Tazama Zaidi ya Vitu Uvionavyo!
MACHO halisi yaonayo vizuri ni baraka. Kwa hakika watu wengi hawawezi kutaja vitu vingi walivyo navyo ambavyo ni vyenye thamani kuliko macho. Hata hivyo, kwa Wakristo kuna aina ya macho yanayotajwa na mtume Paulo ambayo ni yenye thamani kuliko macho halisi yaonayo vizuri. “Tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana,” akaandika Paulo. (2 Wakorintho 4:18) Ni lazima huu uwe mwono wa kipekee kwelikweli uwezao kumfanya mtu aone visivyoonekana! Twaweza kuuita mwono bora kabisa wa kiroho.
Kwa Nini Tuuhitaji?
Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na uhitaji sana wa aina hii ya macho ya kiroho. Walikuwa wakifanya huduma yao ya Kikristo chini ya magumu mengi. Paulo alieleza jambo hili hivi: “Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi.”—2 Wakorintho 4:8, 9.
Japo hali hizo, wanafunzi waaminifu walisimama imara. Wakiwa na tumaini lenye nguvu kwa Mungu, wao waliweza kusema kama alivyosema Paulo: “Hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku.” Lakini, ni nini kilicholeta huku kufanywa upya kila siku? Paulo aliendelea kusema: “Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”—2 Wakorintho 4:16-18.
Paulo alikuwa akitia moyo ndugu zake wa kiroho wasiruhusu matatizo, magumu, minyanyaso—dhiki za aina zozote—zizuie mwono wao wa thawabu tukufu ambayo ilikuwa imewekwa mbele yao. Walipaswa kutazama zaidi ya hali walizokuwa wakipata, wakikaza macho yao kwenye tokeo lenye furaha la mwendo wa Kikristo. Hilo ndilo jambo lililowawezesha kufanyiza upya kila siku azimio lao la kuendelea mbele na vita. Wakristo leo vilevile wanahitaji kuwa na macho mazuri kiroho.
Ona Dhiki za Sasa Kuwa za Muda Tu!
Tupende tusipende, kila siku sisi huona vitu ambavyo hatungependa kuona. Tukitazama kioo ni lazima tuone kasoro na mawaa kwenye mwili wetu wa halisi, jambo lionyeshalo kutokamilika kwetu kimwili. Tuchunguliapo kioo cha Neno la Mungu, sisi huona kasoro na mawaa ya kiroho, kwetu wenyewe na vilevile kwa wengine. (Yakobo 1:22-25) Na tutazamapo gazeti la kila siku au televisheni, visa vya ukosefu wa haki, ukatili, na msiba hutokeza na kutuletea huzuni.
Shetani angependa kutukatisha tamaa kwa sababu ya vitu tuonavyo au tukengeushwe na kuanza kusita-sita katika imani. Tunaweza kuzuiaje jambo hili lisitendeke? Ni lazima tufuate kielelezo kilichowekwa na Yesu Kristo, kama mtume Petro alivyopendekeza aliposema hivi: “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akaawachia kielelezo, mfuate nyayo zake.” (1 Petro 2:21) Katika kila hali ya maisha ya Kikristo, Yesu alikuwa kielelezo kikamilifu.
Akirejezea Yesu kuwa kiolezo chetu, Petro hasa alitaja kwamba Yesu aliteseka. Kwa kweli Yesu aliteseka sana alipokuwa duniani. Akiwa “stadi wa kazi” wa Yehova aliyekuwapo wakati wa uumbaji wa mwanadamu, yeye alijua hasa kusudi la Mungu kwa wanadamu. (Mithali 8:30, 31) Lakini sasa alijionea mwenyewe kile ambacho dhambi na kutokamilika kilichowafanya wawe. Kila siku aliona naye alilazimika kushughulikia kutokamilika na udhaifu mbalimbali wa watu. Ni lazima jambo hilo lilimletea majaribu sana.—Mathayo 9:36; Marko 6:34.
Mbali na dhiki za wengine, Yesu pia alipata dhiki. (Waebrania 5:7, 8) Lakini akiwa na macho makamilifu ya kiroho, yeye alitazama zaidi ya vitu hivyo na kuona thawabu ya kutukuzwa kwa uhai usioweza kufa kwa sababu ya mwendo wake wa uaminifu wa maadili. Kisha akiwa Mfalme wa Kimesiya, yeye angekuwa na pendeleo la kuinua wanadamu wenye matatizo kutoka kwa hali yao mbaya kurudia ukamilifu ambao Yehova alikusudia awali. Kukazia macho matazamio haya ya wakati ujao yasiyoonekana kulimsaidia kudumisha shangwe katika utumishi wa kimungu japo dhiki alizopata kila mara. Paulo aliandika baadaye: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:2, NW.
Yesu hakukubali kamwe hali zenye magumu na majaribu zimfanye akate tamaa, akengeushwe, au kusitasita katika imani. Tukiwa wanafunzi wake, ni lazima tufuate kielelezo chake kizuri sana.—Mathayo 16:24.
Kazia Akili Vitu vya Milele Visivyoonekana!
Akizungumzia kile kilichomwezesha Yesu kuvumilia, Paulo pia alitaja mwendo tupaswao kufuata alipoandika: “Acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu, tumkaziapo macho Wakili Mkuu na Mkamilishaji wa imani yetu, Yesu.” (Waebrania 12:1, 2, NW) Ndiyo, ili kukimbia mwendo wa Kikristo kwa mafanikio na kwa shangwe, ni lazima tutazame zaidi ya vitu vilivyopo tu mbele yetu. Lakini ‘tutamkaziaje macho’ Yesu, na kufanya hivyo kutatufanyia nini?
Kwa kielelezo, katika 1914, Yesu aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, naye atawala kutoka mbinguni. Bila shaka, hayo yote hayaonekani kwa macho yetu halisi. Na bado, ‘tukimkazia macho’ Yesu, macho yetu ya kiroho yatatusaidia kuona kwamba yeye yuko tayari kuchukua hatua ya kumaliza mfumo wa mambo ulio mwovu wa sasa na kumweka Shetani na majeshi yake ya roho waovu katika vifungo vya kutotenda. Na kwa kutazama zaidi, macho yetu ya kiroho yatafunua ulimwengu mpya mzuri ajabu ambamo “mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 19:11-16; 20:1-3; 21:4.
Basi, badala ya kulemezwa na dhiki za muda tu ambazo huenda tukalazimika kukabili kila siku, mbona tusikazie macho vitu ambavyo ni vya milele? Kwa macho ya imani, mbona tusitazame zaidi ya magonjwa na pupa zilizo katika dunia hii iliyochafuliwa na kuona paradiso iliyojaa watu wenye afya bora, wenye furaha, na wenye kujali? Mbona tusitazame zaidi ya kasoro zetu, za kimwili na kiroho, na kujiona tukiondolewa mambo hayo milele kwa ustahili wa dhabihu ya fidia ya Kristo? Mbona tusitazame zaidi ya uharibifu unaoachwa na vita, uhalifu, na jeuri na kuona wafufuliwa wapya wakifundishwa katika amani na uadilifu wa Yehova?
Kwa kuongezea, ‘kumkazia macho’ Yesu kungetia ndani pia kukaza macho yetu ya kiroho juu ya yale ambayo Ufalme, ingawa hauonekani kwa macho, tayari umetimiza miongoni mwa watu wa Mungu duniani: muungano, amani, upendo, shauku ya kidugu, na ufanisi wa kiroho. Baada ya kuona vidio United by Divine Teaching, mwanamke mmoja Mkristo katika Ujerumani aliandika hivi: “Kwa kuendelea vidio hiyo itanisaidia kudumisha akilini kwamba ndugu na dada zetu wengi Wakristo kotekote ulimwenguni sasa hivi wanamtumikia Yehova kwa uaminifu mshikamanifu—nao wanafanya hivyo wajapopata upinzani. Muungano wetu wa kidugu ni wenye thamani kama nini katika ulimwengu wenye jeuri na chuki!”
Je, wewe pia ‘unawaona’ Yehova, Yesu, malaika waaminifu, na mamilioni ya Wakristo wenzetu wakisimama kando yako? Ikiwa ndivyo, hutahangaishwa kupita kiasi na “hangaiko la mfumo huu wa mambo” liwezalo kukusimamisha kwa kukuvunja moyo na kukufanya kuwa “asiyezaa matunda” katika utumishi wa Kikristo. (Mathayo 13:22, NW) Basi, ‘mkazie macho’ Yesu kwa kukaza macho yako ya kiroho kwenye Ufalme wa Mungu uliosimamishwa na baraka zao za wakati huu na za wakati ujao.
Ishi Uone Visivyoonekana!
Kwa kuona tofauti kubwa iliyoko kati ya ulimwengu mpya wa milele wa Mungu na ulimwengu wa kale wa leo unaoporomoka, twapaswa kusukumwa kujiendesha hivi kwamba tutahesabiwa kuwa twastahili kuishi na kuona kihalisi vitu tuwezavyo kuona kupitia tu macho ya imani leo. Halaiki za wenye kufufuliwa hawataamini macho yao wakati watakapoamka na kuona dunia iliyo paradiso ikiwa tofauti sana na ulimwengu walioona kabla ya kufa. Ebu wazia shangwe yetu kwa kuwa hai kuwakaribisha na kuwaeleza yale ambayo Mungu amefanya!—Linganisha Yoeli 2:21-27.
Ndiyo, macho mazuri ya kiroho ni yenye thamani kama nini, na ni muhimu kama nini kuyadumisha yakiona vizuri! Twaweza kufanya hivyo kwa kuwa na funzo la binafsi la Biblia kwa ukawaida, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kusema na wengine kuhusu tumaini letu lenye kutegemea Biblia, na zaidi ya yote, kusali kwa ajili mwongozo wa kimungu. Jambo hili litadumisha macho yetu ya kiroho yakiwa yanaona vizuri sana, yakituwezesha kutazama zaidi ya vitu tuvionavyo!