Jambo Kuu Maishani Mwako Ni Nini?
“Unijulishe njia nitakayoiendea.”—ZABURI 143:8.
1. Mfalme Solomoni alifikia mkataa gani juu ya ufuatiaji mbalimbali wa kibinadamu na mambo yanayotimizwa?
LABDA wewe wafahamu kwamba maisha yamejaa utendaji mbalimbali na mahangaiko. Uyafikiriapo, waweza kuona kwamba baadhi yayo si muhimu. Utendaji na mahangaiko mengine si ya maana sana au hata huwa ya ubatili. Jambo la kwamba unatambua hilo lamaanisha una upatano na mmoja wa watu wenye hekima zaidi, Mfalme Solomoni. Baada ya kupitia kwa ukamili utendaji mbalimbali wa maisha, yeye alifikia mkataa huu: “Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.” (Mhubiri 2:4-9, 11; 12:13) Hilo lina umaana gani kwetu leo?
2. Watu wenye kumhofu Mungu wapaswa kujiuliza swali gani la msingi, hilo likiongoza kwenye maswali gani yanayohusiana na hilo?
2 Ikiwa wataka ‘kumcha Mungu na kuzishika amri zake,’ jiulize swali hili lenye kuvutia, ‘Jambo kuu maishani mwangu ni nini?’ Ni kweli, huenda usilifikirie kwa uzito swali hilo kila siku, lakini kwa nini usilifikirie sasa? Kwa hakika, hilo lakumbusha maswali fulani yanayohusiana na hilo, kama, ‘Je, huenda nikawa nakaza fikira isivyofaa juu ya kazi yangu au maishilio yangu au vitu vya kimwili? Nyumba yangu, familia yangu, na wapendwa wangu wana umaana gani maishani mwangu?’ Huenda kijana akauliza hivi, ‘Elimu huvuta uangalifu na wakati wangu kadiri gani? Kwa kweli, je, napendezwa hasa na hobi, mchezo, au namna fulani ya vitumbuizo au tekinolojia?’ Na hata umri wetu au hali yetu iwe ni nini, twapaswa kujiuliza kwa kufaa, ‘Kumtumikia Mungu kuna sehemu gani maishani mwangu?’ Yamkini ungekubali uhitaji wa kupanga mambo ya kutangulizwa. Lakini ni jinsi gani na ni wapi tuwezapo kupata msaada ili kuyapanga kwa hekima?
3. Kupanga mambo ya kutangulizwa kwahusisha nini kwa Wakristo?
3 “Kuu” lina maana ya msingi ya jambo linalotangulia mambo yote mengine au linalohitaji kufikiriwa kwanza. Kama wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova au wewe umo miongoni mwa wale mamilioni ya wanafunzi wenye moyo mweupe wa Neno la Mungu wanaoshirikiana nao, fikiria kweli hii: “Kwa kila jambo, kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu.” (Mhubiri 3:1) Kwa haki, hilo latia ndani kuonyesha kwako hangaiko lenye upendo kuelekea mahusiano ya familia. (Wakolosai 3:18-21) Lahusisha kufanya uandalizi wa haki kwa ajili ya watu wa nyumbani kwako kwa kufanya kazi ya kimwili. (2 Wathesalonike 3:10-12; 1 Timotheo 5:8) Na ili kuubadili mwendo wa kawaida waweza kutumia wakati wa kushughulikia hobi au vitumbuizo au tafrija za pindi kwa pindi. (Linganisha Marko 6:31.) Lakini, baada ya kufikiria kwa uzito, je, huoni kwamba hakuna lolote kati ya mambo hayo lililo kuu maishani? Jambo jingine ni la maana zaidi.
4. Wafilipi 1:9, 10 (NW), huhusianaje na kupanga kwetu mambo ya kutangulizwa?
4 Labda watambua kwamba kanuni zenye kuongoza za Biblia ni misaada yenye thamani katika kupanga mambo ya kutangulizwa na kufanya maamuzi yenye hekima. Kwa kielelezo, kwenye Wafilipi 1:9, 10 (NW), Wakristo wanasihiwa sana “kuzidi bado hata zaidi na zaidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” Kwa kusudi jipi? Mtume Paulo aliongeza hivi: “Mpate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.” Je, hilo halipatani na akili? Kwa msingi wa ujuzi sahihi, Mkristo mwenye utambuzi aweza kuamua ni jambo gani lipasalo kuwa lenye upendezi wa kwanza—kuwa kuu—maishani.
Kigezo Kionyeshacho Jambo Kuu
5. Katika kufafanua kigezo walichoachiwa Wakristo, Maandiko huonyeshaje jambo lililokuwa kuu maishani mwa Yesu?
5 Twaona upande wenye thamani wa ujuzi, katika maneno haya ya mtume Petro: “Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, akawaachia kielelezo, mfuate nyayo zake.” (1 Petro 2:21) Ndiyo, ili kupata vidokezi vionyeshavyo jambo kuu maishani ni gani, twaweza kuchunguza maoni ya Yesu Kristo kuhusu jambo hilo. Zaburi 40:8 ilisema hivi kiunabii juu yake: “Kuyafanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” Hivyo ndivyo alivyotoa wazo lilo hilo: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.”—Yohana 4:34; Waebrania 12:2.
6. Twaweza kuwaje na matokeo yaleyale ambayo Yesu alikuwa nayo katika kuweka mapenzi ya Mungu kwanza?
6 Kazia uangalifu ufunguo huo—kuyatenda mapenzi ya Mungu. Kielelezo cha Yesu chakazia jambo ambalo wanafunzi wake wapaswa kwa kufaa, kulifanya liwe kuu maishani mwao, kwa maana alisema kwamba “kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake.” (Luka 6:40) Na Yesu alipokuwa akitembea katika njia ambayo Baba yake alikusudia, alionyesha kwamba kulikuwa na “furaha tele” katika kuweka mapenzi ya Mungu kuwa jambo kuu. (Zaburi 16:11; Matendo 2:28) Je, waona kinachodokezwa na hilo? Wafuasi wa Yesu wachaguapo kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo kuu maishani mwao, wao watakuwa na “furaha tele” na uhai ulio halisi. (1 Timotheo 6:19) Kwa hiyo kuna sababu zaidi ya moja ifanyayo kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kutangulizwa maishani mwetu.
7, 8. Yesu alikabili majaribu gani, nasi twaweza kujifunza nini kutokana na hilo?
7 Mara baada ya Yesu kuonyesha kujitoa kwake ili kuyatenda mapenzi ya Mungu, Ibilisi alijaribu kumkengeusha. Jinsi gani? Kwa kumshawishi katika mambo matatu. Kila mara Yesu alijibu kwa maneno ya Kimaandiko, yaliyo wazi. (Mathayo 4:1-10) Lakini majaribu zaidi yalimngojea—mnyanyaso, dhihaka, kusalitiwa na Yudasi, mashtaka yasiyo ya kweli, kisha kifo juu ya mti wa mateso. Bado, hakuna mojawapo ya majaribu hayo yaliyomfanya Mwana mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu ageuze njia yake. Katika hali ya hatari, Yesu alisali hivi: “Si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo. . . . Mapenzi yako yatimizwe.” (Mathayo 26:39, 42) Je, kila moja wetu hapaswi kusukumwa kwa kina kirefu na sehemu hii ya kigezo tulichoachiwa, ikitufanya ‘tudumu katika kusali’?—Warumi 12:12.
8 Ndiyo, tupangapo mambo yetu ya kutangulizwa maishani, mwongozo wa kimungu ni wenye kusaidia sana, hasa ikiwa twakabili maadui wa ile kweli na wapinzani wa mapenzi ya Mungu. Kumbuka kule kusihi kwa Mfalme Daudi akiomba mwongozo alipopatwa na upinzani wa adui. Tutaona hilo tuchunguzapo sehemu ya Zaburi 143. Hiyo yapaswa kutusaidia tutambue jinsi tuwezavyo kuimarisha uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Yehova na kutiwa nguvu ili kuweka kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kwanza maishani mwetu.
Yehova Husikia na Kujibu Sala Zetu
9. (a) Ingawa Daudi alikuwa mtenda-dhambi, maneno na vitendo vyake vyafunua nini? (b) Kwa nini tusikate tamaa katika kufanya lililo sawa?
9 Ingawa alikuwa binadamu mwenye dhambi awezaye kufa, Daudi alikuwa na imani kwamba Yehova angesikia kusihi kwake. Aliomba hivi kwa unyenyekevu: “Ee BWANA, uisikie sala yangu, uzisikilize dua zangu, kwa uaminifu wako unijibu kwa haki yako [“uadilifu wako,” NW]. Wala usimhukumu mtumishi wako, maana kwako hakuna aliye hai mwenye haki.” (Zaburi 143:1, 2) Daudi alitambua kutokamilika kwake, hata hivyo moyo wake ulikuwa kamili kumwelekea Mungu. Hivyo, alikuwa na uhakika kwamba angepokea jibu katika uadilifu. Je, hilo halitutii moyo? Ingawa twapungukiwa na uadilifu wa Mungu, twaweza kuwa na uhakika kwamba yeye hutusikia ikiwa mioyo yetu ni kamili kumwelekea yeye. (Mhubiri 7:20; 1 Yohana 5:14) Huku tukidumu katika kusali, ni lazima tuazimie ‘kuushinda ubaya kwa wema’ katika siku hizi zenye uovu.—Warumi 12:20, 21; Yakobo 4:7.
10. Kwa nini Daudi alikuwa na vipindi vyenye hangaiko?
10 Daudi alikuwa na maadui, sawa na tulivyo nao. Alipokuwa mtoro kutoka kwa Sauli, aliyelazimika kutafuta kimbilio katika mahali pasipo na watu, pasipofikika, au alipokuwa mfalme aliyesumbuliwa na maadui, Daudi alikuwa na vipindi vyake vyenye hangaiko. Alifafanua jinsi hilo lilivyomwathiri: “Adui ameifuatia nafsi yangu . . . Amenikalisha mahali penye giza . . . Na roho yangu imezimia ndani yangu, moyo wangu ndani yangu umesituka [“umejionyesha kuwa wenye kutiwa ganzi,” NW].” (Zaburi 143:3, 4) Je, umekuwa na sababu ya kuhisi vivyo hivyo?
11. Watumishi wa siku ya kisasa wa Mungu wamekabili vipindi vipi vyenye hangaiko?
11 Msongo wa adui, majaribu kwa sababu ya ugumu mkali wa kiuchumi, ugonjwa mbaya, au matatizo mengine yenye kusababisha hangaiko yamewafanya watu fulani wa Mungu wahisi kwamba roho yao ingekata tamaa. Pindi fulani mioyo yao pia imekuwa kana kwamba imetiwa ganzi. Ni kana kwamba wao mmoja-mmoja wamelia hivi: “Wewe, uliyetuonyesha mateso mengi, mabaya, utatuhuisha tena . . . Urejee tena na kunifariji moyo.” (Zaburi 71:20, 21) Wao wamesaidiwaje?
Jinsi ya Kukabili Jitihada za Adui
12. Mfalme Daudi alikabilianaje na hatari na majaribu?
12 Zaburi 143:5 yaonyesha kile Daudi alichofanya alipokabiliwa na hatari na majaribu makubwa: “Nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.” Daudi alikumbuka jinsi Mungu alivyoshughulika na watumishi Wake na jinsi yeye mwenyewe alivyokuwa amepata ukombozi. Aliyatafakari yale ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili ya jina Lake kuu. Ndiyo, Daudi alifuliza kujishughulisha na kazi za Mungu.
13. Tukabilipo majaribu, kufikiria kwetu vielelezo vya kale na vya kisasa vya watumishi waaminifu kutatusaidiaje kuvumilia?
13 Je, sisi hatujakumbuka mara nyingi jinsi ambavyo Mungu ameshughulika na watu wake? Bila shaka tumefanya hivyo! Hilo latia ndani rekodi iliyowekwa na lile “wingu kubwa la mashahidi” katika nyakati za kabla ya Ukristo. (Waebrania 11:32-38; 12:1) Wakristo watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walitiwa moyo pia ‘kuzikumbuka siku za kwanza’ na yale waliyokuwa wamevumilia. (Waebrania 10:32-34) Namna gani yale mambo yaliyoonwa na watumishi wa Mungu katika nyakati za kisasa, kama yale yaliyosimuliwa katika Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom?a Masimulizi yaliyoandikwa humo na kwingineko hutuwezesha tukumbuke jinsi ambavyo Yehova amewasaidia watu wake wavumilie marufuku, vifungo vya gerezani, utendaji wa vikundi vya wafanya-ghasia, na kambi za mateso na za kazi ya kulazimishwa. Kumekuwa na majaribu katika nchi zilizogawanywa na vita, kama vile Burundi, Liberia, Rwanda, na iliyokuwa Yugoslavia. Upinzani ulipojidhihirisha, watumishi wa Mungu walivumilia kwa sababu ya kudumisha uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova. Mkono wake ulitegemeza wale waliofanya kule kuyatenda mapenzi yake kuwa jambo kuu maishani mwao.
14. (a) Ni kipi kimojawapo vielelezo vionyeshavyo jinsi Mungu amemtegemeza mtu akiwa katika hali ambayo huenda ikafanana na yetu? (b) Unajifunza nini kutokana na kielelezo hicho?
14 Hata hivyo, huenda ukaitikia kwamba hujapata kutendwa kinyama jinsi hiyo, na huenda ukahisi kwamba si yamkini kwamba utapatwa kutendwa hivyo wakati wowote. Lakini, kutegemeza kwa Mungu watu wake, hakujafanywa sikuzote katika hali ambazo wengine huenda wakaziona kuwa zenye kutokeza sana. Yeye amewategemeza watu wengi mmoja-mmoja waonwao kuwa wa “wastani” katika hali za “kawaida.” Hapa pana kimojawapo tu cha vielelezo vingi: Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1996, lilikuwa na simulizi la Penelope Makris? Ni kielelezo bora sana kama nini cha uaminifu-maadili wa Kikristo! Je, waweza kukumbuka kile alichovumilia kutoka kwa majirani, jinsi alivyopambana na magonjwa mabaya, na jitihada alizotia ili kukaa katika huduma ya wakati wote? Namna gani lile jambo lenye kuthawabisha aliloona katika Mytilene? Hoja ni, Je, wewe huona vielelezo hivyo kuwa msaada kwetu sote katika kupanga mambo ya kutangulizwa, tukiweka kule kuyatenda mapenzi ya Mungu kuwa jambo la kwanza maishani mwetu?
15. Ni yapi baadhi ya matendo ya Yehova tupaswayo kuyatafakari?
15 Kuutafakari utendaji mbalimbali wa Yehova, kwatuimarisha kama kulivyomwimarisha Daudi. Katika kulitimiza kusudi lake, Yehova alifanya uandalizi kwa ajili ya wokovu kupitia kifo, ufufuo, na utukuzo wa Mwana wake. (1 Timotheo 3:16) Ameusimamisha Ufalme wake wa kimbingu, akaondolea mbali Shetani na roho zake waovu kutoka mbinguni, na kurudisha ibada ya kweli duniani. (Ufunuo 12:7-12) Amejenga paradiso ya kiroho na amewabariki watu wake kwa kuwapa ongezeko. (Isaya 35:1-10; 60:22) Sasa watu wake wanatoa ushahidi wa mwisho kabla ya dhiki kubwa kutokea kwa ghafula. (Ufunuo 14:6, 7) Ndiyo, tuna mengi ya kutafakari.
16. Twatiwa moyo kujishughulisha na nini, na kufanya hivyo kutatia nini moyoni mwetu?
16 Kufuliza kujishughulisha na kazi ya mikono ya Mungu badala ya kujishughulisha sana na jitihada za kibinadamu kwatia moyoni mwetu kwamba nguvu anazotumia Yehova haziwezi kuzuiwa na mtu. Lakini kazi hizo hazihusishi tu zile kazi za kimwili za ajabu za uumbaji huko mbinguni na hapa duniani. (Ayubu 37:14; Zaburi 19:1; 104:24) Kazi zake za ajabu zatia ndani matendo ya ukombozi kwa ajili ya watu wake kutoka kwa wapinzani walio adui, kama ilivyoonyeshwa katika mambo yaliyoonwa na watu wake wachaguliwa wa kale.—Kutoka 14:31; 15:6.
Kujua Njia ya Kuiendea
17. Yehova alikuwa halisi kwa Daudi kadiri gani, na twaweza kuhakikishiwaje na hilo?
17 Daudi alisali akiomba msaada ili unyevunyevu wa uhai ulio ndani yake usipate kukauka: “Nakunyoshea mikono yangu; nafsi yangu inakuonea kiu kama nchi kame. Ee BWANA, unijibu hima, roho yangu imelegea, usinifiche uso wako, nisifanane nao washukao shimoni.” (Zaburi 143:6, 7) Daudi, aliyekuwa mtenda-dhambi, alijua kwamba Mungu aliifahamu hali yake. (Zaburi 31:7) Nyakati nyingine huenda sisi pia tukahisi kwamba hali yetu ya kiroho imefikia kiwango cha chini. Lakini hali si bila tumaini. Yehova, asikiaye sala zetu, aweza kuharakisha kurudi kwetu kwa kutuburudisha kupitia wazee wenye upendo, makala katika Mnara wa Mlinzi, au sehemu za mkutano zionekanazo kuwa zimekusudiwa sisi hasa.—Isaya 32:1, 2.
18, 19. (a) Twapaswa kumsihi Yehova kwa bidii tukimwomba nini? (b) Twaweza kuwa na uhakika juu ya nini?
18 Kumtumaini kwetu Yehova hutusukuma tumsihi hivi: “Unifanye kusikia fadhili zako asubuhi, kwa maana nimekutumaini wewe. Unijulishe njia nitakayoiendea.” (Zaburi 143:8) Je, yeye alimtamausha Dada Makris, aliyekuwa mbali na wengine akiwa katika kisiwa cha Kigiriki? Basi je, atakutamausha ufanyapo kule kuyatenda mapenzi yake kuwa jambo kuu maishani mwako? Ibilisi na mawakili wake wangependa kuizuia au kuikomesha kabisa kazi yetu ya kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu. Tuwe twatumikia katika nchi ambamo ibada ya kweli huruhusiwa kwa ujumla au twatumikia mahali ambapo imekandamizwa, sala zetu zenye muungano zapatana na ombi hili la unyenyekevu la Daudi: “Ee BWANA, uniponye na adui zangu; nimekukimbilia Wewe.” (Zaburi 143:9) Usalama wetu dhidi ya kupatwa na afa la kiroho wategemea kukaa katika mahali pa siri pa Aliye Juu Zaidi Sana.—Zaburi 91:1.
19 Usadikisho wetu juu ya jambo lililo kuu una msingi thabiti. (Warumi 12:1, 2) Basi, kinza jitihada za ulimwengu za kukulazimisha ufuate yale ambayo huo wafikiri kuwa ya maana katika taratibu ya mambo ya kibinadamu. Endelea kuruhusu kila sehemu ya maisha yako ionyeshe jambo unalojua kuwa ndilo kuu—kule kuyatenda mapenzi ya Mungu.—Mathayo 6:9, 10; 7:21.
20. (a) Tumejifunza nini juu ya Daudi kwenye Zaburi 143:1-9? (b) Wakristo leo huonyeshaje roho ya Daudi?
20 Mistari tisa ya kwanza ya Zaburi 143 hukazia uhusiano wa kibinafsi wa karibu wa Daudi pamoja na Yehova. Alipozingiwa na maadui, alimsihi Mungu kwa uhuru ili kupata mwongozo. Aliumwaga moyo wake, akitafuta msaada wa kujua njia iliyo sawa ya kuendea. Ndivyo ilivyo leo kwa habari ya mabaki ya watiwa-mafuta kwa roho walio duniani pamoja na waandamani wao. Wao huona uhusiano wao pamoja na Yehova kuwa wenye thamani wamsihipo wakiomba mwongozo. Wanaweka kwanza kule kuyatenda mapenzi ya Mungu, ijapokuwa misongo kutoka kwa Ibilisi na ulimwengu.
21. Kwa nini ni jambo la maana kwetu kuweka kielelezo chema ikiwa tutawafundisha wengine jambo lipaswalo kuwa kuu maishani mwao?
21 Mamilioni wanaojifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova wanahitaji kutambua kwamba kule kuyatenda mapenzi ya Mungu ndilo jambo kuu. Twaweza kuwasaidia kuelewa hilo tunapozungumzia sura ya 13 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, inayokazia kanuni zinazohusika katika kuwa watiifu kwa Neno.b Bila shaka, wao wapaswa kuona kielelezo chema cha yale tunayowafundisha katika maisha yetu. Baada ya kipindi kifupi kwa kulinganishwa, wao pia watakuja kujua njia wapaswayo kuiendea. Mamilioni hao watambuapo kibinafsi jambo lipaswalo kuwa lenye umaana zaidi maishani mwao, wengi watasukumwa kuchukua hatua za kujiweka wakfu na kubatizwa. Baadaye, kutaniko laweza kuwasaidia waendelee kufuliza kuenenda katika njia ya uhai.
22. Ni maswali gani yatakayochunguzwa katika makala inayofuata?
22 Wengi hukiri kwa utayari kwamba mapenzi ya Mungu yapaswa kuwa yenye umaana zaidi maishani mwao. Lakini, Yehova huwafundishaje watumishi wake kwa kuendelea kufanya mapenzi yake? Hilo huwaletea manufaa zipi? Maswali hayo yatachunguzwa, pamoja na mazungumzo juu ya mstari wa msingi, Zaburi 143:10, katika makala ifuatayo.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa katika 1993 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Kilichochapishwa katika 1995 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
Jibu Lako Ni Nini?
◻ Kwa kutumia Wafilipi 1:9, 10 (NW), twaweza kupangaje mambo ya kutangulizwa?
◻ Yesu alionyeshaje jambo lililokuwa kuu maishani mwake?
◻ Twaweza kujifunza nini kutokana na vitendo vya Daudi alipokuwa chini ya jaribu?
◻ Zaburi 143:1-9 hutusaidia katika njia gani leo?
◻ Ni jambo gani lipaswalo kuwa kuu maishani mwetu?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Vitendo vya Daudi vilithibitisha kutegemea kwake Yehova
[Hisani]
Imetolewa upya kutoka Illustrirte Pracht - Bibel/Heilige Schrift des Alten und Neuen Testaments, nach der deutschen Uebersetzung D. Martin Luther’s