Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
Kweli ya Biblia Yaunganisha Familia
LEO, katika sehemu nyingi za ulimwengu, ni kama muungano wa familia hauko tena. Hata hivyo, Biblia hufunua siri ya muungano wa familia. Fikiria maneno haya ya Yesu: “Kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.” (Mathayo 7:24) Maelfu ya familia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova zimetimiza muungano kwa kutumia maneno hayo na kwa kutumia Biblia ikiwa msingi wa kujenga familia iliyounganika. Wengine pia wanapata muungano huo kama vile ono lifuatalo lionyeshavyo.
Daniel alipokuwa akitumikia jeshini katika Ufaransa, padri mmoja wa jeshi alidokeza kwamba Daniel anunue Biblia, naye alifanya hivyo, akaanza kuisoma kwa kawaida. Hatimaye alihamishiwa Tahiti. Baadhi ya wanajeshi wenzi wa Daniel walikuwa wa Dini ya Adventi, na wengine walikuwa wa Dini ya Mormoni. Mara nyingi mazungumzo yao yaligeuka na kuwa habari ya dini. Siku moja sajenti mkuu alimjulisha Daniel kwa mke wake, aliyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Mke huyo alitumia alasiri nzima akijibu maswali mengi ya Daniel, akampa anwani ya mojayapo makutaniko ya Mashahidi wa Yehova katika Tahiti. Upesi alianza funzo la Biblia la kawaida.
Wazazi wa Daniel walioishi Ufaransa walikuwa Wakatoliki wenye mioyo myeupe sana. Babake alikuwa mshauri wa shule na aliongoza mafunzo ya kidini kwenye shule ya Katoliki. Kwa kuwa alitaka kushiriki na wazazi wake baadhi ya mambo ya kiroho yenye thamani sana aliyokuwa akijifunza, Daniel alianza kutia katika barua zake kwao, mambo machache kutoka katika Biblia.
Mwanzoni mamake Daniel alifurahia, lakini akashtuka kupata jina Yehova katika barua moja ya mwanawe. Siku chache baadaye, alisikia programu ya redio iliyowaonyesha Mashahidi wa Yehova kuwa “kidhehebu hatari.” Yeye alimwandikia Daniel, akimwomba aache kushirikiana na Mashahidi mara iyo hiyo. Hata hivyo, Daniel aliendelea kufanya maendeleo katika funzo lake la Biblia na upesi akafanya mipango ya kuacha jeshi na kurudi Ufaransa.
Mara aliporudi nyumbani, Daniel alitumia kila jioni—nyakati nyingine hadi usiku sana—katika mazungumzo marefu ya Biblia pamoja na mamake. Hatimaye mamake alikubali kuandamana na Daniel kwenye Jumba la Ufalme. Alipohudhuria mkutano wake wa kwanza, alivutiwa sana hivi kwamba alianza kuwa na funzo lake mwenyewe la Biblia kwa kawaida. Alifanya maendeleo ya haraka akabatizwa upesi.
Babake Daniel alikuwa mtu mvumilivu lakini alikuwa mwenye kujitoa sana kwa kazi yake na utendaji wake mbalimbali wa kidini. Bado, katika pindi moja alipeleka mke wake na Daniel kwenye mkusanyiko wa wilaya kwa gari. Hiyo ilikuwa katika Julai 14, na alikuwa amepanga kutazama gwaride ya Siku ya Bastille jijini. Alipokuwa akingoja, aliamua kwa udadisi kutazama ndani ya jumba la mkusanyiko. Alivutiwa na utaratibu na amani aliyoona miongoni mwa watu wa Yehova, na alipotembea kupitia idara mbalimbali za mkusanyiko kila mtu alikuwa akimwita “ndugu.” Alisahau kabisa juu ya gwaride ya Siku ya Bastille akabaki hadi mwisho wa mkusanyiko. Aliomba funzo la Biblia akafanya maendeleo ya haraka katika kujifunza kweli. Hata hivyo, alipoendelea kujifunza alihisi kutostareheka kazini mwake, kwa hiyo akiwa na umri wa miaka 58, aliacha kazi yake. Sasa wote watatu katika familia hiyo wamejiweka wakfu na kubatizwa na wanamtumikia Yehova pamoja kwa muungano.
Kweli ya Biblia ndiyo iliyounganisha familia ya Daniel. Yaweza pia kuunganisha familia nyinginezo zikijifunza na kuitumia kwa moyo wote.y