“Adui wa Mwisho” Atashindwa!
ULIPOKUWA mtoto, huenda ikawa uliogopa giza. Huenda ikawa hadithi zenye kuogofya na hata vioja fulani vilikutia wasiwasi mwingi. Ilikupa uhakikishio kama nini wakati mama au baba yako alipoacha taa ikiwaka huku ukijaribu kupata usingizi!
Kifo vilevile huwaogopesha wengi. Lakini, si lazima iwe hivyo. Kwa nini? Kwa sababu ya vile kifo kilivyo hasa.
Mjue Adui Wako
Mfalme Sulemani wa Israeli la kale mwenye hekima alijulisha hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Kulingana na wazo hilo lililopuliziwa kimungu lipatikanalo katika Biblia yako mwenyewe, kifo ni kinyume cha uhai tu. Wafu hawana maisha ya kuwa na fahamu.
Akirejezea kifo kwa njia ya kielezi, mtume Mkristo Paulo aandika hivi: “Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako [kichomi chako, NW]?” Ni nini kile kichomi kitokezacho kifo? Paulo asema hivi: “Uchungu wa [kichomi cha, NW] mauti ni dhambi.” (1 Wakorintho 15:55, 56; Hosea 13:14) Basi, ni nini chanzo cha kichomi hicho chenye kuua? Kwingineko katika Maandiko, Paulo asema hivi: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Mtume haachi shaka lolote juu ya utambulisho wa “mtu [huyo] mmoja” asemapo hivi: “Katika Adamu wote wanakufa.” (1 Wakorintho 15:22) Ndiyo, kupitia kutokutii kwa babu yetu wa kwanza, Adamu, sisi sote twaweza kupatwa na kichomi cha kifo.—Mwanzo 3:1-19.
Tukiwa na afya njema na familia yenye upendo katika mazingira yenye kupendeza, hakuna yeyote kati yetu angechagua kufa. Hata hivyo, kama vile Biblia ionyeshavyo, “wakati na tukio lisilotazamiwa” laweza kutunyang’anya uhai. (Mhubiri 9:11, NW) Kwa kweli, hatujui kitakachoupata uhai wetu kesho. (Yakobo 4:14) Jambo moja ni hakika—sisi sote tumerithi dhambi na kifo. Kwa hiyo, kifo hutunyemelea na kushambulia kama adui.
Kukabiliana na Kifo cha Mpendwa
Kifo ni adui hasa kinaposhambulia mpendwa. Mke mmoja mwenye ugonjwa usiotibika alimwambia mume wake hivi alipokuwa akitazamia kufa, “wewe utaathiriwa vibaya zaidi.” Kwa nini angeweza kusema hivyo? Kwa sababu Biblia husema hivi: “Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [Sheoli, NW, kaburi la kawaida la ainabinadamu] uendako wewe.” (Mhubiri 9:10) Wafu hawateseki tena. Lakini mzigo wa majonzi hutwishwa watu wa ukoo na marafiki waliobaki. Je! lolote laweza kufanywa juu ya kuteseka huko?
Kurasa za Neno la Mungu, Biblia, zina maneno mengi ya faraja. Kwa kielelezo, kusoma na kutafakari juu ya zaburi ni chanzo kimoja cha kitulizo kwa hakika. Kwa kweli maneno kama haya ni yenye kufariji: “Na ahimidiwe Bwana [Yehova, NW], siku kwa siku hutuchukulia mzigo wetu; Mungu ndiye wokovu wetu.”—Zaburi 68:19.
Chanzo kingine cha faraja ni kutaniko la Kikristo. Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo aliandika hivi: “Uwaheshimu wajane walio wajane kweli kweli. Lakini mjane akiwa ana watoto au wajukuu [wanaoweza kumtunza kimwili], na wajifunze kwanza kuyatenda yaliyo wajibu wao kwa jamaa zao wenyewe, na kuwalipa wazazi wao. Kwa kuwa hili lakubalika mbele za Mungu. Mjane asiandikwe isipokuwa umri wake amepata miaka sitini; naye amekuwa mke wa mume mmoja; naye ameshuhudiwa kwa matendo mema; ikiwa amelea watoto, ikiwa amekaribisha wageni, ikiwa amewaosha watakatifu miguu, ikiwa amewasaidia wateswao, ikiwa amefuata kwa bidii kila tendo jema.” (1 Timotheo 5:3, 4, 9, 10) Leo vilevile Mashahidi wa Yehova husaidia na kufariji waamini wenzao wa jinsi hiyo.
Mara nyingi rekebisho lililo kubwa zaidi ambalo waliofiwa walazimika kufanya ni la kihisiamoyo. “Nilimpenda mke wangu sana,” akaandika mwanamume mmoja ambaye mwenzi wake alikufa miaka miwili iliyotangulia. “Tukio hili ndilo lenye kuhuzunisha zaidi maishani mwangu, na naliona kuwa gumu sana kuvumilia.” Mtu ambaye ameoa au kuolewa kwa muda fulani ameshiriki maisha yake katika uhusiano wa kibinadamu ulio wa karibu zaidi. Mwenzi wa ndoa anapokufa, mwenzi anayebaki huhisi hasara kubwa kiasili. Huyo aweza kumwendea nani ili kupata msaada?
Katika hali kama hizo, washiriki wazuri Wakristo waweza kuwa wenye kujenga. “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu,” yasema mithali moja yenye hekima. (Mithali 17:17) Mjane wa kike au mjane wa kiume huhitaji msaada—marafiki watoao utegemezo halisi. Marafiki wenye hekima humtia moyo mwenye majonzi azungumze, hata ikiwa kufanya hivyo kwaleta machozi. Labda Mkristo ambaye tayari amepatwa na uchungu na maumivu ya moyo ya kupoteza mwenzi aweza kutoa msaada fulani wenye fadhili. ‘Semeni kwa kuliwaza walioshuka moyo,’ Biblia hushauri. (1 Wathesalonike 5:14, NW) Lakini kumbuka kwamba wajane wa kike na wajane wa kiume huwakumbuka wenzi wao wa ndoa kwa hamu. Kwa hiyo, waliofiwa wapaswa kuwafunulia wengine mawazo yao ya siri wakiwa tu chini ya hali zinazowezesha wote wadumishe mwenendo safi.—1 Petro 2:12.
Dawa bora zaidi kwa ajili ya umivu liletwalo na kifo ni kuendelea kuwa na shughuli nyingi katika kuwasaidia wengine—si jambo rahisi kwa wale ambao huamini kwamba wao ndio wanaohitaji msaada! Hapa ndipo kutokuwa na ubinafsi huhusika. Kuwafanyia wengine mambo bila ubinafsi kwasaidia kuondosha huzuni na majonzi, kwani Yesu alisema hivi: “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.
Ushindi Juu ya Kifo
Kichomi cha nyuki chaweza kuumiza sana, hata kuua. Lakini kwa kawaida, kuondolewa kwa kichomaji cha mdudu kilichokazwa imara katika ngozi yako kitasaidia kuleta kitulizo. Lakini kuna mataraja gani ya kupata kitulizo kutoka kichomi kitokezacho kifo?
Baada ya kueleza kwamba dhambi ndiyo kichomi kitokezacho kifo, Paulo apaaza mshangao hivi: “Mungu na ashukuriwe atupaye kushinda kwa Bwana wetu Yesu Kristo.” (1 Wakorintho 15:57) Ushindi juu ya kifo unahusianaje na Kristo? Yesu alionyesha kwamba ni hivyo aliposema hivi juu yake mwenyewe: “Mwana wa Adamu [ha]kuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Mathayo 20:28) Ndiyo, kwa wale wazoeao imani katika Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, na dhabihu ya fidia ambayo Yehova ameandaa kupitia yeye, kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu hakitatokeza hali ya kutokuwako yenye kudumu.—Yohana 3:16.
Maneno haya ya Yesu yanatia moyo kwelikweli: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:28, 29.
Karne kadhaa kabla ya hapo, nabii wa Mungu Isaya alikuwa ametabiri hivi: “[Yehova Mungu] a[ta]meza mauti hata milele; na Bwana MUNGU [Yehova, NW] atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isaya 25:8) Tena, kwenye Ufunuo 21:4, Biblia hutoa taraja hili zuri ajabu: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena, kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Kwa kutiwa nguvu na tumaini hilo la Biblia kwa wale walalao katika kifo, wale waliofiwa hawahitaji ‘kuhuzunika kama na wengine wasio na tumaini.’—1 Wathesalonike 4:13.
Jaribu kuona akilini yale ambayo Mungu ameiwekea ainabinadamu, kama vile imefunuliwa katika Biblia. “Dhiki ile iliyo kuu” ambayo yakaribia sana yamaanisha maangamizo kwa mfumo mwovu wa mambo uliopo. (Ufunuo 7:14) Wale wazoeao dini bandia wameharibiwa. Sehemu zenye kutawala na za kibiashara zenye pupa ambazo huchangia njaa kali na vita zimeondoka. Yesu Kristo achukua hatua kumtia katika abiso Shetani Ibilisi, ambaye amesababisha vifo vya wanadamu wengi. Halafu Kristo aanza Utawala wake wa Mileani (Miaka Elfu), ambao katika huo atumia thamani ya dhabihu yake ya fidia kwa ainabinadamu. Wafu warudi katika ufufuo ambao umetumainiwa, na nuru kutoka katika Neno la Mungu yang’aa kwa wangavu sana hivi kwamba maoni ya ushirikina juu ya kifo, adui ya ainabinadamu, hayako tena. Wote walio hai wakati huo wana fursa ya kujifunza njia za Mungu na kufuata viwango vyake vyenye uadilifu.—Mithali 4:18; Matendo 24:15; Waebrania 2:14, 15; Ufunuo 18:4-8; 19:19-21; 20:1-3.
‘Hapo ndipo mwisho,’ asema Paulo, ‘Kristo Yesu atakapompa Mungu Baba ufalme wake. Maana yeye amiliki hata Mungu awekapo maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho kifo, atakapobatilishwa.’ (1 Wakorintho 15:24-26) Kila ulemavu utokanao na dhambi ya Adamu umeondoka. Mtihani wa mwisho watukia, na wampendao Mungu waupita kwa uaminifu. (Ufunuo 20:4-10) Wakiisha kurejezwa kwenye ukamilifu, wanadamu hao watiifu waishi, si kwa miaka sabini tu au hata miaka mia na kumi, bali milele. Hiyo ni zawadi iliyoje kutoka kwa Mungu kupitia Mwana wake mpendwa!—Warumi 6:23.
Kwa hiyo basi, wewe waweza kuishi muda gani? Muda wa maisha yako waweza kurefuka kwa umilele wote. Kwa kuwa waishi katika “wakati wa mwisho” wa ulimwengu huu, huenda usife kamwe. (Danieli 12:4; Yohana 11:25, 26; 17:3) Ukifanya mapenzi ya kimungu, waweza kuishi hadi kuingia ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa.—2 Petro 3:13.
Hata hivyo, ikiwa wewe ni mzee-mzee, wahitaji kufikiria kwa uhalisi uwezekano wa kufa. Kwa hakika, tumaini la ufufuo huleta shangwe. Lakini huenda ukajiuliza jinsi Yehova atakavyopanga maisha ya familia katika mfumo mpya huo wa mambo. Usiruhusu mambo hayo yakuhangaishe, kwani Yehova atahakikishia furaha yenye kudumu ya wale walio waaminifu kwake milele.
“Siku [hizi] za mwisho” zenye hatari za mfumo mwovu wa Shetani ziendeleapo hadi umalizio wazo, usiruhusu hofu ya kifo ikunyang’anye pendeleo la kumtumikia Yehova sasa. (2 Timotheo 3:1) Ukimpoteza mpendwa katika kifo, jiliwaze mwenyewe kwa kufikiria hali yacho ya muda tu. (Ufunuo 20:13, 14) Itibari katika tumaini la ufufuo. Halafu, iwe waingia ule ulimwengu mpya kwa kuokoka dhiki kubwa au kwa ufufuo, uwe na uhakikishio wa ile ahadi hakika iliyopuliziwa kwamba kifo, adui wa mwisho, kitabatilishwa.—Ufunuo 7:9, 14.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Washiriki wazuri Wakristo waweza kuwajenga kiroho wale waliofiwa
[Picha katika ukurasa wa 7]
Kuwa na shughuli nyingi katika kuwasaidia wengine hupunguza majonzi yasababishwayo na kifo cha mpendwa