Dumisheni Muungano Katika Siku Hizi za Mwisho
“Mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili . . . , kama mnasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili.”—WAFILIPI 1:27.
1. Kuna tofauti gani kati ya Mashahidi wa Yehova na ulimwengu?
HIZI ni “siku za mwisho.” Bila shaka, “nyakati za hatari” zipo hapa. (2 Timotheo 3:1-5) Katika “wakati [huu] wa mwisho,” wenye msukosuko wao katika jamii ya kibinadamu, Mashahidi wa Yehova hutokeza wakiwa tofauti kabisa kwa sababu ya amani na muungano wao. (Danieli 12:4) Lakini kila mtu mmoja-mmoja aliye wa familia ya tufeni pote ya waabudu wa Yehova anatakwa ajitahidi sana kudumisha muungano huo.
2. Paulo alisema nini kuhusu kudumisha muungano, na ni swali gani tutakalozungumzia?
2 Mtume Paulo alionya kwa upole Wakristo wenzake kudumisha muungano. Aliandika hivi: “Mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili ya Kristo, ili, nikija na kuwaona ninyi, au nisipokuwapo, niyasikie mambo yenu, kama mnasimama imara katika roho moja, kwa moyo mmoja mkiishindania imani ya Injili; wala hamwaogopi adui zenu, katika neno lo lote; kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ninyi ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu.” (Wafilipi 1:27, 28) Maneno ya Paulo huonyesha kwa wazi kwamba ni lazima tufanye kazi pamoja tukiwa Wakristo. Basi, ni nini kitakachotusaidia kudumisha muungano wetu wa Kikristo katika nyakati hizi zilizo ngumu?
Nyenyekea Mapenzi ya Kimungu
3. Ni wakati gani na jinsi gani wale Wasio Wayahudi wa kwanza wasiotahiriwa walikuwa wafuasi wa Kristo?
3 Njia moja ya kudumisha muungano wetu ni kunyenyekea mapenzi ya kimungu nyakati zote. Huenda hilo likataka turekebishe kufikiri kwetu. Fikiria wanafunzi Wayahudi wa mapema wa Yesu Kristo. Mtume Petro alipowahubiri kwa mara ya kwanza Wasio Wayahudi ambao hawakutahiriwa katika 36 W.K., Mungu aliwapa hao watu wa mataifa roho takatifu, nao wakabatizwa. (Matendo, sura ya 10) Kufikia wakati huo, Wayahudi, wageuzwa-imani kwenye Dini ya Kiyahudi pekee, na Wasamaria ndio waliokuwa wafuasi wa Yesu Kristo.—Matendo 8:4-8, 26-38.
4. Baada ya kueleza yale yaliyokuwa yametendeka kuhusiana na Kornelio, Petro alisema nini, na hilo lilitokeza jaribu gani kwa wanafunzi Wayahudi wa Yesu?
4 Mitume na wale ndugu wengine katika Yerusalemu walipopata kujua kuhusu kugeuzwa imani kwa Kornelio na Wasio Wayahudi wengine, walipendezwa kuisikia ripoti ya Petro. Baada ya kueleza yale yaliyokuwa yametendeka kuhusiana na Kornelio na Wasio Wayahudi wengine wenye kuamini, huyo mtume alimalizia kwa maneno haya: “Basi ikiwa Mwenyezi Mungu amewapa wao [waamini Wasio Wayahudi] karama ile ile [ya roho takatifu] aliyotupa sisi [Wayahudi] tuliomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani niweze kumpinga Mungu?” (Matendo 11:1-17) Hilo lilitokeza jaribu kwa wafuasi Wayahudi wa Yesu Kristo. Je, wangenyenyekea mapenzi ya Mungu na kuwakubali waamini Wasio Wayahudi kuwa waabudu wenzao? Au muungano wa watumishi wa Yehova wa kidunia ungekuwa hatarini?
5. Mitume na wale ndugu wengine waliitikiaje jambo la hakika kwamba Mungu alikuwa amewapa Wasio Wayahudi nafasi ya kutubu, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na mtazamo huo?
5 Simulizi hilo lasema hivi: “[Mitume na wale ndugu wengine] waliposikia hayo, waliacha ubishi [“walikubali kwa kimya,” NW] wakamtukuza Mungu wakisema, ‘Mungu amewapa watu wa mataifa mengine nafasi ya kutubu na kuwa na uzima!’” (Matendo 11:18, HNWW) Mtazamo huo ulihifadhi na kuendeleza muungano wa wafuasi wa Yesu. Punde si punde tu, kazi ya kuhubiri ikasonga mbele miongoni mwa Wasio Wayahudi, au watu wa mataifa, na baraka ya Yehova ilikuwa juu ya utendaji huo mbalimbali. Sisi wenyewe twapaswa kukubali kwa kimya wakati ushirikiano wetu unapoombwa kuhusiana na kufanyizwa kwa kutaniko jipya au rekebisho fulani la kitheokrasi linapofanywa chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Mungu. Ushirikiano wetu wa moyo wote utampendeza Yehova nao utatusaidia kudumisha muungano wetu katika siku hizi za mwisho.
Ambatana na Kweli
6. Kweli ina matokeo gani juu ya muungano wa waabudu wa Yehova?
6 Tukiwa sehemu ya familia ya waabudu wa Yehova, tunadumisha muungano kwa sababu sisi sote ‘tumefundishwa na Mungu’ nasi twashikamana sana na kweli yake iliyofunuliwa. (Yohana 6:45; Zaburi 43:3) Kwa kuwa mafundisho yetu yanategemea Neno la Mungu, sisi sote husema kwa upatano. Sisi hukubali kwa furaha chakula cha kiroho kinachotolewa na Yehova kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mathayo 24:45-47) Kufundishwa huko kunakopatana hutusaidia kudumisha muungano wetu ulimwenguni pote.
7. Sisi mmoja-mmoja tukiona ugumu wa kuelewa jambo fulani, tufanyeje, na tusifanye nini?
7 Namna gani ikiwa sisi mmoja-mmoja twaona ugumu kuelewa au kukubali jambo fulani? Twapaswa kusali ili kupata hekima na kufanya utafiti katika Maandiko na vichapo vya Kikristo. (Mithali 2:4, 5; Yakobo 1:5-8) Huenda mazungumzo pamoja na mzee yakasaidia. Ikiwa jambo hilo lingali haliwezi kueleweka, huenda ikafaa zaidi kutolihangaikia sana. Labda habari zaidi juu ya jambo hilo itatangazwa, ndipo uelewevu wetu utakapopanuliwa. Hata hivyo, lingekuwa kosa kujaribu kuwasadikisha wengine kutanikoni wakubali wazo letu wenyewe lililo tofauti. Kufanya hivyo kungekuwa kusababisha hali ya kutopatana, si kujitahidi kuhifadhi muungano. Yafaa zaidi kama nini ‘kuendelea kutembea katika kweli’ na kuwatia wengine moyo wafanye hivyo!—3 Yohana 4, NW.
8. Ni mtazamo gani kuelekea kweli unaofaa?
8 Katika karne ya kwanza, Paulo alisema hivi: “Wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana.” (1 Wakorintho 13:12) Ingawa Wakristo wa mapema hawakufahamu mambo yote, waliendelea kuwa wenye muungano. Sasa sisi tuna uelewevu wa wazi zaidi juu ya kusudi la Yehova na Neno lake la kweli. Acheni basi tushukuru kwa ajili ya kweli ambayo tumepokea kupitia ‘mtumwa mwaminifu.’ Na acheni tushukuru kwamba Yehova ametuongoza kupitia tengenezo lake. Ingawa hatujawa na kiwango kilekile cha ujuzi sikuzote, hatujawa wenye njaa kali au wenye kiu ya kiroho. Badala ya hivyo, Mchungaji wetu, Yehova, ameendelea kutuunganisha naye ametutunza vizuri.—Zaburi 23:1-3.
Utumie Ulimi Sawasawa!
9. Ulimi unaweza kutumiwaje ili kuendeleza muungano?
9 Kuutumia ulimi ili kuwatia wengine moyo ni njia ya maana ya kuendeleza muungano na roho ya udugu. Ile barua iliyosuluhisha swali juu ya tohara, kama ilivyotumwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza, ilikuwa chanzo cha kitia-moyo. Baada ya kuisoma, wanafunzi Wasio Wayahudi katika Antiokia ‘walitiwa moyo, wakafurahi.’ Yuda na Sila, waliokuwa wametumwa kutoka Yerusalemu wakiwa na barua hiyo, “walizungumza na hao ndugu kwa muda mrefu wakiwatia moyo na kuwaimarisha.” Pasipo shaka, kuwapo kwa Paulo na Barnaba pia kuliwatia moyo na kuwaimarisha ndugu wenzao katika Antiokia. (Matendo 15:1-3, 23-32, HNWW) Twaweza kufanya vivyo hivyo tunapokusanyika kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na ‘kutiana moyo’ kupitia kuwapo kwetu na maelezo yetu yenye kujenga.—Waebrania 10:24, 25, NW.
10. Ili kudumisha muungano, ni jambo gani ambalo huenda likawa lazima lifanywe iwapo hali ya kutukana inatokea?
10 Hata hivyo, matumizi mabaya ya ulimi yaweza kutisha muungano wetu. “Ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu,” akaandika mwanafunzi Yakobo. “Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana.” (Yakobo 3:5) Yehova huchukia wale wanaosababisha ugomvi. (Mithali 6:16-19) Mazungumzo hayo yaweza kusababisha ukosefu wa muungano. Basi, namna gani kukiwa na hali ya kutukana, yaani, kurundika matukano juu ya mtu fulani au kumtolea usemi wenye kutukana? Wazee watajaribu kumsaidia huyo mkosaji. Hata hivyo, mtukanaji asiyetubu apaswa kutengwa na ushirika ili amani, utaratibu, na muungano wa kutaniko uweze kudumishwa. Kwani, Paulo aliandika hivi: “Msichangamane na mtu aitwaye ndugu, akiwa ni . . . mtukanaji . . . hata kula naye.”—1 Wakorintho 5:11.
11. Kwa nini unyenyekevu ni wa maana ikiwa tumesema jambo fulani ambalo limesababisha mkazo kati yetu na mwamini mwenzetu?
11 Kuuzuia ulimi hutusaidia kudumisha muungano. (Yakobo 3:10-18) Lakini tuseme kwamba jambo fulani ambalo tumesema linasababisha mkazo kati yetu na Mkristo mwenzetu. Je, isingefaa kuchukua hatua ya kwanza katika kufanya amani na ndugu yetu, tukiomba msamaha ikiwa lazima? (Mathayo 5:23, 24) Ni kweli, jambo hilo lataka unyenyekevu, au hali ya akili ya kujishusha chini, lakini Petro aliandika hivi: “Jifungeni unyenyekevu [“hali ya akili ya kujishusha chini,” NW], mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema.” (1 Petro 5:5) Unyenyekevu utatusukuma ‘tutafute amani’ pamoja na ndugu zetu, tukikiri makosa yetu na kuomba msamaha ifaavyo. Hilo husaidia kudumisha muungano wa familia ya Yehova.—1 Petro 3:10, 11.
12. Twaweza kuutumiaje ulimi ili kuendeleza na kudumisha muungano wa watu wa Yehova?
12 Twaweza kuendeleza roho ya familia miongoni mwa wale walio katika tengenezo la Yehova tukitumia ulimi wetu sawasawa. Kwa kuwa hivyo ndivyo Paulo alivyofanya, yeye aliweza kuwakumbusha Wathesalonike hivi: “Kama mjuavyo, jinsi tulivyomwonya kila mmoja wenu kama baba awaonyavyo watoto wake mwenyewe, tukiwatia moyo na kushuhudia; ili mwenende kama ilivyo wajibu wenu kwa Mungu.” (1 Wathesalonike 2:11, 12) Akiwa ameweka kielelezo chema kuhusu jambo hili, Paulo aliweza kuwahimiza Wakristo wenzake ‘waseme kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.’ (1 Wathesalonike 5:14, NW) Ebu fikiria yale mema mengi tuwezayo kufanya kwa kuutumia ulimi ili kuwaliwaza, kuwatia moyo, na kuwajenga wengine. Ndiyo, “neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!” (Mithali 15:23) Zaidi ya hayo, usemi wa aina hiyo husaidia kuendeleza na kudumisha muungano wa watu wa Yehova.
Uwe Mwenye Kusamehe!
13. Kwa nini tuwe wenye kusamehe?
13 Kumsamehe mtu aliyefanya jambo la kuudhi ambaye ameomba msamaha ni jambo la maana ikiwa tutadumisha muungano wa Kikristo. Na twapaswa kusamehe mara nyingi kadiri gani? Yesu alimwambia Petro hivi: “Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.” (Mathayo 18:22) Ikiwa sisi ni watu wasiosamehe, tunapinga masilahi yetu wenyewe. Jinsi gani? Uhasama na kufungia moyoni kinyongo kutatunyang’anya amani ya akili. Na tukijulikana kuwa wakatili na wasiosamehe, huenda tukajiletea hali ya kutengwa na wengine. (Mithali 11:17) Kuweka kinyongo hakumpendezi Mungu na kwaweza kuongoza kwenye dhambi nzito. (Mambo ya Walawi 19:18) Kumbuka kwamba Yohana Mbatizaji alikatwa kichwa kwa sababu ya njama aliyokula Herodia mwovu, aliyekuwa “akifungia moyoni kinyongo” dhidi yake.—Marko 6:19-28, NW.
14. (a) Mathayo 6:14, 15 hutufundisha nini kuhusu msamaha? (b) Je, tungoje ombi la msamaha sikuzote kabla ya kumsamehe mtu?
14 Sala ya kigezo ya Yesu inatia ndani maneno haya: “Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila tumwiaye.” (Luka 11:4) Ikiwa sisi ni watu wasiosamehe, kuna hatari kwamba siku fulani Yehova Mungu hatatusamehe dhambi zetu tena, kwa maana Yesu alisema hivi: “Mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Basi msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.” (Mathayo 6:14, 15) Kwa hiyo tukitaka kwelikweli kufanya sehemu yetu katika kudumisha muungano katika familia ya waabudu wa Yehova, tutakuwa wenye kusamehe, labda tukisahau tu jambo lenye kuudhi ambalo huenda likawa limesababishwa na hali ya kutofikiri na lisilokuwa na nia yoyote mbovu. Paulo alisema hivi: “Mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi.” (Wakolosai 3:13) Tunapokuwa wenye kusamehe, tunasaidia kudumisha muungano wenye thamani wa tengenezo la Yehova.
Muungano na Maamuzi ya Kibinafsi
15. Ni jambo gani ambalo huwasaidia watu wa Yehova kudumisha muungano wanapofanya maamuzi ya kibinafsi?
15 Mungu alituumba tuwe viumbe vyenye uhuru wa kujichagulia mwendo tunaotaka kufuata tukiwa na pendeleo na daraka la kufanya maamuzi ya kibinafsi. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20; Wagalatia 6:5) Hata hivyo, twaweza kudumisha muungano wetu kwa sababu tunatii sheria na kanuni za Biblia. Tunazifikiria tunapofanya maamuzi ya kibinafsi. (Matendo 5:29; 1 Yohana 5:3) Tuseme swali latokea kuhusu kutokuwamo. Twaweza kufanya uamuzi wa kibinafsi wenye maarifa kwa kukumbuka kwamba sisi “si wa ulimwengu” na kwamba ‘tumefua panga zetu ziwe majembe.’ (Yohana 17:16; Isaya 2:2-4) Vivyo hivyo, tunapolazimika kufanya uamuzi wa kibinafsi kuhusu uhusiano wetu na Serikali, tunachunguza yale yanayosemwa na Biblia kuhusu kumrudishia “Mungu vilivyo vyake,” huku tukijitiisha wenyewe kwa “mamlaka zilizo kubwa” katika mambo ya kilimwengu. (Luka 20:25, HNWW; Warumi 13:1-7, NW; Tito 3:1, 2) Ndiyo, kuzifikiria sheria na kanuni za Biblia tunapofanya maamuzi ya kibinafsi husaidia kudumisha muungano wetu wa Kikristo.
16. Twaweza kusaidiaje kudumisha muungano tunapofanya maamuzi ambayo si sawa wala si kosa Kimaandiko? Toa kielezi.
16 Twaweza kusaidia kudumisha muungano wa Kikristo hata tunapofanya uamuzi ulio wa kibinafsi kabisa na ambao si sawa wala si kosa Kimaandiko. Jinsi gani? Kwa kuonyesha ufikirio wenye upendo kwa wengine ambao huenda wakaathiriwa na uamuzi wetu. Ili kutoa kielezi: Katika lile kutaniko katika Korintho la kale, swali lilitokea kuhusu nyama iliyotolewa ikiwa dhabihu kwa sanamu. Bila shaka, Mkristo asingeshiriki katika sherehe ya ibada ya sanamu. Hata hivyo, haikuwa dhambi kula masalio ya nyama ya aina hiyo yenye kuondolewa damu ifaavyo, iliyouzwa katika soko la watu wote. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 10:25) Lakini, dhamiri za Wakristo fulani zilisumbuliwa juu ya kula nyama hiyo. Kwa hiyo Paulo aliwahimiza Wakristo wengine waepuke kuwakwaza hao. Kwa kweli, aliandika hivi: “Chakula kikimkwaza ndugu yangu, hakika sitakula nyama hata milele, nisije nikamkwaza ndugu yangu.” (1 Wakorintho 8:13) Kwa hiyo hata ikiwa hakuna sheria au kanuni fulani ya Biblia inayohusika, ni jambo lionyeshalo upendo kama nini kuwafikiria wengine tunapofanya maamuzi ya kibinafsi ambayo yangeweza kuathiri muungano wa familia ya Mungu!
17. Ni jambo gani ambalo lafaa kufanywa inapokuwa lazima tufanye maamuzi ya kibinafsi?
17 Tusipokuwa na uhakika juu ya hatua ya kuchukua, ni jambo la hekima kuamua kwa njia inayotuacha tukiwa na dhamiri safi, na wengine wapaswa kustahi uamuzi wetu. (Warumi 14:10-12) Bila shaka, inapokuwa lazima tufanye uamuzi wa kibinafsi, twapaswa kuutafuta mwongozo wa Yehova katika sala. Sawa na mtunga-zaburi, twaweza kusali hivi kwa uhakika: “Unitegee sikio lako. . . . Ndiwe genge langu na ngome yangu; kwa ajili ya jina lako uniongoze, unichunge.”—Zaburi 31:2, 3.
Dumisheni Muungano wa Kikristo Sikuzote
18. Paulo alitoaje kielezi cha muungano wa kutaniko la Kikristo?
18 Katika 1 Wakorintho sura ya 12, Paulo alitumia mwili wa kibinadamu ili kutoa kielezi cha muungano wa kutaniko la Kikristo. Alikazia kutegemeana na umaana wa kila mshiriki. “Kama vyote vingekuwa kiungo kimoja, mwili ungekuwa wapi?” akauliza Paulo. “Lakini sasa viungo ni vingi, ila mwili ni mmoja. Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi.” (1 Wakorintho 12:19-21) Vivyo hivyo, sote katika familia ya waabudu wa Yehova hatufanyi kazi ileile. Lakini, tuna muungano, nasi twahitajiana.
19. Twaweza kunufaikaje na maandalizi ya Mungu ya kiroho, na ndugu mmoja mwenye umri mkubwa alisemaje kuhusu hilo?
19 Sawa na vile mwili huhitaji chakula, utunzi, na mwelekezo, sisi twahitaji maandalizi ya kiroho ambayo Mungu hutupa sisi kupitia Neno, roho, na tengenezo lake. Ili kunufaika na maandalizi hayo, ni lazima tuwe sehemu ya familia ya Yehova ya kidunia. Baada ya miaka mingi katika utumishi wa Mungu, ndugu mmoja aliandika hivi: “Nashukuru sana kwamba nimeishi kulingana na ujuzi wa makusudi ya Yehova tangu siku zile za mapema kabla tu ya 1914 wakati ambapo yote hayakuwa wazi sana . . . hadi siku hii ambapo kweli yang’aa kama vile jua la adhuhuri. Ikiwa kuna jambo moja ambalo limekuwa la maana zaidi kwangu, limekuwa lile la kuendelea kuwa karibu na tengenezo la Yehova lionekanalo. Ono langu la mapema lilinifundisha jinsi lisivyo jambo la hekima kutegemea kusababu kwa kibinadamu. Mara akili yangu ilipofanya uamuzi juu ya jambo hilo, niliazimia kukaa karibu na hili tengenezo jaminifu. Mtu aweza kwa njia gani nyingine kupata upendeleo na baraka ya Yehova?”
20. Tuazimie kufanya nini kuhusu muungano wetu tukiwa watu wa Yehova?
20 Yehova amewaita watu wake kutoka katika giza la kilimwengu na ukosefu wa muungano. (1 Petro 2:9) Ametuingiza katika muungano wenye baraka pamoja naye mwenyewe na pamoja na waamini wenzetu. Muungano huo utakuwamo katika mfumo mpya wa mambo ulio karibu sana sasa. Basi katika siku hizi za mwisho za hatari, acheni tuendelee ‘kujivika upendo’ na kufanya kila tuwezalo ili kuendeleza na kudumisha muungano wetu wenye thamani.—Wakolosai 3:14.
Ungejibuje?
◻ Kwa nini kufanya mapenzi ya Mungu na kuambatana na kweli kutatusaidia kudumisha muungano?
◻ Muungano unahusianaje na matumizi yafaayo ya ulimi?
◻ Ni jambo gani linalohusika katika kuwa watu wenye kusamehe?
◻ Twaweza kudumishaje muungano tunapofanya maamuzi ya kibinafsi?
◻ Kwa nini muungano wa Kikristo udumishwe?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Sawa na vile mchungaji huyu awekavyo kundi lake likiwa pamoja, ndivyo Yehova awekavyo watu wake wakiwa na muungano
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kwa kuomba msamaha kwa unyenyekevu tunapofanya jambo lenye kuudhi, tunasaidia kuendeleza muungano