Walifanya Mapenzi ya Yehova
Filipo Ambatiza Ofisa Mwethiopia
HUKU akisafiri kwa gari lake, Mwethiopia alikuwa akiutumia wakati wake kwa hekima. Alikuwa akisoma kwa sauti—zoea la kawaida miongoni mwa wasafiri wa karne ya kwanza. Mtu huyo mahususi alikuwa ofisa “mwenye mamlaka chini ya Kandake malkia wa Kushi.”a Alikuwa “juu ya hazina yake yote”—kihalisi, alikuwa waziri wa fedha. Ofisa huyo alikuwa akisoma Neno la Mungu ili apate ujuzi.—Matendo 8:27, 28.
Mweneza-evanjeli Filipo alikuwa karibu na hapo. Malaika alikuwa amemwelekeza aende hapo, na sasa aliambiwa: “Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo.” (Matendo 8:26, 29) Twaweza kuwazia Filipo akijiuliza, ‘Mtu huyu ni nani? Anasoma nini? Kwa nini nimeelekezwa kwake?’
Filipo alipokuwa akikimbia kandokando ya hilo gari, alimsikia Mwethiopia akisoma maneno haya: “Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi.”—Matendo 8:32, 33.
Mara moja Filipo alilitambua fungu hilo la maneno. Lilikuwa kutoka katika maandishi ya Isaya. (Isaya 53:7, 8) Yule Mwethiopia alishangazwa na yale aliyokuwa akisoma. Filipo akaanzisha mazungumzo kwa kuuliza hivi: “Je! yamekuelea haya unayosoma?” Mwethiopia akajibu hivi: “Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza?” Kisha akamsihi Filipo ajiunge naye katika gari lake.—Matendo 8:30, 31.
“Ni Nini Kinachonizuia Nisibatizwe?”
“Nakuomba,” yule Mwethiopia akamwambia Filipo, “nabii huyu; asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine?” (Matendo 8:34) Kutatanika kwa Mwethiopia hakukuwa kwenye kushangaza, kwa kuwa utambulishi wa “kondoo,” au “mtumishi,” wa unabii wa Isaya ulikuwa umekuwa fumbo kwa muda mrefu. (Isaya 53:11) Lazima iwe ilikuwa wazi kama nini Filipo alipomtangazia huyo Mwethiopia “habari njema za Yesu”! Baada ya muda huyo Mwethiopia akasema: “Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Kwa hiyo Filipo akambatiza papo hapo.—Matendo 8:35-38.
Je, hilo lilikuwa tendo la haraka-haraka? Sivyo hata kidogo! Huyo Mwethiopia alikuwa mgeuzwa-imani Myahudi.b Kwa hiyo tayari alikuwa mwabudu wa Yehova mwenye ujuzi wa Maandiko, kutia ndani na unabii mbalimbali wa Kimesiya. Hata hivyo, ujuzi wake haukuwa kamili. Sasa kwa kuwa alikuwa amepata habari hiyo muhimu juu ya fungu la Yesu Kristo, huyo Mwethiopia alifahamu yale ambayo Mungu alitaka afanye naye alikuwa tayari kutii. Ubatizo ulifaa.—Mathayo 28:18-20; 1 Petro 3:21.
Baadaye, “Roho wa Bwana akamnyakua Filipo.” Akaendelea na mgawo mwingine. Huyo Mwethiopia “alikwenda zake akifurahi.”—Matendo 8:39, 40.
Somo Kwetu Sisi
Tukiwa watumishi wa Yehova wa siku ya sasa, tuna wajibu wa kuwasaidia watu mmoja-mmoja wenye mioyo ya haki wajifunze kweli ya Neno la Mungu. Wengi wamepata mafanikio katika kuwatolea wengine habari njema huku wakisafiri au katika hali nyinginezo zisizo rasmi. Likiwa tokeo la kazi ya kuhubiri Ufalme, kila mwaka mamia ya maelfu hufananisha wakfu wao kwa Yehova Mungu kwa kubatizwa.
Bila shaka, wale walio wapya hawapasi kuharakishwa kwenye ubatizo. Kwanza ni lazima wapate ujuzi sahihi juu ya Yehova Mungu na juu ya Mwanae, Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Kisha lazima watubu, waache mwenendo mbaya na kugeuka ili kujipatanisha na viwango vya Mungu. (Matendo 3:19) Hilo huchukua muda, hasa ikiwa fikira na mwenendo mbaya zimekwisha thibitika. Ingawa wapya wapaswa kuhesabu gharama ya uanafunzi wa Kikristo, baraka kubwa hutokana na kuingia katika uhusiano wa kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu. (Linganisha Luka 9:23; 14:25-33.) Wale ambao ni Mashahidi wa Yehova huwaongoza hao wapya kwa idili kwenye tengenezo analotumia Mungu ili kutimiza mapenzi yake. (Mathayo 24:45-47) Sawa na huyo Mwethiopia, wapya hao watafurahia kujifunza na kutii yale ambayo Mungu ataka wafanye.
[Maelezo ya Chini]
a “Kandake” si jina bali ni jina la cheo (sawa na “Farao” na “Kaisari”) lililotumiwa kwa mfuatano wa malkia mbalimbali wa Ethiopia.
b Wageuzwa-imani walikuwa wasio-Wayahudi walioamua kushikamana na Sheria ya Kimusa.—Mambo ya Walawi 24:22.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Kwa Nini Aliitwa Towashi?
Kotekote katika simulizi la Matendo sura ya 8, yule Mwethiopia anarejezewa kuwa “towashi.” Hata hivyo, kwa kuwa Sheria ya Kimusa haikuruhusu mwanamume aliyehasiwa kuingia katika kutaniko, ni wazi kwamba mwanamume huyo hakuwa towashi katika maana halisi. (Kumbukumbu la Torati 23:1) Neno “towashi” katika Kigiriki laweza kutumiwa kwa mtu aliye na cheo cha juu. Kwa njia hiyo, huyo Mwethiopia alikuwa ofisa chini ya yule malkia wa Ethiopia.