Mateseko ya Binadamu—Je, Yataisha Kamwe?
MAONO ya kuogofya baada ya mlipuko wa bomu katika soko lenye kujaa watu la Sarajevo; maangamizi na kukatwa-katwa katika Rwanda; watoto wenye njaa wanaong’ang’ania chakula katika Somalia; familia zilizoduwaa zikihesabu vitu zilivyopoteza baada ya tetemeko la ardhi katika Los Angeles; watu walio hoi katika Bangladesh yenye mafuriko. Maono kama haya ya mateseko ya binadamu yatukabili kila siku katika televisheni au magazetini.
Matokeo ya kuhuzunisha ya mateseko ya binadamu ni kwamba hayo hufanya watu fulani wapoteze imani katika Mungu. “Kuwapo kwa uovu sikuzote kumeleta ukosefu mbaya sana wa imani,” kulingana na habari iliyotangazwa na jamii ya Kiyahudi katika Marekani. Waandikaji hurejezea vifo katika kambi za mateso za Nazi kama vile Auschwitz na mabomu kama lile lililolipuka juu ya Hiroshima. “Swali la jinsi Mungu mwenye haki na nguvu angeruhusu maangamizi ya watu wengi wasio na hatia husumbua dhamiri ya mtu wa kidini na kushangaza sana,” watungaji wasema.
Kwa huzuni, ripoti zisizokuwa na mwisho za kuhuzunisha zaweza kuwa na tokeo la kufanya hisia za wanadamu kufa ganzi. Maadamu marafiki na watu wa ukoo hawajahusika, wengi hujikuta bila kuhangaishwa na mateseko ya wengine.
Hata hivyo, uhakika wa kwamba tuna uwezo wa kuhisi huruma, angalau kwa wapendwa wetu wenyewe, wapasa kutuambia jambo fulani kuhusu Mfanyi wetu. Biblia husema kwamba mwanadamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu,” na “kwa sura [yake].” (Mwanzo 1:26, 27) Hii haimaanishi ya kwamba wanadamu wanafanana na Mungu kwa sura. Sivyo, maana Yesu Kristo alieleza kwamba “Mungu ni Roho,” na “roho haina mwili na mifupa.” (Yohana 4:24; Luka 24:39) Kufanywa kwa sura ya Mungu hurejezea uwezo wetu wa kuonyesha sifa kama za Mungu. Hivyo basi, maana wanadamu walio na akili timamu huhisi huruma kwa wale watesekao, lazima tukate kauli Muumba wa mwanadamu, Yehova Mungu, ni mwenye huruma na kwamba yeye huwa na hisia zenye kina sana kwa uumbaji wake wa wanadamu wanaoteseka.—Linganisha Luka 11:13.
Njia moja ambayo Mungu ameonyesha huruma yake ni kwa kuandalia binadamu maelezo yaliyoandikwa ya sababu za kuteseka. Amefanya hivyo katika Neno lake, Biblia. Biblia huonyesha waziwazi kwamba Mungu alimuumba mwanadamu kufurahia maisha, si ili ateseke. (Mwanzo 2:7-9) Hiyo pia hufunua kwamba wanadamu wa kwanza walijiletea wenyewe mateseko kwa kukataa utawala wa uadilifu wa Mungu.—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Warumi 5:12.
Ijapokuwa hili, bado Mungu ahisi huruma kwa wanadamu wanaoteseka. Hili laonyeshwa wazi na ahadi yake ya kumaliza mateseko ya binadamu. “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4; ona pia Isaya 25:8; 65:17-25; Warumi 8:19-21.
Ahadi hizi za ajabu zathibitisha kwamba Mungu ana hisi kuelekea mateseko ya binadamu na kwamba ameazimia kuyaondoa. Lakini ni nini hasa kwanza kilichotokeza mateseko ya binadamu, na kwa nini Mungu ameyaruhusu yaendelee hadi siku yetu?
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]
Jalada na ukurasa wa 32: Alexandra Boulat/Sipa Press
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Kevin Frayer/Sipa Press