Maisha Mapya kwa Wazazi Wetu wa Kale Waliokufa
JE, Neno la Mungu, Biblia, hufundisha kwamba kila mtu hupita tu na kuendelea na maisha katika makao ya roho wakati wa kifo? La, haifundishi hivyo. Biblia inatoa tumaini ajabu la maisha baada ya kifo, lakini si kwa njia ambayo wengi hufikiri inafanya.
Fikiria yale Biblia isemayo juu ya babu yetu wa kwanza, Adamu. Yehova alimfanyiza “kwa mavumbi ya ardhi.” (Mwanzo 2:7) Adamu alikuwa na fursa ya kuishi milele kwa furaha duniani. (Mwanzo 2:16, 17) Hata hivyo, aliasi dhidi ya Muumba wake mwenye upendo, na tokeo likawa kifo.
Adamu alienda wapi baada ya kufa? Mungu alimwambia: ‘Utairudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’—Mwanzo 3:19.
Adamu alikuwa wapi kabla Yehova amwumbe kutoka kwa mavumbi? Hakuwa popote. Hakuishi. Kwa hiyo Yehova aliposema kwamba Adamu ‘angeirudia ardhi,’ ni lazima awe alimaanisha tu kwamba Adamu angekosa uhai tena, kama tu mavumbi. Adamu ‘hakuvuka’ kuwa baba mwanzilishi wa ulimwengu wa roho za wazazi wa kale waliokufa. Wala hakuvuka kwenda kupata uhai wa raha mustarehe mbinguni wala kupata mateseko ya milele katika mahali pa mateso. Mpito wa pekee aliofanya ulikuwa ni kutoka uhai hadi kukosa uhai, kutoka hali ya kuwapo hadi ile ya kutokuwapo.
Vipi juu ya wanadamu wengine wote? Je, wazao wa Adamu pia hukoma kuwa hai wakati wa kifo? Biblia yajibu: “Wote [wanadamu na wanyama pia] huendea mahali pamoja; wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhubiri 3:19, 20.
Hali ya Wafu
Ndiyo, wafu hawana uhai, hawawezi kusikia, kuona, kusema, wala kufikiri. Kwa kielelezo, Biblia yasema: “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote . . . Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja.” Biblia yasema pia hivi: “Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi] uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 6, 10.
Basi, kulingana na Neno la Mungu, watu wanapokuwa hai, wanajua juu ya kifo. Hata hivyo, kifo kitokeapo hawajui lolote. Wao hawasimami kando ya maiti yao, wakiona mambo yanayofanywa kwayo. Katika hali ya kutokuwapo hakuna raha wala uchungu, wala shangwe wala huzuni. Wafu hawajui juu ya wakati unaopita. Wamo katika hali ya kutofahamu lolote ambayo ni nzito kuliko usingizi wowote.
Ayubu, mtumishi wa Mungu katika nyakati za kale, alijua kwamba watu hawakuendelea kuishi baada ya kifo. Pia alielewa kwamba bila Mungu kuingilia mambo, hakungekuwa na tumaini la kupata uhai tena. Ayubu alisema: “Mtu mwenye uwezo hufa na kulala kabisa; na mwanadamu wa dunia huisha, naye yuko wapi? Ni lazima [a]lale na asiamke.” (Ayubu 14:10, 12, New World Translation) Hakika Ayubu hakutarajia kwamba afapo angejiunga na wazazi wake wa kale waliokufa katika ulimwengu wa roho.
Tumaini la Ufufuo
Kwa kuwa waishio hukoma kuishi wafapo, swali muhimu ni lile lililoulizwa na Ayubu alipouliza hivi: “Mtu mwenye uwezo akifa, je, aweza kuishi tena?” Ayubu mwenyewe alijibu hivi: “Siku zote za utumishi wangu wa lazima [wakati uliotumiwa kaburini] nitangoja, mpaka kitulizo changu kije. Wewe [Yehova] utaita, nami nitakujibu. Kwa maana kazi za mkono wako utatamani.”—Ayubu 14:14, 15, NW.
Kwa maneno mengine, ingawa Ayubu angepita na kuingia katika hali ya kutokuwapo, Mungu hangemsahau. Ayubu alikuwa na imani kwamba wakati ungekuja ambapo Yehova Mungu ‘angemwita’ arudi katika uhai kupitia ufufuo.
Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alionyesha kwamba tumaini la Ayubu katika ufufuo lilikuwa halisi. Yesu alithibitisha kwamba wafu waweza kuinuliwa. Kwa njia gani? Kwa kufanya hivyo yeye mwenyewe! Yeye hakuwapo amfufue Ayubu, lakini Yesu alipokuwa duniani alimfufua mwana wa mjane mmoja kutoka jiji la Naini. Yesu pia alimwinua kumrudisha katika uhai binti mwenye umri wa miaka 12 wa mtu mmoja aliyeitwa Yairo. Naye alimfufua rafiki yake Lazaro, aliyekuwa amekufa kwa siku nne.—Luka 7:11-15; 8:41, 42, 49-56; Yohana 11:38-44.
Kuongezea kufanya miujiza hiyo, Yesu alisema juu ya ufufuo mkubwa wa wakati ujao. Yeye alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Baadaye, mtume Paulo, ambaye Yehova alimtumia kufufua kijana mmoja mwanamume, pia alieleza itikadi yake katika ufufuo wa wakati ujao. Yeye alisema: “Nina tumaini kwa Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”—Matendo 20:7-12; 24:15.
Marejezo haya ya Kimaandiko ya ufufuo wa wakati ujao hayahusu kuendelea kuishi katika makao ya roho. Hayo yaelekezea wakati ambapo mamilioni ya wafu watarudia uhai wakiwa na miili halisi hapahapa duniani. Wafufuliwa hao hawatakuwa watu wasio na kumbukumbu la maisha yao ya awali duniani. Hawatakuwa wamezaliwa tena wakiwa vitoto vichanga. Badala ya hivyo, watakuwa watu walewale kabla ya kufa, wakiwa na kumbukumbu zilezile na utu uleule. Watajitambua wenyewe na kutambulika kwa wengine. Itakuwa shangwe kama nini watu hao wajiungapo na marafiki na familia zao! Na itasisimua kama nini kukutana na wazazi wetu wa kale waliokufa!
Ufufuo wa Kupata Uhai Mbinguni
Je, Yesu hakusema kwamba baadhi ya watu wangeenda mbinguni? Ndiyo, alisema. Ile jioni kabla auawe, yeye alisema: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi . . . maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.” (Yohana 14:2, 3) Yesu alikuwa akizungumza na mitume wake waaminifu, lakini maneno yake hayamaanishi kwamba watu wote wazuri wanaenda mbinguni.
Yesu alionyesha kwamba wale wafufuliwao kwenda mbinguni ni lazima watimize matakwa mengine zaidi ya kuishi tu maisha ya uadilifu. Takwa moja ni kuwa na ujuzi sahihi wa Yehova na makusudi yake. (Yohana 17:3) Matakwa mengine ni kudhihirisha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo na kumtii Mungu. (Yohana 3:16; 1 Yohana 5:3) Na bado takwa jingine ni ‘kuzaliwa mara ya pili’ ukiwa Mkristo aliyebatizwa na kuzaliwa kwa roho takatifu ya Mungu. (Yohana 1:12, 13; 3:3-6) Takwa jingine zaidi la uhai wa kimbingu ni kuvumilia kama Yesu alivyovumilia, ukithibitika kuwa mwaminifu kwa Mungu hadi kifo.—Luka 22:29; Ufunuo 2:10.
Kuna sababu nzuri ya kutaka matakwa hayo ya hali ya juu. Wale wafufuliwao kwenda mbinguni wana kazi muhimu ya kufanya. Yehova alijua kwamba serikali za kibinadamu hazingeweza kusimamia mambo ya dunia kwa mafanikio. Kwa hiyo alipanga kuwe na serikali ya kimbingu, au Ufalme, ambayo ingetawala wanadamu. (Mathayo 6:9, 10) Yesu angekuwa Mfalme wa Ufalme huo. (Danieli 7:13, 14) Wengine waliochaguliwa kutoka duniani na kufufuliwa kwenda mbinguni wangetawala naye. Biblia ilitabiri kwamba wafufuliwa hao wangekuwa “ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wa[nge]miliki juu ya nchi.”—Ufunuo 5:10.
Je, idadi kubwa ya watu ingetimiza matakwa ya ufufuo wa kimbingu? La. Kwa sababu zisizo kosa lao, wengi wa wale wanaolala katika kifo hawastahili. Wengi hawakuwa na fursa ya kutosha kujifunza kuhusu kweli juu ya Yehova na makusudi yake. Wao waliishi na kufa bila ujuzi wowote wa Yesu Kristo au wa Ufalme wa Mungu.
Yesu aliwaita wale ambao wangeenda mbinguni “kundi dogo.” (Luka 12:32) Baadaye ilifunuliwa kwamba idadi ya wale “walionunuliwa kutoka katika dunia” ili kutawala pamoja na Kristo mbinguni ingekuwa 144,000. (Ufunuo 14:1-3, NW; 20:6) Ingawa 144,000 ni idadi kubwa iwezayo kutoshea yale “makao mengi” aliyoyarejezea Yesu, ni ndogo inapolinganishwa na mabilioni ya watu ambao wametoka kwa Adamu.—Yohana 14:2.
Matukio Yanayotangulia Ufufuo wa Kidunia
Ebu tupitie yale ambayo tayari tumezungumzia. Kulingana na Biblia, wale wanaokufa hawana uhai katika kifo mpaka wafufuliwe na Yehova Mungu. Wengine hufufuliwa kupata uhai mbinguni, ambako watatawala pamoja na Yesu Kristo katika serikali ya Ufalme. Watu wengi zaidi watafufuliwa duniani, wawe raia wa Ufalme huo.
Kwa sehemu, kupitia ufufuo wa kidunia, Yehova atatimiza kusudi lake kuhusu dunia. Yehova aliiumba ili “ikaliwe.” (Isaya 45:18) Ilikuwa iwe makao ya kudumu ya wanadamu. Kwa hiyo, mtunga-zaburi aliimba: “Mbingu ni mbingu za BWANA, bali nchi amewapa wanadamu.”—Zaburi 115:16.
Kabla ya ufufuo wa kuishi duniani kuanza, mabadiliko makubwa lazima yatokee. Labda utakubali kwamba halikuwa kusudi la Mungu dunia ijae vita, uchafuzi, uhalifu, na jeuri. Matatizo haya husababishwa na watu ambao hawana staha kwa Mungu na sheria zake zenye uadilifu. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ‘utawaharibu wale waiharibuo dunia’—hiyo ikiwa hatua kubwa ya kutekeleza mapenzi yake duniani. (Ufunuo 11:18) Ufalme utaharibu watu wote waovu, ukiacha waadilifu waishi duniani milele.—Zaburi 37:9, 29.
Paradiso Duniani
Wale wafufuliwao katika dunia iliyosafishwa watakuwa wapole, watu wenye kujali, wafanyao yaliyo sawa. (Linganisha Mathayo 5:5.) Chini ya usimamizi wenye upendo wa Ufalme wa Mungu, wao wataishi maisha yenye furaha katika usalama. Biblia yatoa mwono huu wa kimbele ulio mzuri ajabu wa hali ambazo zitaenea wakati huo: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
Ndiyo, dunia itageuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:43, NW) Ebu wazia hilo litamaanisha nini! Hospitali na makao ya kutunzia wagonjwa hayatatumika tena. Katika Paradiso, wale ambao sasa wanapatwa na madhara ya uzee watakuwa na nguvu na afya nzuri tena. (Ayubu 33:25; Isaya 35:5, 6) Makao ya maziko, makaburi, na mawe ya makaburi hayatakuwapo tena. Kupitia Ufalme wake, Yehova ‘atameza mauti hata milele.’ (Isaya 25:8) Baraka hizo hakika zaweza kumaanisha maisha mapya kwetu na kwa wazazi wetu wa kale waliokufa.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Wale wafufuliwao duniani watakuwa raia wa Ufalme