Masomo Kutokana na Miujiza ya Yesu
“NA SIKU ya tatu palikuwa na arusi huko Kana, mji wa Galilaya . . . Yesu naye alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake. Hata divai ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, Hawana divai.” Tukio hili liliandaa nafasi ya muujiza wa kwanza wa Yesu.—Yohana 2:1-3.
Je, tatizo kama hilo halikuwa dogo sana, duni sana, kumwambia Yesu? Aeleza msomi mmoja wa Biblia: “Ukaribishaji-wageni katika Mashariki ulikuwa daraka takatifu . . . Ukaribishaji-wageni halisi, hasa kwenye karamu ya arusi, ulitaka wingi wa vyakula na vinywaji. Ikiwa vitu hivyo [vingekwisha] kwenye karamu ya arusi, familia na mume na mke hao wachanga wangeaibika sikuzote.”
Kwa hiyo Yesu alichukua hatua. Aliona “mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha.” Desturi ya kutawadha kabla ya milo ilikuwa ya kawaida kati ya Wayahudi, na maji mengi yalikuwa yakihitajiwa ili kutumikia mahitaji ya waliopo. “Jalizeni mabalasi maji,” Yesu akawaamuru wale waliokuwa wakitumikia wageni. Yesu hakuwa “mkuu wa meza,” lakini alisema moja kwa moja na kwa mamlaka. Simulizi lasema hivi: “Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji [yalikuwa yamepata] kuwa divai.”—Yohana 2:6-9; Marko 7:3.
Yaweza kuonekana kuwa jambo la ajabu kwamba jambo la kawaida kama arusi lingekuwa mahali pa muujiza wa kwanza wa Yesu, lakini tukio hilo lafunua mengi kuhusu Yesu. Yeye alikuwa mseja, na kwa matukio kadha wa kadha alizungumzia faida za useja na wanafunzi wake. (Mathayo 19:12) Hata hivyo, kuwapo kwake kwenye karamu ya arusi kulifunua kwamba hakupinga ndoa. Alikuwa mwenye usawaziko, mwenye kuunga mkono mpango wa ndoa; aliuona kuwa jambo la heshima machoni pa Mungu.—Linganisha Waebrania 13:4.
Yesu hakuwa mtawa-shupavu ambaye wachoraji wa kanisa baadaye walimwonyesha kuwa. Kwa wazi alifurahia kuwa miongoni mwa watu naye hakuchukia kushirikiana nao. (Linganisha Luka 5:29.) Hivyo matendo yake yaliwekea kielelezo wafuasi wake. Yesu mwenyewe alionyesha kwamba hawakupaswa kuwa wenye uzito au kuudhika isivyohitajika—kana kwamba uadilifu ulimaanisha ukosefu wa shangwe. Kinyume cha hayo, baadaye Wakristo waliamriwa: “Furahini katika Bwana sikuzote.” (Wafilipi 4:4) Wakristo leo hujihadhari kuweka tafrija ikiwa katika mipaka ifaayo. Wao hupata shangwe yao katika utumishi wa Mungu, lakini wakifuata kielelezo cha Yesu, pindi kwa pindi wao hupata wakati wa kufurahia ushirika wa mmoja na mwenzake katika kikao cha kijamii.
Ona pia wororo wa hisiamoyo za Yesu. Hakulazimika kufanya muujiza. Hakukuwa na unabii kuhusu jambo hili uliobidi kutimizwa. Inaonekana kwamba, Yesu alisukumwa tu na hangaiko la mama yake na hali mbaya ya mume na mke waliokuwa wakioana. Alijali hisia zao akataka wasione aibu. Je, hilo halijengi uhakika wako kwamba Kristo anapendezwa kikweli na wewe—hata shida zako za kila siku?—Linganisha Waebrania 4:14-16.
Kwa kuwa kila mtungi “lapata kadiri ya nzio mbili tatu” za maji, kiasi kikubwa sana cha divai kilihusika katika muujiza wa Yesu—labda lita 390 (galoni 105)! (Yohana 2:6) Kwa nini kiasi kikubwa namna hiyo kilihitajika? Yesu hakuwa akiendeleza ulevi, jambo ambalo Mungu hulaumu. (Waefeso 5:18) Badala ya hilo, alikuwa akionyesha ukarimu wa kimungu. Kwa sababu divai ilikuwa kinywaji cha kawaida, mabaki yoyote yangetumiwa kwenye pindi nyinginezo.—Linganisha Mathayo 14:14-20; 15:32-37.
Wakristo wa mapema waliiga kielelezo cha Yesu cha ukarimu. (Linganisha Matendo 4:34, 35.) Na watu wa Yehova leo wanatiwa moyo vilevile ‘kuwapa watu vitu.’ (Luka 6:38) Hata hivyo, muujiza wa kwanza wa Yesu una umaana wa kiunabii. Unaelekeza kwenye wakati ujao ambapo Mungu ataandaa kwa ukarimu “karamu ya vitu vinono, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake,” akiondolea mbali njaa kabisa.—Isaya 25:6.
Lakini, vipi ile miujiza mingi aliyoifanya Yesu iliyohusisha ponyo la kimwili? Twaweza kujifunza nini kutokana nayo?
Kufanya Mema Wakati wa Sabato
“Simama, jitwike godoro lako, uende.” Yesu alimwambia mtu aliyekuwa amekuwa mgonjwa kwa miaka 38 maneno hayo. Simulizi hilo la Gospeli laendelea: “Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake, akaenda.” Kwa kushangaza, si wote waliopendezwa na mabadiliko haya ya hali. Simulizi hilo lasema: “Wayahudi wakamwudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya sabato.”—Yohana 5:1-9, 16.
Sabato ilikusudiwa kuwa siku ya pumziko na ya kushangilia kwa wote. (Kutoka 20:8-11) Hata hivyo, kufikia siku ya Yesu, ilikuwa imekuwa mvurugo wa sheria zilizofanywa za kuonea. Msomi Alfred Edersheim aliandika kwamba katika visehemu virefu vya Talmud vya sheria ya Sabato, “mambo yanazungumzwa kwa uzito kana kwamba ni ya umuhimu wa kidini, ambayo mtu asingewazia hata kidogo kwamba mwenye kufikiri kuzuri angefikiria kwa uzito.” (The Life and Times of Jesus the Messiah) Marabi waliwekea umuhimu wa kufa na kupona sheria hafifu, za kulemaza zilizoendesha karibu kila sehemu ya maisha ya Myahudi—mara nyingi bila kujali hisia za kibinadamu. Sheria moja ya Sabato iliamuru: “Ikiwa jengo lamwangukia mtu na kuna shaka kama yupo au la, au ikiwa yuko hai au amekufa, au ikiwa ni mtu wa mataifa au ni Mwisraeli, waweza kumwondolea magofu. Ikiwa watamkuta akiwa hai waweza kumwondolea magofu hata zaidi; lakini ikiwa [yeye ni] mfu wamwache.”—Tractate Yoma 8:7, The Mishnah, iliyotafsiriwa na Herbert Danby.
Yesu alionaje kubishania huko kwa kisheria juu ya mambo madogo madogo? Aliposhambuliwa kwa ajili ya kuponya wakati wa Sabato, yeye alisema: “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi.” (Yohana 5:17) Yesu hakuwa akifanya kazi ya kimwili ili ajitajirishe. Badala ya hilo, alikuwa akifanya mapenzi ya Mungu. Kama vile Walawi walivyoruhusiwa kuendelea na utumishi wao mtakatifu wakati wa Sabato, kwa haki Yesu angeweza kuendelea na wajibu wake mbalimbali aliogawiwa na Mungu akiwa Mesiya bila kuihalifu Sheria ya Mungu.—Mathayo 12:5.
Maponyo ya Yesu ya siku ya Sabato pia yaliwafunua waandishi na Mafarisayo Wayahudi kuwa wenye “haki kupita kiasi”—wasiopindika na wasio na usawaziko katika kufikiri kwao. (Mhubiri 7:16) Kwa kweli, hayakuwa mapenzi ya Mungu kwamba matendo mema yazuiliwe siku fulani za juma; wala Mungu hakukusudia Sabato iwe zoea la kisheria lisilo na maana. Yesu alisema kwenye Marko 2:27: “Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu, si mwanadamu kwa ajili ya sabato.” Yesu aliwapenda watu, wala si sheria za kulemaza.
Hivyo yafaa kwa Wakristo leo kutokuwa washupavu au wenye kufikiria sana ufuataji wa sheria. Wale wenye mamlaka kutanikoni huepuka kuwekea wengine mizigo kwa sheria na maoni yaliyofanywa na wanadamu yapitayo kiasi. Kielelezo cha Yesu pia chatutia moyo kutafuta fursa za kufanya mema. Kwa mfano, Mkristo hangefikiri kamwe kwamba atashiriki kweli za Biblia wakati tu anaposhiriki kirasmi katika huduma ya nyumba kwa nyumba au wakati ambapo yuko jukwaani akitoa hotuba. Mkristo, asema mtume Petro, apaswa ‘awe tayari sikuzote kumjibu kila mtu aulizaye habari za tumaini lililo ndani yake.’ (1 Petro 3:15, italiki ni zetu.) Kufanya yaliyo mema hakuna vizuizi vya wakati.
Somo la Huruma
Muujiza mwingine wenye kutokeza umerekodiwa katika Luka 7:11-17. Kulingana na simulizi hilo, Yesu “alikwenda mpaka mji mmoja uitwao Naini, na wanafunzi wake walifuatana naye pamoja na mkutano mkubwa.” Mpaka siku ya leo, makaburi yaweza kuonekana upande wa kusini-mashariki wa kijiji cha kisasa cha Waarabu cha Neini. “Alipokaribia lango la [jiji],” alikutana na hali yenye makelele. “Hapo palikuwa na maiti anachukuliwa nje, ni mwana pekee wa mamaye ambaye ni mjane, na watu wa [jiji] wengi walikuwa pamoja naye.” H. B. Tristram alisema kwamba “njia ya kufanya maziko haijabadilika” tangu nyakati za kale, akiongeza: “Mimi nimewahi kuona wanawake wakitangulia jeneza, wakiongozwa na wanawake wajuao kuomboleza. Huinua mikono yao ghafula, hung’oa nywele zao, kwa wonyesho mwingi wa huzuni, na kuliitaita kwa sauti kubwa jina la aliyekufa.”—Eastern Customs in Bible Lands.
Miongoni mwa mvurugo kama huo wenye makelele alitembea mjane mwenye huzuni ambaye kuonekana kwake kwenyewe lazima kuwe kulionyesha uchungu mwingi. Akiwa tayari amempoteza mumeye, alimwona mwanaye kuwa, kwa maneno ya mtungaji Herbert Lockyer, “tegemeo la uzee wake, na faraja ya upweke wake—tegemeo na nguzo ya nyumba. Kwa kumpoteza mwanaye wa pekee, tegemeo la mwisho lililobaki lilikuwa limeondolewa.” (All the Miracles of the Bible) Itikio la Yesu lilikuwa nini? Katika maneno ya Luka yenye ufasaha, “Bwana alipomwona alimwonea huruma, akamwambia, Usilie.” Ule usemi ‘kumwonea huruma’ umetolewa katika neno la Kigiriki limaanishalo kihalisi “matumbo.” Lamaanisha “kuchochewa kihisiamoyo kindani sana.” (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) Ndiyo, hisiamoyo za Yesu zilichochewa sana.
Yaelekea mama wa Yesu mwenyewe alikuwa mjane wakati huo, kwa hiyo huenda alijua uchungu wa kufiwa kwa kumpoteza baba yake mlezi, Yusufu. (Linganisha Yohana 19:25-27.) Mjane huyo hakuhitaji kumsihi Yesu. Kwa hiari, “akakaribia, akaligusa jeneza,” ijapokuwa uhakika wa kwamba chini ya Sheria ya Kimusa kugusa maiti kulimfanya mtu awe asiye safi. (Hesabu 19:11) Kupitia nguvu zake za kimuujiza, Yesu angeweza kuondoa chanzo chenyewe cha kutokuwa safi! “Akasema, Kijana, nakuambia, Inuka. Yule maiti akainuka, akaketi, akaanza kusema. Akampa mama yake.”
Somo lenye kuchochea la huruma kama nini! Wakristo hawapaswi kuiga mitazamo yenye ubaridi ya ukosefu wa upendo, iliyo dhahiri katika “siku [hizi] za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Kinyume cha hilo, 1 Petro 3:8 lahimiza: “Neno la mwisho ni hili; mwe na nia moja, wenye kuhurumiana, wenye kupendana kama ndugu, wasikitikivu, wanyenyekevu.” Wakati mtu tunayemjua apatwapo na kifo au ugonjwa mbaya, sisi hatuwezi kumfufua au kumponya aliye mgonjwa. Lakini twaweza kutoa msaada na faraja yenye kutumika, pengine tu kwa kuwapo na kulia pamoja nao.—Warumi 12:15.
Ufufuo huu wenye kutazamisha uliofanywa na Yesu pia unaelekezea kwenye wakati ujao—wakati ambapo “wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka”! (Yohana 5:28, 29) Duniani kote, waliofiwa watahisi binafsi huruma ya Yesu wakati mama, baba, watoto, na marafiki waliokufa watakaporudi kutoka makaburini!
Masomo ya Miujiza
Kwa wazi, basi, miujiza ya Yesu ilikuwa zaidi ya maonyesho ya nguvu yenye kusisimua. Ilimtukuza Mungu, ikiwekea kigezo Wakristo wanaosihiwa “kumtukuza Mungu.” (Warumi 15:6) Ilitia moyo kutenda mema, kuonyesha ukarimu, kuonyesha huruma. La maana zaidi, ilitumika kuwa matendo yenye ono la kimbele lenye nguvu la yatakayofanywa wakati wa Utawala wa Mileani wa Kristo.
Alipokuwa duniani, Yesu alifanya matendo yake yenye nguvu katika kisehemu kidogo cha dunia. (Mathayo 15:24) Akiwa Mfalme aliyetukuzwa, enzi yake itaenea duniani kote! (Zaburi 72:8) Huko nyuma, wale waliopata kuponywa na kufufuliwa kwa miujiza yake mwishowe walikufa. Chini ya utawala wake wa kimbingu, dhambi na kifo zitaondolewa kabisa, zikifungulia njia uhai wa milele. (Warumi 6:23; Ufunuo 21:3, 4) Ndiyo, miujiza ya Yesu inaelekezea njia wakati ujao mtukufu. Mashahidi wa Yehova wamesaidia mamilioni kukuza tumaini halisi la kuwa sehemu ya huo. Hadi wakati huo uje, miujiza ya Yesu Kristo imeandaa mwonjo wenye kustaajabisha kama nini wa yale yatakayotokea karibuni!
[Picha katika ukurasa wa 7]
Yesu ageuza maji kuwa divai