduma. Wazazi wasio na mwenzi wa ndoa wanahitaji sifa zizo hizo wanapowasaidia watoto wao. Ni lazima wazazi waelewe si yale tu yanayosemwa na washiriki wa familia bali pia yale yanayoachwa nje bila kusemwa. Hilo lataka utambuzi, wakati, na subira. Hiyo ni sababu moja kwa nini Petro aliweza kusema kwamba waume wanapaswa kuwa wenye ufikirio na kukaa pamoja na wake zao kulingana na ujuzi.—1 Timotheo 3:4, 5, 12; 1 Petro 3:7.

Hatari za Kuepukwa

7, 8. (a) Ni nini kinachohitajiwa ikiwa familia itaepuka kuvunjika kiroho? (b) Ni nini kinachohitajiwa zaidi ya mwanzo mzuri katika mwendo wa Kikristo? (Mathayo 24:13)

7 Kwa nini kuelekeza fikira kwenye hali ya kiroho ya familia ni jambo la maana? Ili kutoa kielezi, tunaweza kuuliza, Kwa nini ni jambo la maana kwa nahodha wa meli kutoa uangalifu mwingi kwa ramani zake anapoongoza meli kupitia maji yenye hatari yaliyo na sehemu zenye maji machache? Katika Agosti 1992 ile meli ya kuvinjari iitwayo Queen Elizabeth 2 (QE2) ilipitishwa katika eneo lenye mafungu ya mchanga na miamba ambamo makosa ya kuongoza meli husemwa kuwa ya kawaida. Mkazi mmoja wa hapo alieleza hivi: “[Manahodha] wengi wamepoteza kazi zao kwa sababu ya eneo hilo.” Meli hiyo QE2 iligonga mwamba uliokuwa chini ya maji. Hilo likawa kosa lenye gharama. Theluthi moja ya meli iliharibika, ikawa lazima meli hiyo isitumiwe kwa majuma kadhaa ili itengenezwe.

8 Vilevile, “nahodha” wa familia akikosa kuchunguza kwa uangalifu ramani, yaani Neno la Mungu, familia yake yaweza kupatwa na madhara ya kiroho kwa urahisi. Kwa mzee wa kutaniko au mtumishi wa huduma, tokeo laweza kuwa kupoteza mapendeleo ndani ya kutaniko na labda madhara mazito kwa washiriki wengine wa familia. Kwa hiyo, ni lazima kila Mkristo awe mwangalifu asiangukie hali ya kutosheka kiroho, akitumainia tu mazoea mazuri ya kujifunza na bidii aliyokuwa nayo zamani. Katika mwendo wetu wa Kikristo, jambo la kwamba tulianza vizuri halitoshi; ni lazima safari ikamilishwe kwa mafanikio.—1 Wakorintho 9:24-27; 1 Timotheo 1:19.

9. (a) Funzo la kibinafsi ni la maana kadiri gani? (b) Ni maswali gani yanayofaa tuwezayo kujiuliza wenyewe?

9 Ili kuepuka hali ya kiroho yenye maji machache, miamba, na mafungu ya mchanga, tunahitaji kwenda sambamba na “ramani” zetu kwa kujifunza Neno la Mungu kwa kawaida. Hatuwezi kutegemea tu lile funzo la msingi lililotuleta ndani ya kweli. Nguvu zetu za kiroho zinategemea programu ya kawaida na yenye usawaziko ya funzo na utumishi. Kwa kielelezo, tunapohudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi la kutaniko tukiwa na toleo hili hasa mkononi, twaweza kujiuliza wenyewe hivi, ‘Je! mimi binafsi, au sisi tukiwa familia, kwa kweli tumejifunza makala hii, tukiyafungua maandiko na kutafakari juu ya matumizi yayo? Au tumeyapiga majibu mstari tu? Je! labda hata tumepuuza kusoma makala hii kabla ya kuhudhuria mkutano?’ Majibu yenye moyo mweupe kwa maswali hayo yaweza kutusukuma tufikirie kwa uzito mazoea yetu ya kujifunza na kuamsha tamaa ya kufanya maendeleo—hiyo ikiwa lazima.—Waebrania 5:12-14.

10. Kwa nini ni jambo la maana kujichunguza mwenyewe?

10 Kwa nini ni jambo la maana kujichunguza hivyo? Kwa sababu tunaishi katika ulimwengu unaotawalwa na roho ya Shetani, ulimwengu unaojaribu, kwa njia za hila, kukengeusha imani yetu katika Mungu na ahadi zake. Ni ulimwengu unaotaka kutushughulisha sana hivi kwamba hatuna wakati wa kushughulikia mahitaji ya kiroho. Kwa hiyo twaweza kujiuliza wenyewe, ‘Je! familia yangu ni yenye nguvu kiroho? Je! mimi nikiwa mzazi ni mwenye nguvu kadiri nipaswavyo kuwa? Je! sisi tukiwa familia tunasitawisha ile kani ya kiroho itendeshayo akili inayotusaidia kufanya maamuzi yenye msingi wa uadilifu na uaminifu-mshikamanifu?’—Waefeso 4:23, 24.

11. Kwa nini mikutano ya Kikristo ni yenye mafaa kiroho? Toa kielelezo.

11 Hali yetu ya kiroho inapasa kuimarishwa na kila mkutano tunaohudhuria. Muda wa saa hizo zenye thamani kwenye Jumba la Ufalme au kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko husaidia kutuburudisha baada ya ule muda wa saa nyingi ambao tunalazimika kutumia tukijaribu kuendelea kuishi katika ulimwengu wa Shetani wenye uadui. Kwa kielelezo, limekuwa jambo la kuburudisha kama nini kujifunza kile kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi! Hilo limetusaidia tupate ufahamu mzuri zaidi juu ya Yesu, maisha yake, na huduma yake. Tumeyasoma kwa uangalifu maandiko yaliyotajwa bila kunakili maneno, tumefanya utafiti wa kibinafsi, na hivyo kujifunza mengi kutokana na kile kielelezo ambacho Yesu aliweka.—Waebrania 12:1-3; 1 Petro 2:21.

12. Huduma ya shambani hutahinije hali yetu ya kiroho?

12 Mtihani mzuri wa hali yetu ya kiroho ni huduma ya Kikristo. Ili tudumu katika ushahidi wetu rasmi na wa vivi hivi, mara nyingi tukikabili watu wenye ubaridi au wanaopinga, tunahitaji msukumo ufaao, upendo kwa Mungu na upendo kwa jirani. Bila shaka, hakuna mtu apendaye kukataliwa mbali, na hilo laweza kutokea katika huduma yetu ya shambani. Lakini tunapaswa kukumbuka kwamba habari njema ndiyo inayokataliwa mbali, si sisi tukiwa watu mmoja mmoja. Yesu alisema hivi: “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. . . . Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.”—Yohana 15:18-21.

Matendo Hupaaza Sauti Kuliko Maneno

13. Mtu mmoja anaweza kudhoofishaje hali ya kiroho ya familia?

13 Ni nini hutokea katika familia wakati washiriki wote isipokuwa mmoja wanapostahi unadhifu na usafi wa nyumba? Katika siku yenye mvua, wote isipokuwa yule msahaulifu, wanakuwa waangalifu wasilete mstari wa matope ndani ya nyumba. Nyayo zenye matope kila mahali ni uthibitisho wa kutojali kwa mtu huyo, akiongezea wengine kazi. Jambo lilo hilo lahusu hali ya kiroho. Mtu mmoja tu mwenye ubinafsi au asiyejali aweza kuharibu sifa njema ya familia. Wote nyumbani, si wazazi tu, wanapaswa kujitahidi kuonyesha nia ya akili ya Kristo. Inaburudisha kama nini wakati wote wanapofanya kazi pamoja wakiwa na uhai wa milele mbele yao! Mtazamo wa familia hiyo ni wa kiroho (wala si wa kujitafutia uadilifu). Hali ya kupuuza mambo ya kiroho inaonekana mara haba katika nyumba hiyo.—Mhubiri 7:16; 1 Petro 4:1, 2.

14. Shetani huweka vishawishi vipi vya kimwili njiani mwetu?

14 Sisi sote tuna mahitaji ya kimwili ya msingi ambayo ni lazima yatimizwe ili kutegemeza maisha yetu kila siku. (Mathayo 6:11, 30-32) Lakini mara nyingi mahitaji yetu hufunikwa na mambo tunayotamani. Kwa kielelezo, mfumo wa Shetani hututolea vidude na vifaa vya aina zote. Ikiwa sikuzote tunataka kuwa na vitu vya kisasa katika mambo yote, hatutaridhika kamwe, kwa kuwa vitu vya kisasa huwa vya zamani upesi, na kitu kipya hutokea. Ulimwengu wa biashara umefanyiza kawaida inayojirudiarudia bila kikomo. Unatushawishi tutafute fedha nyingi zaidi ili kuridhisha tamaa yetu ya kupata vitu zaidi. Laweza kuongoza kwenye “tamaa nyingi zisizo na maana” au “mapendezi ya kipumbavu na ya hatari.” Hilo laweza kutokeza maisha yasiyo na usawaziko yakiwa na wakati unaozidi kupungua wa kushiriki katika utendaji wa kiroho.—1 Timotheo 6:9, 10; The Jerusalem Bible.

15. Kielelezo cha kichwa cha familia ni cha maana katika njia gani?

15 Hapa pia, kielelezo kinachowekwa na kichwa cha nyumba ya Kikristo ni cha maana sana. Mtazamo wake wenye usawaziko kuelekea madaraka ya kilimwengu na ya kiroho unapaswa kuwachochea wale washiriki wengine wa familia. Kwa hakika lingekuwa jambo lenye kudhuru ikiwa baba angetoa maagizo bora kabisa lakini ashindwe kuishi kulingana na maneno yake mwenyewe. Watoto wanaweza kutambua upesi ule mwelekeo wa maisha ya fanya-kama-nisemavyo-si-kama-nifanyavyo. Vivyo hivyo, mzee wa kutaniko au mtumishi wa huduma anayewatia moyo wengine katika huduma ya nyumba kwa nyumba na ambaye hajiungi sana na familia yake katika utendaji huo, upesi hukosa kuaminika katika familia na katika kutaniko pia.—1 Wakorintho 15:58; linganisha Mathayo 23:3.

16. Twaweza kujiuliza maswali gani?

16 Kwa hiyo, tunaweza kuyachunguza maisha zetu kwa faida. Je! tunajishughulisha sana katika kutimiza mafanikio ya kilimwengu tukipuuza kufanya maendeleo ya kiroho? Je! tunafanya maendeleo katika ulimwengu lakini kurudi nyuma katika kutaniko? Kumbuka shauri hili la Paulo: “Taarifa hii ni aminifu. Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye atamani kazi nzuri.” (1 Timotheo 3:1, NW) Kujali madaraka katika kutaniko ni wonyesho dhahiri zaidi wa hali yetu ya kiroho kuliko kupandishwa cheo kazini. Ni lazima usawaziko wenye uangalifu udumishwe ili kutowaruhusu waajiri wetu watuongoze kana kwamba tulijiweka wakfu kwao na si kwa Yehova.—Mathayo 6:24.

Uwasiliano Wenye Maana Huendeleza Hali ya Kiroho

17. Ni nini kinachochangia kusitawishwa kwa upendo wa kweli katika familia?

17 Mamilioni ya nyumba leo yamekuja kwa kweli kuwa kama makao ya kulala tu. Namna gani? Washiriki wa familia huja nyumbani kulala na kula tu, kisha wanaondoka upesi. Wanaketi mezani kufurahia mlo pamoja mara haba sana. Hakuna uhusiano wa karibu katika familia. Tokeo ni nini? Hakuna uwasiliano, hakuna mazungumzo ya maana. Na hilo laweza kutokeza ukosefu wa kupendezwa na washiriki wengine, labda ukosefu wa hangaiko la kweli. Tunapopendana, tunafanya wakati wa kuzungumza na kusikiliza. Tunatia moyo, na tunasaidia. Sehemu hiyo ya hali ya kiroho inatia ndani uwasiliano wa maana kati ya mume na mke na kati ya wazazi na watoto.b Hilo hutaka wakati na busara tunapojaribu kupata habari kutoka kwa mmoja na mwenzake ili kushiriki furaha zetu, maono, na matatizo yetu.—1 Wakorintho 13:4-8; Yakobo 1:19.

18. (a) Mara nyingi ni nini huwa kizuizi kikubwa cha uwasiliano? (b) Ni nini msingi wa mahusiano yenye maana?

18 Uwasiliano mzuri unataka wakati na jitihada. Unamaanisha kuweka kando wakati wa kuongea na kusikilizana. Kimojawapo vizuizi vikubwa zaidi kwa hilo ni kile chombo chenye kutumia wakati mwingi ambacho huchukua mahali pa heshima katika nyumba nyingi—yaani televisheni. Hilo hutokeza mwito wa kupaswa kujibu swali—je! televisheni hukudhibiti, au wewe huidhibiti? Kudhibiti televisheni kunataka azimio thabiti—kutia ndani nia yenye nguvu ya kuizima. Lakini kufanya hivyo kutatufungulia njia ya kupatana tukiwa washiriki wa familia na tukiwa ndugu na dada za kiroho. Mahusiano yenye maana hutaka uwasiliano mzuri, kupata kuelewana, mahitaji yetu na shangwe zetu, kuambiana kadiri tunavyothamini yale mambo yote yenye fadhili ambayo tumefanyiwa. Yaani, mazungumzo ya maana huonyesha kwamba tunawathamini wengine.—Mithali 31:28, 29.

19, 20. Tukiwajali wote katika familia, tutafanya nini?

19 Kwa hiyo, tukijaliana katika mazingira ya familia—na hilo latia ndani kuwajali washiriki wa familia wasio waamini—tutakuwa tukichangia sana kujenga na kudumisha hali yetu ya kiroho. Katika mazingira ya familia, tutakuwa tukifuata shauri hili la Petro: “Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu; watu wasiolipa baya kwa baya, au laumu kwa laumu; bali wenye kubariki; kwa sababu hayo ndiyo mliyoitiwa ili mrithi baraka.”—1 Petro 3:8, 9.

20 Tunaweza kuwa na baraka ya Yehova sasa tukijitahidi kudumisha hali yetu ya kiroho, na hilo laweza kuchangia kurithi kwetu baraka yake wakati ujao tunapopokea ile zawadi ya uhai wa milele kwenye dunia-paradiso. Kuna mambo mengine ambayo tunaweza kufanya tukiwa familia ili kusaidiana kiroho. Makala ifuatayo itazungumzia manufaa za kufanya mambo pamoja tukiwa familia.—Luka 23:43; Ufunuo 21:1-4.

[Maelezo ya Chini]

a Hali ya kiroho hufasiliwa kuwa “kuhisi upesi au kushikamana na kanuni za kidini: sifa au hali ya kuwa mtu wa kiroho.” (Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary) Mtu wa kiroho ni kinyume cha mtu wa kimwili, wa kinyama.—1 Wakorintho 2:13-16; Wagalatia 5:16, 25; Yakobo 3:14, 15; Yuda 19.

b Ili kupata madokezo zaidi juu ya uwasiliano wa familia, ona Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1991, kurasa 20-2.

Je! Wakumbuka?

◻ Hali ya kiroho ni nini?

◻ Kichwa cha familia anaweza kuigaje kielelezo cha Kristo?

◻ Tunaweza kuepukaje matisho dhidi ya hali yetu ya kiroho?

◻ Ni nini kiwezacho kudhoofisha hali ya kiroho ya familia?

◻ Kwa nini ni muhimu kuwa na uwasiliano wenye maana?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko huimarisha familia kiroho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki