Kujiweka Wakfu—Kwa Nani?
“Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda, nasi tutatii.”—KUTOKA 24:7.
1, 2. (a) Watu wengine wamejitoa kwa mambo gani? (b) Je, wakfu ni jambo lihusulo watu wa kidini tu?
KATIKA Februari 1945, marubani wa ndege ya kijeshi Zero-fighter wa kikosi cha Japani cha Yatabe Flying Corps walikuwa wamekusanyika katika ukumbi fulani. Kila mmoja alipewa kipande cha karatasi cha kuandikia kama angejitolea kuwa mshiriki wa kikosi cha kushambulia cha kamikaze. “Nilifikiri mwito wangu ulikuwa kujidhabihu katika wakati wa hatari ya kitaifa,” asema ofisa mmoja aliyekuwapo wakati huo. “Kwa kuchochewa kihisiamoyo kujifanya nipatikane, nilijitoa kwa ajili ya utume huo.” Alizoezwa kuendesha na kuwa rubani wa Ohka (ndege-roketi ya kujiua) na kuigongesha kwenye meli ya vita ya adui. Hata hivyo, vita iliisha kabla ya yeye kuwa na fursa ya kufanya hivyo na hivyo kufa kwa ajili ya nchi yake na maliki wake. Japani iliposhindwa vitani, imani yake katika maliki ilivunjika.
2 Wakati mmoja, wengi Japani walikuwa wamejitoa kwa maliki, ambaye waliamini kuwa mungu aliye hai. Katika nchi nyingine, kumekuwa na kungali kuna vitu vingine vya kupewa ujitoaji. Mamilioni wamejitoa kwa Mariamu, Buddha, au vijimungu vingine—ambavyo mara nyingi huwakilishwa na sanamu. Kwa kuvutwa na usemaji wa ajabu, wengine humwaga fedha zao ambazo wamechuma kwa bidii mifukoni mwa waeneza evanjeli wa televisheni katika kuwaunga mkono jambo ambalo ni sawa na ujitoaji. Baada ya vita, Wajapani waliovunjika moyo walitafuta kitu kipya ambacho wangeweza kuweka wakfu maisha zao kwacho. Kwa wengine, kitu hicho kilikuwa kazi. Iwe Mashariki au Magharibi, wengi hujiweka wakfu kwa ukusanyaji wa mali. Vijana hufuatisha sana maisha yao na wanamuziki fulani, ambao wao huiga mitindo-maisha yao. Idadi kubwa leo wamekuwa wenye kujiabudu, wakifanya tamaa zao wenyewe kuwa kitu cha kupewa ujitoaji wao. (Wafilipi 3:19; 2 Timotheo 3:2) Lakini je, vitu hivyo au watu hao kweli wastahili ujitoaji wa mtu wa moyo wote?
3. Vitu fulani vya kupewa ujitoaji vimethibitikaje kuwa vya bure?
3 Wanapokabili uhalisi, mara nyingi waabudu wa sanamu hukata tamaa. Matokeo ya ujitoaji kwa sanamu huwa kuvunjika moyo waabudu hao wanapong’amua kwamba sanamu zao ni “kazi ya mikono ya wanadamu” tu. (Zaburi 115:4) Wakati kashfa zinazohusu waeneza evanjeli mashuhuri zinapofunuliwa, watu wenye moyo mweupe huhisi wamekatishwa tamaa. Ule uchumi “usio thabiti” ulipoisha, wafanyakazi walipatwa na mivurugo ya akilini kwa kuwa walijipata kwenye orodha ya wale waliokuwa wameondoshwa kazi kwa muda. Kupungua kwa utendaji wa kiuchumi hivi karibuni kuliathiri sana waabudu wa Mammon. Madeni yaliyopatikana kwa tumaini la kuchuma fedha nyingi yalikuwa mzigo wa kulemea kukiwa na taraja kidogo la kulipa madeni hayo. (Mathayo 6:24, NW kielezi-chini) Wanamuziki mashuhuri wa roki na watumbuizaji wengine wanapokufa au umashuhuri wao kufifia, waabudu wao huachwa hivi tu. Na wale ambao wamefuata njia ya kujipendeza sana mara nyingi huvuna matunda machungu.—Wagalatia 6:7.
4. Ni nini husukuma watu kuweka maisha zao wakfu kwa vitu vya bure?
4 Ni nini huwasukuma watu wajiweke wakfu kwa ubatili wa jinsi hiyo? Kwa kadiri kubwa, ni roho ya ulimwengu chini ya Shetani Ibilisi. (Waefeso 2:2, 3) Uvutano wa roho hiyo huonekana kwa njia mbalimbali. Mtu aweza kudhibitiwa na mapokeo ya familia ambayo imekabidhiwa na wazazi wake wa kale. Elimu na malezi yaweza sana kuwa na uvutano juu ya fikira. Mazingira ya mahali pa kazi yaweza kusukuma “mashujaa wa makampuni” kwenye uraibu wa kazi ambao waweza kuhatarisha uhai. Tamaa ya kupata mali zaidi inachochewa na mtazamo wa ulimwengu wa kufuatia vitu vya kimwili. Mioyo ya wengi inafisidiwa, ikiwasukuma wajitoe kwenye tamaa zao wenyewe zenye ubinafsi. Wao hushindwa kuchunguza kama vitu hivyo wanavyofuatilia vyastahili ujitoaji wao.
Taifa Lililojiweka Wakfu
5. Ni wakfu gani uliowekwa kwa Yehova miaka zaidi ya 3,500 iliyopita?
5 Miaka zaidi ya 3,500 iliyopita, taifa moja la watu lilipata kitu chenye kustahili zaidi kupewa ujitoaji. Wao walijiweka wakfu kwa Mungu mwenye enzi kuu, Yehova. Likiwa kikundi, taifa la Israeli lilitangaza wakfu walo kwa Mungu katika jangwa la Sinai.
6. Ni nini kilichopaswa kuwa umaana wa jina la Mungu kwa Waisraeli?
6 Ni nini kilichowasukuma Waisraeli watende kwa njia hiyo? Walipokuwa utumwani Misri, Yehova alimpa Musa utume awaongoze kwenye uhuru. Musa aliuliza jinsi alivyopaswa kumtambulisha huyo Mungu aliyekuwa amemtuma, na Mungu alijifunua kuwa “Mimi nitathibitika kuwa kile ambacho mimi nitathibitika kuwa.” Yeye alimwelekeza Musa kuwaambia wana wa Israeli hivi: “Mimi nitathibitika kuwa amenituma kwenu.” (Kutoka 3:13, 14, NW) Usemi huo ulionyesha kwamba Yehova huwa chochote kile kinachohitajika ili kukamilisha makusudi yake. Yeye angejifunua kuwa Mtimizaji wa ahadi kwa njia ambayo mababu za Waisraeli hawakupata kujua kamwe.—Kutoka 6:2, 3.
7, 8. Waisraeli walikuwa na uthibitisho upi mbalimbali kwamba Yehova alikuwa Mungu astahiliye ujitoaji wao?
7 Waisraeli walishuhudia kuteseka kwa nchi ya Misri na watu wayo kwa yale Mapigo Kumi. (Zaburi 78:44-51) Kisha, yaelekea watu zaidi ya milioni tatu kati yao, kutia na wanawake na watoto, walifunganya mizigo na kuhama nchi ya Gosheni katika usiku mmoja, ambalo lenyewe lilikuwa jambo lenye kutokeza sana. (Kutoka 12:37, 38) Halafu, kwenye Bahari Nyekundu, Yehova alijifunua kuwa “mtu wa vita” alipookoa watu wake kutoka kwa vikosi vya kijeshi vya Farao kwa kuitenganisha bahari ili kuruhusu Waisraeli wapite na baadaye kwa kuifunga ili kuzamisha Wamisri waliokuwa wakifuatia. Likiwa tokeo, “Israeli akaiona ile kazi kubwa aliyoifanya BWANA juu ya Wamisri, ndipo hao watu wakamcha BWANA, wakamwamini BWANA.”—Kutoka 14:31; 15:3; Zaburi 136:10-15.
8 Kana kwamba bado walikosa uthibitisho juu ya kile kimaanishwacho na jina la Mungu, Waisraeli walinung’unika dhidi ya Yehova na mwakilishi wake Musa juu ya upungufu wa chakula na maji. Yehova alituma kware, akanyesha mana, na kusababisha maji yabubujike kutoka mwambani huko Meriba. (Kutoka 16:2-5, 12-15, 31; 17:2-7) Yehova aliwaokoa pia Waisraeli kutoka kwa shambulio la Waamaleki. (Kutoka 17:8-13) Waisraeli hawangeweza kwa njia yoyote kukanusha yale ambayo Yehova alimtangazia Musa baadaye: “BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.” (Kutoka 34:6, 7) Kwa kweli, Yehova alijithibitisha kuwa kitu chenye kustahili kupewa ujitoaji wao.
9. Kwa nini Yehova aliwapa Waisraeli fursa ya kuonyesha wakfu wao kumtumikia, nao waliitikiaje?
9 Ingawa Yehova alikuwa na haki ya kuwamiliki Waisraeli kwa sababu alikuwa amewakomboa kutoka Misri, yeye, akiwa Mungu mwenye fadhili na rehema, aliwapa fursa ya kuonyesha kwa hiari tamaa yao ya kumtumikia. (Kumbukumbu la Torati 7:7, 8; 30:15-20) Yeye aliorodhesha pia masharti ya agano kati yake na Waisraeli. (Kutoka 19:3-8; 20:1–23:33) Musa alipowaambia masharti hayo, Waisraeli walitangaza hivi: “Hayo yote aliyoyanena BWANA tutayatenda, nasi tutatii.” (Kutoka 24:3-7) Kwa hiari yao wenyewe, wakawa taifa lililojiweka wakfu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.
Uthamini Huongoza Kwenye Wakfu
10. Wakfu wetu kwa Yehova wapaswa utegemee nini?
10 Yehova, aliye Muumba, aendelea kustahili ujitoaji wetu wa nafsi yote. (Malaki 3:6; Mathayo 22:37; Ufunuo 4:11) Hata hivyo, wakfu wetu haupaswi utegemee imani isiyo ya kiakili, hisiamoyo za muda tu, wala kubembelezwa na wengine—hata wazazi. Lazima utegemee ujuzi sahihi wa ile kweli kumhusu Yehova na uthamini kwa ajili ya yale ambayo Yehova ametufanyia. (Warumi 10:2; Wakolosai 1:9, 10; 1 Timotheo 2:4) Kama vile Yehova alivyowapa Waisraeli fursa ya kuonyesha wakfu wao kwa hiari, ndivyo yeye hutupa sisi nafasi ya kujiweka wakfu kwa hiari na kuonyesha wakfu huo hadharani.—1 Petro 3:21.
11. Funzo letu la Biblia limefunua nini kumhusu Yehova?
11 Kupitia funzo la Biblia, twaja kumjua Mungu akiwa mtu. Neno lake hutusaidia tutambue sifa zake kama vile zionyeshwavyo katika uumbaji. (Zaburi 19:1-4) Twaweza kuona kutokana na Neno lake kwamba yeye si Utatu wa kifumbo asiyeweza kueleweka. Yeye hashindwi vitani na hivyo halazimiki kukanusha Uungu wake. (Kutoka 15:11; 1 Wakorintho 8:5, 6; Ufunuo 11:17, 18) Kwa sababu yeye ametimiza ahadi zake, tunakumbushwa kile kimaanishwacho na jina lake zuri, Yehova. Yeye ndiye Mkusudiaji Mtukufu. (Mwanzo 2:4, NW kielezi-chini; Zaburi 83:18; Isaya 46:9-11) Kwa kujifunza Biblia, twaja kuelewa kwa wazi jinsi alivyo mwaminifu na mwenye kutumainika.—Kumbukumbu la Torati 7:9; Zaburi 19:7, 9; 111:7.
12. (a) Ni nini lituvutalo kwa Yehova? (b) Maono ya maisha halisi yaliyorekodiwa katika Biblia humsukumaje mtu atake kumtumikia Yehova? (c) Wewe wahisije juu ya kumtumikia Yehova?
12 Jambo hasa lituvutalo kwa Yehova ni utu wake wenye upendo. Biblia huonyesha jinsi alivyo mwenye upendo, mwenye kusamehe, na mwenye rehema anaposhughulika na wanadamu. Fikiria jinsi alivyomfanikisha Ayubu baada ya Ayubu kudumisha uaminifu-maadili wake kwa uaminifu. Ono la Ayubu lakazia kwamba “Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.” (Yakobo 5:11; Ayubu 42:12-17) Fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Daudi alipozini na kuua kimakusudi. Ndiyo Yehova yu tayari kusamehe hata dhambi nzito wakati mtenda-dhambi amkaribiapo akiwa na “moyo uliovunjika na kupondeka.” (Zaburi 51:3-11, 17) Fikiria njia ambayo Yehova alishughulika na Sauli wa Tarso, ambaye mwanzoni alikuwa mnyanyasaji wa watu wa Mungu mwenye kuazimia. Vielelezo hivyo vyakazia rehema na nia ya Mungu yenye ukarimu ya kutumia wale waliotubu. (1 Wakorintho 15:9; 1 Timotheo 1:15, 16) Paulo alihisi kwamba angeweza kutoa uhai wake hasa kwa ajili ya kumtumikia Mungu huyu mwenye upendo. (Warumi 14:8) Je, wewe huhisi vivyo hivyo?
13. Ni wonyesho gani mkubwa wa upendo kwa upande wa Yehova uchocheao wale wenye mioyo ifaayo wajiweke wakfu kwake?
13 Yehova aliwaandalia Waisraeli wokovu kutoka utumwa katika Misri, naye ameandaa njia ya kutuokoa kutoka utumwa wa dhambi na kifo—yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Paulo asema hivi: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Warumi 5:8) Mpango huo wenye upendo huchochea wale wenye mioyo ifaayo wajiweke wakfu kwa Yehova kupitia Yesu Kristo. “Maana, upendo wa Kristo watubidisha; maana tumehukumu hivi, ya kwamba mmoja alikufa kwa ajili ya wote, basi walikufa wote; tena alikufa kwa ajili ya wote, ili walio hai wasiwe hai tena kwa ajili ya nafsi zao wenyewe, bali kwa ajili yake yeye aliyekufa akafufuka kwa ajili yao.”—2 Wakorintho 5:14, 15; Warumi 8:35-39.
14. Je, ujuzi pekee kuhusu shughuli za Yehova watosha kutusukuma tuziweke maisha zetu wakfu kwake? Eleza.
14 Bado, kuwa na ujuzi kuhusu utu wa Yehova na kushughulika kwake na wanadamu hakutoshi. Uthamini wa kibinafsi kuelekea Yehova lazima ukuzwe. Hilo laweza kufanywaje? Kwa kutumia Neno la Mungu maishani mwetu na kujionea kwamba kanuni zinazopatikana ndani yalo hufanya kazi kwelikweli. (Isaya 48:17) Lazima tuhisi kwamba Yehova ametuokoa kutoka katika tope la ulimwengu huu mwovu ulio chini ya utawala wa Shetani. (Linganisha 1 Wakorintho 6:11.) Katika kung’ang’ana kwetu kufanya yaliyo sawa, twajifunza kumtegemea Yehova, na twajionea kwamba Yehova ni Mungu aliye hai, “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 62:8; 65:2, NW) Upesi twahisi tukiwa karibu sana naye na twaweza kumwambia kwa siri hisia zetu za ndani kabisa. Ile hisia changamfu ya kumpenda Yehova yaongezeka ndani yetu. Hilo bila shaka litatuongoza sisi tuweke maisha zetu wakfu kwake.
15. Ni nini kilichomhamasisha mtu mmoja, ambaye hapo zamani alikuwa amejitolea kwa kazi, amtumikie Yehova?
15 Wengi wamekuja kumjua Mungu huyu mwenye upendo, Yehova, na wameweka maisha zao wakfu kumtumikia. Fikiria kielelezo cha fundi mmoja wa stima aliyekuwa na biashara yenye kusitawi. Kulikuwa na nyakati ambazo alikuwa akianza kazi asubuhi na kufanya kazi muda wote wa mchana hadi usiku akija nyumbani saa 11 alfajiri iliyofuata. Baada ya kupumzika kwa karibu muda wa saa moja, alikuwa akienda kufanya kazi iliyofuata. “Nilikuwa nimejitolea kwa kazi yangu,” yeye akumbuka. Mke wake alipoanza kujifunza Biblia, yeye alijiunga naye. Mtu huyo asema: “Miungu yote niliyokuwa nimeijua kufikia wakati huo ilikuwa ikingoja kutumikiwa tu, bila kufanya lolote la kutunufaisha. Lakini Yehova alichukua hatua ya kwanza akamtuma Mwana wake mzaliwa-pekee duniani kwa kujidhabihu sana kibinafsi.” (1 Yohana 4:10, 19) Katika miezi kumi, mtu huyo alijiweka wakfu kwa Yehova. Baada ya hilo, alikazia fikira kumtumikia Mungu aliye hai. Alianza huduma ya wakati wote, akahama ili kutumika mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Yeye, kama vile mitume, ‘aliacha vyote na kumfuata Yesu.’ (Mathayo 19:27) Baada ya miezi miwili, yeye na mke wake waliitwa kutumika kwenye tawi la Watch Tower Bible and Tract Society katika nchi walimoishi, ili aweze kusaidia na kazi ya stima. Kwa miaka zaidi ya 20, yeye amekuwa akifanya kazi kwenye tawi, akifanya kazi aipendayo—si kwa ajili yake mwenyewe bali kwa ajili ya Yehova.
Onyesha Wakfu Wako Hadharani
16. Ni zipi baadhi ya hatua ambazo mtu angechukua katika kujiweka wakfu kwa Yehova?
16 Baada ya kujifunza Biblia kwa muda fulani, vijana na wazee vilevile watakuja kumthamini Yehova na yale ambayo amewafanyia. Hilo lapasa kuwasukuma wajitoe kwa Mungu. Huenda ukawa mmoja wao. Waweza kujiwekaje wakfu kwa Yehova? Baada ya kupata ujuzi sahihi kutoka katika Biblia, wapaswa utende kwa kupatana na ujuzi huo na kudhihirisha imani katika Yehova na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Tubu na kugeuka kutoka kwenye mwendo wowote wa zamani wenye dhambi. (Matendo 3:19) Kisha utafikia hatua ya wakfu, kwa kuuonyesha kwa maneno mazito ya sala kwa Yehova. Bila shaka sala hiyo itapenya akilini mwako kwa kudumu, kwani itakuwa mwanzo wa uhusiano mpya na Yehova.
17. (a) Kwa nini wazee hupitia maswali yaliyotayarishwa pamoja na wale waliojiweka wakfu karibuni? (b) Ni hatua gani ya maana ipaswayo kuchukuliwa upesi baada ya wakfu wa mtu, na kwa kusudi gani?
17 Kama vile Musa alivyowaeleza Waisraeli masharti ya kuingia katika uhusiano wa agano pamoja na Yehova, wazee katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova husaidia wale ambao wamejiweka wakfu karibuni wachunguze kile hasa kinachohusika. Wao hutumia maswali yaliyotayarishwa ili kuhakikisha kwamba kila mmoja aelewa mafundisho ya msingi ya Biblia na kufahamu kile kinachohusika katika kuwa Shahidi wa Yehova. Halafu, sherehe ya kuonyesha wakfu huo hadharani yafaa sana. Kwa asili, mmoja aliyejiweka wakfu karibuni ana hamu ya kujulisha wengine kwamba ameingia katika uhusiano huo wenye pendeleo na Yehova. (Linganisha Yeremia 9:24.) Hilo lafanywa ifaavyo kwa kubatizwa kwa maji kwa ufananisho wa wakfu. Kuzamishwa majini kisha kuinuliwa kwafananisha kwamba anakufa kwa habari ya mwendo wake wa maisha wa zamani wa kujipendeza na anainuliwa kwenye njia mpya ya maisha, ya kufanya mapenzi ya Mungu. Hiyo si sakramenti, wala si desturi kama ile sherehe ya misogi ya Dini ya Shinto ambayo katika hiyo mtu adhaniwa kuwa amesafishwa kwa maji.a Badala ya hivyo, ubatizo ni tangazo la hadharani la wakfu ambao umewekwa tayari katika sala.
18. Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba wakfu wetu hautakuwa bure?
18 Pindi hiyo yenye uzito ni ono lisilosahaulika, likimkumbusha mtumishi huyu mpya wa Mungu juu ya uhusiano wenye kudumu alio nao sasa na Yehova. Tofauti na ule wakfu wa yule rubani wa kamikaze kwa nchi yake na kwa maliki wake, wakfu huo kwa Yehova hautakuwa wa bure, kwani yeye ni Mungu mweza yote wa milele atimizaye yote yale akusudiayo kufanya. Yeye, na yeye peke yake, anastahili ujitoaji wetu wa nafsi yote.—Isaya 55:9-11.
19. Ni nini litakalozungumzwa katika makala ifuatayo?
19 Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika katika wakfu. Kwa kielelezo, wakfu huathirije maisha yetu ya kila siku? Hilo litazungumziwa katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kurasa 194-195.
Je, Wakumbuka?
◻ Kwa nini wakfu kama vile uonwavyo ulimwenguni umeishia katika kuvunjika moyo?
◻ Ni nini kilichowasukuma Waisraeli wajiweke wakfu kwa Yehova?
◻ Ni nini kitusukumacho tujiweke wakfu kwa Yehova leo?
◻ Sisi twajiwekaje wakfu kwa Mungu?
◻ Ni nini umaana wa ubatizo wa maji?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Israeli katika Sinai lajiweka wakfu kwa Yehova