Wewe Husuluhishaje Matatizo?
Tendo fulani lisilofaa—na ndovu wa tatu katika safu ya ndovu watano waliofinyangwa kwa kauri aanguka kutoka kwenye ubao. Ni lazima ndovu huyo arudishwe. Ama sivyo upatano wa seti nzima ya ndovu hao utapotezwa. Lakini, ni vigumu sana kuirudisha, nawe wahisi hustahili. Ni lazima utafute shauri au hata kuuliza mstadi fulani amrudishe.
UPATANO kati ya ndugu na dada wa kiroho ni wenye thamani sana kuliko mapambo tu. Mtunga-zaburi aliimba hivi kwa kufaa: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.” (Zaburi 133:1) Nyakati nyingine yaweza kuwa vigumu kusuluhisha tatizo kati yako na Mkristo mwenzako. Isitoshe, wengine hawafanyi hivyo kwa njia ifaayo. Mara nyingi ‘kurudisha uhusiano’ hutokeza uchungu isivyofaa au hakufanywi vizuri sana, kukiacha alama mbaya zinazoonekana.
Wakristo fulani hutafuta kuingiza isivyofaa wazee waliowekwa rasmi katika mambo ambayo wao wenyewe waweza kushughulikia. Hilo laweza kuwa hivyo kwa sababu hawajui hasa jambo la kufanya. “Wengi wa ndugu zetu hawajui jinsi ya kutumia shauri la Biblia ili kusuluhisha matatizo yao,” akaeleza hivyo ndugu mmoja mwenye ujuzi wa muda mrefu katika kutoa shauri la Biblia. “Mara nyingi sana,” yeye akaendelea, “wao hawafuati njia ya Yesu ya kufanya mambo.” Basi, Yesu alisema nini hasa juu ya jinsi Mkristo apaswa kusuluhisha matatizo baina yake na ndugu yake? Ni kwa nini ni muhimu kufahamu sana shauri hili na kujifunza jinsi ya kulitumia?
Matatizo Madogo-Madogo
Basi, ukileta sadaka [“zawadi,” NW] yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.”—Mathayo 5:23, 24.
Yesu aliposema maneno hayo, Wayahudi walikuwa na desturi ya kutoa dhabihu, au kutoa zawadi, kwenye madhabahu ya hekalu kule Yerusalemu. Ikiwa Myahudi alimkosea Mwisraeli mwenzake, mkosaji angetoa toleo zima la kuteketezwa au toleo la dhambi. Kielelezo kilichotolewa na Yesu ni cha pindi muhimu zaidi. Mtu huyo awapo penye madhabahu na akaribia kutoa zawadi yake kwa Mungu, akumbuka kwamba ndugu yake ana jambo dhidi yake. Naam, Mwisraeli huyo alihitaji kuelewa kwamba kupatana na ndugu yake kulikuwa muhimu kuliko kutimiza wajibu huo wa kidini.
Ingawa matoleo hayo yalikuwa takwa la Sheria ya Musa, hayo hayakuwa na thamani kubwa zaidi machoni pa Mungu. Nabii Samueli alimwambia hivi Mfalme Sauli aliyekosa uaminifu: “Je! BWANA huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu sawasawa na kuitii sauti ya BWANA? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikia kuliko mafuta ya beberu.”—1 Samweli 15:22.
Katika Mahubiri ya Mlima, Yesu alirudia kule kutanguliza mambo ya maana zaidi naye akaonyesha wanafunzi wake kwamba ni lazima wasuluhishe matatizo yao kabla ya kutoa matoleo. Leo, matoleo ambayo Wakristo wana wajibu wa kutoa ni ya hali ya kiroho—“dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Waebrania 13:15) Hata hivyo, kanuni ile ingali inatumika. Mtume Yohana aonyesha vilevile kwamba ingekuwa bure kwa mtu kudai kwamba ampenda Mungu ikiwa anachukia ndugu yake.—1 Yohana 4:20, 21.
Kwa kupendeza, mtu yule akumbukaye kwamba ndugu yake alikuwa na jambo dhidi yake ndiye anayepaswa kuchukua hatua ya kwanza. Unyenyekevu anaoonyesha kwa kuchukua hatua hiyo labda utatokeza matunda mazuri. Yaelekea kwamba mtu ambaye amekosewa hatakataa kusikiliza mtu anayemjia akikiri makosa yake. Sheria ya Musa ilisema kwamba ilikuwa ni lazima kitu chochote kilichochukuliwa kiharamu kirudishwe kabisa na ilikuwa lazima sehemu ya tano iongezwe. (Mambo ya Walawi 6:5) Kurudisha uhusiano wenye amani na upatano vilevile kutarahisishwa ikiwa mkosaji aonyesha tamaa yake ya kuchukua hatua hata zaidi ya wajibu wake, kihalisi, kurekebisha madhara yoyote ambayo huenda alisababisha.
Hata hivyo, majaribio ya kurudisha uhusiano wenye amani hayafaulu nyakati zote. Kitabu cha Mithali chatukumbusha kwamba ni vigumu kusuluhisha matatizo na mtu ambaye haiitikii kwa urahisi. Mithali 18:19 lasema: “Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; na mashindano ni kama mapingo ya ngome.” Tafsiri nyingine yasema hivi: “Ni vigumu zaidi kushinda ndugu aliyekosewa kuliko jiji lenye nguvu: Na mashindano yao ni kama nguzo za ngome.” (The Englishman’s Bible) Hata hivyo, hatimaye jitihada zenye unyoofu na unyenyekevu zaelekea zitafaulu kama wao ni waamini wenzi wanaotaka kumpendeza Mungu. Lakini kama kuna shtaka la dhambi nzito, shauri la Yesu lililoandikwa katika Mathayo sura ya 18 huhitaji kutumiwa.
Kusuluhisha Matatizo Makubwa
“Na ndugu yako akikukosea, enenda ukamwonye, wewe na yeye peke yenu; akikusikia, umempata nduguyo. La, kama hasikii, chukua pamoja nawe tena mtu mmoja au wawili, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno lithibitike. Na asipowasikiliza wao, liambie kanisa [“kutaniko,” NW]; na asiposikiliza kanisa pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru.”—Mathayo 18:15-17.
Vipi ikiwa Myahudi (au baadaye, Mkristo) angepata matatizo mazito baina yake na mwabudu wa Yehova mwenzake? Yule ambaye alifikiri kwamba amefanyiwa dhambi ndiye aliyepaswa kuchukua hatua ya kwanza. Angezungumzia mambo hayo pamoja na mkosaji kwa faragha. Akijaribu kutotetea upande wake, hakika ataelekea zaidi kupata ndugu yake, hasa kama tatizo lilikuwa ni kutoelewana ambako kungesuluhishwa kirahisi. Kila kitu kingesuluhishwa kwa urahisi zaidi ikiwa wale wanaohusika kwa njia ya moja kwa moja zaidi ndio watu pekee wanaojua habari hiyo.
Hata hivyo, huenda hatua ya kwanza isitoshe. Ili kushughulika na hali hiyo, Yesu alisema hivi: “Chukua pamoja nawe . . . mmoja au wawili.” Hao hasa waweza kuwa mashahidi waliojionea kisa hicho. Labda walisikia mmoja wa watu hao akichongea mwingine, au hata wale wanaochukuliwa walikuwa mashahidi wa mapatano yaliyoandikwa ambayo sasa watu hao wawili watofautiana juu yayo. Kwa upande mwingine, wale wanaochukuliwa wangekuwa mashahidi iwapo mambo yoyote, kama vile ushuhuda ulioandikwa au kusemwa kwa mdomo, yatokezwa kuthibitisha sababu ya tatizo. Hapa pia, ni idadi ndogo iwezekanavyo—“mmoja au wawili”—ndio wanaopaswa kujua jambo hilo. Jambo hilo lingefanya mambo yasiwe mabaya zaidi ikiwa tatizo lilikuwa ni kutoelewana tu.
Yule aliyekosewa apaswa kuwa na makusudi gani? Je! ajaribu kushusha heshima ya Mkristo mwenzake na kumtaka avunje heshima yake? Kwa kufikiria shauri la Yesu, Wakristo hawapaswi kuwa wepesi kushutumu ndugu zao. Mkosaji akitambua kosa lake, aombe msamaha, na ajaribu kurekebisha mambo, yule aliyetendewa dhambi atakuwa ‘amempata nduguye.’—Mathayo 18:15.
Ikiwa jambo hilo halingeweza kusuluhishwa, lingepelekwa kutanikoni. Zamani, jambo hilo lilimaanisha wazee wa Wayahudi lakini baadaye, ikawa wazee wa kutaniko la Kikristo. Huenda mtenda-kosa alilazimika kufukuzwa kutanikoni. Hilo ndilo linalomaanishwa na “kama mtu wa mataifa na mtoza ushuru,” watu ambao Wayahudi waliepuka. Hatua hiyo nzito haingechukuliwa na Mkristo yeyote mmoja-mmoja. Wazee waliowekwa rasmi, wanaowakilisha kutaniko, pekee ndio wana mamlaka ya kuchukua hatua kama hiyo.—Linganisha 1 Wakorintho 5:13.
Uwezekano wa mtenda-kosa asiyetubu kutengwa na ushirika waonyesha kwamba Mathayo 18:15-17 halisemi juu ya matatizo madogo-madogo. Yesu alikuwa akirejezea makosa mazito, na ambayo yangesuluhishwa kati ya watu wawili wanaohusika. Kwa kielelezo, kosa laweza kuwa uchongezi, likiharibu kabisa sifa ya mchongewa. Au laweza kuhusika na mambo ya kifedha, kwa sababu mistari ifuatayo ina kielezi cha Yesu juu ya mtumwa mkatili aliyekuwa amesamehewa deni kubwa. (Mathayo 18:23-35) Mkopo usiolipwa kwa wakati uliotakikana waweza kuwa tu tatizo la muda liwezalo kusuluhishwa kati ya watu wawili. Lakini laweza kuwa dhambi nzito, yaani, wizi, ikiwa mwenye deni akataa kwa ukaidi kulipa deni lake.
Dhambi nyingine haziwezi kusuluhishwa kati ya Wakristo wawili tu. Kulingana na Sheria ya Musa, dhambi nzito zilikuwa ziripotiwe. (Mambo ya Walawi 5:1; Mithali 29:24) Vivyo hivyo, dhambi nzito ihusuyo utakaso wa kutaniko ni lazima iripotiwe kwa wazee wa Kikristo.
Lakini, visa vingi vya kutoelewana kati ya Wakristo havihusiki na hatua hiyo.
Je! Ungeweza Kusamehe Tu?
Baada tu ya Yesu kueleza jinsi ya kusuluhisha matatizo mazito, alifundisha somo jingine muhimu. Twasoma hivi: “Kisha Petro akamwendea akamwambia, Bwana, ndugu yangu anikose mara ngapi nami nimsamehe? hata mara saba? Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini [“mara sabini na saba,” NW].” (Mathayo 18:21, 22) Katika pindi nyingine Yesu aliwaambia wafuasi wake wasamehe “mara saba katika siku moja.” (Luka 17:3, 4) Kwa wazi, basi, wafuasi wa Kristo wanawajibika kusuluhisha matatizo kwa kusameheana kabisa.
Hili ni jambo linalohitaji jitihada nyingi sana. “Ndugu fulani hawajui kamwe jinsi ya kusamehe,” akasema mtu mmoja aliyenukuliwa hapo mwanzoni. Naye akaongezea: “Wao hushangaa mtu fulani awaelezapo kwamba wao waweza kuchagua kusamehe, ili kwanza kabisa tudumishe amani katika kutaniko la Kikristo.”
Mtume Paulo aliandika hivi: ‘Mchukuliane, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.’ (Wakolosai 3:13) Kwa hiyo, kabla ya kumwendea ndugu ambaye huenda alitukosea, ingekuwa vizuri kufikiria maswali haya yafuatayo: Je! lastahili kusema naye juu ya kosa hilo? Je! siwezi kamwe kusahau yaliyopita kwa roho ya kweli ya Ukristo? Kama ningekuwa katika hali yake, je, nisingetaka nisamehewe? Na nikiamua nisimsamehe, je, naweza kumtarajia Mungu anijibu sala zangu na kunisamehe? (Mathayo 6:12, 14, 15) Maswali kama hayo yaweza kutusaidia sana tuwe wenye kusamehe.
Tukiwa Wakristo, mojapo daraka letu muhimu ni kudumisha amani katika kutaniko la watu wa Yehova. Kwa hiyo, tutumieni shauri la Yesu. Hilo litatusaidia tusameheane kabisa. Roho kama hiyo ya kusamehe itachangia upendo wa kidugu ambao ni kitambulisho cha wafuasi wa Yesu.—Yohana 13:34, 35.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Wakristo waweza kusuluhisha matatizo yao kwa kufuata shauri la Yesu