Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 1/15 kur. 24-30
  • Mikusanyiko Yenye Kusisimua Yaendeleza Ufundishaji wa Kimungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mikusanyiko Yenye Kusisimua Yaendeleza Ufundishaji wa Kimungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Alasiri ya Siku ya Kwanza
  • Asubuhi ya Pili
  • Alasiri ya Pili
  • Asubuhi ya Siku ya Tatu
  • Alasiri ya Siku ya Tatu
  • Asubuhi ya Nne
  • Alasiri ya Mwisho
  • Walimu wa Neno la Mungu Wahimizwa Watimize Kazi Yao
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” Wakusanyika kwa Shangwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Mtukuze Mungu, Si Mwanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Watekelezaji wa Neno la Munngu Hupata Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 1/15 kur. 24-30

Mikusanyiko Yenye Kusisimua Yaendeleza Ufundishaji wa Kimungu

LEO, ulimwengu unapokea habari nyingi mno. Katika televisheni na redio, kwa namna ya vitabu au kupitia kompyuta, kuna ugavi wa ujuzi ambao karibu hauna kikomo juu ya habari yoyote ile iwazikayo. Bado, watu hupatwa na magonjwa na kufa. Uhalifu, njaa, na umaskini uko kotekote duniani, na matatizo ya kihisiamoyo huwaathiri watu zaidi kuliko wakati mwingine wowote. Ujuzi wote unaopatikana umeshindwa kusahihisha mambo. Kwa nini? Kwa sababu ainabinadamu imepuuza hekima ya Mungu.

Basi, yafaa kama nini kwamba, “Ufundishaji wa Kimungu” kilikuwa ndicho kichwa kilichochaguliwa kwa ajili ya mikusanyiko ya hivi karibuni ya Mashahidi wa Yehova! Programu iliwakumbusha wale waliokuwapo kwamba ni ufundishaji upatikanao katika Neno la Mungu, Biblia pekee, ulio na thamani halisi yenye kuokoa uhai.

Mkusanyiko wa kwanza ulianza Alhamisi, Juni 3, katika Uniondale, New York, U.S.A. Tangu wakati huo na kuendelea, programu ilitolewa katika majiji tofauti-tofauti katika nchi moja baada ya nyingine, ikiishia katika kontinenti za Afrika na Amerika Kusini.

Alasiri ya Siku ya Kwanza

Kila siku ilikuwa na kichwa kilichokazia sehemu fulani ya ufundishaji wa kimungu. Kwa kielelezo, programu kwa ajili ya siku ya kwanza ilitegemea kichwa “Kujua Mafundisho Yatokayo kwa Mungu.” (Yohana 7:17) Wazo hilo lilikuzwa vema siku ilipoendelea.

Baada ya wimbo na sala, mwenyekiti wa mkusanyiko alifungua programu kwa hotuba yenye kichwa “Ufundishaji wa Kimungu Hutuleta Pamoja.” Alionyesha kwamba watu wa Yehova wameunganika kwa kujifunza njia Zake na kutembea katika vijia Vyake. (Mika 4:1-5) Ufundishaji wa kimungu hutia nguvu muungano wao. Wakusanyikaji walitiwa moyo washangilie katika ushirika wao uliounganika.—Zaburi 133:1-3.

Baadaye kidogo katika alasiri hiyo, mikutano ya kutaniko ya kawaida ilizungumziwa katika mfululizo wenye kichwa “Mikutano Inayotuagiza Juu ya Njia za Yehova.” Msemaji wa kwanza aliwakumbusha wakusanyikaji kwamba tukutanapo pamoja, sisi humheshimu Yehova na hivyo kupokea baraka Yake. Msemaji aliyefuata alikazia uhitaji wa kushiriki katika mikutano. Katika kufanya hivyo, twamsifu Yehova hadharani, twaonyesha imani yetu, na kutia nguvu imani ya wengine. Msemaji wa tatu katika mfululizo huo alionyesha uhitaji wa kuzoea yale tunayojifunza mikutanoni. Ni lazima tuwe “watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu.”—Yakobo 1:22.

Yaliyofuata ni mazungumzo mazuri juu ya kumwimbia Yehova sifa. Wimbo wa kuhisiwa moyoni ni sehemu ya maana ya ibada yetu. Hotuba hiyo ilifuatwa na hotuba ya msingi, “Ufundishaji wa Kimungu Hushinda.” Kilikuwa kichwa bora sana kama nini! “Yehova ndiye Chanzo cha ufundishaji bora zaidi ambao yeyote aweza kupokea,” akasema msemaji. Kisha, baada ya mazungumzo mafupi juu ya muujiza wa ubongo wa kibinadamu, alisema hivi: “Twapaswa kutumia uwezo wetu wa kufikiri hasa ili tupokee ufundishaji wa kimungu. Huo pekee ndio hutokeza hekima ya kweli.” Ni kweli kama nini!

Asubuhi ya Pili

“Endeleeni Kuyapamba Mafundisho ya Mwokozi Wetu, Mungu” kilikuwa ndicho kichwa cha siku ya pili ya mkusanyiko. (Tito 2:10, NW) Kanuni hiyo ilitokeza katika hotuba “Ufundishaji wa Kimungu Dhidi ya Mafundisho ya Mashetani.” Ndiyo, roho waovu wana mafundisho yao. (1 Timotheo 4:1) Kama vile msemaji huyo alivyoeleza, ufundishaji wa kimungu huishinda “hekima” ya Shetani kwa kufunua mafundisho bandia na njia za Ibilisi zenye hila. Kwa sababu hiyo, Wakristo wapatao 4,500,000 wenye mioyo ifaayo si watumwa tena katika giza la Shetani.—Yohana 8:32.

Bado, ni lazima tuendelee kumkinza Shetani. Hilo lilikaziwa kwa hotuba “Je! Unakinza Roho ya Ulimwengu?” Roho ya ulimwengu huu ni yenye kufisha. Hiyo hutia moyo adili zenye kushusha heshima, maoni ya kuasi mamlaka, na tamaa kubwa ya kupata vitu vya kimwili. Ni lazima Mkristo ajichunguze daima. Je! bado ana viwango vya juu kwa habari ya yale atazamayo, asikilizayo, au asomayo? Kwa kutia moyo, msemaji alisema: “Tunawapongeza ninyi akina ndugu, dada, na wachanga kwa ajili ya jitihada kubwa ambayo tayari mnafanya kuhusu jambo hili.”—1 Yohana 2:15-17.

Kuna jambo moja linalofanya iwe vigumu kukinza roho ya ulimwengu. Hilo ni nini? Sisi sote si wakamilifu. Kweli, Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, lakini ni lazima bado tupige vita dhidi ya mbetuko wa kufanya dhambi. Hilo lilizungumziwa katika hotuba “Kushindana na Mshiko wa Dhambi juu ya Mwili Wenye Dhambi.” Miongoni mwa mambo mengine, msemaji alisema kwamba sisi twaweza kushinda katika kung’ang’ana kwetu dhidi ya dhambi tukijivika utu mpya na kuepuka chochote kinachotosheleza mielekeo yetu yenye dhambi.

“Fanya Fundisho Lenye Afya Liwe Njia Yako ya Maisha” ndicho kilikuwa kichwa cha hotuba iliyofuata. Wengine hufikiria afya yao ya kimwili kupita kiasi. Lakini, kwa kweli, afya ya kiroho ni ya maana zaidi. Msemaji alikazia uhitaji wa kuchukua madaraka yetu kwa uzito kwa habari hiyo, na alikuwa na maneno ya kutia moyo hasa wanawake Wakristo. Alisema hivi: “Twathamini sana akina dada wenye umri mkubwa zaidi na dada wenye umri mdogo zaidi pia ambao ni wenye usawaziko mzuri katika bidii yao kwa ajili ya huduma na katika kutunza madaraka ya kibinafsi.” Ndiyo, na sisi sote twamshukuru Yehova kwa ajili ya fundisho lenye afya litutenganishalo na ulimwengu.

Hotuba yenye kichwa “Ufundishaji wa Kimungu Hufunua Kusudi la Uhai,” ndiyo iliyomalizia programu ya asubuhi. Msemaji alisema hivi, “Wakati mmoja au mwingine, karibu kila mtu huja kujiuliza, ‘Kusudi la uhai ni nini?’” Kwa hoja zenye nguvu, alithibitisha kwamba ni Biblia tu hutoa jibu halisi kwa swali hilo. Kisha, msemaji huyo alionyesha kwamba ahadi za Mungu za ajabu hutupa sisi kusudi la uhai kwa njia yenye matokeo. Yaelekea, wengi kati ya wasikilizaji walikuwa wakifikiri hivi, ‘Hili ndilo jambo hasa ambalo watu katika eneo langu wahitaji kusikia.’ Baraza Linaloongoza lilikubaliana na hilo. Broshua mpya, yenye kichwa, Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai? ilitolewa mwishoni mwa hotuba hiyo. Kila mtu alifurahi kama nini! Pumziko la katikati ya siku lilitoa fursa ya kupitia kichapo hicho kipya.

Alasiri ya Pili

Hotuba ya kwanza katika alasiri ilikuwa na kichwa chenye kufariji “Mtwikeni Yehova Mahangaiko Yenu Yote.” Mambo mengi husababisha hangaiko; lakini, Neno la Mungu husema kwamba twapaswa kumtupia mahangaiko yetu yote. (1 Petro 5:6, 7) Kweli, matatizo mengine huendelea, na kwa habari hiyo msemaji alihimiza hivi: ‘Uwe mwenye subira. Mngojee Yehova. Amini kwa uthabiti kwamba kufuata Biblia ndilo jambo lifaalo zaidi sikuzote. Tukikazia mioyo yetu Yehova, tutakuja kufurahia “amani ya Mungu” ipitayo akili zote.’—Wafilipi 4:6, 7.

Hotuba nne zilizofuata zilionyesha kwamba ufundishaji wa kimungu hutumika kuhusiana na maisha ya familia. Ile ya kwanza, “Kufanya Ndoa Iwe Muungano Wenye Kudumu,” iliwakumbusha wakusanyikaji kwamba machoni pa Yehova ndoa si jambo liwezalo kutupiliwa mbali, kama vile ionwavyo na wengi ulimwenguni. Hata hivyo, ili kuifanikisha ndoa, ni lazima tufuate mwongozo wa Yehova. Yeye alitufanya sisi. Kwa hiyo, Neno lake lililopuliziwa lina shauri bora zaidi la ndoa lipatikanalo.

Hotuba “Jitahidi Kwa Ajili ya Wokovu wa Nyumba Yako” ilizungumzia magumu ya kutunza familia katika nyakati hizi za hatari. (2 Timotheo 3:1) Wazazi huwafundisha watoto wao usafi wa kimwili, tabia nzuri, jinsi ya kufanya kazi, na jinsi ya kuwa wakarimu na wenye kujali kuelekea wengine. La maana zaidi, ni lazima wafundishe wazao wao wawe watumishi wa Yehova wenye kujitoa.—Mithali 22:6.

Katika mazungumzo yaliyofuata, “Wazazi, Watoto Wenu Wahitaji Uangalifu wa Pekee,” msemaji aliwakumbusha wakusanyikaji uhitaji wa kupongeza watoto, bila kupuuza udhaifu wao mbalimbali. Ni lazima wazazi wawe macho kuona hasa mibetuko kuelekea ukosefu wa kufuatia yaliyo haki, kupenda vitu vya kimwili, au ubinafsi.

Wakusanyikaji wachanga zaidi hasa walisikiliza kwa uangalifu hotuba “Vijana—Mnatii Mafundisho ya Nani?” Mambo ni magumu kwa Wakristo wachanga leo. Kwenda sambamba na ulimwengu ni rahisi, lakini hilo huongoza kwenye kifo. Ingawa kuchagua kushikamana na ufundishaji wa kimungu huhitaji moyo mkuu kwa kijana, hilo huleta baraka nyingi sasa na uhai wa milele baadaye.—1 Timotheo 4:8.

Siku ya pili ilimalizika kwa drama yenye kuchangamsha moyo Vijana Wamkumbukao Muumba Wao Sasa. Katika utangulizi, mwelekezi aliwaita vijana walio katika tengenezo la Mungu “jeshi la kitheokrasi linaloshiriki kwa uaminifu-mshikamanifu katika utumishi wa kujitolea kwa Yehova Mungu na Kristo Yesu, Mfalme wa kimbingu aliyewekwa rasmi.” Yeye akaongeza hivi: “Vijana wetu kwa kweli wanatimiza jambo jema!” Drama hiyo ilionyesha kwa wazi kwamba mzazi akimzoeza mtoto wake vema, hilo litamfaidi mtoto akuapo na kumtumikia Yehova akiwa peke yake.

Asubuhi ya Siku ya Tatu

Kichwa cha siku ya tatu kilikuwa “Endeleeni Kufundisha Watu wa Mataifa Yote.” (Mathayo 28:19, 20) Bila shaka wakusanyikaji walitazamia shauri la wakati ufaao juu ya kazi ya kuhubiri, nao hawakukatishwa tamaa. Mfululizo wenye kichwa “Kutimiza kwa Shangwe Agizo Letu la Kuhubiri na Kufundisha” ulitia nguvu azimio lao la kuendelea kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi. Hotuba ya kufungua ilizungumzia ziara za kwanza; ya pili, ziara za kurudia; na ya tatu, mafunzo ya Biblia. Wamishonari ulimwenguni pote walikuwa wamealikwa kurudi nyumbani na kuhudhuria mkusanyiko pamoja na familia na marafiki wao. Katika mahali fulani-fulani, wamishonari walishiriki katika sehemu hiyo ya programu. Ilipendeza kupokea mwono-ndani katika mafanikio wanayopata katika migawo yao. Hotuba iliyofuata, “Kufikia Kila Mtu na Habari Njema” ilizungumzia matokeo ya kutoa ushahidi vivi hivi.

Asubuhi ilimalizika kwa hotuba ya ubatizo, ambayo sikuzote ni jambo kuu kwenye makusanyiko makubwa ya Mashahidi wa Yehova. Katika mkusanyiko mmoja baada ya mwingine, vikundi vikubwa vya watu waliojiweka wakfu karibuni vilisimama mbele ya umati uliokuwa umekusanyika na kujibu ndiyo kwa hakika yale maswali mawili yaliyoelekezwa kwao. Kisha walibatizwa hadharani. Ni ithibati yenye nguvu kama nini ya matokeo matukufu ya ufundishaji wa kimungu!

Alasiri ya Siku ya Tatu

Programu ya alasiri ilianza kwa mazungumzo ya Kimaandiko yenye kina. Mashahidi wa Yehova wanafahamu maneno ya Mathayo sura ya 24 na Luka sura ya 21. Je! wengine walifikiri kwamba hakuna jambo jipya ambalo lingeweza kusemwa juu ya sura hizo za Biblia? Walikosea kama nini! Zile hotuba “Ni Nini Itakayokuwa Ishara ya Kuwapo Kwako?” na “Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?” ziliwaongoza wakusanyikaji kupitia mazungumzo yenye kusisimua juu ya sehemu za sura hizo mbili na zilitoa maelezo ya karibuni zaidi juu ya mistari kadhaa. Kulikuwa na mazungumzo yenye uchangamfu baada ya kipindi hicho huku wakusanyikaji wakizungumzia maoni yao pamoja kuona ikiwa walikuwa wameelewa mambo makuu. Bila shaka, maswali mengi yatajibiwa wakati habari hiyo inapochapishwa katika Mnara wa Mlinzi.

Kichwa cha funzo la Biblia kiliendelezwa katika hotuba “Majibu Yenye Kuarifu kwa Maswali Yako ya Biblia.” Kisha programu ikaelekeza fikira kwenye habari nyingine tofauti. Mwaka 1993 ulitia alama mwaka wa 50 wa Watchtower Bible School of Gilead. Hotuba “Miaka Hamsini ya Mazoezi ya Wamishonari Katika Gileadi na Utendaji Wayo” iliwaonyesha wakusanyikaji yale yaliyokuwa yametimizwa katika kipindi hicho. Ikiwa kulikuwapo wamishonari wowote wakati wa hotuba “Mambo Yaliyotimizwa Katika Kueneza Evanjeli Katika Shamba la Tufeni Pote,” wao walialikwa washiriki baadhi ya maono yao pamoja na wasikilizaji. Kusikia masimulizi ya wamishonari kulisisimua sana!

Hotuba iliyofuata, “Sababu Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Hufuliza Kulinda,” ilikuwa somo jingine la historia. Ilionyesha kwamba Wakristo wamekuwa wakilinda tangu karne ya kwanza W.K. hadi sasa. Hilo liliongoza kwenye jambo jingine lenye kushangaza. Mapema katika hotuba iliyofuata, yenye kichwa “Wapiga Mbiu ya Ufalme Walio Watendaji Duniani Pote,” msemaji aliinua buku kubwa (ikiwa lilipatikana tayari katika lugha ya mahali fulani) na kusema: “Ni furaha kutangaza hapa leo kutolewa kwa kitabu hiki kipya, chenye kichwa Mashahidi wa Yehova—Wapiga Mbiu ya Ufalme wa Mungu.” Kitabu hicho kina simulizi lenye mambo mengi juu ya historia ya Mashahidi wa Yehova ya ki-siku-hizi. Chasimulia habari yenye kusisimua juu ya uvumilivu, maazimio, na mafanikio, kikitoa ithibati yenye nguvu ya utendaji wa roho ya Yehova juu ya watumishi wake.

Asubuhi ya Nne

Tayari ilikuwa siku ya mwisho ya mkusanyiko. Kichwa cha siku hiyo, “Kujinufaisha Wenyewe kwa Ufundishaji wa Kimungu,” kiliahidi upeo mzuri kwa programu. (Isaya 48:17) Asubuhi fikira za wakusanyikaji zilikaziwa mfululizo wa hotuba tatu zenye nguvu. Ukiwa na kichwa “Ujumbe Wenye Kuonya Uliopuliziwa wa Yeremia—Kwa Ajili ya Wakati Uliopita na wa Kisasa,” mfululizo huo ulikuwa na mazungumzo ya mstari kwa mstari juu ya Yeremia sura za 23, 24, na 25. Sura hizo zina ujumbe wenye nguvu kama nini! Ni lazima Israeli lisilo jaminifu la siku za Yeremia lilitetemeka kwa sababu ya maonyo yake ya waziwazi, yaliyopuliziwa kimungu. Ulimwengu mzima ulitetemeka hata zaidi wakati maonyo hayo yalipotimizwa. Je! mambo ni tofauti leo? Hasha. Mashahidi wa Yehova huhubiri kwa moyo mkuu ujumbe wa Mungu wa hukumu. Hatimaye, mfumo huu mzima wa mambo utalazimika kukabili matendo ya Yehova ya hukumu. Hilo litamaanisha uharibifu kamili kwa ulimwengu wa Shetani.

Jumapili asubuhi ilimalizika kwa drama ya pili, Usidanganyike Wala Kumdhihaki Mungu. Kwa njia ya wazi, ilionyeshwa jinsi ufundishaji wa kimungu waweza kutulinda tusivutwe na vidio na muziki ushushao heshima na tusivutwe na mwelekeo wa kupanda fitina miongoni mwa Wakristo wenzetu. Kwenye umalizio wa drama hiyo, mwenyekiti alinukuu maneno haya yenye kuchochea fikira ya mmoja wa waigizaji: “Sisi si wasioweza kuambukizwa na uvutano wa ulimwengu. Tusipoukinza, ulimwengu waweza kufisidi fikira zetu kwa hila. Iwe tutabaki waaminifu au la itategemea kile ambacho tumekuwa tukipanda.” Ni kweli kama nini!

Alasiri ya Mwisho

Mkusanyiko ulikuwa ukikaribia mwisho kwa haraka msemaji alipokwenda jukwaani kutoa hotuba ya watu wote yenye kichwa, “Ufundishaji Wenye Kusaidia Kwa Ajili ya Nyakati Zetu Zenye Hatari.” Kwa njia iliyo wazi na yenye kufuatana, alitambulisha matatizo makuu yanayotuathiri leo na kuonyesha njia kadhaa ambazo ufundishaji wa kimungu waweza kutusaidia tufurahie maisha bora zaidi. Alisema kwamba ikiwa tunafuata ufundishaji wa Kimaandiko sasa, tutaweza kuufuata milele katika ulimwengu mpya wa Yehova.

Baada ya muhtasari wa somo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, ulikuwa wakati wa hotuba ya mwisho. Msemaji alipitia kwa haraka mambo makuu ya ile programu ya siku nne akawakumbusha wakusanyikaji juu ya vichapo vipya. Alitangaza pia kwamba vidio ya pili katika ule mfululizo The Bible—A Book of Fact and Prophecy ingetolewa karibuni. Kwa kweli, vidio hiyo yenye kichwa, The Bible—Mankind’s Oldest Modern Book inapatikana sasa katika Kiingereza. Ripoti zenye kugusa moyo zilisomwa kutoka mahali ambapo pana hatari kuu, kama vile Bosnia na Herzegovina. Kwa kumalizia, msemaji alisoma maneno ya Mhubiri 12:13: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”

Hicho ni kikumbusha kizuri kama nini! Acheni tuishi kwa ajili ya ile siku ambayo ainabinadamu yote itasifu Mfunzi wetu Mtukufu, Yehova, na kutii ufundishaji wake wa kimungu.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Mikusanyiko ya “Ufundishaji wa Kimungu” katika Moscow na Kiev ilitokeza shangwe kuu

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

1. Kwa kubatizwa, wengi walifananisha wakfu wao kwa Mungu

2. Mkusanyikaji mwenye umri wa miaka 100 alisisimuka kupokea kichapo kipya

3, 4. Drama zenye kuchochea fikira zilithaminiwa sana

5. Wamishonari waliohojiwa kwenye mikusanyiko walikazia manufaa za ufundishaji wa kimungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki