Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w95 10/1 kur. 8-13
  • Je, Mungu Hutangulizwa Katika Familia Yako?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Mungu Hutangulizwa Katika Familia Yako?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtego wa Upinzani wa Familia
  • Kuukabili Ugumu Huo kwa Mafanikio
  • Thawabu Nzuri Iwezayo Kupatikana
  • Kujifunza Kutokana na Yesu
  • Waume, Wake—Mwigeni Kristo!
  • Jinsi ya Kufanya Maisha ya Familia Yako Yawe Yenye Furaha
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Waume, Tambueni Ukichwa wa Kristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kufanikisha Maisha ya Jamaa
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
w95 10/1 kur. 8-13

Je, Mungu Hutangulizwa Katika Familia Yako?

“Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote.”—MARKO 12:29, 30.

1. Ni muhimu kadiri gani kwamba tumpende Yehova?

“KATIKA amri zote ni ipi iliyo ya kwanza?” mwandishi mmoja alimwuliza Yesu. Badala ya kutoa maoni yake mwenyewe, Yesu alijibu swali lake kwa kunukuu kutoka katika Neno la Mungu kwenye Kumbukumbu la Torati 6:4, 5. Alijibu hivi: “Ya kwanza ndiyo hii, Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho [“nafsi,” NW] yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”—Marko 12:28-30.

2. (a) Yesu alilazimika kukabili upinzani gani? (b) Ni nini nyakati nyingine chaweza kufanya iwe vigumu kumpendeza Yehova?

2 Ili kutii amri ambayo Yesu aliita ya kwanza—ya maana zaidi—ni lazima sikuzote tufanye yampendezayo Yehova. Yesu alifanya hivyo, hata ingawa katika pindi moja mtume Petro alipinga mwendo wa Yesu, na katika pindi nyingine hata watu wake wa ukoo wa karibu walifanya hivyo. (Mathayo 16:21-23; Marko 3:21; Yohana 8:29) Vipi ukijikuta katika hali kama hiyo? Tuseme washiriki wa familia wanataka ukome kujifunza Biblia na kushiriki pamoja na Mashahidi wa Yehova. Je, utamtanguliza Mungu kwa kufanya yampendezayo? Je, ni Mungu anayetangulizwa, hata kama washiriki wa familia wanaweza kupinga jitihada zako za kumtumikia?

Mtego wa Upinzani wa Familia

3. (a) Matokeo ya mafundisho ya Yesu yaweza kuwa nini katika familia? (b) Washiriki wa familia waweza kuonyeshaje ni nani wanayempenda zaidi?

3 Yesu hakupuuza ugumu uwezao kutokea wakati wengine katika familia wapingapo yule mshiriki anayekubali mafundisho yake. “Adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake,” akasema Yesu. Lakini, matokeo hayo mabaya yajapotokea, Yesu alionyesha ni nani aliyepaswa kutangulizwa akisema: “Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili.” (Mathayo 10:34-37) Twamtanguliza Yehova Mungu kwa kufuata mafundisho ya Mwana wake, Yesu Kristo, ambaye ni “chapa ya nafsi [ya Mungu].”—Waebrania 1:3; Yohana 14:9.

4. (a) Yesu alisema ni nini kilichohusika katika kuwa mfuasi wake? (b) Ni katika maana gani Wakristo wachukie washiriki wa familia?

4 Pindi nyingine Yesu alipokuwa akijadili jambo lililohusika hasa katika kuwa mfuasi wake wa kweli, alisema: “Mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.” (Luka 14:26) Bila shaka Yesu hakumaanisha kwamba wafuasi wake wachukie kihalisi washiriki wa familia zao, kwa kuwa aliwaamuru watu wapende hata adui zao. (Mathayo 5:44) Badala ya hivyo, hapa Yesu alimaanisha kwamba ni lazima wafuasi wake wapende washiriki wa familia kidogo kuliko wanavyompenda Mungu. (Linganisha Mathayo 6:24.) Kwa kupatana na uelewevu huo, Biblia yasema kwamba Yakobo ‘alimchukia’ Lea na kumpenda Raheli, jambo lililomaanisha kwamba hakumpenda Lea kama alivyompenda dada yake, Raheli. (Mwanzo 29:30-32, NW) Hata “nafsi,” au maisha yetu, Yesu akasema, yapasa kuchukiwa, au kupendwa kidogo kuliko Yehova!

5. Shetani hutumiaje vibaya kwa ujanja mpango wa familia?

5 Akiwa Muumba na Mpaji-Uhai, Yehova anastahili ujitoaji kamili kutoka kwa watumishi wake wote. (Ufunuo 4:11) “Nampigia Baba magoti,” mtume Paulo akaandika, “ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa.” (Waefeso 3:14, 15) Yehova alifanyiza mpango wa familia kwa njia nzuri ajabu hivi kwamba washiriki wa familia wana shauku ya kiasili kwa kila mmoja. (1 Wafalme 3:25, 26; 1 Wathesalonike 2:7) Hata hivyo, Shetani Ibilisi hutumia vibaya kwa ujanja shauku hii ya kiasili ya familia, ambayo hutia ndani tamaa ya kupendeza wapendwa. Yeye huzidisha upinzani wa familia, na wengi hupata ugumu wa kusimama imara kwa ajili ya kweli ya Biblia wanapoukabili.—Ufunuo 12:9, 12.

Kuukabili Ugumu Huo kwa Mafanikio

6, 7. (a) Washiriki wa familia wanaweza kusaidiwaje kujua umuhimu wa funzo la Biblia na ushirika wa Kikristo? (b) Twaweza kuonyeshaje kwamba kweli twawapenda washiriki wa familia yetu?

6 Utafanya nini ukilazimika kuchagua kati ya kumpendeza Mungu au kumpendeza mshiriki wa familia? Je, utasababu kwamba Mungu hatazamii tujifunze Neno lake na kuzitumia kanuni zalo ikiwa kujifunza kwetu kunatokeza mvurugo wa familia? Lakini ebu lifikirie jambo hili. Ukishindwa kisha ukomeshe funzo lako la Biblia au ushirika wako pamoja na Mashahidi wa Yehova, wapendwa wako watapataje kujua kwamba ujuzi sahihi wa Biblia ni jambo la kupata uhai ama kifo?—Yohana 17:3; 2 Wathesalonike 1:6-8.

7 Twaweza kutoa kielezi hiki kwa jambo hilo: Labda mshiriki wa familia ana tamaa ya kupita kiasi ya alkoholi. Je, kupuuza au kukubali tatizo lake la unywaji kutamsaidia kweli? Je, ingekuwa afadhali kudumisha amani kwa kukubali tabia yake bila kufanya jambo lolote kuhusu tatizo lake? La, labda unakubali kwamba ingekuwa bora kujaribu kumsaidia kushinda tatizo lake la unywaji, hata kama hilo lamaanisha kukabili hasira na matisho yake. (Mithali 29:25) Vivyo hivyo, ukiwapenda kwa kweli washiriki wa familia yenu, hutashindwa na jitihada zao za kukukomesha kujifunza Biblia. (Matendo 5:29) Ni kwa kuchukua msimamo thabiti kwamba unaweza kuwasaidia kujua kwamba kuishi kwa kupatana na mafundisho ya Kristo kwamaanisha uhai wetu wenyewe.

8. Tunanufaikaje na jambo la kwamba Yesu alifanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu?

8 Kumtanguliza Mungu kwaweza kuwa vigumu sana nyakati nyingine. Lakini kumbuka kwamba Shetani pia alifanya iwe vigumu kwa Yesu kufanya mapenzi ya Mungu. Lakini Yesu hakushindwa; alivumilia hata uchungu mkali wa mti wa mateso kwa ajili yetu. “Yesu Kristo [ni] Mwokozi wetu,” Biblia yasema. “Alikufa kwa ajili yetu.” (Tito 3:6; 1 Wathesalonike 5:10) Je, hatushukuru kwamba Yesu hakushindwa na upinzani? Kwa sababu alivumilia kifo cha dhabihu, tuna matazamio ya kupata uhai udumuo milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu kwa kudhihirisha imani katika damu ya Yesu iliyomwagwa.—Yohana 3:16, 36; Ufunuo 21:3, 4.

Thawabu Nzuri Iwezayo Kupatikana

9. (a) Wakristo waweza kushirikije katika kuokoa wengine? (b) Hali ya familia ya Timotheo ilikuwaje?

9 Je, ulitambua kwamba hata wewe unaweza kushiriki katika kuokoa wengine, kutia ndani watu wa ukoo wapendwa? Mtume Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Dumu katika mambo hayo [ambayo ulikuwa umefundishwa]; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16, italiki ni zetu.) Timotheo aliishi katika familia iliyogawanyika, baba yake Mgiriki akiwa mtu asiyeamini. (Matendo 16:1; 2 Timotheo 1:5; 3:14) Ingawa hatujui kama baba ya Timotheo alikuja kuwa mwamini baadaye, uwezekano wa kwamba alikuja kuwa mwamini uliongezwa sana na mwenendo mwaminifu wa mke wake, Eunike, na wa Timotheo.

10. Wakristo waweza kufanya nini kwa niaba ya wenzi wao wasioamini?

10 Maandiko yafunua kwamba waume na wake wanaoshikilia kwa uthabiti kweli ya Biblia waweza kuchangia kuokoa wenzi wao wasio Wakristo kwa kuwasaidia kuwa waamini. Mtume Paulo aliandika: “Iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye, asimwache. Na mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe. Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?” (1 Wakorintho 7:12, 13, 16) Mtume Petro alifafanua jinsi wake wawezavyo kuokoa waume zao, akiwahimiza hivi: “Watiini waume zenu; kusudi, ikiwa wako wasioliamini Neno, wavutwe kwa mwenendo wa wake zao, pasipo lile Neno.”—1 Petro 3:1.

11, 12. (a) Maelfu ya Wakristo wamepokea thawabu gani, nao walifanya nini ili kuipokea? (b) Eleza ono la mshiriki mmoja wa familia aliyethawabishwa kwa sababu ya uvumilivu wenye uaminifu.

11 Katika miaka ya majuzi maelfu ya watu wamekuja kuwa Mashahidi wa Yehova baada ya kupinga utendaji wa Kikristo wa watu wao wa ukoo walio Mashahidi kwa miezi mingi na hata miaka mingi. Hiyo ni thawabu nzuri kama nini kwa Wakristo ambao wamedumisha uthabiti, na ni baraka iliyoje kwa wale waliokuwa wapinzani wakati mmoja! Akiwa na hisia katika sauti yake, mzee mmoja Mkristo mwenye miaka 74 alisimulia hivi: “Mara nyingi mimi humshukuru mke wangu na watoto wangu kwa kuishika kweli katika miaka niliyowapinga.” Alisema kwamba kwa miaka mitatu yeye alikataa katakata hata kuruhusu mke wake aseme naye juu ya Biblia. “Lakini alitumia akili,” akasema, “akaanza kunitolea ushahidi akinikanda miguu. Nashukuru kama nini kwamba hakushindwa na upinzani wangu!”

12 Mume mwingine aliyepinga familia yake aliandika: ‘Nilikuwa adui mkubwa sana wa mke wangu kwa sababu baada ya yeye kupata kweli, nilikuwa nikimtisha, nasi tuligombana kila siku; yaani, sikuzote nilianzisha ugomvi. Lakini wapi; mke wangu alishikamana na Biblia. Basi miaka 12 ikapita nikipigana vikali dhidi ya kweli na dhidi ya mke wangu na mtoto wangu. Kwao wawili, nilikuwa Ibilisi mwenyewe.’ Hatimaye mtu huyo akaanza kuchanganua maisha yake. ‘Nikaona jinsi nilivyokuwa nimekuwa mbaya,’ akaeleza. ‘Nilisoma Biblia, na kwa sababu ya mafundisho yayo, sasa mimi ni Shahidi aliyebatizwa.’ Ebu fikiria thawabu tukufu ya mke huyo, ndiyo, alisaidia ‘kuokoa mume wake’ kwa kuvumilia upinzani wake kwa miaka 12!

Kujifunza Kutokana na Yesu

13. (a) Ni lipi somo kuu ambalo waume na wake wapaswa kujifunza kutokana na mwendo wa maisha wa Yesu? (b) Watu wanaopata ugumu wa kunyenyekea mapenzi ya Mungu wananufaikaje na kielelezo cha Yesu?

13 Somo kuu ambalo waume na wake wanapaswa kujifunza kutokana na mwendo wa maisha wa Yesu ni lile la utii kwa Mungu. “Nafanya sikuzote yale yampendezayo,” Yesu akasema. “Siyatafuti mapenzi yangu mimi, bali mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 5:30; 8:29) Hata pindi moja Yesu alipopata kwamba hapendi jambo fulani la mapenzi ya Mungu, alikuwa mtiifu. “Ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki,” alisali. Lakini akaongezea kwa haraka: “Walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Yesu hakumwomba Mungu abadili mapenzi Yake; yeye alionyesha kwamba alimpenda Mungu kikweli kwa kunyenyekea kwa utiifu mapenzi yoyote yale ya Mungu kwake. (1 Yohana 5:3) Kumtanguliza Mungu sikuzote, kama alivyofanya Yesu, ni muhimu sana kwa ajili ya mafanikio si katika maisha ya useja tu bali pia katika maisha ya ndoa na ya familia. Ona kwa nini ni hivyo.

14. Wakristo wengine husababuje isivyofaa?

14 Kama ilivyotajwa mapema, waamini wanapomtanguliza Mungu, wao hutafuta kuendelea kuishi na wenzi wao wasioamini na mara nyingi wao huwasaidia kuweza kupata wokovu. Hata kama wenzi wote wawili ni waamini, huenda ndoa yao isiwe nzuri. Kwa sababu ya mielekeo yenye dhambi, waume na wake hawawi na mawazo ya upendo kuelekeana sikuzote. (Warumi 7:19, 20; 1 Wakorintho 7:28) Wengine hata hufikia hatua ya kutafuta mwenzi mwingine, ingawa hawana msingi wa Kimaandiko wa kupata talaka. (Mathayo 19:9; Waebrania 13:4) Wao husababu kwamba kwao hilo ndilo jambo bora, kwamba mapenzi ya Mungu kwa waume na wake kuishi pamoja ni magumu sana. (Malaki 2:16; Mathayo 19:5, 6) Bila shaka hii ni hali nyingine ya kuwa na fikira za kibinadamu badala ya zile za Mungu.

15. Kwa nini kumtanguliza Mungu ni ulinzi?

15 Ni ulinzi ulioje kumtanguliza Mungu! Wenzi wa ndoa wanaofanya hivyo watajaribu kushikamana pamoja na kujaribu kusuluhisha matatizo yao kwa kutumia shauri la Neno la Mungu. Hivyo wao huepuka maumivu mengi ya moyoni ambayo hutokea mapenzi yake yanapopuuzwa. (Zaburi 19:7-11) Jambo hilo linatolewa kielezi na wenzi fulani wachanga ambao, walipokuwa karibu kabisa kupata talaka, waliamua kufuata shauri la Biblia. Miaka mingi baadaye mke alipofikiria shangwe aliyokuwa amepata katika ndoa yake, alisema hivi: “Ni lazima niketi na kulia machozi nifikiriapo uwezekano wa kwamba ningeishi nikiwa nimetengana na mume wangu miaka hiyo yote. Kisha mimi husali kwa Yehova Mungu na kumshukuru kwa shauri lake na mwongozo wake uliotupatanisha katika uhusiano huu wenye furaha.”

Waume, Wake—Mwigeni Kristo!

16. Yesu aliweka kielelezo gani kwa wote waume na wake?

16 Yesu, ambaye sikuzote alimtanguliza Mungu, aliweka kielelezo kizuri ajabu kwa wote waume na wake, na ni vizuri wakifuate kwa uangalifu. Waume wanahimizwa kuiga njia ambayo Yesu alidhihirisha ukichwa wake mwororo juu ya washiriki wa kutaniko la Kikristo. (Waefeso 5:23) Na wake Wakristo wanaweza kujifunza kwa kielelezo cha Yesu kisicho na waa cha utii kwa Mungu.—1 Wakorintho 11:3.

17, 18. Ni katika njia zipi Yesu aliweka kielelezo chema kwa waume?

17 Biblia huamuru hivi: “Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile yule Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yalo.” (Waefeso 5:25, NW) Njia kubwa ambayo Yesu alionyesha upendo wake kwa kutaniko la wafuasi wake ilikuwa kuwa rafiki wao wa karibu. “Nimewaita rafiki,” akasema Yesu, “kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.” (Yohana 15:15) Fikiria ule wakati wote ambao Yesu alitumia akizungumza na wanafunzi wake—yale mazungumzo mengi sana aliyokuwa nayo pamoja nao—na uhakika aliowapa! Je, huo si kielelezo kizuri kwa waume?

18 Yesu alipendezwa sana na wanafunzi wake naye aliwapenda kikweli. (Yohana 13:1) Walipokosa kuelewa vizuri mafundisho yake, yeye alichukua wakati faraghani na kuyafafanua. (Mathayo 13:36-43) Je, waume, hali ya kiroho ya mke wako ni ya maana kadiri hiyo kwako? Je, unatumia muda pamoja naye, ukihakikisha kwamba nyote wawili mnaelewa vizuri sana kweli za Biblia akilini na moyoni? Yesu aliandamana na mitume wake katika huduma, labda akiwazoeza mmoja-mmoja. Je, wewe huandamana na mke wako katika huduma, ukishiriki naye katika ziara za nyumba kwa nyumba na katika kuongoza mafunzo ya Biblia?

19. Jinsi Yesu alivyoshughulikia udhaifu mbalimbali wa mitume wake yawekeaje waume kielelezo?

19 Hasa alipokuwa akishughulikia mapungufu ya mitume wake ndipo Yesu aliandaa kielelezo kizuri sana kwa waume. Katika mlo wake wa mwisho pamoja na mitume wake, yeye angeweza kutambua roho ya ushindani iliyokuwa ikiwarudia-rudia. Je, aliwakemea vikali? La, bali aliosha miguu ya kila mmoja kwa unyenyekevu. (Marko 9:33-37; 10:35-45; Yohana 13:2-17) Je, wewe humwonyesha mke wako saburi kama hiyo? Badala ya kulalamika kwa sababu ya udhaifu anaorudia-rudia, je, unajaribu kwa saburi kumsaidia na kumfikia moyo kupitia kielelezo chako? Yaelekea wake wataitikia upendo huo wenye huruma kama mitume walivyofanya hatimaye.

20. Wake Wakristo hawapaswi kusahau nini kamwe, naye ni nani anayeandaliwa akiwa kielelezo chao?

20 Wake pia wahitaji kumfikiria Yesu, ambaye hakusahau kamwe kwamba “kichwa cha Kristo ni Mungu.” Sikuzote alijinyenyekeza kwa Baba yake wa kimbingu. Vivyo hivyo, wake hawapaswi kusahau kwamba “kichwa cha mwanamke ni mwanamume,” ndiyo, kwamba mume ndiye kichwa. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Mtume Petro aliwahimiza wake Wakristo kufikiria kielelezo cha “wanawake watakatifu” wa nyakati za mapema, hasa kile cha Sara, ‘aliyemtii Abrahamu, akamwita Bwana.’—1 Petro 3:5, 6.

21. Kwa nini ndoa ya Abrahamu na Sara ilifanikiwa lakini ile ya Loti na mke wake ikashindwa?

21 Yaonekana Sara aliacha makao ya starehe katika jiji lenye utajiri ili kuishi katika mahema katika bara la kigeni. Kwa nini? Je, ni kwa sababu alipendelea maisha hayo? Haielekei hivyo. Je, ni kwa sababu mume wake alimwambia aende? Bila shaka hilo lilikuwa jambo moja lililochangia, kwa kuwa Sara alimpenda na kumstahi Abrahamu kwa sababu ya sifa zake za kimungu. (Mwanzo 18:12) Lakini sababu kubwa iliyomfanya aende pamoja na mume wake ni upendo wake kwa Yehova na tamaa yake ya moyoni ya kufuata mwelekezo wa Mungu. (Mwanzo 12:1) Alifurahia sana kumtii Mungu. Kwa upande mwingine, mke wa Loti alisita-sita kufanya mapenzi ya Mungu akaangalia nyuma kwa kutamani vitu alivyoacha katika mji wa kwao wa Sodoma. (Mwanzo 19:15, 25, 26; Luka 17:32) Huo ulikuwa mwisho wenye msiba kama nini kwa ndoa hiyo—kwa sababu tu hakumtii Mungu!

22. (a) Ni kujichunguza kupi ambako washiriki wa familia watafanya kwa hekima? (b) Tutazungumzia nini katika funzo lifuatalo?

22 Hivyo, tukiwa mume au mke, ni muhimu kujiuliza hivi, ‘Je, tunamtanguliza Mungu katika familia yetu? Je, ninajaribu kikweli kutimiza fungu la familia ambalo Mungu amenipa? Je, ninafanya jitihada ya kweli ya kumpenda mwenzi wangu na kumsaidia kupata au kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova?’ Katika familia nyingi mna watoto pia. Tutazungumzia fungu la wazazi na uhitaji wa wote wawili kusaidia watoto kumtanguliza Mungu.

Je, Wakumbuka?

◻ Matokeo ya mafundisho ya Yesu yaweza kuwa nini kwa familia nyingi?

◻ Maelfu ya Wakristo walio thabiti wamepokea thawabu gani?

◻ Ni nini kitakachosaidia wenzi kuepuka ukosefu wa adili na talaka?

◻ Waume waweza kujifunza nini kutokana na kielelezo cha Yesu?

◻ Wake wanaweza kuchangiaje ndoa yenye furaha?

[Picha katika ukurasa wa10]

Sara alichangiaje mafanikio ya ndoa yake?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki