Yale Ambayo Viumbe “Vyenye Hekima ya Kisilika” Vyaweza Kutufundisha
UTHIBITI-HALIJOTO, kizuia-ugandaji, kuondoa chumvi katika maji ya bahari, na sona ni mavumbuzi ambayo yamekuja kujulikana sana na wanadamu katika karne ya 20. Hata hivyo, yalikuwapo katika ulimwengu wa wanyama maelfu ya miaka mapema. Ndiyo, wanadamu hufaidika kwa kuvichunguza viumbe hivyo “vyenye hekima ya kisilika.” (Mithali 30:24-28; Ayubu 12:7-9, linganisha NW.) Yaonekana kwamba wanyama fulani wamekuwa walimu wasiosema wa wanadamu, nasi twaweza kupata upendezi mkubwa kwa kuwachunguza.
Je, twaweza kufaidika kwa kufikiria vitabia vya wanyama fulani? Yesu Kristo aliwafananisha wafuasi wake na kondoo, nyoka, njiwa, na hata nzige. Alikuwa akifikiria nini alipowafananisha wafuasi wake na viumbe hivyo? Acheni tuone.
“Kondoo Wangu Waisikia Sauti Yangu”
Kondoo hutajwa katika Biblia zaidi ya mara 200. Kama ielezavyo Smith’s Bible Dictionary, “kondoo ni mfano wa upole, subira, na unyenyekeo.” Katika Isaya sura ya 53, Yesu mwenyewe alifananishwa kiunabii na kondoo. Yafaa kama nini kwamba awalinganishe wafuasi wake na mnyama huyohuyo! Lakini ni sifa zipi hasa za kondoo ambazo Yesu alikuwa akifikiria?
“Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata,” akasema Yesu. (Yohana 10:27) Kwa njia hiyo alikazia upole wa wanafunzi wake na hamu yao ya kumfuata. Kondoo halisi humsikiliza mchungaji wao na wako tayari kumfuata. Pia mchungaji ana ushikamano wa karibu na kundi la kondoo.
Kundi la kondoo laweza kuwa limetawanyika malishoni likila nyasi, lakini kila kondoo huendelea kuwa na muungano pamoja na kundi zima. Kwa njia hiyo, hao wanyama wahisipo hawana usalama au wakiwa na woga, “wao waweza kujikusanya pamoja upesi,” chasema kitabu Alles für das Schaf (Kila Jambo Kwa Ajili Ya Kondoo). Kondoo wakitoroka ili kuponyoka hatari, wao hufanya hivyo wakiwa kundi, wakitua nyakati fulani-fulani ili kuchunguza hali tena. “Kukimbia hatua kwa hatua huwezesha wana-kondoo na wanyama dhaifu zaidi kwenda sambamba. Kundi hilo la mifugo hata huwatolea ulinzi wa pekee.” Twaweza kujifunza nini kutokana na mwenendo huo?
Wakristo wa kweli leo hawatawanyiki miongoni mwa madhehebu na mafarakano ya Jumuiya ya Wakristo. Badala ya hivyo, wamekusanyika katika kundi moja la kondoo. Kila Mkristo huhisi ushikamano wa kibinafsi na kundi hili la Mungu, na huo huchangia muungano wa tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Tatizo litokeapo wakati wowote—liwe ni ugonjwa mbaya, vita, au msiba wa kiasili—kila mwabudu hutafuta mwongozo na ulinzi wapi? Katika tengenezo la Yehova, ambalo hutoa usalama wa kiroho.
Shauri la Biblia hupatikanaje? Kupitia vichapo kama Mnara wa Mlinzi na jarida-jenzi lalo Amkeni! Magazeti hayo na mikutano ya Kikristo hata hutoa msaada wa pekee kwa wale wanaohitaji utunzaji wa ziada, kama wana-kondoo na kondoo dhaifu zaidi katika kundi. Kwa mfano, uangalifu hutolewa kwa wazazi walio peke yao na wale wanaoteseka na hali ya mshuko-moyo. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kama nini kusoma kila gazeti, kuhudhuria kila mkutano wa kutaniko, na kutumia yale tunayojifunza! Kwa njia hiyo sisi huonyesha upole na ushikamano wenye nguvu na kundi la Mungu.—1 Petro 5:2.
“Wenye Hadhari Kama Nyoka na Bado Kuwa Wasio na Hatia Kama Njiwa”
Kamusi Smith’s Bible Dictionary yasema hivi: “Kotekote Mashariki nyoka alitumiwa kuwa mfano wa kanuni mbovu, ya roho ya kuasi.” Kwa upande mwingine, “njiwa wangu” ulikuwa usemi wa mapenzi. (Wimbo Ulio Bora 5:2, NW) Basi, Yesu alikuwa akifikiria nini, alipowatia moyo wafuasi wake wawe “wenye hadhari kama nyoka na bado kuwa wasio na hatia kama njiwa”?—Mathayo 10:16, NW.
Yesu alikuwa akitoa maagizo kwa ajili ya kuhubiri na kufundisha. Wanafunzi wake wangeweza kutarajia maitikio tofautitofauti. Wachache wangeonyesha upendezi, hali wengine wangekataa habari njema. Watu fulani hata wangenyanyasa watumishi hao wa kweli wa Mungu. (Mathayo 10:17-23) Wanafunzi walipaswa waitikieje mnyanyaso?
Katika Das Evangelium des Matthäus (Gospeli ya Mathayo), Fritz Rienecker asema hivi kuhusu Mathayo 10:16: “Busara . . . lazima iambatane na uaminifu-maadili, moyo mweupe, na unyoofu, chochote kisije kikatokea na kuwapa maadui sababu halali za kulalamika. Mabalozi wa Yesu wamo miongoni mwa wapinzani wakatili, wasioonyesha ufikirio na washambuliao mitume bila huruma na wapatapo fursa yoyote ndogo. Kwa hiyo, ni lazima—sawa tu na nyoka—kufuliza kuwa waangalifu sana juu ya wapinzani, na kuiangalia hali tena na tena, macho na hisi zikiwa tayari; kuweza kuidhibiti hali bila kutumia ujanja au udanganyifu, kuwa safi na wanyoofu katika neno na tendo na kwa njia hiyo kujithibitisha kuwa kama njiwa.”
Watumishi wa Mungu wa siku ya kisasa waweza kujifunza nini kutokana na maneno ya Yesu yanayopatikana kwenye Mathayo 10:16? Leo, watu huitikia habari njema kwa njia sawa na ile waliyoitikia katika karne ya kwanza. Wakabiliwapo na mnyanyaso, Wakristo wa kweli wahitaji kuunganisha busara ya nyoka na usafi wa njiwa. Wakristo hawatumii kamwe udanganyifu au ukosefu wa haki wala hawana ufisadi, wao ni wa kweli, na hufuatia haki watangaziapo wengine ujumbe wa Ufalme.
Ili kutoa kielezi: Wafanyakazi wenzi kazini, vijana shuleni, au hata washiriki wa familia yako mwenyewe huenda wakasema mambo yenye kuumiza juu ya itikadi zako ukiwa Shahidi wa Yehova. Itikio la mara moja huenda likawa kuitikia kwa njia iyo hiyo kwa kuwa mwenye kuumiza vivyo hivyo juu ya imani yao. Lakini je, hiyo humaanisha kuwa bila hatia? Bila shaka la. Ukiwaonyesha wanaokuchambua kuwa yale wasemayo hayana athari yoyote juu ya mwenendo wako wenye kupendeza, huenda wao wakabadilika tu na kuwa wazuri. Ndipo ungekuwa mwenye busara na bila lawama—‘mwenye hadhari kama nyoka, na bado asiye na hatia kama njiwa.’
‘Nzige Walikuwa Kama Farasi Waliowekwa Tayari kwa Vita’
Gazeti GEO laripoti kwamba katika 1784, Afrika Kusini ilishambuliwa na “kundi kubwa zaidi [la nzige] ambalo limepata kuandikishwa katika historia iliyorekodiwa.” Kundi hilo lilifunika eneo la kilometa 5,200 za mraba, eneo ambalo ukubwa walo ni mara tano zaidi ya ule wa Hong Kong. Kamusi Smith’s Bible Dictionary yasema kwamba nzige “huharibu sana mimea katika nchi wanamoenda.”
Katika ufunuo wake aliopewa na Mungu wa mambo ambayo yangetendeka katika “siku ya Bwana,” Yesu alitumia njozi ya kundi la nzige. Ilisemwa hivi kuwahusu: ‘Walikuwa kama farasi waliowekwa tayari kwa vita.’ (Ufunuo 1:1, 10; 9:3-7) Ufananisho huo ulikuwa na maana gani?
Kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wameelewa kwamba wale nzige wa Ufunuo sura ya 9 huwakilisha watumishi watiwa-mafuta wa Mungu walio duniani katika karne hii.a Wakristo hao wamegawiwa kazi mahususi—kuhubiri ujumbe wa Ufalme duniani pote na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Hilo hutaka washinde vizuizi na kudumu katika kazi yao. Ni nini ambacho kingeweza kutolea jambo hilo kielezi vizuri zaidi kuliko nzige wasioshindwa?
Ingawa nzige si mrefu sana zaidi ya sentimeta tano, yeye husafiri kwa ukawaida umbali wa kati ya kilometa 100 na kilometa 200 kwa siku. Nzige wa jangwani huenda hata akafikia umbali wa kilometa 1000. Gazeti GEO laeleza kwamba “mabawa yake hupepea mara 18 kwa sekunde moja na kwa muda upatao saa 17 kwa siku—jambo ambalo hakuna mdudu mwingine yeyote awezaye kufanya.” Ni kazi kubwa kama nini kwa kiumbe hicho kidogo!
Wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova wako imara katika kueneza habari njema ya Ufalme. Sasa wanahubiri katika mabara zaidi ya 230. Watumishi hao wa Mungu hushinda magumu mengi ili kushiriki katika kuitimiza hiyo kazi. Wao hukabili matatizo ya aina gani? Ubaguzi, vizuizi vya kisheria, magonjwa, kuvunjika moyo, na upinzani kutoka kwa watu wa ukoo ni mambo machache tu. Lakini hakuna lolote ambalo limeweza kuzuia maendeleo yao. Wao hushikamana na kazi yao yenye kupewa na Mungu.
Endeleeni Kuonyesha Sifa za Kikristo
Ndiyo, Yesu aliwafananisha wafuasi wake na kondoo, nyoka, njiwa, na nzige. Hilo kwa kweli lafaa katika siku yetu. Kwa nini? Kwa kuwa mwisho wa mfumo huu wa mambo wakaribia, na matatizo yanazidi kukandamiza kuliko wakati mwingine wowote.
Wakifikiria maneno yenye kutoa kielezi ya Yesu, Wakristo wa kweli huendelea kushikamana na kundi la Mungu na hukubali shauri kwa upole kutoka tengenezo la Yehova. Wao hulinda na wako macho kuona hali ambazo zingeweza kuzuia utendaji wao wa Kikristo, huku wakibaki bila lawama katika mambo yote. Zaidi ya yote, wao hudumu katika kufanya mapenzi ya Mungu wakabilipo vizuizi. Nao huendelea kujifunza kutoka kwa viumbe fulani “vyenye hekima ya kisilika.”
[Maelezo ya Chini]
a Ona Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., sura ya 22.