Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 3/15 kur. 10-15
  • Yehova Mungu wa Kusudi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Mungu wa Kusudi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu wa Kusudi
  • Makusudi Yake Yafunuliwa Hatua kwa Hatua
  • Kunurishwa
  • Wengi Huchagua Kutojua
  • Fuata Nuru ya Ulimwengu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wachukuaji Nuru—Kwa Kusudi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Kusudi la Mungu kwa Kufanya Wengine ‘Wazaliwe Mara ya Pili’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Kusudi Lenyewe la Uhai
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 3/15 kur. 10-15

Yehova Mungu wa Kusudi

“Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.”—ISAYA 14:24.

1, 2. Watu wengi husema nini juu ya kusudi la uhai?

WATU kila mahali huuliza hivi: “Kusudi la uhai ni nini?” Kiongozi mmoja wa kisiasa wa Magharibi alisema hivi: “Watu wengi zaidi ya wakati mwingine wowote wanauliza, ‘Sisi ni nani? Kusudi letu ni nini?’” Gazeti moja lilipoomba maoni ya vijana juu ya suala la ni nini kusudi la uhai, majibu ya kawaida yalikuwa: “Kufanya lolote ambalo moyo wako watamani.” “Kuishi kila dakika ya maisha yako kwa ukamili zaidi.” “Kuishi kwa raha na starehe.” “Kuzaa watoto, kufurahi, na kisha kufa.” Wengi wao walihisi kwamba uhai ndio uu huu tu. Hakuna mtu aliyesema juu ya kusudi la uhai duniani lenye kudumu muda mrefu.

2 Msomi mmoja Mkonfusho alisema hivi: “Kusudi kuu la uhai limo katika kuwapo kwetu kwa kibinadamu, ambako ni kwa kawaida.” Kulingana na hayo, watu wangeendelea kuzaliwa, wang’ang’ane kwa miaka 70 au 80, kisha wafe na wasiwepo milele. Mwanasayansi mmoja wa mageuzi alisema hivi: “Huenda tukatamani kupata jibu la ‘juu zaidi’—lakini hakuna lolote.” Kwa wanamageuzi hao, uhai ni mng’ang’ano wa kuendelea kuishi, mwisho wao ukiwa kifo. Falsafa hizo hutokeza maoni yasiyo na tumaini juu ya uhai.

3, 4. Hali za ulimwengu huathirije vile wengi waonavyo uhai?

3 Watu wengi hushuku kama uhai una kusudi wanapoona kwamba kuwapo kwa binadamu kumejaa taabu nyingi sana. Katika wakati wetu, ambapo mwanadamu apaswa kuwa amefikia kilele cha utimizo wa kiviwanda na kisayansi, karibu watu bilioni moja ulimwenguni pote ni wagonjwa mahututi au hawana lishe bora. Mamilioni ya watoto hufa kila mwaka kutokana na sababu kama hizo. Zaidi ya hayo, kwa sababu ya vita, karne hii ya 20 imekuwa na vifo vingi mara nne zaidi ya miaka mia nne iliyotangulia ikiwekwa pamoja. Uhalifu, jeuri, utumizi wa dawa za kulevya, kuvunjika kwa familia, UKIMWI na maradhi mengineyo yanayopitishwa kingono—orodha ya mambo yasiyofaa huongezeka. Viongozi wa ulimwengu hawana utatuzi kwa matatizo hayo.

4 Kwa kufikiria hali hizo, mtu mmoja alisema hivi juu ya yale ambayo wengi huamini: “Uhai hauna kusudi. Ikiwa mambo haya yote mabaya yanatukia, basi uhai hauna maana sana.” Na mtu mmoja mzee-mzee alisema hivi: “Kwa muda mrefu wa maisha yangu, nimekuwa nikijiuliza ni kwa nini nipo hapa. Ikiwa kuna kusudi, mimi sijali tena.” Kwa hiyo kwa sababu watu wengi hawajui kwa nini Mungu huruhusu kuteseka, hali za ulimwengu zenye kutaabisha huwafanya wakose tumaini halisi kwa ajili ya wakati ujao.

5. Kwa nini dini za ulimwengu huu huongeza mvurugo juu ya kusudi la uhai?

5 Hata viongozi wa kidini wamegawanyika, na hawana uhakika, juu ya kusudi la uhai. Aliyekuwa kiongozi wa Kathedro ya St. Paul jijini London alisema hivi: “Maishani mwangu mwote nimejitahidi sana kupata kusudi la kuishi. . . . Nimeshindwa.” Ni kweli, makasisi wengi hufundisha kwamba watu wanapokufa, wale wema huenda mbinguni na wale wabaya huenda kwenye helo yenye moto milele. Lakini maoni hayo bado huacha ainabinadamu duniani iendelee na mwendo wayo wa kuteseka. Na ikiwa kusudi la Mungu lilikuwa watu waishi mbinguni, kwa nini yeye hakuwafanya tu kuwa viumbe wa kimbingu kwanza, kama alivyowafanya malaika, na hivyo aepushe wanadamu wasiteseke sana? Kwa hiyo ni jambo la kawaida kuwa na mvurugo juu ya kusudi la uhai duniani au kukataa kuamini kwamba uhai una kusudi lolote.

Mungu wa Kusudi

6, 7. Biblia hutuambia nini juu ya Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima?

6 Lakini, Biblia Takatifu, kile kitabu chenye kuenezwa kwa wingi zaidi ya vyote katika historia, hutuambia kwamba Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote mzima, ni Mungu wa kusudi. Hiyo hutuonyesha kwamba yeye ana kusudi la muda mrefu, ambalo kwa kweli, ni la milele kwa ajili ya jamii ya kibinadamu duniani. Na Yehova akusudiapo jambo, halina budi kutukia. Kama vile mvua ichipushavyo mbegu, asema Mungu, “ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.” (Isaya 55:10, 11) Lolote Yehova asemalo atatimiza, “ndivyo itakavyotokea.”—Isaya 14:24.

7 Sisi binadamu twaweza kuwa na uhakika kamili kwamba yule Mweza Yote atatimiza ahadi zake, kwani Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2; Waebrania 6:18) Atuambiapo kwamba atafanya jambo fulani, neno lake ni uhakikisho kwamba litatimia. Ni kana kwamba tayari limetimizwa. Yeye ajulisha hivi: “Mimi ni Mungu, wala hapana mwingine; mimi ni Mungu, wala hapana aliye kama mimi; nitangazaye mwisho tangu mwanzo, na tangu zamani za kale mambo yasiyotendeka bado; nikisema, Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote. . . . Nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya.”—Isaya 46:9-11.

8. Je! wale wanaotaka kumjua Mungu kikweli waweza kumpata?

8 Isitoshe, Yehova “hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba.” (2 Petro 3:9) Kwa sababu hiyo, yeye hataki mtu yeyote akose kumjua. Nabii aitwaye Azaria alisema hivi: “Mkimtafuta [Mungu] ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi.” (2 Mambo ya Nyakati 15:1, 2) Kwa hiyo, wale ambao wataka kumjua Mungu na makusudi yake kikweli waweza bila shaka kufanya hivyo ikiwa watafanya jitihada ya kumtafuta yeye.

9, 10. (a) Ni nini kimeandaliwa kwa wale wanaotaka kumjua Mungu? (b) Jitihada ya kuchunguza katika Neno la Mungu hutuwezesha sisi kufanya nini?

9 Wamtafute wapi? Kwa wale wanaomtafuta Mungu kikweli, yeye ameandaa Neno lake, Biblia. Kupitia roho takatifu yake, kani ya utendaji ileile aliyotumia kuumba ulimwengu wote mzima, Mungu alielekeza wanaume waaminifu waandike yale tunayohitaji kujua juu ya makusudi yake. Kwa kielelezo, kuhusu unabii wa Biblia, mtume Petro alisema: “Unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW].” (2 Petro 1:21) Vivyo hivyo, mtume Paulo alijulisha hivi: “Kila andiko, [ni] lenye pumzi ya Mungu, [na] lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili [mwenye uwezo kamili, NW], amekamilishwa [amepewa vifaa kikamili, NW] apate kutenda kila tendo jema.”—2 Timotheo 3:16, 17; 1 Wathesalonike 2:13.

10 Angalia kwamba Neno la Mungu hutuwezesha kuwa ‘wenye uwezo kamili, waliopewa vifaa kikamili.’ Hilo huwezesha mtu awe na uhakika Mungu ni nani, makusudi yake ni nini, na yale atakayo kutoka kwa watumishi wake. Hilo ni la kutazamiwa kutoka kwa kitabu kilichotungwa na Mungu. Na ndicho chanzo pekee tunachoweza kutafuta ili kupata ujuzi sahihi juu ya Mungu. (Mithali 2:1-5; Yohana 17:3) Kwa kufanya hivyo, hatutakuwa “tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu.” (Waefeso 4:13, 14) Mtunga-zaburi alisema hivi juu ya maoni yanayofaa: “Neno lako [Mungu] ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.”—Zaburi 119:105.

Makusudi Yake Yafunuliwa Hatua kwa Hatua

11. Yehova amefunuaje makusudi yake kwa ainabinadamu?

11 Mwanzoni kabisa mwa familia ya kibinadamu, Yehova alifunua makusudi yake kuelekea dunia hii na wanadamu walioko juu yayo. (Mwanzo 1:26-30) Lakini wazazi wetu wa kwanza walipokataa enzi kuu ya Mungu, ainabinadamu iliingia katika giza la kiroho na kifo. (Warumi 5:12) Hata hivyo, Yehova alijua kwamba kungekuwa na wale ambao wangetaka kumtumikia. Kwa hiyo, kwa karne nyingi zilizopita, yeye amefunua makusudi yake hatua kwa hatua kwa watumishi wake waaminifu. Baadhi ya wale aliowasiliana nao ni Enoki (Mwanzo 5:24; Yuda 14, 15), Noa (Mwanzo 6:9, 13), Abrahamu (Mwanzo 12:1-3), na Musa (Kutoka 31:18; 34:27, 28). Nabii wa Mungu Amosi aliandika hivi: “Hakika Bwana MUNGU [Yehova, NW] hatafanya neno lo lote, bila kuwafunulia watumishi wake manabii siri yake.”—Amosi 3:7; Danieli 2:27, 28.

12. Yesu alitoaje nuru zaidi juu ya makusudi ya Mungu?

12 Mwana wa Mungu, Yesu Kristo alipokuwa duniani yapata miaka 4,000 baada ya uasi katika Edeni, mambo mengi madogo-madogo juu ya makusudi ya Yehova yalifunuliwa. Ilikuwa hivyo hasa kuhusu kusudi la Mungu la kusimamisha Ufalme wa kimbingu ambao utatawala juu ya dunia. (Danieli 2:44) Yesu alifanya Ufalme huo uwe kichwa kikuu cha mafundisho yake. (Mathayo 4:17; 6:10) Yeye na wanafunzi wake walifundisha kwamba chini ya Ufalme, kusudi la awali la Mungu kwa ajili ya dunia na ainabinadamu lingetimizwa. Dunia ingebadilishwa kuwa paradiso inayokaliwa na wanadamu wakamilifu, ambao wangeishi milele. (Zaburi 37:29; Mathayo 5:5; Luka 23:43; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:4) Zaidi ya hiyo, kwa miujiza ambayo Mungu aliwapa uwezo wa kufanya, Yesu na wanafunzi wake walionyesha yale ambayo yangetukia katika ulimwengu huo mpya.—Mathayo 10:1, 8; 15:30, 31; Yohana 11:25-44.

13. Kwa habari ya shughuli za Mungu pamoja na jamii ya kibinadamu, ni badiliko gani lililotukia kwenye Pentekoste 33 W.K.?

13 Kwenye Pentekoste 33 W.K., siku 50 baada ya kifo cha Yesu, roho ya Mungu ilimwagwa juu ya kutaniko la wafuasi wa Kristo. Hiyo ilifanya mahali pa Israeli lisilo jaminifu wakiwa watu wa agano la Yehova pachukuliwe. (Mathayo 21:43; 27:51; Matendo 2:1-4) Kumwagwa kwa roho takatifu kwenye pindi hiyo kulikuwa uthibitisho kwamba, kuanzia wakati huo na kuendelea, Mungu angefunua kweli juu ya makusudi yake kupitia wakala huo mpya. (Waefeso 3:10) Wakati wa karne ya kwanza W.K., kiunzi cha kitengenezo cha kutaniko la Kikristo kikaanzishwa.—1 Wakorintho 12:27-31; Waefeso 4:11, 12.

14. Watafutaji kweli waweza kutambuaje kutaniko la Kikristo la kweli?

14 Leo, watafutaji kweli waweza kutambua kutaniko la Kikristo la kweli kwa wonyesho walo wenye kuendelea wa sifa kuu ya Mungu, upendo. (1 Yohana 4:8, 16) Kwelikweli, upendo wa kidugu ni alama yenye kutambulisha Ukristo wa kweli. Yesu alisema hivi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” “Amri yangu ndiyo hii, Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 13:35; 15:12) Na Yesu aliwakumbusha wasikilizaji wake hivi: “Ninyi mmekuwa rafiki zangu, mkitenda niwaamuruyo.” (Yohana 15:14) Kwa hiyo watumishi wa kweli wa Mungu ni wale wanaoishi kupatana na sheria ya upendo. Wao hawasemi tu juu ya upendo, kwani “imani pasipo matendo imekufa.”—Yakobo 2:26.

Kunurishwa

15. Watumishi wa Mungu waweza kuwa na uhakika juu ya jambo gani?

15 Yesu alitabiri kwamba kwa kupita kwa wakati, kutaniko la Kikristo la kweli lingenurishwa zaidi na zaidi juu ya makusudi ya Mungu. Yeye aliahidi wafuasi wake hivi: “Huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW], ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote.” (Yohana 14:26) Yesu alisema hivi pia: “Tazama, mimi nipo pamoja nanyi sikuzote, hata ukamilifu wa dahari [umalizio wa mfumo wa mambo, NW].” (Mathayo 28:20) Hivyo, kunurishwa juu ya kweli ya Mungu na makusudi yake huongezeka miongoni mwa watumishi wa Mungu. Ndiyo, “njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—Mithali 4:18.

16. Kunurishwa kwetu kiroho hutuambia nini juu ya mahali tulipo kwa habari ya makusudi ya Mungu?

16 Leo, nuru hiyo ya kiroho ni nyangavu kuliko wakati mwingine wowote, kwani tumo katika wakati ambapo unabii mwingi wa Biblia unatimizwa au unakaribia kutimizwa. Huo watuonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo ulio mwovu. Huu ndio wakati uitwao “umalizio wa mfumo wa mambo”; utafuatwa na ulimwengu mpya wa Mungu. (2 Timotheo 3:1-5, 13; Mathayo 24:3-13, NW) Kama ilivyotabiriwa na Danieli, Ufalme wa kimbingu wa Mungu karibuni “utavunja falme hizi zote [zilizoko sasa] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

17, 18. Ni unabii gani mwingi mtukufu unaotimizwa sasa?

17 Miongoni mwa unabii mwingi unaotimizwa sasa ni ule uliorekodiwa katika mstari wa 14 wa Mathayo sura ya 24. Hapo Yesu alisema hivi: “Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.” Kazi hiyo ya kuhubiri Ufalme inafanywa na mamilioni ya Mashahidi wa Yehova duniani pote. Na kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu wanajiunga nao. Hiyo yapatana na unabii kwenye Isaya 2:2, 3, unaosema kwamba “katika siku za mwisho” za ulimwengu huu mwovu, watu kutoka mataifa mengi wangekuja kwenye ibada ya kweli ya Yehova, naye ‘angewafundisha njia zake, nao wangekwenda katika mapito yake.’

18 Wapya hao wanamiminika kwenye ibada ya Yehova, “kama wingu,” kama ilivyotabiriwa kwenye Isaya sura ya 60, mstari wa 8. Mstari wa 22 waongeza hivi: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari; Mimi, BWANA [Yehova, NW], nitayahimiza hayo wakati wake.” Uthibitisho waonyesha kwamba wakati huo ndio sasa. Na wapya waweza kuwa na uhakika kwamba kwa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, wamelipata kutaniko la Kikristo la kweli.

19. Kwa nini twasema kwamba wapya wanaoshirikiana na Mashahidi wa Yehova wanakuja kwenye kutaniko la Kikristo la kweli?

19 Kwa nini twaweza kusema hivyo kwa uhakika? Kwa sababu wapya hao, kutia na mamilioni ambao tayari wamo katika tengenezo la Yehova, wameweka maisha zao wakfu kwa Mungu na wanafanya mapenzi yake. Hiyo yatia ndani kuishi kupatana na ile sheria ya upendo wa kimungu. Uthibitisho mmoja wa hilo ni kwamba, Wakristo hao wamefua ‘panga zao zikawa majembe, na mikuki yao ikawa miundu, wala hawajifunzi vita tena kamwe.’ (Isaya 2:4) Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wamefanya hivyo kwa sababu wao ni wenye upendo. Hiyo yamaanisha kwamba hawawezi kamwe kuchukua silaha za vita dhidi ya mmoja na mwenzake au mtu mwingine yeyote. Katika jambo hilo wao ni wa pekee—tofauti na dini za ulimwengu. (Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:10-12, 15) Wao hawajihusishi na utukuzo wa taifa wenye kugawanya, kwani wanafanyiza udugu wa tufeni pote uliounganishwa na upendo, kile “kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:14, NW; Mathayo 23:8; 1 Yohana 4:20, 21.

Wengi Huchagua Kutojua

20, 21. Kwa nini walio wengi sana wa ainabinadamu wamo katika giza la kiroho? (2 Wakorintho 4:4; 1 Yohana 5:19)

20 Ingawa nuru ya kiroho miongoni mwa watumishi wa Mungu yazidi kung’aa, idadi ya watu wa sehemu iliyobaki ya dunia inatokomea zaidi na zaidi katika giza la kiroho. Hawamjui Yehova au makusudi yake. Nabii wa Mungu alieleza juu ya wakati huu aliposema hivi: “Maana, tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Ni hivyo kwa sababu wao hawadhihirishi upendezi wa kweli katika kujifunza juu ya Mungu, wala hawaonyeshi tamaa ya kujaribu kumpendeza. Yesu alisema hivi: “Na hili ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu. Maana kila mtu atendaye mabaya huichukia nuru, wala haji kwenye nuru, matendo yake yasije yakakemewa.”—Yohana 3:19, 20.

21 Watu kama hao hawana upendezi wa kweli wa kutaka kujua mapenzi ya Mungu. Badala ya hivyo, wao hukazia fikira zao kufanya mapenzi yao wenyewe. Kwa kupuuza mapenzi ya Mungu, wao hujiweka katika hali iliyo hatari, kwani Neno lake hujulisha hivi: “Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria, hata sala yake ni chukizo.” (Mithali 28:9) Watapatwa na matokeo ya mwendo wao waliochagua. Mtume Paulo aliandika hivi: “Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”—Wagalatia 6:7.

22. Watu wengi wanaotaka kumjua Mungu wanafanya nini sasa?

22 Hata hivyo, kuna watu wengi wanaotaka kujua mapenzi ya Mungu, wanaomtafuta kikweli, na wanaovutwa kwake. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi,” chasema Yakobo 4:8. Juu ya watu kama hao Yesu alisema hivi: “Yeye aitendaye kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yaonekane wazi ya kuwa yametendwa katika Mungu.” (Yohana 3:21) Na Mungu amekusudia kuwe na wakati ujao ulio mzuri kama nini kwa wale wanaokuja kwenye nuru! Makala yetu ifuatayo itazungumzia mataraja hayo yenye kusisimua.

Wewe Ungejibuje?

◻ Watu wengi husema nini juu ya kusudi la uhai?

◻ Yehova hujifunuaje kama Mungu wa kusudi?

◻ Ni mnurisho gani mkubwa uliotokea katika karne ya kwanza W.K.?

◻ Kutaniko la Kikristo la kweli laweza kutambuliwaje leo?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki