Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 3/15 kur. 4-7
  • Sala Zilizo Ndani ya Biblia Zastahili Kuchunguzwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala Zilizo Ndani ya Biblia Zastahili Kuchunguzwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Angalia Teso la Mjakazi Wako’
  • ‘Mimi Ni Mtoto Mdogo Tu’
  • “Wote Wawe na Umoja”
  • “Maombi Yenu na Yajulishwe Mungu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Boresha Sala Zako Kupitia Funzo la Biblia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Sala Zako Zinafunua Nini Kukuhusu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 3/15 kur. 4-7

Sala Zilizo Ndani ya Biblia Zastahili Kuchunguzwa

MWANAMKE fulani mwenye mahangaiko, mfalme fulani, na Mwana wa Mungu mwenyewe walitoa sala tutakazochunguza. Kila sala ilitokezwa na hali tofauti-tofauti. Hata hivyo, hali kama hizo zingeweza kutuathiri leo. Twaweza kujifunza nini kutokana na vielelezo hivi?

‘Angalia Teso la Mjakazi Wako’

Je, wewe unang’ang’ana na tatizo lisilokoma? Au je, umelemewa na hangaiko? Basi una hali inayofanana na ile ya Hana kabla hajamzaa mtoto wake wa kwanza, Samweli. Yeye hakuwa na mwana naye alikuwa akidhihakiwa na mwanamke mwingine. Kwa kweli, hali ya Hana ilimhuzunisha na kumhangaisha hivi kwamba hangeweza kula. (1 Samweli 1:2-8, 15, 16) Yeye alimsihi Yehova na akatoa dua ifuatayo:

“Ee BWANA wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa BWANA huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe.”—1 Samweli 1:11.

Angalia kwamba Hana hakusema kwa ujumla. Alisali kwa Yehova akiwa na ombi hususa (mtoto wa kiume) naye akaambatanisha hili na azimio hususa atakalofanya (kumtoa amtumikie Mungu). Jambo hili latufunza nini?

Unapokuwa katika shida, sema sala yako kihususa. Hata ikiwa tatizo lako ni nini—iwe ni hali ya nyumbani mwako, upweke, au afya iliyodhoofika—sali kwa Yehova kuhusu hilo. Mfafanulie shida yako ilivyo hasa na jinsi unavyohisi. “Kila jioni mimi humkabidhi Yehova mahangaiko yangu yote,” akasema mjane aitwaye Louise. “Nyakati nyingine yanakuwa mengi sana, lakini nayataja waziwazi kila mojapo.”

Kusema na Yehova kwa mitajo iliyo hususa huleta manufaa. Kufanya hivyo hutusaidia kufafanua tatizo letu, ambalo laweza kuonekana dogo. Kusema sala hususa hutupunguzia mahangaiko. Hata kabla sala yake kujibiwa, Hana alihisi uhakikisho, “wala uso wake haukukunjamana tena.” (1 Samweli 1:18) Zaidi ya hayo, kusema kwa usahihi hutufanya tuwe macho kutambua jibu la sala yetu. “Kadiri nisemavyo sala zangu kwa usahihi,” akasema Bernhard, Mkristo katika Ujerumani, “ndivyo majibu yalivyo wazi zaidi.”

‘Mimi Ni Mtoto Mdogo Tu’

Hata hivyo, huenda mtu akahisi hangaiko la aina nyingine ikiwa anapokea mgawo fulani ambao yeye ahisi haustahili. Je, nyakati nyingine unahisi kushindwa na daraka ulilopewa na Yehova? Au je, watu fulani hukuona ukiwa hufai katika mgawo wako? Sulemani mchanga alikuwa katika hali hiyo alipotiwa mafuta awe mfalme wa Israeli. Wanaume fulani mashuhuri walipendelea kwamba mtu mwingine awe kwenye kiti cha ufalme. (1 Wafalme 1:5-7, 41-46; 2:13-22) Mapema katika utawala wake, Sulemani alitoa ombi katika sala:

“Ee BWANA, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako . . . nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. . . . Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya.”—1 Wafalme 3:7-9.

Sulemani katika sala yake alikazia uhusiano wake na Yehova, juu ya pendeleo alilokuwa amepewa, na juu ya uwezo wa kutimiza mgawo huo. Katika njia hiyohiyo, tunapopewa daraka tunalohisi kwamba linapita uwezo wetu, twapaswa kumsihi Mungu atuandae kufanya kazi hiyo. Fikiria maono yafuatayo:

“Ninapoulizwa kushughulikia daraka kubwa zaidi katika ofisi ya tawi ya Watch Tower Society,” aeleza Eugene, “nilihisi kutoliweza hata kidogo. Kulikuwa na wengine waliokuwa na sifa zaidi za kustahili na waliokuwa na uzoefu mwingi zaidi. Siku mbili zilizofuata nililala kwa muda mfupi sana, nikitumia wakati mwingi zaidi katika sala, jambo lililonipa nguvu na uhakika uliohitajika.”

Roy aliombwa kutoa hotuba ya mazishi baada ya kifo cha ghafula na chenye msiba cha rafiki mchanga aliyejulikana sana. Kwa hakika mamia wangehudhuria. Roy alifanya nini? “Nilisali sana mara nyingi ili nipate nguvu na uwezo wa kupata maneno yafaayo kueleza mawazo yenye kujenga na kutoa faraja.”

Kadiri Muumba ‘ahimizapo mambo’ na kadiri tengenezo lake liongezekapo, tokeo la kawaida ni kwamba wengi wa watumishi wake wanakabidhiwa daraka. (Isaya 60:22) Ikiwa unaombwa kuwa na ushirika fulani ulioongezeka, uwe na uhakika kwamba Yehova aweza kukuongezea ujuzi, mazoezi, au uwezo wowote unaokosekana. Mfikie Mungu katika njia ileile Sulemani aliyofanya, naye atakuandaa utimize mgawo huo.

“Wote Wawe na Umoja”

Hali ya tatu itokeayo leo ni ile ya kutakiwa kuwakilisha kikundi katika sala. Tunapoombwa kutoa sala kwa niaba ya wengine, twapaswa kusali juu ya nini? Fikiria ile sala ya Yesu iliyorekodiwa katika Yohana sura 17. Yeye alitoa sala hii wafuasi wake wakiwapo wakati wa jioni yake ya mwisho akiwa mwanadamu. Ni sihi za aina gani alizoelekeza kwa Baba yake wa kimbingu?

Yesu alikazia miradi ya wote na tumaini lililoshirikiwa na wale waliokuwapo. Yeye alitaja kutukuzwa kwa jina la Yehova Mungu na kujulishwa kwa Ufalme. Yesu alikazia thamani ya uhusiano wa binafsi pamoja na Baba na Mwana, wenye msingi wa ujuzi wa Maandiko. Yeye alizungumza juu ya kujitenga na ulimwengu, jambo ambalo lingewatayarisha wafuasi wake kwa upinzani. Kristo pia alimwomba Baba yake kuwalinda wanafunzi hao na kuwaunganisha katika ibada ya kweli.

Ndiyo, Yesu alikazia umoja. (Yohana 17:20, 21) Mapema jioni hiyo, wanafunzi walikuwa wamejihusisha na mabishano yasiyo ya ukomavu. (Luka 22:24-27) Hata hivyo, katika sala, Kristo alitafuta si kulaumu bali kuunganisha. Katika njia hiyo hiyo, sala za familia na za kutaniko zapaswa kuendeleza upendo na kutafuta kushinda mabishano kati ya mmoja na mwenzake. Wale wanaowakilishwa wapaswa kuvutwa pamoja katika umoja.—Zaburi 133:1-3.

Umoja huu unaonyeshwa wakati wale wanaosikiliza wasemapo, “Amina,” au “Na iwe hivyo,” katika kumalizia. Ili jambo hili liwezekane, lazima waelewe na kukubaliana na kila lililosemwa. Hivyo, haingefaa, kutaja katika sala jambo lisilojulikana na watu fulani waliopo. Kwa kielelezo, mzee anayewakilisha kutaniko katika sala huenda akaomba baraka ya Yehova juu ya ndugu au dada fulani aliye mgonjwa sana. Lakini ingelikuwa bora zaidi ikiwa angelifanya hivyo ikiwa tu walio wengi wa wale anaowakilisha wanamjua mtu huyo nao wamesikia juu ya ugonjwa huo.

Angalia, pia, kwamba Yesu hakusema juu ya mahitaji ya binafsi ya kila mshiriki wa kikundi hicho. Kufanya hivyo kungelihusisha kutaja mambo ya binafsi yajulikanayo tu na watu fulani. Mahangaiko ya binafsi ni habari ifaayo kwa sala za binafsi, zinazoweza kusemwa kirefu na kwa undani zaidi kama mtu atakavyo.

Mtu apaswa kujitayarishaje ili kuwakilisha kusanyiko kubwa la waabudu katika sala? Mkristo mmoja mwenye ujuzi aeleza hivi: “Mimi hufikiria kimbele jambo la kutolea shukrani, maombi ambayo ndugu huenda wakawa nayo, na sihi ambazo ningeliweza kutaja kwa niaba yao. Nayapanga maoni yangu, kutia ndani semi za kusifu, katika mpangilio ufaao katika akili yangu. Kabla ya kusema sala ya watu wote, mimi husema sala ya moyoni, nikiomba msaada ili niwakilishe ndugu kwa njia ya heshima.”

Hata hali zako ziweje, yaelekea utapata sala fulani katika Biblia iliyosemwa na mtu fulani katika hali kama yako. Sala zilizo nyingi katika Maandiko ni uthibitisho wa fadhili zenye upendo za Mungu. Kuzisoma sala hizi na kuzitafakari kutakusaidia utajirishe sala zako.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

SALA ZIJULIKANAZO KATIKA BIBLIA

Watumishi wa Yehova walitoa sala chini ya hali mbalimbali. Je, unaweza kujipatanisha na hali moja au zaidi zifuatazo?

Je, unahitaji uongozi kutoka kwa Mungu, kama Eliezeri alivyohitaji?—Mwanzo 24:12-14.

Je, unaelekeana na hatari, kama Yakobo alivyokuwa?—Mwanzo 32:9-12.

Je, unataka kumjua Mungu vizuri zaidi, kama Musa alivyotaka?—Kutoka 33:12-17.

Je, unakabiliwa na wapinzani, kama Eliya alivyokuwa?—1 Wafalme 18:36, 37.

Je, kuhubiri ni kugumu kwako, kama ilivyokuwa kwa Yeremia?—Yeremia 20:7-12.

Je, unahitaji kutubu dhambi na kutafuta msamaha, kama Danieli alivyofanya?—Danieli 9:3-19.

Je, unakabili mnyanyaso, kama wanafunzi wa Yesu walivyokabili?—Matendo 4:24-31.

Ona pia Mathayo 6:9-13; Yohana 17:1-26; Wafilipi 4:6, 7; Yakobo 5:16.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

JAMBO LA KUSALI UNAPOPIGANA NA ZOEA LILILOKUSHIKA SANA

Je, unang’ang’ana dhidi ya udhaifu unaorudirudi? Sala zilizorekodiwa katika Biblia zawezaje kuwa zenye manufaa? Jifunze kutoka kwa Daudi, aliyesali nyakati mbalimbali kuhusu udhaifu wake mwenyewe.

Daudi aliimba hivi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu.” (Zaburi 139:23) Ilikuwa tamaa ya Daudi kwamba Yehova Mungu atafutetafute tamaa, hisiamoyo, au mwelekeo usiofaa. Kwa maneno mengine, Daudi alitegemea msaada wa Yehova katika kuepuka dhambi.

Lakini udhaifu mbalimbali wa Daudi ulimshinda, naye alifanya dhambi sana. Hapa tena, sala ilimsaidia—pindi hii kurudisha uhusiano wake pamoja na Mungu. Kulingana na Zaburi 51:2, Daudi alisihi hivi: “Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu.”

Sisi pia twaweza kusali kwa unyenyekevu juu ya msaada wa Yehova ili tuache mielekeo isiyofaa. Hili litatuimarisha kushinda udhaifu uliotushika kabisa nalo laweza kutusaidia kuepuka dhambi. Tukirudia dhambi, twapaswa tumwendee Yehova tena tukimsihi kwamba atusaidie tuendelee na vita hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Sala zisemwazo kwa niaba ya kikundi fulani zapaswa kukazia matumaini ya Kimaandiko na miradi ya kiroho ishirikiwayo na wote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki