Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 2/15 kur. 4-7
  • Kuteseka Kutakapokuwa Hakupo Tena

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuteseka Kutakapokuwa Hakupo Tena
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Asitekeleze Mapenzi Yake Mara Moja?
  • Kwa Nini Asiwalazimishe Watu Wafanye Lililo Sawa?
  • Namna Gani Wahasiriwa Wote Wasio na Hatia?
  • Kitulizo Halisi kwa Wale Wanaoteseka?
  • Kule “Kurudishwa kwa Mambo Yote”
  • Biblia Inasema Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Faraja kwa Wanaoteseka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Swali la 3: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Niteseke?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 2/15 kur. 4-7

Kuteseka Kutakapokuwa Hakupo Tena

KUTESEKA hakukuwa sehemu ya kusudi la Mungu la awali kwa familia ya kibinadamu. Hakubuni kuteseka wala hakutaki. ‘Ikiwa ni hivyo,’ huenda ukauliza, ‘kulianzaje, na kwa nini Mungu amekuruhusu kuendelee hata sasa?’—Linganisha Yakobo 1:13.

Jibu lapatikana katika rekodi ya mapema zaidi ya historia ya mwanadamu, Biblia, hasa kitabu cha Mwanzo. Chasema kwamba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walimfuata Shetani Ibilisi katika uasi wake dhidi ya Mungu. Matendo yao yalizusha masuala ya msingi yaliyoshambulia msingi wenyewe wa sheria na utaratibu wa ulimwengu wote mzima. Walipodai haki ya kujiamulia lililokuwa jema na lililokuwa baya, walisai enzi kuu ya Mungu. Walisaili haki yake ya kutawala na kuwa mwamuzi pekee wa “mema na mabaya.”—Mwanzo 2:15-17; 3:1-5.

Kwa Nini Asitekeleze Mapenzi Yake Mara Moja?

‘Kwa nini, basi, Mungu hakutekeleza mapenzi yake mara moja?’ huenda ukauliza. Kwa wengi jambo hilo laonekana kuwa rahisi sana. ‘Mungu angalikuwa na nguvu. Angalizitumia kuwaharibu hao waasi,’ wao wasema. (Zaburi 147:5) Lakini jiulize hili, ‘Je, mimi hukubaliana bila kusitasita na wale wote wanaotumia nguvu nyingi zaidi ili kutekeleza mapenzi yao? Je, mimi sihisi kisilika hisi ya machukio mtawala wa kimabavu atumiapo vikundi vya kijeshi ili kuwaondolea mbali adui zake?’ Watu wengi wenye akili timamu hushtushwa na jambo kama hilo.

‘Ah,’ wasema, ‘lakini ikiwa Mungu angetumia nguvu hizo, hakuna yeyote angesaili matendo yake.’ Je, una hakika? Je, si kweli kwamba watu husaili matumizi ya nguvu ya Mungu? Wanasaili ni kwa nini hajazitumia nyakati fulani, kama vile katika kuvumilia kwake uovu. Nao wanasaili kwa nini amezitumia nyakati nyingine. Hata Abrahamu mwaminifu alitatizwa na matumizi ya Mungu ya nguvu dhidi ya adui Zake. Wakumbuka Mungu alipoamua kuharibu Sodoma. Abrahamu alihofu kimakosa kwamba watu wema wangekufa pamoja na wabaya. Alipinga kwa nguvu hivi: “Haiwezekani kwako kufanya namna hii, kuharibu wenye haki pamoja na waovu.” (Mwanzo 18:25, Zaire Swahili Bible) Hata watu wenye akili timamu kama vile Abrahamu wanahitaji uhakikishio kwamba nguvu kamili hazitatumiwa vibaya.

Bila shaka, Mungu angaliweza kuwaharibu papo hapo Adamu, Hawa, na Shetani. Lakini wazia jinsi hilo lingaliweza kuwaathiri malaika wengine au viumbe wengine wa wakati ujao, ambao huenda baadaye wangepata kujua juu ya matendo yake. Je, hilo lingaliweza kuwaacha na maswali yenye kusumbua juu ya uhalali wa utawala wa Mungu? Je, hilo lisingalimfichua Mungu kwenye shtaka la kwamba alikuwa, kwa hakika, aina fulani ya mtawala wa kimabavu mwenye kupiga ubwana, kama Nietzsche alivyomfafanua, Mungu ambaye huondolea mbali kwa ukatili yeyote anayempinga?

Kwa Nini Asiwalazimishe Watu Wafanye Lililo Sawa?

‘Je, Mungu asingaliweza kuwalazimisha watu wafanye lililo sawa tu?’ huenda wengine wakauliza. Basi, fikiria hili pia. Katika historia yote, serikali zimejaribu kuwafanya watu wajipatanishe na njia zazo za kufikiri. Serikali fulani au watawala mmoja-mmoja wamezoea aina mbalimbali za kupiga ubongo msasa, huenda ikawa kwa kutumia dawa za kulevya au upasuaji, wakiwanyang’anya wahasiriwa wao ile zawadi ya ajabu ya hiari. Je, hatuthamini kuwa viumbe hai walio huru kuchagua, hata ikiwa zawadi hiyo yaelekea kutumiwa vibaya? Je, twaruhusu jitihada ya serikali yoyote au ya mtawala yeyote ya kuiondoa hiari hiyo?

Basi, Mungu angeweza kufanya nini kingine badala ya kutumia nguvu mara moja ili kutekeleza sheria? Yehova Mungu aliamua kwamba njia bora zaidi ya kushughulikia huo uasi ni kwa kuruhusu kipindi cha muda cha kutokuwa chini ya utawala wake kwa ajili ya wale waliokataa sheria zake. Hilo lingeruhusu familia ya kibinadamu, iliyozaliwa na Adamu na Hawa, kipindi chenye mipaka cha kujitawala bila ya kuwa chini ya sheria ya Mungu. Kwa nini alifanya hilo? Kwa kuwa alijua kwamba, baada ya muda, uthibitisho usiokanika ungetokea, ukithibitisha kwamba njia yake ya kutawala sikuzote huwa sawa na ya haki, hata atumiapo nguvu zake zisizo na mipaka kutekeleza mapenzi yake, na kwamba, punde si punde, uasi wowote dhidi yake utatokeza maafa.—Kumbukumbu la Torati 32:4; Ayubu 34:10-12; Yeremia 10:23.

Namna Gani Wahasiriwa Wote Wasio na Hatia?

‘Kwa wakati uliopo, namna gani wahasiriwa wote wasio na hatia?’ huenda ukauliza. ‘Je, kwa kweli wastahili maumivu yao ili kuthibitisha hoja fulani ya sheria?’ Mungu hakuruhusu uovu uwepo ili tu kuthibitisha hoja fulani isiyo dhahiri ya sheria. Kinyume cha hilo, ni ili kuthibitisha mara moja kwa wakati wote kweli ya msingi kwamba yeye peke yake ndiye mwenye enzi kuu na kwamba kutii sheria zake ni kwa lazima kwa ajili ya amani na furaha yenye kuendelea ya viumbe wake wote.

Jambo moja la maana kukumbukwa ni kwamba Mungu ajua kwamba aweza kurekebisha kabisa madhara yoyote ambayo kuwapo kwa uovu kwaweza kuletea familia ya kibinadamu. Ajua kwamba hatimaye, kile kipindi cha muda cha maumivu na kuteseka kitakuwa na tokeo lenye manufaa. Mfikirie mama anayemshika mtoto wake kwa nguvu huku daktari amtiapo uchungu wa kumdunga kwa chanjo ili kumpa kinga dhidi ya maradhi fulani ambayo ikiwa sivyo yangaliweza kumwua mtoto. Hakuna mama anayetaka mtoto wake ahisi maumivu. Hakuna daktari anayetaka kusababishia mgonjwa wake msononeko. Wakati uleule, mtoto haelewi sababu ya yale maumivu, lakini baadaye ataelewa kwa nini liliruhusiwa.

Kitulizo Halisi kwa Wale Wanaoteseka?

Huenda wengine wakahisi kwamba kujua tu mambo hayo huenda kusiwatulize sana wale wanaoteseka. Hans Küng ataarifu kwamba ufafanuzi wa kiakili wa kuwako kwa kuteseka ni “kwenye manufaa kwa mwenye kuteseka kama vile mhadhara juu ya kemia ya vyakula ni wenye manufaa kwa mtu anayeumia kwa njaa.” Yeye auliza hivi: “Je, kufikiri kwote kwa werevu kwaweza kwa kweli kutolea mtu kitia-moyo ambaye karibu amelemewa na kuteseka?” “Kufikiri kwote kwa werevu” kwa wanadamu wanaopuuza Neno la Mungu, Biblia, hakujawatia-moyo wale wanaoteseka. Kufikiri huko kwa kibinadamu kumeongezea tu lile tatizo kwa kudokeza kwamba Mungu alikusudia mwanadamu ateseke na kwamba dunia ilibuniwa kuwa bonde la machozi au uwanja wa kutahinia wale ambao hatimaye watapata uhai mbinguni. Ni kufuru kama nini!

Hata hivyo, Biblia yenyewe hutoa kitulizo halisi. Haitoi tu ufafanuzi thabiti juu ya kuwako kwa kuteseka bali pia hujenga uhakika katika ahadi ya hakika ya Mungu kwamba atarekebisha madhara yote ambayo kuruhusiwa huku kwa kuteseka kwa muda kumesababisha.

Kule “Kurudishwa kwa Mambo Yote”

Karibuni sana sasa Mungu atarudisha mambo yote yawe jinsi alivyokusudia yawe kabla ya viumbe wake wa kibinadamu wa kwanza kuasi. Wakati wake uliowekwa rasmi wa utawala wa kujitegemea wa mwanadamu wakaribia kwisha. Twaishi wakati ambapo atamtuma “Yesu, ambaye mbingu, kwa kweli, lazima imweke ndani yayo yenyewe hadi nyakati za kurudishwa kwa mambo yote ambayo Mungu alisema kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu wa wakati wa kale.”—Matendo 3:20, 21.

Yesu Kristo atafanya nini? Ataondoa maadui wote wa Mungu duniani. (2 Wathesalonike 1:6-10) Huo hautakuwa ufishaji wa upesi, kama ule ufanywao na watawala wa kimabavu wa kibinadamu. Ule uthibitisho mwingi unaothibitisha matokeo yenye msiba ya utawala mbovu wa mwanadamu utaonyesha kwamba Mungu ana haki kabisa ya kutumia nguvu zake zisizo na mipaka ili kutekeleza mapenzi yake karibuni. (Ufunuo 11:17, 18) Mwanzoni hilo litamaanisha “dhiki” ambayo dunia haijapata kuona hapo mbele, inayofanana na Furiko la Siku ya Noa, lakini iliyo kubwa zaidi. (Mathayo 24:21, 29-31, 36-39) Watakaookoka “dhiki [hiyo] kubwa” watajionea “majira ya kuburudisha” waonapo utimizo wa ahadi zote za Mungu zilizotolewa “kupitia kinywa cha manabii wake watakatifu.” (Matendo 3:19; Ufunuo 7:14-17) Mungu ameahidi nini?

Manabii wa Mungu wa kale wasema kwamba kutakuwako mwisho wa kuteseka kunakosababishwa na vita na umwagikaji wa damu. Kwa kielelezo, Zaburi 46:9 hutuambia hivi: “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” Hakutakuwa tena na wahasiriwa wasio na hatia na wakimbizi wasiopendeza, waliobakwa, waliolemazwa, na waliouawa katika vita vikatili! Nabii Isaya asema hivi: “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.

Manabii pia wanatabiri mwisho wa kuteseka kunakosababishwa na uhalifu na ukosefu wa haki. Andiko la Mithali 2:21, 22 laahidi kwamba “wanyofu watakaa katika nchi” na kwamba wanaosababisha maumivu na kuteseka “watang’olewa.” Hakutakuwa tena na ‘mtu mmoja kuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Waovu wote wataondolewa milele. (Zaburi 37:10, 38) Kila mmoja ataweza kuishi katika amani na usalama, huru kutokana na kuteseka.—Mika 4:4.

Isitoshe, manabii pia wanaahidi kwamba kutakuwa na mwisho wa kuteseka kunakosababishwa na magonjwa ya kimwili na ya kihisia-moyo. (Isaya 33:24) Isaya aahidi kwamba vipofu, mabubu, wasiojiweza, na wale wote walio na magonjwa na maradhi wataponywa. (Isaya 35:5, 6) Mungu hata atageuza matokeo ya kifo. Yesu alitabiri kwamba “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Katika ono lake la “mbingu mpya na dunia mpya,” mtume Yohana aliambiwa kwamba “Mungu mwenyewe . . . atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.” (Ufunuo 21:1-4) Wazia hilo! Hakuna maumivu, hakuna machozi, hakuna kupaaza kilio, hakuna kifo—hakuna kuteseka tena!

Mambo yoyote ya huzuni kubwa ambayo huenda yakawa yalitokea wakati wa kuvumiliwa huku kwa muda kwa uovu yatarekebishwa. Hata makumbukumbu ya maumivu na kuteseka kwa kibinadamu—ambako hakukukusudiwa kamwe na Mungu—yatafutwa kabisa. “Taabu za kwanza zimesahauliwa . . . Mambo ya kwanza hayatakumbukwa,” Isaya alitabiri. (Isaya 65:16, 17) Kusudi la Mungu la awali la kuwa na familia kamilifu ya kibinadamu ikiishi katika amani na furaha kamili kwenye dunia iliyo paradiso litatimizwa kikamili. (Isaya 45:18) Uhakika katika enzi kuu yake utakuwa kamili. Ni pendeleo kama nini kuishi wakati ambapo Mungu atakomesha kuteseka kwote kwa kibinadamu, wakati ambapo aonyesha kwamba yeye si aina fulani ya mtu “mwenye kupiga ubwana, mlaghai, mpunjaji, mfishaji,” kama Nietzsche alivyodai, lakini kwamba sikuzote yeye ni mwenye upendo, mwenye hekima, na mwenye haki katika kutumia kwake nguvu zake kamili!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Watawala fulani wamezoea kupiga ubongo msasa, wakiwanyang’anya wahasiriwa wao hiari

[Hisani]

UPI/Bettmann

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kuteseka kukiwa hakupo tena, wote watafurahia uhai kikamili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki