Thawabu ya Ayubu—Chanzo cha Tumaini
“BWANA akaubarikia huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake.” —AYUBU 42:12.
1. Yehova hufanyia watu wake nini, hata majaribu yawafanyapo wawe dhaifu sana?
YEHOVA “huwapa thawabu wale wamtafutao.” (Waebrania 11:6) Yeye huchochea vilevile watu wake waliojitoa kwake ili watoe ushahidi kwa moyo mkuu, hata kama majaribu yamewafanya wawe dhaifu kama wafu. (Ayubu 26:5; Ufunuo 11:3, 7, 11) Ndivyo mambo yalivyokuwa kwa Ayubu aliyekuwa akiteseka. Ingawa alishtakiwa kwa uongo na wafariji watatu bandia, yeye hakunyamazishwa na hofu ya wanadamu. Badala ya hivyo, yeye alitoa ushahidi wenye ujasiri.
2. Ingawa Mashahidi wa Yehova wamepatwa na mnyanyaso na magumu, wao wametokaje katika majaribu yao?
2 Mashahidi wa Yehova wengi wa siku hizi wamepatwa na minyanyaso na magumu makubwa sana hivi kwamba wamekaribia kifo. (2 Wakorintho 11:23) Hata hivyo, kama Ayubu, wao wameonyesha upendo kwa Mungu nao wamefuatia uadilifu. (Ezekieli 14:14, 20) Wao pia wametoka katika majaribu yao wakiwa wameazimia kumpendeza Yehova, na kuimarishwa kutoa ushahidi kwa ujasiri, na kujawa na tumaini la kweli.
Ayubu Atoa Ushahidi Wenye Ujasiri
3. Ayubu alitoa ushahidi wa aina gani katika mazungumzo yake ya mwisho?
3 Katika mazungumzo yake ya mwisho, Ayubu alitoa ushahidi ulio mkuu hata zaidi kuliko alivyokuwa ametoa awali. Aliwanyamazisha kabisa wafariji wake bandia. Kwa maneno yenye kuchoma, yeye alisema: “Jinsi ulivyomsaidia huyo asiye na uwezo!” (Ayubu 26:2) Ayubu alimsifu Yehova, ambaye uwezo wake waning’iniza tufe la dunia pasipo kitu hewani na kuning’iniza mawingu yaliyojaa maji juu ya dunia. (Ayubu 26:7-9) Na bado, Ayubu alisema kwamba maajabu hayo ni ‘viunga tu vya njia za Yehova.’—Ayubu 26:14.
4. Ayubu alisema nini juu ya uaminifu wa maadili, na kwa nini angeweza kujieleza hivyo yeye mwenyewe?
4 Akiwa na hakika kwamba hana hatia, Ayubu alitangaza hivi: “Hata nitakapokufa sitajiondolea uelekevu [“uaminifu wa maadili,” NW] wangu.” (Ayubu 27:5) Tofauti na mashtaka yasiyo ya kweli aliyofanyiwa, yeye hakuwa amefanya jambo lolote la kumfanya astahili kile kilichompata. Ayubu alijua kwamba Yehova hasikilizi sala za waasi-imani bali atawathawabisha watu wenye kushika uaminifu wa maadili. Jambo hilo laweza kutukumbusha kwamba hivi karibuni dhoruba ya Har–Magedoni itaondosha waovu mbali kutoka kwenye mamlaka yao, nao hawataokoka mkono wa Mungu usioachilia kitu. Hadi wakati huo, watu wa Yehova watatembea katika uaminifu wa maadili wao.—Ayubu 27:11-23.
5. Ayubu alifafanuaje hekima ya kweli?
5 Ebu wazia wale watatu wenye hekima ya kilimwengu wakisikiliza Ayubu aonyeshapo kwamba mwanadamu ametumia stadi zake kupata dhahabu, fedha, na hazina nyinginezo katika ardhi na baharini. “Naam,” yeye asema, “kima cha hekima chapita marijani.” (Ayubu 28:18) Wafariji bandia wa Ayubu hawangeweza kununua hekima ya kweli. Hiyo yatokana na Muumba wa upepo, mvua, umeme, na ngurumo. Kwa kweli, “hofu [yenye kicho] ya Yehova—hiyo ndiyo hekima, na kuepukana na mabaya ni uelewevu.”—Ayubu 28:28, NW.
6. Kwa nini Ayubu alisema juu ya maisha yake ya mapema?
6 Ajapopata mateseko mengi, Ayubu hakuacha kumtumikia Yehova. Badala ya kumwacha Aliye Juu Zaidi Sana, mtu huyu wa uaminifu wa maadili alitamani sana “ukaribu wa ndani pamoja na Mungu” aliokuwa nao zamani. (Ayubu 29:4, NW) Ayubu hakuwa akijisifu alipotaja jinsi ‘alivyomwokoa maskini, alivyojivika haki, na kuwa baba kwa mhitaji.’ (Ayubu 29:12-16) Badala ya hivyo, yeye alikuwa akitaja mambo hakika ya maisha yake akiwa mtumishi mwaminifu wa Yehova. Je, wewe umejiwekea rekodi nzuri kama hiyo? Bila shaka, Ayubu vilevile alikuwa akifichua uongo wa mashtaka aliyofanyiwa na wale wanafiki watatu.
7. Ayubu alikuwa mtu wa aina gani?
7 Ayubu alichekelewa na wanaume wachanga ‘ambao baba zao aliwadharau hata kuwaweka na mbwa wa kundi lake.’ Alichukiwa na kutemewa mate. Ingawa alipata pigo sana, Ayubu hakuonyeshwa ufikirio. (Ayubu 30:1, 10, 30) Lakini kwa sababu alikuwa amejitoa kabisa kwa Yehova, yeye alikuwa na dhamiri safi naye angeweza kusema: “Na nipimwe katika mizani iliyo sawasawa, ili Mungu aujue uelekevu [“uaminifu wa maadili,” NW] wangu.” (Ayubu 31:6) Ayubu hakuwa mzinzi wala mwenye hila, naye hakukosa kuwasaidia wenye uhitaji. Ingawa alikuwa amekuwa tajiri, yeye hakutumaini katika mali ya kimwili. Isitoshe, Ayubu hakujiingiza katika ibada ya sanamu kwa kujitolea kwa vitu visivyo na uhai, kama mwezi. (Ayubu 31:26-28) Akimtumaini Mungu, yeye aliweka kielelezo kizuri cha kufuatwa akiwa mshika uamininifu wa maadili. Ajapopatwa na mateseko mengi na kuwapo kwa wafariji bandia, Ayubu alijitetea kwa ustadi sana na kutoa ushahidi wenye kutokeza sana. Maneno yake yalipofikia kikomo, yeye alimtazamia Mungu akiwa Hakimu na Mthawabishaji wake.—Ayubu 31:35-40.
Elihu Asema
8. Elihu alikuwa nani, naye alionyeshaje staha pamoja na ujasiri?
8 Karibu na hapo palikuwa mwanamume mchanga Elihu, mzao wa Buzi mwana wa Nahori na hivyo yeye ni mtu wa ukoo wa mbali wa rafiki ya Yehova Abrahamu. (Isaya 41:8) Elihu alionyesha staha kwa watu wenye umri mkubwa zaidi kwa kusikiliza pande zote mbili za mjadala. Lakini, aliongea kwa moyo mkuu kuhusu mambo ambayo hao walikosea. Mathalani, hasira yake iliwaka juu ya Ayubu kwa sababu alikuwa “amejipa haki mwenyewe zaidi ya Mungu.” Ghadhabu ya Elihu hasa ilielekezwa dhidi ya wale wafariji watatu bandia. Taarifa zao zaonekana kuwa zamtukuza Mungu lakini kwa kweli zilimletea suto kwa kuwa zilikuwa upande wa Shetani wa lile bishano. ‘Akijaa maneno’ na kuchochewa na roho takatifu, Elihu alikuwa shahidi wa Yehova asiyependelea upande wowote.—Ayubu 32:2, 18, 21.
9. Elihu alidokezaje juu ya kurudishwa kwa hali nzuri ya Ayubu?
9 Ayubu alikuja kuhangaikia zaidi kujitetea kwake mwenyewe kuliko kumtetea Mungu. Kwa kweli, alikuwa ameshindana na Mungu. Hata hivyo, nafsi ya Ayubu ilipokaribia kifo jambo fulani lilidokeza kurudia kwake afya nzuri. Kwa njia gani? Naam, Elihu alisukumwa kusema kwamba Yehova alimpendelea Ayubu kwa ujumbe huu: “Mwokoe asishuke shimoni; mimi nimeuona ukombozi. Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.”—Ayubu 33:24, 25.
10. Ayubu alikuwa ajaribiwe kwa kadiri gani, lakini twaweza kuwa na hakika gani kwa kufikiria 1 Wakorintho 10:13?
10 Elihu alimsahihisha Ayubu aliyesema kwamba hakuna faida katika kumfurahia Mungu kwa kudumisha uaminifu wa maadili. Elihu alisema: “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu; wala mwenyezi kufanya uovu. Kwani atamlipa binadamu kwa kazi yake.” Ayubu alitenda pasipo kufikiri alipokazia uadilifu wake mwenyewe, lakini alifanya hivyo bila ujuzi na ufahamu wa ndani wa kutosha. Elihu aliongezea hivi: “Laiti Ayubu angejaribiwa hata mwisho, kwa kuwa amejibu kama watu waovu.” (Ayubu 34:10, 11, 35, 36) Kwa njia iyo hiyo, imani na uaminifu wa maadili wetu waweza kuthibitishwa kabisa ‘tukijaribiwa hata mwisho’ kwa njia fulani. Hata hivyo, Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo hawezi kutuacha tujaribiwe kuliko vile tuwezavyo kustahimili.—1 Wakorintho 10:13.
11. Tujaribiwapo sana, twapaswa kukumbuka nini?
11 Elihu alipoendelea, alionyesha tena kwamba Ayubu alikuwa akikazia mno uadilifu wake mwenyewe. Fikira zapaswa kukazwa kwa Mfanyi Mtukufu wetu. (Ayubu 35:2, 6, 10) Mungu “hauhifadhi uhai wa waovu, lakini huwapa wateswao haki yao,” Elihu akasema. (Ayubu 36:6) Hakuna mtu awezaye kutoza hesabu njia ya Mungu na kusema kwamba hajakuwa mwadilifu. Yeye ametukuka kuliko tunavyojua, na hesabu ya miaka yake haitafutiki. (Ayubu 36:22-26) Tujaribiwapo sana, kumbuka kwamba Mungu wetu aishiye milele ni mwadilifu naye atatuthawabisha kwa matendo yetu yenye uaminifu yanayomletea sifa.
12. Maelezo ya mwisho ya Elihu yaonyesha nini kuhusu hali ya Mungu ya kutekeleza hukumu juu ya waovu?
12 Elihu alipokuwa akisema, kulikuwa na dhoruba iliyokuwa ikija. Ilipokaribia, moyo wake ulianza kupiga na kutetema. Yeye alisema juu ya mambo makubwa yaliyofanywa na Yehova na kusema: “Sikiliza neno hili, Ee Ayubu; simama kimya, uzifikiri kazi za Mungu za ajabu.” Kama Ayubu twahitaji kufikiria kazi za ajabu na staha yenye kicho ya Mungu. “Yeye Mwenyezi hatuwezi kumwona,” Elihu akasema. “Yeye ni mkuu mwenye uweza; tena mwenye hukumu, na mwingi wa haki, hataonea. Kwa hiyo watu humwogopa.” (Ayubu 37:1, 14, 23, 24) Maelezo ya kumalizia ya Elihu yatukumbusha kwamba karibuni Mungu atekelezapo hukumu juu ya waovu, yeye hatapuuza haki na uadilifu naye atahifadhi wale wanaomhofu wakiwa waabudu wake wenye kicho. Ni pendeleo kama nini kuwa miongoni mwa washika uaminifu wa maadili kama hao wamkubalio Yehova kuwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima! Vumilia kama alivyovumilia Ayubu, na usimruhusu Ibilisi akutoe kutoka mahali pako palipobarikiwa miongoni mwa umati huu wenye furaha.
Yehova Amjibu Ayubu
13, 14. (a) Yehova alianza kumwuliza Ayubu maswali kuhusu nini? (b) Twaweza kujifunza mambo yapi kwa maswali mengine ambayo Mungu alimwuliza Ayubu?
13 Ni lazima Ayubu alishangaa kama nini Yehova alipomzungumzia kutoka katika upepo wa kisulisuli! Upepo huo ulikuwa tendo la Mungu, si kama ule upepo ambao Shetani alitumia kuangusha nyumba na kuua watoto wa Ayubu. Ayubu alishindwa na maneno Mungu alipouliza hivi: “Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya nchi? . . . Au ni nani aliyeliweka jiwe lake la pembeni, hapo nyota za asubuhi zilipoimba pamoja, na wana wote wa Mungu walipopiga kelele kwa furaha?” (Ayubu 38:4, 6, 7) Yehova alimwuliza Ayubu swali baada ya swali kuhusu bahari, vazi la dunia la mawingu, mapambazuko, malango ya kifo, nuru na giza, na vikundi vya nyota. Ayubu hangeweza kusema lolote alipoulizwa: “Je! unazijua amri zilizoamuriwa mbingu?”—Ayubu 38:33.
14 Maswali mengine yalionyesha kwamba kabla ya mwanadamu kuumbwa na kupewa mamlaka juu ya samaki, ndege, wanyama, na viumbe vitambaavyo, Mungu alikuwa akiwaandalia—bila msaada au shauri lolote la binadamu. Maswali zaidi ya Yehova yalitaja viumbe kama fahali wakali, mbuni, na farasi. Ayubu aliulizwa: “Je! tai hupaa juu kwa amri yako, na kufanya kioto chake mahali pa juu?” (Ayubu 39:27) Bila shaka la! Ebu wazia jinsi Ayubu alivyoitikia Mungu alipomwuliza hivi: “Je! mwenye hoja atashindana na Mwenyezi?” Si ajabu kwamba Ayubu alisema: “Tazama, mimi si kitu kabisa, nikujibu nini? Naweka mkono wangu kinywani pangu.” (Ayubu 40:2, 4) Kwa kuwa Yehova huwa sahihi sikuzote, iwapo tupate shawishi la kulalamika dhidi yake, twapaswa ‘kuweka mkono wetu kinywani petu.’ Maswali ya Mungu vilevile yalitukuza ukuu, staha, na nguvu zake, kama zionyeshwavyo na uumbaji.
Behemothi na Leviathani
15. Kwa kawaida Behemothi huonwa kuwa mnyama gani, na ni zipi baadhi ya sifa zake?
15 Kisha Yehova alitaja Behemothi, ambaye kwa kawaida huonwa kuwa kiboko. (Ayubu 40:15-24, NW) Akitokeza sana kwa ukubwa wake, uzani mzito sana, na ngozi ngumu sana, mnyama huyo alaye mimea “hula nyasi.” Uwezo wake na nishati zake zatokana na viuno vyake na mishipa ya tumbo lake. Mifupa ya miguu yake ni yenye nguvu kama “mirija ya shaba.” Behemothi hana wasiwasi katika maji yaendayo kasi bali yeye huogelea kwa urahisi dhidi ya mwendo wa maji.
16. (a) Ufafanuzi wa Leviathani wafaana na kiumbe kipi, na ni yapi baadhi ya mambo ya hakika yanayomhusu? (b) Uwezo wa Behemothi na Leviathani waweza kudokeza nini kuhusu kutimiza migawo yetu katika utumishi wa Yehova?
16 Mungu pia alimwuliza Ayubu hivi: “Je! waweza kumvua Leviathani kwa ndoana ya samaki, au kutumia kamba kuufunga ulimi wake?” Ufafanuzi wa Leviathani wafaana na mamba. (Ayubu 41:1-34, NW) Hatafanya mapatano ya amani pamoja na mtu yeyote, na hakuna binadamu mwenye hekima awezaye kuthubutu kukiamsha kiumbe hicho cha majini. Mishale haiwezi kumkimbiza, naye “hucheka mshindo wa mkuki ukitupwa.” Leviathani mwenye ghadhabu huchemsha kilindi mfano wa nyungu ya mafuta. Jambo la kwamba Leviathani na Behemothi wana nguvu sana zaidi ya Ayubu lilisaidia kumnyenyekeza. Ni lazima sisi pia tukiri kwa unyenyekevu kwamba sisi wenyewe si wenye uwezo. Twahitaji hekima na nguvu zitokanazo na Mungu ili kuepuka meno ya Shetani, yule Joka, na kutimiza migawo yetu katika utumishi wa Yehova.—Wafilipi 4:13; Ufunuo 12:9.
17. (a) Ayubu ‘alimwonaje Mungu’? (b) Ni nini kilichothibitishwa na maswali ambayo Ayubu alishindwa kujibu, nayo yaweza kutusaidiaje?
17 Akiwa amenyenyekezwa kabisa, Ayubu alitambua maoni yake mabaya na kukiri kwamba alikuwa amesema bila ujuzi. Lakini, yeye alikuwa ameonyesha imani kwamba ‘angemwona Mungu.’ (Ayubu 19:25-27) Hilo lingetendekaje, kwa kuwa hakuna binadamu awezaye kumwona Yehova akaishi? (Kutoka 33:20) Kwa kweli, Ayubu aliona wonyesho wa uwezo wa kimungu, akasikia neno la Mungu, naye akapata kufunguliwa macho yake ya uelewevu ili aone kweli kuhusu Yehova. Kwa hiyo Ayubu ‘alitubu katika mavumbi na majivu.’ (Ayubu 42:1-6) Yale maswali mengi aliyoshindwa kujibu yalithibitisha ukuu kabisa wa Mungu na kuonyesha uduni wa mwanadamu, hata yule ambaye amejitoa kabisa kwa Yehova kama Ayubu. Jambo hilo latusaidia kuona kwamba mapendezi yetu yasiwekwe juu ya kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi kuu yake. (Mathayo 6:9, 10) Hangaiko letu kuu lapaswa kuwa kudumisha uaminifu wa maadili kwa Yehova na kuheshimu jina lake.
18. Wafariji bandia wa Ayubu walihitaji kufanya nini?
18 Lakini vipi juu ya wale wafariji bandia waliojiona kuwa wenye uadilifu? Yehova alikuwa na haki ya kuua Elifazi, Bildadi, na Sofari kwa sababu ya kutosema kweli kumhusu, kama Ayubu alivyokuwa amefanya. “Jitwalieni ng’ombe waume saba, na kondoo waume saba, mkamwendee mtumishi wangu Ayubu,” Mungu akasema, “mjisongezee sadaka ya kuteketezwa; na huyo mtumishi wangu Ayubu atawaombea ninyi.” Ilikuwa lazima hao watatu wajinyenyekeze ili kukubali. Ayubu mwenye kushika uaminifu wa maadili alikuwa asali kwa ajili yao, na Yehova alikubali sala yake. (Ayubu 42:7-9) Lakini vipi juu ya mke wa Ayubu, aliyekuwa amemhimiza akufuru Mungu afe? Yaonekana kwamba alipatanishwa naye kwa rehema ya Mungu.
Thawabu Zilizoahidiwa Zatupa Tumaini
19. Kuhusu Ayubu, Yehova alionyeshaje ukuu Wake juu ya Ibilisi?
19 Mara tu Ayubu alipoacha kuhangaikia mateseko yake na kuhuishwa katika utumishi wa Mungu, Yehova alimbadilishia hali. Baada ya Ayubu kusali kwa ajili ya wale watatu, Mungu ‘akaugeuza uteka wake’ na kumpa ‘mara mbili kuliko hayo aliyokuwa nayo.’ Yehova alionyesha ukuu Wake juu ya Ibilisi kwa kugeuza mkono wa Shetani wenye kuambukiza maradhi na kumponya Ayubu kimwujiza. Mungu vilevile alikinza kundi la mashetani kwa kumzingira tena Ayubu kwa ukigo kwa kutumia malaika Zake.—Ayubu 42:10; Zaburi 34:7.
20. Ni katika njia zipi Yehova alimthawabisha na kumbariki Ayubu?
20 Ndugu za Ayubu, dada zake, na watu aliowajua wakaendelea kuja kula naye, kumwonea huruma, na kumfariji juu ya msiba ambao Yehova aliruhusu umpate. Kila mmoja wao alimpa Ayubu pesa na pete ya dhahabu. Yehova alibariki mwisho wa Ayubu kuliko mwanzo wake, hivi kwamba akawa na kondoo 14,000, ngamia 6,000, na jozi za ng’ombe 1,000, na punda-wake 1,000. Ayubu pia alikuja kupata wana saba na binti watatu, idadi ileile aliyokuwa nayo mbeleni. Binti zake—Yemima, Kesia, na Keren-hapuhu—walikuwa wanawake warembo zaidi katika nchi, Ayubu akawapa urithi miongoni mwa ndugu zake. (Ayubu 42:11-15) Isitoshe, Ayubu aliishi kwa miaka mingine 140 na kuona vizazi vinne vya uzao wake. Masimulizi hayo yamalizia hivi: “Basi Ayubu akafa, mzee sana mwenye kujawa na siku.” (Ayubu 42:16, 17) Kuongezwa kwa uhai wake kulikuwa kazi ya kimwujiza ya Yehova Mungu.
21. Twasaidiwaje na masimulizi ya Maandiko kuhusu Ayubu, nasi twapaswa kuazimia kufanya nini?
21 Masimulizi ya Maandiko kuhusu Ayubu yatufanya tujihadhari juu ya mbinu za Shetani na kutusaidia kuona jinsi enzi kuu ya ulimwengu wote mzima yahusiana na uaminifu wa maadili wa binadamu. Kama Ayubu, wote wampendao Mungu watajaribiwa. Lakini twaweza kuvumilia jinsi Ayubu alivyovumilia. Alitoka katika majaribu yake akiwa na imani na tumaini, na thawabu zake zilikuwa nyingi. Tukiwa watumishi wa Yehova leo, tuna imani na tumaini la kweli. Na kuna tumaini tukufu kama nini ambalo Mthawabishaji Mkuu ameweka mbele ya kila mmoja wetu! Kukumbuka thawabu ya kimbingu kutawasaidia watiwa-mafuta kumtumikia Mungu kwa uaminifu mshikamanifu kwa maisha yao yote yanayobaki hapa duniani. Wengi wenye mataraja ya duniani hawatakufa kamwe, lakini wale watakaokufa watathawabishwa kwa ufufuo katika Paradiso duniani, pamoja na Ayubu mwenyewe. Wakiwa na tumaini la kweli kama hilo mioyoni na akilini, wale wote wanaompenda Mungu na wamthibitishe Shetani kuwa mwongo kwa kusimama zizima upande wa Yehova wakiwa washika uaminifu wa maadili na waungaji mkono kwa uthabiti wa enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima.
Ungejibuje?
◻ Ni yapi baadhi ya mambo yaliyotajwa na Ayubu katika jibu lake la mwisho kwa wafariji wake bandia?
◻ Elihu alithibitikaje kuwa shahidi wa Yehova asiyependelea upande wowote?
◻ Ni yapi baadhi ya maswali ya Mungu kwa Ayubu, nayo yalikuwa na matokeo gani?
◻ Umenufaikaje na masimulizi ya Maandiko kuhusu Ayubu?
[Picha katika ukurasa wa 18]
Maneno ya Yehova kuhusu Behemothi na Leviathani yalisaidia kumnyenyekeza Ayubu