Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 7/1 kur. 8-13
  • Unajilisha Katika Meza Ipi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unajilisha Katika Meza Ipi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuepuka “Meza ya Mashetani”
  • “Mtumwa Mwaminifu” Aandaa Meza ya Yehova
  • Jihadhari na Chakula Chenye Sumu Katika Meza ya Mashetani
  • Ni Meza ya Yehova Pekee Itakayodumu
  • Yaliyomo
    Amkeni!—2024
  • Yesu Ana Nguvu Kuliko Roho Waovu
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
  • Ufundishaji wa Kimungu Dhidi ya Mafundisho ya Mashetani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Tunaweza Kuwapinga Roho Waovu Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 7/1 kur. 8-13

Unajilisha Katika Meza Ipi?

“Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani.”—1 WAKORINTHO 10:21.

MANENO haya yaliyovuviwa ya mtume Paulo yaonyesha kwamba wanadamu wameandaliwa meza mbili za mfano mbele yao. Kila meza inatambuliwa kwa aina ya chakula cha mfano kilichowekwa juu yayo, na sisi sote twala katika meza moja au ile nyingine. Lakini, kama tunataka kumpendeza Mungu, hatuwezi kuwa tunajilisha katika meza yake na wakati uo huo tuwe tunatafuna kidogo-kidogo chakula cha meza ya mashetani. Mtume Paulo alionya hivi: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu; nami sipendi ninyi kushirikiana na mashetani. Hamwezi kunywea kikombe cha Bwana na kikombe cha mashetani. Hamwezi kushirikiana katika meza ya Bwana na katika meza ya mashetani.”—1 Wakorintho 10:20, 21.

2 Maneno ya Paulo yatukumbusha dhabihu za ushirika ambazo Waisraeli wa kale walitoa kwa kufuata Sheria ya Yehova. Madhabahu ya Mungu iliitwa meza, na mtu yule aliyekuwa akimleta mnyama wa kutolewa dhabihu alisemekana kuwa na ushirika pamoja na Yehova na makuhani. Kwa njia gani? Kwanza, Yehova alishiriki katika dhabihu hiyo kwa sababu damu ilinyunyizwa juu ya madhabahu yake na mafuta yaliteketezwa na moto uliokuwa chini. Pili, kuhani alishiriki kwa njia ya kwamba yeye (na familia yake) walikula nyama ya kidari na ya mguu wa kulia ya mnyama aliyetolewa dhabihu. Na tatu, mtoa dhabihu alishiriki kwa kula sehemu iliyobaki. (Mambo ya Walawi 7:11-36) Leo, kushiriki katika meza ya Yehova kwamaanisha kwamba twampa aina ya ibada anayotaka, kama walivyofanya Yesu na mitume wake. Ili kufanya hivyo, ni lazima tujilishe kiroho kile ambacho Yehova aandaa kupitia Neno lake na tengenezo lake. Waisraeli, waliofurahia ushirika wa pekee pamoja na Yehova katika meza yake, walikatazwa kutoa dhabihu kwa mashetani katika meza yao. Waisraeli wa kiroho na waandamani wao wa “kondoo wengine” wanakatazwa vivyo hivyo kimungu.—Yohana 10:16.

3 Mtu angekuaje na hatia ya kushiriki meza ya mashetani katika siku zetu? Kwa kutumikia masilahi ya kitu chochote kinachompinga Yehova. Meza ya mashetani inatia ndani propaganda zote za kishetani, ambazo zimekusudiwa kutupotosha na kutuondosha kwa Yehova. Ni nani angetaka kulisha moyo wake na akili yake sumu kama hiyo? Wakristo wa kweli hukataa kushiriki katika dhabihu ambazo watu wengi zaidi leo hutolea miungu ya vita na mali.—Mathayo 6:24.

Kuepuka “Meza ya Mashetani”

4 Swali ambalo sisi sote twakabili ni, Ninajilisha katika meza ipi? Hatuwezi kuepuka hakika ya kwamba ni lazima tule katika meza moja au ile nyingine. (Linganisha Mathayo 12:30.) Sisi hatungetaka kushiriki kimakusudi katika meza ya mashetani. Kufanya hivyo kungetufanya tupoteze upendeleo wa Mungu wa pekee wa kweli aishiye, Yehova. Kwa upande mwingine, kushiriki chakula katika meza ya Yehova pekee kwatuongoza kwenye uhai wa milele katika furaha! (Yohana 17:3) Kuna msemo usemao kwamba mtu ni kile akulacho. Basi, yeyote atakaye kuwa na afya bora kimwili na kiakili ni lazima achunge lishe yake. Kama vile chakula chenye mafuta mengi kisichofaa mwili, ingawa hupikwa vitamu kwa vikolezo vya kemikali, hakiendelezi afya yetu ya kimwili, ndivyo propaganda za ulimwengu huu zilivyokolezwa mawazo ya mashetani ni chakula kisichofaa mwili cha mfano kitakachofisidi akili zetu.

5 Mtume Paulo alitabiri kwamba katika siku za mwisho watu wangepotoshwa na “mafundisho ya mashetani.” (1 Timotheo 4:1) Mafundisho kama hayo ya mashetani hayapatikani tu katika itikadi za dini bandia bali pia zinaenezwa sana katika njia nyinginezo. Kwa kielelezo, twahitaji kuchunguza na kuchanganua aina ya vitabu na magazeti ambayo sisi na watoto wetu husoma, twatazama vipindi gani vya televisheni, na twatazama michezo gani ya kuigiza na sinema za aina gani. (Mithali 14:15) Kama tunapenda kusoma hadithi zenye kubuniwa wakati wa starehe, je, hizo zina jeuri isiyofaa, ngono ya waziwazi, au vitendo vya uasiliani-roho? Kama tunasoma habari zisizo za kubuniwa ili tufundishwe, je, zinafundisha falsafa au njia ya maisha ‘isiyo ya jinsi ya Kristo’? (Wakolosai 2:8) Je! zinaendeleza makisio matupu, au zinapendekeza kujiingiza katika vyama vya kijamii vya kilimwengu? Je! zinakuza tamaa ya kuwa tajiri sana? (1 Timotheo 6:9) Je! ni kichapo kinachofundisha kwa ujanja mafundisho yenye kugawanya ambayo si ya Kikristo? Kama jibu ni ndiyo na twaendelea kukisoma au kukitazama kitu kama hicho, twajihatarisha kujilisha katika meza ya mashetani. Leo, kuna mamia ya maelfu ya vichapo vinavyoendeleza falsafa za ulimwengu zinazoonekana kuwa za akili ya juu na za kisasa. (Mhubiri 12:12) Lakini hakuna hata moja ya propaganda hizo ambayo kwa kweli ni mpya; wala haifaidi mtu ama kufanya hali yake iwe bora zaidi, kwa jinsi ambavyo maneno ya ujanja ya Shetani kwa Hawa hayakuifanya hali ya Hawa iwe bora.—2 Wakorintho 11:3.

6 Kwa hiyo, Shetani atualikapo tuonje chakula chake kisichofaa cha kishetani, tufanye nini? Kama alivyofanya Yesu alipojaribiwa na Shetani kwamba ageuze mawe yawe mikate. Yesu alimjibu hivi: “Imeandikwa, Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” Na Ibilisi alipomtolea Yesu “milki zote za ulimwengu, na fahari yake” ikiwa angeanguka na kufanya tendo moja la ibada kwa Shetani, Yesu alimjibu: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.”—Mathayo 4:3, 4, 8-10.

7 Meza ya Yehova na meza iliyoandaliwa na maadui wake wa kishetani haziwezi kupatanishwa! Ndiyo, jambo hilo limepata kujaribiwa wakati uliopita. Kumbuka Waisraeli wa kale katika siku za nabii Eliya. Watu walidai kumwabudu Yehova, lakini waliamini kwamba miungu mingine, kama Baali, wangeleta ufanisi. Eliya aliwaendea watu na kusema: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? BWANA akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! mfuateni yeye.” Bila shaka, Waisraeli walikuwa wakichechea “kwanza kwa mguu mmoja kisha kwa ule mwingine.” (1 Wafalme 18:21; The Jerusalem Bible) Eliya aliwatolea mwito makuhani wa Baali wathibitishe uungu wa mungu wao. Yule Mungu ambaye angeleta moto kutoka mbinguni kwenye dhabihu angethibitika kuwa Mungu wa kweli. Zijapokuwa jitihada zao nyingi, makuhani wa Baali walishindwa. Kisha Eliya akasali kwa usahili hivi: “Ee BWANA, unisikie, ili watu hawa wajue ya kuwa wewe, BWANA, ndiwe Mungu.” Mara hiyo moto kutoka kwa Yehova ukaja kutoka mbinguni na kuteketeza dhabihu ya mnyama iliyofurikwa maji. Wakichochewa na wonyesho huo usiotilika shaka wa uungu wa Yehova, watu walimtii Eliya na kuua manabii wote 450 wa Baali. (1 Wafalme 18:24-40) Kwa hiyo, ni lazima tutambue leo kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli na kuamua kwa uthabiti kulisha katika meza yake pekee kama bado hatujaanza kufanya hivyo.

“Mtumwa Mwaminifu” Aandaa Meza ya Yehova

8 Bwana Yesu Kristo alitabiri kwamba wakati wa kuwapo kwake “mtumwa mwaminifu mwenye akili” angeandalia wanafunzi wake chakula cha kiroho: “Heri mtumwa yule, ambaye Bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amin nawaambieni, atamweka juu ya vitu vyake vyote.” (Mathayo 24:45-47) Mtumwa huyo ni jamii ya Wakristo waliojiweka wakfu na kutiwa mafuta bali si mtu mmoja fulani. Jamii hii imeweka katika meza ya Yehova chakula bora zaidi cha kiroho kwa mabaki ya watiwa-mafuta pamoja na “mkutano mkubwa.” Sasa wakiwa zaidi ya milioni nne, mkutano mkubwa umechukua msimamo wao pamoja na mabaki ya watiwa-mafuta kwa ajili ya enzi kuu ya ulimwengu wote wa Yehova Mungu na kwa ajili ya Ufalme wake atakaotumia kutakasa jina lake takatifu.—Ufunuo 7:9-17.

9 Jamii hii ya mtumwa mwaminifu imekuwa ikitumia Watch Tower Bible and Tract Society ili kuandalia Mashahidi wa Yehova wote lishe ya kiroho. Huku Jumuiya ya Wakristo na mfumo wote wa mambo unaosalia ukifa njaa kwa sababu ya ukosefu wa chakula cha kiroho chenye kutoa uhai, watu wa Yehova wamo karamuni. (Amosi 8:11) Jambo hilo latimiza unabii wa Isaya 25:6: “BWANA wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.” Kama mistari ya 7 na 8 ionyeshavyo, karamu hiyo itaendelea milele. Wote ambao leo wamo katika tengenezo la Yehova linaloonekana wana baraka kama nini, na baraka hiyo itaendelea kuwapo kama nini katika wakati ujao!

Jihadhari na Chakula Chenye Sumu Katika Meza ya Mashetani

10 Chakula kilicho katika meza ya mashetani ni chenye sumu. Kwa kielelezo, fikiria chakula kinachoandaliwa na jamii ya mtumwa mwovu na waasi-imani. Hakiandai lishe bora wala hakijengi; hakifai. Haiwezekani, kwa sababu waasi-imani wamekoma kujilisha katika meza ya Yehova. Matokeo ni kwamba utu mpya wowote waliokuwa wamesitawisha umetoweka. Wanasukumwa na uchungu wa moyo bali si na roho takatifu. Wana kusudi moja tu—kuwapiga wale waliokuwa watumwa wenzao, kama Yesu alivyotabiri.—Mathayo 24:48, 49.

11 Kwa kielelezo, huko nyuma katika 1909, msimamizi wa wakati huo wa Watch Tower Society, C. T. Russell, aliandika kuhusu wale waliotoka katika meza ya Yehova kisha wakaanza kuwatenda vibaya wale waliokuwa watumwa wenzao. The Watch Tower la Oktoba 1, 1909, lilisema hivi: “Wote wanaojitenga na Sosaiti na kazi yayo, badala ya kujijenga au kujenga wengine katika imani na katika matunda ya roho, wao waonekana kufanya kinyume sana—wanajaribu kujeruhi ile Njia ambayo wakati mmoja walitumikia, na, kwa makelele yao mengi au machache wao hupotea kabisa, wakijidhuru wenyewe na wengine wenye roho ya ushindani kama yao. . . . Wengine wakifikiri kwamba wanaweza kupata chakula kizuri kama hiki au hata kizuri zaidi katika meza nyinginezo, au kwamba wao wenyewe waweza kutokeza chakula kizuri kama hiki au hata kizuri zaidi—hao nao wafuate njia zao. . . . Lakini huku tukiruhusu wengine waende popote pale na kila mahali kutafuta chakula na nuru ya kuwatosheleza, inashangaza kwamba wale wanaokuwa maadui wetu hufuata njia nyingine tofauti kabisa. Badala ya kusema kishujaa kwa namna ya kilimwengu, ‘Nimepata kitu nipendacho zaidi; kwaheri!’ wao wanakuwa wenye hasira, wenye ukorofi, wenye chuki, wenye ugomvi, ‘kazi za mwili na ibilisi’ kwa kadiri ambavyo hatujaona watu wa kilimwengu wakionyesha. Wanaonekana kama wamejaa kichaa, kichaa cha Kishetani. Baadhi yao watupiga na kisha wadai kwamba ni sisi tuliowapiga. Wako tayari kusema na kuandika uongo mtupu na kujishusha kufanya maovu.”

12 Naam, waasi-imani huchapisha vichapo vilivyopotoka, vyenye nusu-kweli, na uongo wa waziwazi. Wao huja kama askari hata katika mikusanyiko ya Mashahidi, wakijaribu kunasa wale wasiojihadhari. Kwa hiyo, ingekuwa hatari sana kwetu kuruhusu udadisi wetu utusukume tujilishe maandishi kama hayo au kusikiliza usemi wao wenye matukano! Ingawa huenda tukafikiri kwamba sisi wenyewe hatuhatarishwi, hatari hiyo ingali ipo. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba baadhi ya vichapo vya waasi-imani vyatokeza uongo kwa “maneno laini” na “maneno yaliyotungwa.” (Warumi 16:17, 18; 2 Petro 2:3) Je! hayo si mambo uwezayo kutazamia yatoke katika meza ya mashetani? Na ingawa waasi-imani huenda wakasema kweli fulani, mara nyingi hizo hutolewa nje ya muktadha kwa lengo la kuondoa wengine kutoka katika meza ya Yehova. Maandishi yao yote yanachambua tu na kuharibu! Hayajengi hata kidogo.

13 Yesu alisema hivi: “Mtawatambua kwa matunda yao.” (Mathayo 7:16) Basi, sasa, ni yapi matunda ya waasi-imani na vichapo vyao? Mambo manne yatambulisha propaganda zao. (1) Ujanja. Waefeso 4:14 lasema kwamba wao ni ‘wajanja katika njia za udanganyifu.’ (2) Uwerevu wenye kiburi. (3) Kukosa upendo. (4) Kutofuatia haki kwa mambo mengi. Hivyo ndivyo vikolezo vya chakula vilivyo katika meza ya mashetani vilivyo hasa, vyote vikikusudiwa kudhoofisha imani ya watu wa Yehova.

14 Na kuna upande mwingine. Waasi-imani wamerudia nini? Mara nyingi, wamerudia tena giza la Jumuiya ya Wakristo na mafundisho yayo, kama vile kuamini kwamba Wakristo wote wanaenda mbinguni. Isitoshe, wengi wao hawadumishi msimamo thabiti wa Kimaandiko kuhusu damu, kutokuwamo, na uhitaji wa kutoa ushahidi juu ya Ufalme wa Mungu. Lakini sisi tumeepuka giza la Babiloni Mkubwa, na hatutaki kamwe kulirudia. (Ufunuo 18:2, 4) Tukiwa watumishi waaminifu-washikamanifu wa Yehova, ni kwa nini tutake hata kuchungulia propaganda zinazotolewa na watu hao waliokataa meza ya Yehova ambao sasa wanawapiga kwa maneno wale wanaotusaidia kutwaa “maneno yenye uzima”?—2 Timotheo 1:13.

15 Watu fulani wanaweza kuwa na udadisi juu ya mashtaka ya waasi-imani. Lakini twapaswa kuzingatia moyoni kanuni iliyo katika Kumbukumbu la Torati 12:30, 31. Hapo Yehova aliwaonya Waisraeli kupitia Musa juu ya mambo ambayo wangeepuka mara tu baada ya kutwaa Bara Lililoahidiwa kutoka kwa wakazi wapagani. “Ujiangalie, usije ukanaswa ukawafuata, wakiisha kuangamizwa mbele yako; wala usije ukauliza habari za miungu yao, ukisema, Mataifa haya waitumikiaje miungu yao? nami nifanye vivyo. Usimtende kama haya BWANA, Mungu wako.” Ndiyo, Yehova Mungu ajua jinsi udadisi wa wanadamu ufanyavyo kazi. Kumbuka Hawa na mke wa Loti vilevile! (Luka 17:32; 1 Timotheo 2:14) Tusisikilize kamwe maneno ya waasi-imani wala matendo yao. Badala ya hivyo, na tuwe wenye shughuli kujenga watu na kujilisha kwa uaminifu-mshikaminifu katika meza ya Yehova!

Ni Meza ya Yehova Pekee Itakayodumu

16 Hivi karibuni, dhiki kubwa itafyatuka kwa ghafula, upesi ikifikia upeo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” (Ufunuo 16:14, 16) Itafikia upeo Yehova aharibupo mfumo huu wa mambo na meza ya mfano ambayo mataifa ya ulimwengu yalikuwa yakijilishia. Yehova atapindua pia tengenezo lote lisiloonekana la Shetani Ibilisi pamoja na umati wa mashetani wake. Wale ambao wameendelea kujilisha katika meza ya kiroho ya Shetani, meza ya mashetani, watalazimishwa kuwapo katika mlo halisi, si wakiwa washiriki, bali wakiwa mlo mkuu wenyewe—kwa uharibifu wao!—Ona Ezekieli 39:4; Ufunuo 19:17, 18.

17 Ni meza ya Yehova pekee itakayodumu. Wale wanaojilisha kwa uthamini katika meza hiyo watahifadhiwa na watapendelewa kula hapo milele. Hawatakabiliwa tena kamwe na upungufu wa chakula cha aina yoyote. (Zaburi 67:6; 72:16) Watamtumikia Yehova Mungu wakiwa na afya bora katika Paradiso! Hatimaye maneno yenye kuchochea sana ya Ufunuo 21:4 yatatimizwa kwa utukufu: “Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena, wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.” Na kwa sababu upinzani hautakuwapo, enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova Mungu itaenea kila mahali milele na milele huku mapendeleo mengi ya kimungu yasiyokwisha yakimwagikia wanadamu waliokombolewa wanaoishi katika dunia-Paradiso. Ili kupata thawabu hiyo, sisi sote na tuazimie kushiriki katika meza ya Yehova pekee, iliyojaa chakula cha kiroho kilicho bora zaidi!

Ungejibuje?

◻ Twaweza kuepukaje kupotoshwa na mafundisho ya kishetani?

◻ Ni kwa nini hatuwezi kwa mafanikio kujilisha katika meza ya Yehova na katika meza ya mashetani?

◻ Waasi-imani huandaa chakula cha aina gani?

Ni kwa nini ni jambo la hatari kuwa na udadisi juu ya mashtaka wanayotoa waasi-imani?

◻ Matunda ya waasi-imani ni yapi?

[Maswali ya Funzo]

1. Ni meza zipi zimeandaliwa mbele yetu, na mtume Paulo atoa onyo gani kuzihusu?

2. (a) Ni meza ipi ya Yehova ilikuwapo katika siku za Israeli ya kale, na ni akina nani walioshiriki katika dhabihu za ushirika? (b) Kushiriki katika meza ya Yehova kwamaanisha nini leo?

3. Mtu awezaje kuwa na hatia ya kushiriki meza ya mashetani katika siku zetu?

4. Sisi sote twakabili swali gani, na ni kwa nini hatungetaka kushiriki kimakusudi katika meza ya mashetani?

5. Twaweza kuepukaje kutwaa mafundisho ya kishetani leo?

6. Shetani atualikapo tuonje chakula chake kisichofaa cha kishetani, tufanye nini?

7. Ni kwa nini twajidanganya wenyewe ikiwa twafikiri twaweza kwa mafanikio kujilisha katika meza ya Yehova na katika meza ya mashetani?

8. Yesu alitabiri kwamba angetumia mtumwa gani kulisha kiroho wanafunzi wake wakati wa kuwapo kwake, na mtumwa huyo anatambuliwa kuwa nani?

9. Jamii ya mtumwa imekuwa ikitumia chombo gani katika kuandaa chakula cha kiroho kwa Mashahidi wa Yehova, na karamu yao ya kiroho yafafanuliwaje kiunabii?

10. (a) Ni chakula cha aina gani kinachoandaliwa na jamii ya mtumwa mwovu, na ni nini kinachowasukuma? (b) Jamii ya mtumwa mwovu wanatendeaje wale waliokuwa watumwa wenzao?

11. C. T. Russell aliandika nini juu ya chaguo la mtu la chakula cha kiroho, naye aliwafafanuaje wale walioacha meza ya Yehova?

12. (a) Waasi-imani wanapigaje watumwa wenzao? (b) Ni kwa nini ni jambo la hatari kujilisha maandishi ya waasi-imani kwa sababu ya udadisi?

13, 14. Ni yapi matunda ya waasi-imani na propaganda zao?

15. Ni kanuni gani ya Biblia inayotusaidia tuamue vizuri tusikiapo mashtaka yanayotolewa na waasi-imani?

16. (a) Hivi karibuni, ni nini kitakachompata Shetani, mashetani wake, na meza ya mfano ambayo mataifa ya ulimwengu yamekuwa yakijilishia? (b) Ni nini kitakachopata wanadamu wote wanaondelea kujilisha katika meza ya mashetani?

17. Ni baraka zipi zinazowajia wale wanaojilisha katika meza ya Yehova pekee?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Meza ya Yehova imejaa chakula cha kiroho kilicho bora zaidi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki