Kweli Juu ya Yesu
YAONEKANA hakuna mwisho wa nadharia na makisio juu ya Yesu alikuwa nani na alitimiza nini. Lakini vipi juu ya Biblia yenyewe? Yatuambia nini juu ya Yesu Kristo?
Isemayo Biblia
Kwa kuisoma Biblia kwa uangalifu, utaona mambo haya makuu ya hakika:
◻ Yesu ndiye Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.—Yohana 3:16; Wakolosai 1:15.
◻ Mileani mbili hivi zilizopita, Mungu aliuhamisha uhai wa Yesu hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi apate kuzaliwa akiwa binadamu.—Mathayo 1:18; Yohana 1:14.
◻ Yesu hakuwa mtu mwema tu. Katika kila jambo alikuwa mrudisho mwaminifu wa utu mzuri wa Baba yake, Yehova Mungu.—Yohana 14:9, 10; Waebrania 1:3.
◻ Wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu alishughulikia kwa upendo mahitaji ya walioonewa. Aliwaponya wagonjwa kimuujiza na hata alifufua wafu.—Mathayo 11:4-6; Yohana 11:5-45.
◻ Yesu alipiga mbiu ya Ufalme wa Mungu kuwa ndio tumaini pekee la ubinadamu wenye taabu, naye aliwazoeza wanafunzi wake waendelee na kazi hii ya kuhubiri.—Mathayo 4:17; 10:5-7; 28:19, 20.
◻ Kwenye Nisani 14 (Aprili 1 hivi), mwaka wa 33 W.K., Yesu alikamatwa, akafanyiwa kesi, akahukumiwa, na kufishwa kwa shtaka lisilo la kweli la uchochezi.—Mathayo 26:18-20; 48–27:50.
◻ Kifo cha Yesu hutumika kikiwa fidia, inayowaweka huru wanadamu waaminio na hali yao yenye dhambi na hivyo ikifungua njia kwenye uhai wa milele kwa wote wanaodhihirisha imani katika yeye.—Warumi 3:23, 24; 1 Yohana 2:2.
◻ Kwenye Nisani 16, Yesu alifufuliwa, na muda mfupi baadaye akapaa kurudi mbinguni apate kumlipa Babaye thamani ya fidia ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu.—Marko 16:1-8; Luka 24:50-53; Matendo 1:6-9.
◻ Akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi wa Yehova, Yesu aliyefufuliwa ana mamlaka kamili ya kutekeleza kusudi la awali la Mungu kwa mwanadamu.—Isaya 9:6, 7; Luka 1:32, 33.
Hivyo, Biblia humtokeza Yesu kuwa mwenye fungu kubwa katika utimizo wa makusudi ya Mungu. Lakini waweza kuwaje na uhakika kwamba huyo ndiye Yesu halisi—Yesu wa kihistoria, aliyezaliwa Bethlehemu akatembea juu ya dunia hii miaka 2,000 hivi iliyopita?
Msingi wa Uhakika
Shaka nyingi zaweza kuondolewa kwa kusoma tu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ukiwa na akili isiyo na upendeleo. Kwa kufanya hivyo utapata kwamba simulizi la Biblia si simulizi la kijuujuu la matukio, kama zilivyo ngano. Badala ya hivyo, majina, nyakati hususa, na sehemu kamili zatajwa. (Kwa kielelezo, ona Luka 3:1, 2.) Zaidi ya hayo, wanafunzi wa Yesu wanaonyeshwa kuwa wenye ufuatiaji wa haki wa pekee, wakiwa na unyoofu ambao humpa msomaji uhakika. Waandikaji hawakupumbaza akili ya yeyote—wala yao wenyewe—wakijaribu kufanyiza rekodi yenye uaminifu. Ndiyo, utaona kwamba Biblia ina kweli.—Mathayo 14:28-31; 16:21-23; 26:56, 69-75; Marko 9:33, 34; Wagalatia 2:11-14; 2 Petro 1:16.
Bado kuna mengine zaidi. Mavumbuzi ya kiakiolojia yamehakikisha tena na tena rekodi ya Biblia. Kwa kielelezo, ukizuru Jumba la Kuhifadhi Vitu vya Kale la Israel katika Yerusalemu, waweza kuona jiwe lenye maandishi yanayomtaja Pontio Pilato. Mavumbuzi mengine ya kiakiolojia yahakikisha Lisaniasi na Sergio Paulo, ambao Biblia hutaja, kuwa watu halisi badala ya viumbe waliobuniwa na Wakristo wa mapema. Matukio yaliyoripotiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (Agano Jipya) yapata uhakikisho mwingi katika marejezo ya waandikaji wa zamani, kutia na Juvenal, Takito, Seneka, Suetonio, Plini Mchanga, Lusiani, Selso, na mwanahistoria Myahudi Yosefo.a
Masimulizi yaliyo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalikubaliwa kwa utayari na maelfu ya watu walioishi katika karne ya kwanza. Hata maadui wa Ukristo hawakukana ukweli wa yale ambayo Yesu aliripotiwa kuwa alisema au kufanya. Juu ya uwezekano wa kwamba utu wa Yesu uliongezewa uzuri na wanafunzi wake baada ya kifo chake, Profesa F. F. Bruce aeleza hivi: “Bila shaka haingewezekana, kama waandikaji fulani waonekanavyo kufikiri, kubuni kwa urahisi hivyo maneno na matendo ya Yesu katika miaka hiyo ya mapema, wakati ambapo wengi wa wanafunzi Wake walikuwa wangali hai, ambao wangeweza kukumbuka yale yaliyokuwa yametendeka na yale ambayo hayakuwa yametendeka. . . . Wanafunzi hawangeweza kuthubutu kufanya makosa (sembuse kubadilishwa kwa kukusudiwa kwa mambo ya hakika), ambayo yangefichuliwa mara moja na wale ambao wangefurahia zaidi kufanya hivyo.”
Sababu Inayowafanya Wasiamini
Hata hivyo, wasomi fulani wangali wakitilia shaka. Huku wakidhania kwamba rekodi za Kibiblia ni za kubuniwa, wanachunguza kwa hamu maandishi ya kiapokrifa na kuyakubali kuwa yenye ustahilifu! Kwa nini? Kwa wazi, rekodi ya Biblia ina mambo ambayo wenye akili wengi wa kisasa hawataki kuamini.
Katika kitabu chake Union Bible Companion, kilichochapishwa katika 1871, S. Austin Allibone aliwasai wenye kutilia shaka. Aliandika hivi: “Muulize yeyote anayedai kutilia shaka kweli ya historia ya Gospeli ana sababu gani ya kuamini kwamba Kaisari alifia Capitol, au kwamba Maliki Charlemagne alitawazwa kuwa Maliki wa Magharibi na Papa Leo 3. katika mwaka wa 800? . . . Sisi huamini madai yote yenye nguvu . . . yaliyofanywa juu ya watu hao; na ni kwa sababu tuna uthibitisho wa kihistoria wa kweli yao. . . . Ikiwa, kwa kutolewa kwa ithibati kama hiyo, wowote wangali wanakataa kuamini, twawaachia mbali kuwa ni wapumbavu waliopotoka au mabaradhuli wasiofaa kitu. Basi, tusemeje juu ya wale ambao, licha ya uthibitisho mwingi ambao umetolewa sasa wa uasilia wa Maandiko Matakatifu, wanadai kuwa hawajasadikishwa? . . . Hawataki kuamini lile linalonyenyekeza kiburi chao, na litakalowalazimisha waishi maisha tofauti.”
Ndiyo, baadhi ya wanaotilia shaka wana makusudio mengine katika kukataa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Tatizo walilo nalo si ustahilifu wayo bali viwango vyayo. Kwa kielelezo, Yesu alisema hivi juu ya wafuasi wake: “Wao si wa ulimwengu, kama mimi nisivyo wa ulimwengu.” (Yohana 17:14) Hata hivyo, Wakristo wengi wa kudai wanahusika kwa kina katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu, hata wanahusika katika vita vyenye kumwaga damu. Badala ya kujipatanisha na viwango vya Biblia, watu wengi wangependelea Biblia ipatane na viwango vyao wenyewe.
Fikiria pia maadili. Yesu alitolea kutaniko la Thiatira shauri lenye nguvu kwa sababu ya kuvumilia zoea la uasherati. “Mimi ndiye achunguzaye viuno [“mafigo,” NW] na mioyo,” aliwaambia, “nami nitampa kila mmoja wenu kwa kadiri ya matendo yake.”b (Ufunuo 2:18-23) Hata hivyo, je, si kweli kwamba watu wengi wanaodai kuwa Wakristo hukataa viwango vya kiadili? Wangeona afadhali wakatae aliyosema Yesu badala ya kukataa mwendo wao usio wa adili.
Wakiwa na mwelekeo wa kutomkubali Yesu wa Biblia, wasomi wameumba Yesu wa mawazo yao wenyewe. Wanakuja kuwa na hatia ya kule kutunga ngano ambako wanawashtaki isivyo kweli waandikaji wa Gospeli. Wanashikilia sehemu za maisha ya Yesu wanazotaka kukubali, wanakataa zile nyingine, na kuongeza mambo yao wenyewe madogo-madogo. Kihalisi, mtu wao mwenye hekima anayezurura au mwanamapinduzi wa kijamii siye Yesu wa kihistoria wanayedai kumtafuta; badala ya hivyo, yeye ni ubuni tu wa mawazo ya kisomi yenye kiburi.
Kumpata Yesu Halisi
Yesu alijitahidi kuamsha mioyo ya wale wenye njaa yenye moyo mweupe ya kupata kweli na uadilifu. (Mathayo 5:3, 6; 13:10-15) Hao huitikia mwaliko huu wa Yesu: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:28-30.
Yesu halisi hapatikani katika vitabu vilivyoandikwa na wasomi wa kisasa; wala hapatikani katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo yamekuwa mahali pa kusitawishia desturi za kufanyizwa na mwanadamu. Waweza kumpata Yesu wa kihistoria katika nakala yako ya Biblia. Je, ungependa kujifunza mengi zaidi juu yake? Mashahidi wa Yehova wangefurahi kukusaidia ufanye hivyo.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa habari zaidi, ona Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, sura ya 5, ukurasa wa 55 hadi wa 70, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Katika Biblia, nyakati nyingine mafigo huwakilisha mawazo na hisia-moyo za mtu zenye kina zaidi.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
KARNE NYINGI ZA UCHAMBUZI
Uchambuzi wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ulianza miaka zaidi ya 200 iliyopita, mwanafalsafa Mjerumani Hermann Samuel Reimarus (1694-1768) alipodai kwa nguvu hivi: “Tuna haki ya kufanya tofauti kabisa kati ya mafundisho ya Mitume katika maandishi yao na yale ambayo Yesu Mwenyewe alipiga mbiu na kufundisha maishani Mwake mwenyewe.” Kuanzia na Reimarus, wasomi wengi wamefundishwa kuhisi vivyo hivyo.
Kitabu The Real Jesus chasema kwamba wachambuzi wengi wa wakati uliopita hawakujiona kuwa waasi-imani. Badala ya hivyo, “walijitambua kuwa Wakristo wa kweli kwa maana walikuwa wamejiweka huru kutokana na vizuizi vya mfumo wa itikadi na ushirikina.” Walihisi kwamba uhakiki ulikuwa “aina ya Ukristo iliyotakatishwa.”
Jambo la hakika lenye kuhuzunisha ni kwamba Jumuiya ya Wakristo imekuwa mahali pa kukuzia desturi za mwanadamu. Mafundisho ya nafsi isiyoweza kufa, Utatu, na helo yenye moto ni baadhi tu ya mafundisho yanayopingana na Biblia. Lakini waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hawakusababisha ufisadi huo wa kweli. Kwa kinyume, walipigana na dalili za kwanza za mafundisho yasiyo ya kweli katikati ya karne ya kwanza, Paulo alipoandika kwamba uasi-imani miongoni mwa wale wanaodai kuwa Wakristo ulikuwa ‘sasa unatenda kazi.’ (2 Wathesalonike 2:3, 7) Twaweza kuwa na uhakika kwamba yaliyomo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ni rekodi ya kweli ya kihistoria na ya kimafundisho.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
GOSPELI ZILIANDIKWA LINI?
Wachambuzi wengi wa Agano Jipya wanasisitiza kwamba Gospeli ziliandikwa muda mrefu baada ya matukio zinayofafanua na kwa hiyo yaelekea lazima ziwe na makosa.
Hata hivyo, uthibitisho wadokeza tarehe ya mapema zaidi ya kuandikwa kwa Mathayo, Marko, na Luka. Maneno ya utangulizi katika nakala kadhaa za hati za Mathayo zaonyesha kwamba uandikaji wa awali ulitukia mapema wapata mwaka wa 41 W.K. Yawezekana kwamba Gospeli ya Luka iliandikwa kati ya mwaka wa 56 na 58 W.K., kwa maana kitabu cha Matendo (yamkini kilichomalizwa kufikia 61 W.K.) chaonyesha kwamba mwandikaji, Luka, tayari alikuwa ameandika “kitabu [chake] kile cha kwanza,” ile Gospeli. (Matendo 1:1) Gospeli ya Marko yafikiriwa kuwa iliandikwa katika Roma wakati wa kufungwa kwa mtume Paulo ama kwa kwanza ama kwa pili—labda kati ya mwaka wa 60 na 65 W.K.
Profesa Craig L. Blomberg akubaliana na kuwekewa tarehe kwa mapema zaidi kwa Gospeli hizo. Yeye aona kwamba hata tuongezapo Gospeli ya Yohana, iliyoandikwa mwishoni mwa karne ya kwanza, “tungali karibu zaidi na matukio ya awali kuliko wasifu mwingi wa kale. Kwa kielelezo, waandikaji wawili wa wasifu wa mapema zaidi wa Aleksanda Mkubwa, Arrian na Plutarch, waliandika miaka zaidi ya mia nne baada ya kifo cha Aleksanda katika 323 K.W.K., na bado wanahistoria kwa ujumla huyaona kuwa yenye kutumainika. Hekaya zilizotiliwa chumvi juu ya maisha ya Aleksanda zilisitawi kadiri muda ulivyopita, lakini nyingi za hekaya hizo zilisitawi wakati wa zile karne nyingi baada ya waandikaji hao wawili.” Sehemu za kihistoria za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo bila shaka zinastahili angalau kuaminiwa kadiri ileile ambavyo historia za kilimwengu zaaminiwa.
[Picha katika ukurasa wa 8]
Kutakuwa na shangwe nyingi sana kwa wote katika Paradiso ya kidunia inayokuja