Jilindeni na Kujiona Waadilifu!
KATIKA karne ya kwanza, Mafarisayo walifurahia sifa nzuri ya kuwa waabudu waadilifu wa Mungu. Walikuwa wanafunzi wenye bidii wa Maandiko nao walisali mara nyingi. Watu fulani waliwaona kuwa wapole na wenye kusababu vizuri. Yosefo, mwanahistoria Myahudi aliandika hivi: “Mafarisayo hupendana nao husitawisha uhusiano wa karibu pamoja na jamii.” Si ajabu kwamba labda wao ndio waliostahiwa zaidi na kuheshimiwa katika jamii ya Kiyahudi wakati huo!
Hata hivyo, leo neno “-a Kifarisayo” na misemo inayohusiana nalo ni ya madharau yanayohusianishwa na unafiki, kujiona kuwa mwadilifu, mtakatifu, mtawa kupita kiasi na mwenye kutoa utumishi wa mdomo. Kwa nini Mafarisayo walipoteza sifa yao nzuri?
Ni kwa sababu, tofauti na Wayahudi walio wengi, Yesu Kristo hakudanganywa na sura ya nje ya Mafarisayo. Aliwalinganisha na “makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.”—Mathayo 23:27.
Ni kweli, walitoa sala ndefu wakisimama kwenye sehemu za umma, lakini walitaka tu waonekane na wengine, kama Yesu alivyosema. Ibada yao ilikuwa ya kujifanya tu. Wao walipenda mahali penye kutokeza zaidi kwenye milo ya jioni na viti vya mbele katika masinagogi. Kwa kuwa ilikuwa lazima Wayahudi wote kuweka pindo kwenye mavazi yao, Mafarisayo walijaribu kuvutia watu kwa kuweka pindo ndefu kupita kiasi. Walivionyesha kwa fahari vibweta vyao vyenye andiko vilivyopanuliwa zaidi walivyovaa kama hirizi. (Mathayo 6:5; 23:5-8) Unafiki wao, pupa yao, na kiburi chao mwishowe ziliwaletea fedheha.
Yesu alieleza hivi kukataliwa kwa Mafarisayo na Mungu: “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.” (Mathayo 15:7-9) Kwa kweli uadilifu wao ulikuwa wa kujiona waadilifu. Kwa kufaa Yesu aliwaonya wanafunzi wake: “Jilindeni na chachu ya Mafarisayo.” (Luka 12:1) Leo, sisi pia ni lazima ‘tujilinde,’ na kujiona waadilifu au tulinde dhidi ya kuwa wanafiki wa kidini.
Tufanyapo hivyo, ni lazima tutambue kwamba mtu hawi mwenye kujiona kuwa mwadilifu kwa siku moja. Badala ya hivyo, mwelekeo huo huja polepole kadiri muda upitavyo. Hata bila kukusudia mtu aweza kuwa na hali zisizofaa kama za Mafarisayo.
Kujiona Kuwa Bora
Ni yapi baadhi ya maelekeo tunayopaswa ‘kujilinda’ nayo? Watu wenye kujiona waadilifu mara nyingi “huongea, na kusimama, na kutazama kana kwamba hawajawahi kamwe kufanya kosa lolote,” chaeleza Encyclopædia of Religion and Ethics. Wenye kujiona waadilifu pia ni wenye kujisifu na kujipendekeza, mambo yaliyokuwa tatizo kuu la Mafarisayo.
Yesu alifafanua mtazamo huo wa Kifarisayo kwa kielelezo hiki: “Watu wawili walipanda kwenda ndani ya hekalu kusali, mmoja Farisayo na yule mwingine mkusanya-kodi. Yule Farisayo alisimama na kuanza kusali mambo haya akijiambia, ‘Ee Mungu, mimi nakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama mkusanya-kodi huyu. Mimi hufunga mara mbili kwa juma, mimi hutoa sehemu ya kumi ya vitu vyote nijipatiavyo.’” Kinyume cha hayo mkusanya-kodi alikubali makosa yake kwa unyenyekevu naye akathibitika kuwa mwadilifu zaidi kuliko Farisayo mwenye majisifu. Yesu alielekeza kielelezo hicho kwa wale “waliojiitibari wenyewe kwamba walikuwa waadilifu na walioona wale wengine kama si kitu.”—Luka 18:9-14, NW.
Tukiwa wanadamu wasiokamilika huenda mara kwa mara tukahisi kwamba sisi ni bora kuliko wengine kwa sababu ya uwezo wetu mbalimbali wa kiasili au mapendeleo. Lakini Wakristo ni lazima waondolee mbali haraka mawazo hayo. Huenda ikawa una ujuzi wa miaka mingi katika maisha ya Kikristo. Huenda ukawa mwalimu stadi wa Biblia. Au labda unadai kuwa umetiwa mafuta ukatawale na Kristo mbinguni. Wengine kutanikoni wana mapendeleo ya pekee wakiwa wahudumu wa wakati wote, wazee, au watumishi wa huduma. Jiulize mwenyewe, ‘Yehova angehisije ikiwa ningetumia alichonipa kuwa msingi wa kuhisi kuwa bora kuliko wengine?’ Kwa kweli, hilo halingempendeza.—Wafilipi 2:3, 4.
Mkristo aonyeshapo roho ya kujiona kuwa bora kwa sababu ya uwezo wake mbalimbali, mapendeleo, au mamlaka aliyopewa na Mungu, kwa kweli anamnyang’anya Mungu utukufu na sifa anayoistahili Yeye pekee. Kwa wazi Biblia huonya Mkristo “asinie makuu kupita ilivyompasa kunia.” Inatuhimiza: “Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili.”—Warumi 12:3, 16.
“Msihukumu”
Kulingana na ensaiklopedia moja ya Biblia, mtu ajionaye kuwa mwadilifu “hujidhania kuwa mwenye kufuata haki au mwenye msimamo mzuri pamoja na Mungu kwa sababu ya kufuata matakwa halali ya sheria bila kujali kusudi layo.” Kitabu kingine hufafanua watu wenye kujiona waadilifu kuwa “watu wenye kufuata dini kupita kiasi wanaotumia wakati wao wote kutafuta uovu wa wengine.”
Mafarisayo walikuwa na hatia ya jambo hilo. Mwishowe sheria zao zilizofanywa na wanadamu zikaonekana kuwa za maana zaidi kuliko sheria na kanuni za Mungu. (Mathayo 23:23; Luka 11:41-44) Walijiweka kuwa mahakimu na walikuwa na mwelekeo wa kuhukumu mtu yeyote ambaye hakufikia viwango vyao wenyewe vya uadilifu. Mtazamo wao wa kujiona kuwa bora na kujiheshimu kupita kiasi uliwafanya watake kuongoza watu wengine. Kushindwa kwao kumwongoza Yesu kuliwaghadhabisha, hivyo wakafanya hila ya kumuua kimakusudi.—Yohana 11:47-53.
Ni jambo lisilopendeza kama nini kuwa pamoja na mtu fulani ajiwekaye kuwa hakimu, akitafuta makosa sikuzote, akichunguza na kutawala kila mtu aliye karibu naye. Kwa kweli, hakuna yeyote kutanikoni aliye na mamlaka ya kulazimisha wengine wawe na maoni kama yake na kufuata sheria alizojitengenezea. (Warumi 14:10-13) Wakristo walio na usawaziko hutambua kwamba sehemu nyingi za maisha ya kila siku ni za kuamriwa na mtu mwenyewe. Hasa wale walio na mwelekeo wa kuwa wenye kutaka ukamilifu na wenye kudai mno ni lazima waache kuhukumu wengine.
Ni kweli kwamba kutaniko la Kikristo limeruhusiwa kuwa na mielekezo inayochangia utendaji mzuri wa tengenezo la Yehova la kidunia. (Waebrania 13:17) Lakini wengine wameharibu mielekezo hiyo au wameongeza sheria zao wenyewe. Katika eneo moja wanafunzi wote wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi walipaswa kuvaa suti na kufunga vifungo vyote vya koti wanapotoa hotuba. Mwanafunzi aliyekosa kufanya hivyo aliondolewa katika shule. Badala ya kuweka sheria kali kama hizo, je, halingekuwa jambo la hekima zaidi na linalopatana na roho ya Neno la Mungu kutoa mwelekezo wa kibinafsi wenye fadhili, unaohitajika?—Yakobo 3:17.
Kujiona kuwa mwadilifu kwaweza pia kuendekeza maoni ya kwamba ikiwa Mkristo anapatwa na matatizo mengi ya kibinafsi, ni lazima iwe hali yake ya kiroho imepungukiwa. Ndivyo hasa Elifazi, Bildadi, na Sofari waliojiona kuwa waadilifu walivyomfikiria Ayubu mwaminifu. Hawakuifahamu kabisa hali ya Ayubu, hivyo ni kiburi kilichowafanya wamhukumu Ayubu kwamba amefanya dhambi. Yehova aliwatia nidhamu kwa ajili ya uchanganuzi wao uliopotoka wa majaribu ya Ayubu.—Ona Ayubu, sura za 4, 5, 8, 11, 18, 20.
Bidii Isiyofaa
Kujiona kuwa mwadilifu na bidii mara nyingi zinahusiana. Mtume Paulo alizungumza juu ya Wayahudi waliokuwa na mwelekeo wa kufuata dini kuwa “wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi; kwa maana, kwa sababu ya kutojua uadilifu wa Mungu bali wakitafuta sana kusimamisha ulio wao wenyewe, hawakujitiisha wenyewe kwa uadilifu wa Mungu.” (Warumi 10:2, 3) Alipokuwa Farisayo, Paulo mwenyewe alikuwa na bidii nyingi kupita kiasi, ingawa bidii yake haikufaa, ikikosa msingi wa uadilifu wa Yehova.—Wagalatia 1:13, 14; Wafilipi 3:6.
Kwa kufaa Biblia huonya hivi: ‘Usiwe mwadilifu kupita kiasi; wala usijiongezee hekima mno; kwani kujiangamiza mwenyewe?’ (Mhubiri 7:16) Kutanikoni huenda Mkristo akaanza kuwa na bidii ya kudhamiria, lakini kudhamiria kwake na bidii yake zaweza kusonga na kuwa kujiona kuwa mwadilifu. Bidii ya kidini inapoongozwa na hekima ya kibinadamu badala ya uadilifu wa Yehova, yaweza kudhuru wengine. Jinsi gani?
Kwa kielelezo, wazazi waweza kujitia sana katika kuhangaikia uhitaji wa kiroho wa wengine, na wakati uleule huenda wakaachilia mahitaji ya familia zao wenyewe. Au huenda wazazi wakawa na bidii nyingi kupita kiasi, wakidai mengi mno kutoka kwa watoto wao kuliko yale watoto wanaweza kutimiza. (Waefeso 6:4; Wakolosai 3:21) Watoto fulani, wakiwa wameshindwa kufikia matakwa hayo yasiyo na kiasi, huiweza hali kwa kuishi maisha maradufu. Mzazi mwenye kusababu vizuri atafikiria mipaka ya familia yake na kufanya marekebisho yanayofaa.—Linganisha Mwanzo 33:12-14.
Bidii kupita kiasi yaweza kutuzuia kuwa na busara, hisia-mwenzi, na wororo, sifa zilizo muhimu tunaposhughulika na wengine. Mtu aweza kufanya bidii sana kuendeleza masilahi ya Ufalme. Hata hivyo, bidii yake iliyopita kiasi yaweza kudhuru wengine. Paulo alisema: “Nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”—1 Wakorintho 13:2, 3.
Mungu Hupendelea Wanyenyekevu
Tukiwa Wakristo twahitaji kutambua tisho la kujiona waadilifu kabla ya kutupata. Ni lazima tuepuke kujiona kuwa bora, tabia ya kuhukumu wengine, na bidii kupita kiasi yenye msingi wa hekima ya kibinadamu.
Huku ‘tukijilinda’ na mitazamo ya Kifarisayo, badala ya kuhukumu wengine kuwa wenye kujiona waadilifu, ingalifaa kukazia fikira mielekeo yetu wenyewe. Ni kweli, Yesu aliwahukumu Mafarisayo na kuwashutumu kuwa “wana wa majoka” wanaostahili uharibifu wa milele. Lakini Yesu angeweza kusoma mioyo ya watu. Sisi hatuwezi.—Mathayo 23:33.
Acheni tutafute uadilifu wa Mungu wala si wetu wenyewe. (Mathayo 6:33) Ni kwa njia hiyo tu tunaweza kupata upendeleo wa Yehova, kwa kuwa Biblia hutusihi hivi: “Jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.”—1 Petro 5:5.