Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 6/1 kur. 11-16
  • Liwazo Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Liwazo Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Yehova—Mungu wa Faraja
  • Yesu na Paulo —Wafariji Wenye Huruma Nyororo
  • Jinsi ya Kuwafariji Wale Wanaohuzunika
  • Mambo ya Kuepuka
  • Maandiko Yafarijiyo
  • “Lieni Pamoja na Watu Wanaolia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Wafariji Wale Wanaohuzunika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • ‘Wafariji Wote Wanaoomboleza’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Jinsi Mungu Anavyotufariji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 6/1 kur. 11-16

Liwazo Kutoka kwa “Mungu wa Faraja Yote”

“Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote.”—2 WAKORINTHO 1:3, 4.

1, 2. Watu wanaohuzunika wanahitaji faraja ya aina gani?

WATU wanaohuzunika wanahitaji faraja ya kweli—si maneno ya kurudiwa-rudiwa tu. Sote tumesikia kwamba ‘utahisi vizuri wakati upitapo,’ lakini katika pindi za mapema za kufiwa, ni mtu gani mwenye huzuni atafarijiwa na wazo hilo? Wakristo wajua kwamba Mungu ameahidi ufufuo, lakini hilo halizuii uchungu wa ndani na mtamauko wa upotezo wa ghafula. Na kwa hakika ikiwa umepoteza mtoto, watoto wengine ambao wangali hai hawawezi kuchukua mahali pa yule mtoto mwenye thamani sana.

2 Katika nyakati za potezo, sisi husaidiwa zaidi na faraja ya kweli, faraja ambayo ina msingi thabiti katika ahadi za Mungu. Twahitaji pia hisia-mwenzi. Kwa kweli hivyo ndivyo imekuwa kwa watu wa Rwanda, na hasa kwa mamia ya familia za Mashahidi wa Yehova huko waliopoteza wapendwa wao katika machinjo hayo makubwa ya kikabila ya kishetani. Je, wote wanaohuzunika waweza kupata faraja kwa nani?

Yehova—Mungu wa Faraja

3. Yehova amewekaje kielelezo cha kutoa faraja?

3 Yehova ameweka kielelezo kwa kutupa sisi sote faraja. Yeye alituma Mwana wake mzaliwa-pekee, Kristo Yesu, duniani ili kutupa sisi faraja na tumaini la milele. Yesu alifundisha hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Pia aliwaeleza wafuasi wake hivi: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Katika pindi nyingine yeye alisema: ‘Mwana wa Adamu hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Na Paulo alisema: “Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi.” (Warumi 5:8) Kupitia maandiko hayo na mengine, twaona upendo wa Mungu na wa Kristo Yesu.

4. Kwa nini mtume Paulo hasa alikuwa na deni kwa Yehova?

4 Mtume Paulo hasa alijua fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Alikuwa amenyakuliwa kutoka hali ya kifo cha kiroho, kutoka kuwa mnyanyasi mkali sana wa wafuasi wa Kristo hadi kuwa Mkristo aliyenyanyaswa mwenyewe. (Waefeso 2:1-5) Yeye aelezea ono lake: “Maana mimi ni mdogo katika mitume, nisiyestahili kuitwa mtume, kwa sababu naliliudhi [“nilinyanyasa,” NW] kanisa la Mungu. Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.”—1 Wakorintho 15:9, 10.

5. Paulo aliandika nini kuhusu faraja itokayo kwa Mungu?

5 Basi, kwa kufaa, Paulo aliandika: “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote; atufarijiye katika dhiki zetu zote ili nasi tupate kuwafariji wale walio katika dhiki za namna zote, kwa faraja hizo, tunazofarijiwa na Mungu. Kwa kuwa kama vile mateso ya Kristo yanavyozidi kwetu, vivyo hivyo faraja yetu inazidi kwa njia ya Kristo. Lakini ikiwa sisi tu katika dhiki, ni kwa ajili ya faraja yenu na wokovu wenu; au ikiwa twafarijiwa, ni kwa ajili ya faraja yenu; ambayo hutenda kazi yake kwa kustahimili mateso yale yale tuteswayo na sisi. Na tumaini letu kwa ajili yenu ni imara, tukijua ya kuwa kama vile mlivyo washiriki wa yale mateso, vivyo hivyo mmekuwa washiriki wa zile faraja.”—2 Wakorintho 1:3-7.

6. Ni nini linalodokezwa na neno la Kigiriki lililotafsiriwa “faraja”?

6 Hayo ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Neno la Kigiriki lililotafsiriwa hapa “faraja” lahusu “kumwita mtu kujiunga nawe.” Kwa hiyo, “ni kusimama kando ya mtu kumtia moyo anapopata majaribu makali sana.” (A Linguistic Key to the Greek New Testament) Msomi mmoja wa Kibiblia aliandika hivi: “Neno hilo . . . sikuzote humaanisha mengi zaidi ya huruma yenye kutuliza. . . . Faraja ya Kikristo ni faraja inayotokeza moyo mkuu, ile faraja imfanyayo mtu aweze kukabili kwa mafanikio mambo yote ambayo maisha yaweza kumletea.” Latia ndani pia maneno yenye kufariji yategemeayo ahadi na tumaini thabiti—ule ufufuo wa wafu.

Yesu na Paulo —Wafariji Wenye Huruma Nyororo

7. Paulo alikuwaje mwenye faraja kwa ndugu zake Wakristo?

7 Paulo alikuwa kielelezo kizuri ajabu kama nini katika kutoa faraja! Aliwaandikia ndugu katika Thesalonike hivi: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na roho zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu. Vile vile, kama mjuavyo, jinsi tulivyomwonya kila mmoja wenu kama baba awaonyavyo watoto wake mwenyewe, tukiwatia moyo na kushuhudia.” Kama ilivyo tu na wazazi wenye upendo wanaojali, sisi sote twaweza kuwaonyesha wengine uchangamfu na uelewevu katika wakati wao wa uhitaji.—1 Wathesalonike 2:7, 8, 11.

8. Kwa nini fundisho la Yesu ni faraja kwa wale wanaohuzunika?

8 Katika kuonyesha hali hiyo ya kujali na fadhili, Paulo alikuwa akiiga tu Kielelezo chake kikubwa, Yesu. Kumbuka ule mwaliko wenye huruma nyororo anaotoa Yesu kwa wote kwenye Mathayo 11:28-30: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” Ndiyo, fundisho la Yesu laburudisha kwa sababu latoa tumaini na ahadi—ahadi ya ufufuo. Hili ndilo tumaini na ahadi ambayo tunawatolea watu, kwa mfano, tunapowaachia broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa. Tumaini hili laweza kutusaidia sote, hata kama tumekuwa tukihuzunika kwa muda mrefu.

Jinsi ya Kuwafariji Wale Wanaohuzunika

9. Kwa nini tusiwe wenye kukosa saburi kwa watu wanaohuzunika?

9 Huzuni haichukui muda fulani tu mara baada ya kifo cha mpendwa. Watu fulani hubeba mzigo wa huzuni yao maishani mwao mwote, hasa wale ambao wamepoteza watoto. Mume na mke walio Wakristo waaminifu katika Hispania walipoteza mwana wao mwenye umri wa miaka 11 katika 1963 kwa ugonjwa wa utando-ubongo. Mpaka leo hii, wao hudondoka machozi wanapozungumza juu ya Paquito. Sherehe za kila mwaka, picha, vikumbusho, vyaweza kuleta kumbukumbu zenye huzuni. Kwa hiyo, hatupaswi kuwa wenye kukosa saburi na kufikiri kwamba wengine wapaswa kuacha kuhuzunikia potezo lao kufikia sasa. Nukuu fulani la kitiba lasema hivi: “Kushuka moyo na kubadilika-badilika kwa tabia kwaweza kudumu hata kwa miaka kadhaa.” Basi, kumbuka kwamba kama vile makovu halisi mwilini huweza kubaki maishani mwote, ndivyo ilivyo na makovu ya kihisia moyo.

10. Ni lazima tufanye nini ili kusaidia wenye kuhuzunika?

10 Ni yapi baadhi ya mambo mengine yenye kutumika tuwezayo kufanya ili kuwafariji wanaohuzunika katika kutaniko la Kikristo? Kwa moyo mweupe kabisa huenda tukamwambia ndugu au dada ahitajiye faraja hivi, “Ikiwa kuna lolote niwezalo kusaidia, nijulishe tu.” Lakini ni mara ngapi mtu aliyefiwa hutupigia simu hasa na kusema, “Nimefikiria jambo ambalo unaweza kunisaidia”? Ni wazi kwamba twahitaji kuchukua hatua ya kwanza inayofaa ikiwa tutawafariji wale waliofiwa. Kwa hiyo, twaweza kufanya nini kwa njia yenye mafaa? Hapa pana madokezo machache yenye kutumika.

11. Usikivu wetu waweza kuwaje faraja kwa wengine?

11 Sikiliza: Mojapo mambo yenye kusaidia zaidi uwezayo kufanya ni kushiriki umizo la yule aliyefiwa kwa kusikiliza. Waweza kuuliza hivi, “Je, ungependa kuongea juu yalo?” Mwache aamue. Mkristo mmoja akumbuka hivi baba yake alipokufa: “Ilinisaidia sana wakati wengine walipouliza lile lililotukia kisha wakasikiliza kwelikweli.” Kama vile Yakobo alivyoshauri, uwe mwepesi kusikiliza. (Yakobo 1:19) Sikiliza kwa saburi na kwa kusikitikia. “Lieni pamoja nao waliao,” yapendekeza Biblia kwenye Warumi 12:15. Kumbuka kwamba Yesu alilia machozi pamoja na Martha na Mariamu.—Yohana 11:35.

12. Twaweza kuwatolea wenye kuomboleza kitia-moyo cha aina gani?

12 Andaa Kitia-Moyo: Kumbuka kwamba mtu aliyefiwa huenda kwanza akahisi kuwa mwenye hatia, akifikiri kwamba labda kulikuwa na mambo zaidi ambayo angefanya. Mhakikishie mtu huyo kwamba yaelekea yote yaliyowezekana yalifanywa (au lolote jingine ujualo kuwa kweli na hakika). Mtie moyo kwamba lile analohisi ni jambo la kawaida tu. Mwambie juu ya wengine unaowajua waliopata nafuu kwa mafanikio kutokana na hasara kama hiyo. Yaani, uwe mwepesi kuguswa moyo na kuwa mwenye kusikitikia. Msaada wetu wenye fadhili waweza kusaidia sana! Sulemani aliandika: “Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa katika vyano vya fedha.”—Mithali 16:24; 25:11; 1 Wathesalonike 5:11, 14.

13. Kuwa kwetu wenye kupatikana kwaweza kusaidiaje?

13 Uwe mwenye kupatikana: Uwe mwenye kupatikana, si kwa zile siku chache za kwanza tu wakati marafiki na watu wa ukoo wengi wapo, bali kwa miezi kadhaa baadaye ikihitajika, wakati wengine wamerudia shughuli zao za kawaida. Kipindi cha huzuni hutofautiana sana, ikitegemea mtu huyo hususa. Upendezi wetu na hali yetu ya kusikitikia ya Kikristo yaweza kuwa yenye umaana sana katika wakati wowote wenye uhitaji. Biblia yasema kwamba “yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” Hivyo, ule msemo, “Rafiki ahitajikaye ni yule wa matendo,” ni ukweli ambao tunapaswa kufuata maishani mwetu.—Mithali 18:24; linganisha Matendo 28:15.

14. Twaweza kuzungumzia nini ili kufariji mfiwa?

14 Zungumzia sifa nzuri za mtu yule aliyekufa: Huu ni msaada mwingine mkubwa unaotolewa kwa wakati ufaao. Shiriki naye mambo chanya ya kuchekesha unayokumbuka juu ya mtu huyo. Usiogope kutumia jina la mtu huyo. Usitende kana kwamba mpendwa huyo aliyekufa hakupata kuishi kamwe au hakuwapo kabisa. Yafariji kujua yaliyosemwa na kichapo kimoja kutoka Shule ya Kitiba ya Harvard: “Aina fulani ya nafuu hupatikana wakati yule mfiwa awezapo hatimaye kufikiria yule aliyekufa bila huzuni nyingi mno . . . Kadiri uhalisi huo mpya unavyotambuliwa na kukubaliwa, ndivyo huzuni huishia kuwa kumbukumbu za kuthaminiwa.” “Kumbukumbu za kuthaminiwa”—inafariji kama nini kukumbuka pindi zile zenye thamani zilizotumiwa na mpendwa wako! Shahidi mmoja aliyepoteza baba yake miaka kadhaa iliyopita alisema hivi: “Kumbukumbu la kipekee kwangu ni kusoma Biblia pamoja na baba yangu muda mfupi baada ya yeye kuanza kujifunza kweli. Na kujilaza kwenye ukingo wa mto tukizungumzia baadhi ya matatizo yangu. Nilikuwa nikimwona baada ya miaka mitatu hadi minne tu, kwa hiyo pindi hizo zilikuwa zenye thamani.”

15. Mmoja aweza kuchukuaje hatua ya kwanza ya kusaidia?

15 Chukua hatua ya kwanza ifaapo: Watu wengine wanaohuzunika wanaweza kushughulikia hali vema kuliko wengine. Kwa hiyo, ikitegemea hali, chukua hatua zenye kutumika ili kusaidia. Mwanamke mmoja Mkristo alikumbuka hivi: “Wengi walisema, ‘Ikiwa kuna jambo niwezalo kufanya, nijulishe.’ Lakini dada mmoja Mkristo hakuuliza. Aliingia ndani ya chumba cha kulala, akatoa matandiko, na kufua matandiko machafu. Mwingine akachukua ndoo, maji, vitu vya kusafishia na kusugua zulia ambalo mume wangu alikuwa ametapikia. Hawa walikuwa marafiki wa kweli, sitawasahau kamwe.” Mahali ambapo kwa wazi panahitaji msaada, chukua hatua ya kwanza—labda kwa kutayarisha mlo, kusaidia kufanya usafi, au kutoa utumishi mbalimbali. Bila shaka, twapaswa kuwa waangalifu tusiwe wenye kuingilia-ingilia mambo wakati mtu aliyefiwa anataka faragha. Hivyo, twapaswa kuzingatia maneno ya Paulo: “Basi, kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema [“fadhili,” NW], unyenyekevu, upole, uvumilivu.” Fadhili, saburi, na upendo hazishindwi kamwe.—Wakolosai 3:12; 1 Wakorintho 13:4-8.

16. Kwa nini barua au kadi yaweza kuandaa faraja?

16 Andika barua au peleka kadi ya kufariji: Jambo linalopuuzwa mara nyingi ni thamani ya barua ya rambirambi au kadi nzuri ya kusikitikia. Faida yayo ni nini? Hiyo yaweza kusomwa tena na tena. Barua hiyo haihitaji kuwa ndefu, lakini yapaswa kuonyesha huruma yako. Yapasa pia kuonyesha hali ya kiroho lakini bila kuwa yenye mahubiri mno. Ujumbe sahili tu “Tuko ili tukutegemeze” waweza kumliwaza.

17. Sala inaweza kuletaje faraja?

17 Sali pamoja nao: Usipuuze umuhimu wa sala zako pamoja na, na kwa ajili ya, Wakristo wenzako waliofiwa. Biblia yasema hivi kwenye Yakobo 5:16, NW: “Dua ya mtu mwadilifu . . . ina kani nyingi.” Kwa kielelezo, wale wanaohuzunika wanapotusikia tukisali kwa ajili yao, hilo huwasaidia kuondoa hisia zisizofaa kama vile kuhisi hatia. Katika pindi ambazo tumekuwa dhaifu, au kuvunjika moyo, Shetani hujaribu kutudhoofisha kwa “hila” zake, au “matendo ya ujanja.” Hapa ndipo tunapohitaji faraja na utegemezo wa sala, kama vile Paulo alivyotaja: “Kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote.”—Waefeso 6:11, 18, Kingdom Interlinear; linganisha Yakobo 5:13-15.

Mambo ya Kuepuka

18, 19. Twaweza kuonyeshaje busara katika mazungumzo yetu?

18 Mtu anapohuzunika, pia kuna mambo yasiyopasa kufanywa au kusemwa. Mithali 12:18 yaonya: “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” Nyakati nyingine, bila kutambua, sisi hukosa kuonyesha busara. Kwa kielelezo, huenda tukasema, “Najua jinsi unavyohisi.” Lakini ndivyo ilivyo kweli? Je, umepatwa na upotezo uo huo? Pia, watu huitikia kwa njia tofauti-tofauti. Huenda ikawa itikio lako halikuwa sawa kabisa na lile la yule mtu anayehuzunika. Yaweza kuwa afadhali kusema hivi, “Kwa kweli nakusikitikia kwa sababu nilipatwa na upotezo kama huu wakati . . . wangu alipokufa muda fulani uliopita.”

19 Pia, lingekuwa jambo la hisia kuepuka kutoa maelezo kuhusu kama mtu huyo aliyefiwa atafufuliwa au la. Baadhi ya ndugu na dada wameumizwa sana na maneno ya kuhukumu yasemwayo juu ya mawezekano ya wakati ujao kwa mwenzi wa ndoa asiyeamini aliyekufa. Sisi si waamuzi wa wale watakaofufuliwa au hawatafufuliwa. Twaweza kufarijika kwamba Yehova, aonaye mioyo, atakuwa mwenye rehema zaidi kuliko jinsi wengi wetu watakavyopata kuwa.—Zaburi 86:15; Luka 6:35-37.

Maandiko Yafarijiyo

20, 21. Ni yapi baadhi ya maandiko yawezayo kutuliza mfiwa?

20 Mmojapo misaada mikubwa zaidi, unapotolewa wakati ufaao ni kufikiria pamoja ahadi za Yehova kwa wafu. Mawazo haya ya Kibiblia yatakuwa yenye msaada hata kama yule aliyefiwa ni Shahidi tayari au mtu ambaye tumekutana naye katika huduma. Baadhi ya maandiko hayo ni yapi? Twajua kwamba Yehova ndiye Mungu wa faraja yote, kwa kuwa alisema: “Mimi, naam, mimi, ndimi niwafarijiye.” Pia alisema: “Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi.”—Isaya 51:12; 66:13.

21 Mtunga-zaburi aliandika: “Hii ndiyo faraja yangu katika taabu yangu, ya kwamba ahadi yako imenihuisha. Nimezikumbuka hukumu zako za kale, Ee BWANA, nikajifariji. Nakuomba, fadhili zako ziwe faraja kwangu, sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako.” Ona kwamba neno “faraja” linatumiwa kwa kurudia-rudia katika mistari hiyo. Naam, twaweza kupata faraja ya kweli kwetu wenyewe na kwa wengine kwa kuendea Neno la Yehova katika wakati wetu wa taabu. Hiyo, pamoja na upendo na huruma ya akina ndugu, yaweza kutusaidia tustahimili upotezo wetu na tujaze maisha yetu tena na utendaji wenye shangwe katika huduma ya Kikristo.—Zaburi 119:50, 52, 76.

22. Ni tazamio jipi lipo mbele yetu?

22 Twaweza pia kushinda huzuni kwa kadiri fulani kwa kuwa wenye shughuli tukisaidia wengine katika msononeko wao. Tugeuzapo fikira zetu kwa wengine wanaohitaji faraja, sisi pia hupata furaha ya kweli ya kutoa kwa njia ya kiroho. (Matendo 20:35) Na tushiriki nao ono la siku ya ufufuo wakati watu wa mataifa yote ya kale, kizazi baada ya kizazi, watakapokuwa wakiwakaribisha wapendwa wao waliokufa kutoka kwa wafu katika ulimwengu mpya. Ni tazamio zuri kama nini! Kutakuwa na machozi ya shangwe kama nini wakati huo tukumbukapo kwamba kwa kweli Yehova ni Mungu “mwenye kuwafariji wanyonge”!—2 Wakorintho 7:6.

Je, Wakumbuka?

◻ Ni kwa njia gani Yehova ni “Mungu wa faraja yote”?

◻ Yesu na Paulo waliwafarijije wenye kuhuzunika?

◻ Ni yapi baadhi ya mambo tuwezayo kufanya ili kufariji wanaohuzunika?

◻ Twapaswa kuepuka nini tunaposhughulika na mfiwa?

◻ Ni yapi maandiko upendayo zaidi ya kufariji katika nyakati za upotezo?

[Picha katika ukurasa wa15]

Kwa busara chukua hatua ya kwanza ya kusaidia wale wanaohuzunika

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki