Je, Umetia Moyo Yeyote Karibuni?
ELENA alikuwa na umri wa miaka 17 tu madaktari walipogundua kwamba alikuwa na kansa ya kifuko cha mayai. Mama yake, Mari, alilazimika kushindana na uchungu wa kumwona Elena katika maumivu makali sana.
Hatimaye, Elena alihamishwa kwenye hospitali fulani katika Madrid, Hispania, kilometa 1,900 kutoka kwao katika Visiwa vya Canary. Katika Madrid kikundi cha madaktari kilijitolea kufanya upasuaji bila damu. (Matendo 15:28, 29) Lakini muda mfupi baada ya upasuaji kuanza, ilidhihirika kwamba hali ya Elena hatimaye ingeongoza katika kifo. Kansa hiyo ilikuwa tayari imeenea kotekote katika mwili wake, na madaktari wapasuaji hawangetuliza tatizo hilo. Elena alikufa siku nane baada ya kuwasili katika Madrid.
Mari hakuhitaji kukabili jaribu hili lenye kuogofya akiwa peke yake. Kwa gharama yao wenyewe, wazee wawili wa Kikristo waliandamana naye na mwana wake mkubwa kwenda Madrid na kubaki huko hadi kifo cha Elena. “Walinisaidia kushindana na hisi ya utupu yenye kukata tamaa niliyohisi ndani,” aeleza Mari. “Sitasahau kamwe kitia-moyo walichonipa. Utegemezo wao wa kiroho na msaada wenye kutumika ulikuwa wenye thamani sana. Walikuwa ‘mahali [pa kweli] pa kujisitiri na dhoruba.’”—Isaya 32:1, 2.
Yehova afurahia kwamba wachungaji kama hawa hutunza kondoo wake kwa wororo sana. (Mithali 19:17; 1 Petro 5:2-4) Hata hivyo, kutoa kitia-moyo si pendeleo la wazee tu. Wakristo wote hukutana pamoja ili ‘kutiana moyo mmoja na mwenzake.’ (Waebrania 10:24, 25, NW) Kitia-moyo ni sehemu asilia ya ushirika wa Kikristo.
Kitia-Moyo Chahusisha Nini?
Sawa tu na jinsi ua zuri liinamavyo linyimwapo maji, ndivyo watu mmoja-mmoja—katika familia na kutanikoni—wawezavyo kunyauka kwa kukosa kitia-moyo. Kwa upande mwingine, kitia-moyo kwa wakati ufaao chaweza kuimarisha wale wakabilio kishawishi, kuchangamsha walioshuka moyo, na kuburudisha wanaotumikia Mungu kwa uaminifu.
Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kitia-moyo” huhusisha wazo la kitulizo, himizo, na faraja. Hivyo basi, kitia-moyo si tu kumweleza mtu kuwa anafanya vizuri. Huenda ikatia ndani kuandaa usaidizi wenye kutumika na msaada wa kiroho.
Kwa kweli, neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kitia-moyo” kihalisi humaanisha “mwaliko wa kuwa katika uandamani wa mtu fulani.” Kutembea kando kwa kando pamoja na ndugu na dada zetu wa kiroho hutuwezesha kutoa utegemezo wa mara hiyo ikiwa mmoja wao angechoka au kujikwaa. (Mhubiri 4:9, 10) Kwa kupendeza, watu wa Yehova “wamtumikia bega kwa bega.” (Sefania 3:9, NW) Na mtume Paulo aliita Mkristo fulani “mwenzi wa nira halisi.” (Wafilipi 4:3, NW) Kufanya kazi pamoja chini ya nira ileile kwa kutumikia bega kwa bega hufanya mzigo kuwa mwepesi, hasa kwa wale wasio na nguvu kiroho.—Linganisha Mathayo 11:29.
Walitoa Kitia-Moyo
Kwa kuwa kitia-moyo ni muhimu sana, acheni tufikirie baadhi ya vielelezo vyacho vya Kimaandiko. Nabii wa Mungu Musa alipokaribia mwisho wa uhai wake, Yehova alimpa Yoshua mgawo wa kuwa kiongozi wa Waisraeli. Huu haukuwa mgawo rahisi, kama Musa mwenyewe alivyojua vyema. (Hesabu 11:14, 15) Kwa hiyo, Yehova alimwambia Musa ‘amwagize Yoshua, amtie moyo mkuu, amtie na nguvu.’—Kumbukumbu la Torati 3:28.
Wakati wa waamuzi wa Israeli, binti ya Yeftha alitenda kupatana na nadhiri ya babaye kwa kuacha tazamio la kuwa na familia ili kutumikia katika patakatifu pa Yehova. Je, dhabihu yake ilikosa kuonekana? La kwa kuwa Waamuzi 11:40 (NW) husema: “Binti za Israeli walikuwa wakienda mwaka baada ya mwaka ili kumpongeza huyo binti ya Yeftha yule Mgileadi, siku nne katika mwaka.” Ziara hizo lazima iwe zilikuwa za kutia moyo sana kwa binti ya Yeftha mwenye kujidhabihu.
Kutoa kitia-moyo wakati mwingine huhitaji moyo mkuu. Wakati wa safari ya kwanza ya mtume Paulo ya kimishonari, alikumbana na upinzani mkali katika majiji ya Asia Ndogo. Aliondoshwa kutoka Antiokia, akanusurika kuuawa katika Ikonia, na kupigwa mawe na kuachwa akifikiriwa kuwa mfu katika Listra. Hata hivyo, muda mfupi baada ya hapo, Paulo na waandamani wake walirudi katika majiji haya, “wakizitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo kubaki katika imani na kusema: ‘Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.’” (Matendo 14:21, 22, NW) Paulo alikuwa tayari kuhatarisha uhai wake ili kutia moyo wanafunzi hawa wapya.
Lakini, wanafunzi wapya si ndio Wakristo pekee wahitajio kitia-moyo. Miaka mingi baadaye Paulo alipitia safari yenye taabu kuelekea Roma, ambapo alikuwa ahukumiwe. Akielekea mwisho wa safari yake, huenda alikuwa amevunjika moyo. Lakini alipofika mahali fulani kilometa 74 kusini-mashariki mwa Roma, alitiwa moyo. Kwa nini? Kwa sababu akina ndugu kutoka Roma walikuwa wamekuja kumlaki katika Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. ‘Alipowaona akamshukuru Mungu na kujipa moyo.’ (Matendo 28:15) Katika pindi sawa na hizo, kuwapo kwetu pekee kwaweza kuwa kitia-moyo sana kwa waamini wenzetu.
Tumia Fursa za Kutoa Kitia-Moyo
Kwa kweli, kuna fursa nyingi za kutoa kitia-moyo. Je, moyo wako uliguswa na hotuba nzuri ya mwanafunzi iliyotolewa na ndugu au dada katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Je, wafurahi kwamba kuna matineja wenye nguvu kiroho katika kutaniko? Je, uvumilivu wa walio wazee-wazee umekupendeza? Je, ulivutiwa na jinsi mmoja wa mapainia alivyotumia Biblia katika huduma ya nyumba kwa nyumba? Basi toa pongezi, na useme jambo la kutia moyo.
Kitia-moyo hutimiza daraka muhimu sana katika familia na vilevile katika kutaniko. Chaweza kusaidia wazazi wawalee watoto wao “katika adabu na maonyo ya Bwana.” (Waefeso 6:4) Kumwambia mtoto kuwa amefanya vizuri, na kueleza kwa nini, kwaweza kutia moyo kweli-kweli! Katika miaka ya utineja, wakati wachanga hukabili majaribu na misongo mingi, kitia-moyo chenye kuendelea chahitajiwa.
Ukosefu wa kitia-moyo wakati wa utoto waweza kuleta madhara. Leo Michael, mzee Mkristo, ni mwenye urafiki, lakini asema hivi: “Baba yangu hakusema hata mara moja kuwa nilifanya chochote vizuri. Kwa hiyo nilikua nikiwa na ukosefu wa kujistahi. . . . Ijapokuwa nina umri wa miaka 50 sasa, bado nathamini kutiwa moyo na rafiki zangu kwamba nafanya kazi nzuri nikiwa mzee. . . . Mambo niliyojionea mwenyewe yamenifunza jinsi kutia moyo wengine kulivyo kwa maana, nami hujitahidi sana kukitoa.”
Ni Nani Wahitajio Kitia-Moyo?
Wazee Wakristo wenye bidii wastahili kitia-moyo. Paulo aliandika hivi: “Tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkiwastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao.” (1 Wathesalonike 5:12, 13) Ni rahisi kuchukulia kazi ya bidii ya wazee kivivi-hivi tu. Lakini maneno ya uthamini wa moyo mweupe na kitia-moyo vyaweza kufanya mzigo wao uonekane kuwa mwepesi.
Wale miongoni mwetu ambao wanavumilia hali ngumu wanahitaji kitia-moyo pia. “Watieni moyo walio dhaifu; watieni nguvu wanyonge,” Biblia yashauri. (1 Wathesalonike 5:14) Wazazi wasio na mwenzi, wajane, matineja, wazee-wazee, na walio na kasoro za mwili ni miongoni mwa wale ambao huenda wakahisi kushuka moyo au kuhisi kuwa dhaifu kiroho pindi kwa pindi.
María ni mwanamke Mkristo ambaye kwa ghafula alijikuta ameachwa na mume wake. Alisema hivi: “Kama Ayubu, nilitaka nife nyakati fulani. [Ayubu 14:13] Na bado niliendelea, kwa msaada wa kitia-moyo nilichopata. Wazee wawili, niliowajua vyema sana walitumia saa nyingi kunisaidia ili nione thamani ya kuendelea katika utumishi wa wakati wote. Na dada wawili wenye kufahamu mambo walinifariji pia, wakisikiliza kwa saburi nilipowamiminia moyo wangu. Kwa kutumia Biblia, walinisaidia nione mambo jinsi Yehova huyaona. Sijui ni mara ngapi tulisoma Zaburi 55:22, lakini najua kwamba kwa kutumia andiko hili, pole kwa pole nilirudia usawaziko wangu wa kiroho na kihisia-moyo. Yote haya yalitukia miaka 12 iliyopita, na nafurahi kusema kuwa nimeendelea katika utumishi wa wakati wote hadi sasa. Maisha yangu ni yenye kuthawabisha na yenye furaha japo maumivu ya kihisia-moyo ya mara kwa mara. Nasadiki kuwa kitia-moyo katika wakati kama huo chaweza kufanya tofauti kubwa sana katika maisha ya mtu.”
Wengine wahitaji kitia-moyo kwa sababu wamefanya makosa na wanajikakamua kuyarekebisha. Labda wamepata karipio lenye upendo. (Mithali 27:6) Wazee ambao wametoa karipio hilo waweza kuwa macho ili kutoa sifa waonapo shauri la Kimaandiko likitumiwa. Maneno yao ya kitia-moyo yatakuwa na manufaa maradufu—kuthibitisha upendo wao kwa mkosaji ili asiwe mwenye ‘huzuni ipitayo kiasi’ na kumkumbusha manufaa za kutumia shauri.—2 Wakorintho 2:7, 8.
Mzee mmoja alifanya kosa zito na kupoteza pendeleo lake la uangalizi katika kutaniko. “Tangazo lilipofanywa kuhusu kuondolewa kwangu uzee, nilifikiri kuwa akina ndugu hawatajihisi wamestarehe nikiwa nao,” yeye asema. “Hata hivyo wazee waliweka sababu ya kuondolewa kuwa siri kabisa na wakanipa kitia-moyo. Kutaniko zima vilevile lilionyesha upendo na uandamani, ambao kwa wazi ulichochea kurudia kwangu hali ya kiroho.”
Iweni Wenye Kutia Moyo
Katika maisha yetu yenye shughuli nyingi, ni rahisi kupuuza kitia-moyo. Lakini kitia-moyo chaweza kuwa chenye mafaa kweli-kweli! Ili kutoa kitia-moyo chenye matokeo, wapaswa kuweka akilini mambo mawili. Kwanza, fikiria kuhusu utakalosema, ili kitia-moyo chako kiwe hususa. Pili, tafuta fursa ya kufikia mtu astahiliye sifa au ahitajiye kujengwa.
Kwa kadiri ufanyavyo hivi, utazidi kuwa mwenye furaha. Viwavyo vyote, Yesu alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35, NW) Kwa kutia moyo wengine, utajitia moyo mwenyewe. Kwa nini usifanye liwe lengo lako kutoa kitia-moyo kwa mtu fulani kila siku?