Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 5/15 kur. 22-25
  • Jinsi ya Kupata Tumaini Katikati ya Hali ya Kukata Tumaini

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kupata Tumaini Katikati ya Hali ya Kukata Tumaini
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tumaini Kujapokuwa Majaribu Mbalimbali
  • Je, Lolote Lenye Manufaa Laweza Kutokana na Majaribu?
  • Itibari Katika Yehova
  • “Mtumaini Yehova”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Yajapokuwa Majaribu, Shikeni Imani Yenu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Ayubu—Mtu Mvumilivu na Mtimilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Tuyaoneje Majaribu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 5/15 kur. 22-25

Jinsi ya Kupata Tumaini Katikati ya Hali ya Kukata Tumaini

EBU wazia kwamba ungepatwa na mambo yafuatayo yaliyoonwa: Mali zako zote za kimwili zinaharibiwa, ukiachwa ukiwa fukara. Watoto wako—shangwe ya uhai wako—wamekufa. Mwenzi wako hakupatii kitia-moyo chochote. Afya yako imeporomoka kihalisi. Kila siku ni masaibu yenye maumivu makali.

Ikiwa hali yako ingekuwa hivyo, je, ungeweza kupata sababu ya kuendelea kuishi? Au ungeshindwa na hali ya kukata tumaini?

Hali mbaya yenye kusikitisha ambayo imefafanuliwa sasa hivi ilikuwa ni mambo halisi yaliyoonwa maishani mwa Ayubu, mtu aliyeishi katika nyakati za Biblia. (Ayubu, sura ya 1 na ya 2) Akiwa ameshuka moyo, Ayubu aliomboleza hivi: “Nafsi yangu inachoka na maisha yangu.” Yeye angalikaribisha kifo kama kitulizo. (Ayubu 10:1; 14:13) Hata hivyo, ijapokuwa aliteseka sana, Ayubu alidumisha uaminifu-maadili wake kwa Mungu. Kwa hiyo Yehova “[aliubariki] huo mwisho wa Ayubu zaidi ya mwanzo wake.” Hivyo alikufa katika amani, “mzee sana mwenye kujawa na siku.”—Ayubu 42:12, 17.

Ayubu aliweka kielelezo katika uvumilivu kinachosifiwa hadi siku hii. Majaribu yake yaliboresha utu wake na yalichochea wengine kufanya kazi njema. (Yakobo 5:10, 11) Lililo la muhimu zaidi ya yote ni kwamba, uaminifu-maadili usio na waa wa Ayubu ulifurahisha moyo wa Yehova. (Mithali 27:11) Hivyo jinamizi la maumivu makali likawa hatimaye ushindi wa sifa ya uchaji Mungu, imani, na uaminifu-maadili uliomletea Ayubu baraka na wote wale ambao wamechochewa kutenda na kielelezo chake.

Tumaini Kujapokuwa Majaribu Mbalimbali

Huenda ukapatwa na majaribu sawa na yaliyompata Ayubu. Huenda ikawa kifo cha mpendwa kimekukumba kihisiamoyo. Huenda ikawa ugonjwa mbaya umefanya maisha yako kuwa masaibu yenye maumivu. Huenda njia yako yote ya maisha ikaonekana imeporomoka kwa sababu ya talaka yenye kuvunja moyo. Huenda ikawa kutofaulu kiuchumi kumekuacha ukiwa fukara. Huenda ukawa shabaha ya mnyanyaso mkali kutoka kwa wapinzani wa ibada ya kweli wenye chuki. Huenda ikawa jitihada za kukabiliana na majaribu yako zimekuacha ukihisi kwamba wakati ujao wako ni usio na tumaini.—1 Petro 1:6.

Badala ya kushindwa na hali ya kukata tumaini, jiulize mwenyewe, ‘Kwa nini ninateseka?’ Unateseka kwa sababu unaishi katika ulimwengu ambao “unakaa katika nguvu ya mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Tokeo ni kwamba, kila mtu huteseka. Katika njia fulani sisi sote tunaathiriwa na chuki inayopuliziwa na Ibilisi dhidi ya ujumbe wa Ufalme, maneno yasiyo na upendo ya wengine, au matendo yenye kuchukiza ya mwenendo wa kutomwogopa Mungu yaliyo ya kawaida sana katika “nyakati [hizi] za hatari.”—2 Timotheo 3:1-5.

Ikiwa jambo fulani lenye kuhuzunisha limetukia katika maisha yako, huenda ikawa ulikuwa mhasiriwa wa “wakati na tukio lisilotazamiwa.” (Mhubiri 9:11, NW) Kwa upande mwingine, nyakati nyingine mambo huharibika maishani kwa sababu ya hali yetu wenyewe yenye dhambi tuliyorithi. (Waroma 5:12) Hata ikiwa umefanya kosa nzito lakini umetubu na kutafuta msaada wa kiroho, usihisi kwamba Mungu amekuacha. (Zaburi 103:10-14; Yakobo 5:13-15) Yeye hutujali zaidi ya mtu mwingine yeyote. (1 Petro 5:6, 7) Waweza kuwa na uhakika kwamba “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Hata jaribu lako liwe lenye kuhuzunisha au gumu jinsi gani, Yehova aweza kukupatia hekima ya kushughulika nalo. (Yakobo 1:5-8) Kumbuka siku zote kwamba Yehova aweza kuponya majeraha yote. Unapokuwa na upendeleo wake, hakuna chochote kiwezacho kukuzuia usipate tuzo ya uhai.—Waroma 8:38, 39.

Je, Lolote Lenye Manufaa Laweza Kutokana na Majaribu?

Kuna msemo wa zamani, “Baada ya dhiki, faraja.” Hiyo ni njia sahili ya kusema kwamba hata hali ziwe mbaya jinsi gani, sikuzote waweza kupata sababu ya kuwa na tumaini. Kusudi la mambo yote yaliyoandikwa katika Neno la Mungu ni kwamba “tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Hata hali yako iwe mbaya jinsi gani, ahadi na kanuni zilizomo katika Biblia zaweza kukuletea shangwe mpya na tumaini.

Maandiko yaonyesha kwamba “dhiki ni ya dakika na ni nyepesi” ilinganishwapo na baraka za milele zinazowekwa mbele ya wale wampendao Mungu. (2 Wakorintho 4:16-18) Biblia huonyesha pia kwamba sifa za kimungu zinazokuzwa katikati ya majaribu ni zenye thamani kubwa kuliko umashuhuri au mali za kimwili. (1 Yohana 2:15-17) Hivyo, hata kuteseka kwaweza kuleta manufaa. (Waebrania 5:8) Kwa hakika, kutumia yale unayojifunza wakati wa majaribu kwaweza kukuletea baraka usizotarajia.

Huenda jaribu gumu likakufanya uwe mwenye fadhili zaidi na mwenye tabia isiyopita kiasi. Huenda ukakubali kwamba katika wakati uliopita ulikuwa na kitabia cha utu kilichoudhi wengine na hata kikazuia maendeleo yako ya kiroho. Labda kilikuwa kujitumaini kupita kiasi. Baada ya kutaabishwa na maafa fulani, huenda ukang’amua ghafula jinsi ulivyo dhaifu na kadiri unavyohitaji wengine. Ikiwa jaribu lako limekufunza somo hilo na umefanya mabadiliko yahitajiwayo, basi limekunufaisha.

Vipi, ikiwa katika wakati uliopita, wengine waliona ni vigumu kushughulika nawe kwa sababu ulikuwa na tatizo la kudhibiti hamaki yako? Hilo huenda likawa limesababisha taabu fulani kuhusiana na afya yako. (Mithali 14:29, 30) Hata hivyo, huenda hali ikawa bora zaidi sasa kwa sababu unategemea roho ya Mungu ikusaidie udhihirishe hali ya kujidhibiti.—Wagalatia 5:22, 23.

Kama wengine, yawezekana wakati mmoja ulikosa huruma ya kuwarehemu wale wakosao. Lakini ikiwa wewe mwenyewe ulitumbukia katika hali ambapo ulihisi uhitaji mkubwa wa kupata rehema, yamkini sasa wewe ni mwenye mbetuko zaidi kuwarehemu wengine. Huruma, hangaiko, na rehema zenye kuchangamsha moyo ulizoonyeshwa zimekufanya ung’amue kwamba wapaswa uonyeshe wakosaji wenye toba sifa zizo hizo. Ikiwa umivu lako limekusukuma kusahihisha udhaifu huo mbalimbali katika utu wako, hiyo ni faida moja umepata kutokana na mambo uliyoyaona. Umejifunza kwamba “rehema huchachawa kwa shangwe ya ushindi juu ya hukumu.”—Yakobo 2:13; Mathayo 5:7.

Vipi ikiwa kutiwa nidhamu na kutaniko la Kikristo kumekugharimu mapendeleo uliyopenda na staha ya wengine? Usishindwe na hali ya kukata tumaini. Hatua ya kutia nidhamu husaidia kuweka kutaniko likiwa safi, lakini malengo yayo hutia ndani kurudishwa kiroho kwa mkosaji. Kwa kukiri wazi, “hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro; lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Ijapokuwa nidhamu yaweza kuwa pigo lenye kukumba, haimwachi mtu mwenye kutubu kwa unyenyekevu awe bila tumaini. Mfalme Daudi wa Israeli la kale alitiwa nidhamu kwa ukali kwa ajili ya kosa fulani, lakini alikuwa mwenye toba na hatimaye alipata pongezi la pekee kuwa mtu wa imani yenye kutokeza.—2 Samweli 12:7-12; Zaburi 32:5; Waebrania 11:32-34.

Jaribu laweza kuwa na tokeo lenye kina juu ya matazamio yako. Huenda ikawa katika wakati uliopita, uangalifu wako ulikaziwa miradi na matimizo ya kufuatia vitu vya kimwili yaliyokuletea utambuzi na hadhi ya kijamii katika ulimwengu huu. Labda jaribu lishirikishalo kutofaulu kiuchumi au hasara za vitu vya kimwili limekaza akili yako juu ya mambo yaliyo ya maana zaidi. (Linganisha Wafilipi 1:10.) Sasa wang’amua kwamba johari za kiroho na miradi katika utumishi mtakatifu ndiyo mambo pekee yaletayo shangwe ya kweli na uradhi wenye kudumu.

Itibari Katika Yehova

Huenda kumtolea Yehova utumishi mtakatifu kukatokeza mnyanyaso na kuteseka mikononi mwa wale wapingao itikadi zako za Kikristo. Huenda ukahisi mwenye kuonewa kwa sababu ya jaribu hilo, lakini manufaa yaweza kutokana nalo. Mtihani huo waweza kutia nguvu imani yako. Isitoshe, huenda wengine wanaonyanyaswa wakatiwa moyo na nguvu kwa kuona udumifu wako. Huenda mashahidi wenye kujionea mwenendo wako mzuri wakachochewa kumtukuza Mungu. Huenda hata wapinzani wako wakaaibika na kukiri kazi zako bora!—1 Petro 2:12; 3:16.

Ili kuepuka hali ya kukata tamaa unyanyaswapo, wahitaji itibari katika Yehova. Neno lake laonyesha kwamba kitulizo kutoka jaribuni kitakuja kwa hakika, lakini huenda kisije upesi kama vile ungetaka. Wakati huohuo, ‘usikate tamaa katika kutenda lililo sawa.’ (2 Wathesalonike 3:13) Fuliza kutafuta njia za kukabiliana na majaribu na kuvumilia. Hata mambo yaonekanapo kuwa yasiyo na tumaini, ‘mtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza. Hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.’ (Zaburi 55:22) Badala ya kujisikitikia, fikiria jinsi wewe umebarikiwa kumjua Yehova, kuwa mmoja wa watu wake, na kuwa na tumaini la uhai usio na mwisho.—Yohana 3:16, 36.

Kaza akili yako juu ya mambo yaliyo muhimu. Mwendee Yehova kila siku katika sala, ukimwomba nguvu za kuvumilia. (Wafilipi 4:6, 7, 13) Achilia mbali wazo lolote la kulipiza kisasi dhidi ya wale wasababishao kuteseka kwako. Acha mambo mikononi mwa Yehova. (Waroma 12:19) Fuliza kutafuta njia za kuboresha utu wako, huku ukikuza sifa za Kikristo. (2 Petro 1:5-8) Thamini kila jambo ufanyiwalo na wengine, wakitia ndani wazee wanaotunza kwa upendo mahitaji yako ya kiroho. (Waebrania 13:7, 17) Uwe mwaminifu kwa Mungu, na ukaze jicho lako juu ya tuzo ya uhai, ukiwa na uhakika kwamba hata kifo hakiwezi kukunyang’anya tuzo hiyo.—Yohana 5:28, 29; 17:3.

Ikiwa sasa unapatwa na sikitiko kubwa au majaribu makali, “mtumaini BWANA kwa moyo wako wote,” na hatimaye shangwe nyingi itachukua mahali pa kihoro na shida. (Mithali 3:5, 6; Yohana 16:20) Furaha itachukua mahali pa huzuni Mungu anapokubariki kama alivyombariki Ayubu. Kuteseka kwa siku hizi hakuna maana yoyote kunapolinganishwa na thawabu yako. (Linganisha Waroma 8:18.) Uvumilivu wako wenye uaminifu waweza kuwatia moyo wengine na kukusaidia kukuza zile sifa nzuri za Kikristo zijazo pamoja na “utu mpya.” (Waefeso 4:23, 24; Wakolosai 3:10, 12-14) Hivyo, basi, pata kitia moyo kutokana na hili shauri lenye hekima la mtume Petro: “Acheni wale wanaoteseka kwa kupatana na mapenzi ya Mungu wafulize kukabidhi nafsi zao kwa Muumba mwaminifu wanapotenda mema.”—1 Petro 4:19.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Uwe kama Ayubu. Usipoteze tumaini kamwe

[Picha katika ukurasa wa 24]

Itibari katika Yehova kwa moyo wako wote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki