Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 1/15 kur. 8-13
  • ‘Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Noa Alitenda kwa Imani Yenye Msingi Mzuri
  • Imani ya Abrahamu
  • Imani Iliyomchochea Musa
  • Wingu Kubwa Sana la Mashahidi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • “Fanyeni Mioyo Yenu Kuwa Imara”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Abrahamu Alikuwa Nani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Yehova Alimwita “Rafiki Yangu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 1/15 kur. 8-13

‘Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona’

“Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.”—2 WAKORINTHO 5:7.

1. ‘Kutembea kwa imani’ kwamaanisha nini?

KILA wakati tusalipo kulingana na miongozo ambayo imeonyeshwa katika Neno la Mungu, twaonyesha kwamba tuna angalau kadiri fulani ya imani. Tuanzapo kuwatolea wengine ushahidi juu ya Ufalme wa Mungu, hilo pia huonyesha imani. Na tuwekapo wakfu maisha zetu kwa Yehova, tunatoa uthibitisho wa kwamba tamaa yetu ni ‘kutembea kwa imani,’ yaani, kufuatia mwendo wa maisha ambao waongozwa na imani.—2 Wakorintho 5:7; Wakolosai 1:9, 10.

2. Kwa nini kushiriki katika utendaji mbalimbali wa kutaniko si lazima kuwe ithibati ya kwamba mtu ana imani?

2 Ikiwa kwa kweli tutaishi hivyo, twahitaji imani yenye msingi mzuri. (Waebrania 11:1, 6) Watu wengi huvutiwa na Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya viwango vya juu vya adili na upendo waonao miongoni mwa Mashahidi. Huo ni mwanzo mzuri, lakini haumaanishi kwamba watu hao wana imani. Wengine huenda wakawa na mwenzi wa ndoa au mzazi aliye na imani yenye nguvu, na huenda wakashiriki katika baadhi ya utendaji wa kiroho kwa sababu ya kielelezo cha mzazi au mwenzi wa ndoa wampendaye. Kuwa na uvutano huo nyumbani mwa mtu kwa kweli ni baraka, lakini huo pia hauwezi kuchukua mahali pa kumpenda Mungu kibinafsi na pa imani ya kibinafsi.—Luka 10:27, 28.

3. (a) Ili tuwe na imani yenye msingi mzuri, sisi binafsi twapaswa kuwa na usadikisho gani kuihusu Biblia? (b) Kwa nini watu fulani hupata kusadikishwa juu ya kupuliziwa kwa Biblia kwa utayari zaidi ya wengine?

3 Wale watembeao kwa imani kwelikweli wamesadikishwa kwa uthabiti kwamba Biblia ndiyo Neno la Mungu. Kuna uthibitisho mwingi wa kwamba Maandiko Matakatifu, kwelikweli, “[ya]mepuliziwa na Mungu.”a (2 Timotheo 3:16) Mtu ahitaji kuchunguza kiasi gani cha uthibitisho huo ili kusadikishwa? Hilo huenda likategemea malezi yake. Kile kimsadikishacho kikamili mtu mmoja huenda kisimshawishi mwingine. Katika visa fulani-fulani, hata ingawa mtu aonyeshwa uthibitisho mwingi usiokanushika, huenda bado akakinza mkataa wenye kupatana na akili utolewao. Kwa nini? Kwa sababu ya tamaa zilizofichwa ndani sana moyoni mwake. (Yeremia 17:9) Hivyo, ingawa huenda mtu akadai kwamba apendezwa na makusudi ya Mungu, huenda moyo wake ukatamani kupata kibali cha ulimwengu. Huenda asitake kuacha namna ya maisha ambayo haipatani na viwango vya Biblia. Hata hivyo, ikiwa mtu yeyote kwa kweli ana njaa ya kuipata kweli, ikiwa ajichunguza kwa unyoofu, na ikiwa ni mnyenyekevu, hatimaye atang’amua kwamba Biblia ndiyo Neno la Mungu.

4. Mtu ahitaji kufanya nini ili apate imani?

4 Mara nyingi katika miezi michache tu, watu wanaosaidiwa kujifunza Biblia hung’amua kwamba tayari wameona ithibati nyingi mno za kwamba hiyo ni Neno la Mungu. Ikiwa hilo lawasukuma wafungue mioyo yao ili wafundishwe na Yehova, ndipo mawazo yao, tamaa zao, na nia zao za ndani kabisa zitakapoundwa hatua kwa hatua na yale wajifunzayo. (Zaburi 143:10) Andiko la Waroma 10:10 lasema kwamba mtu hudhihirisha imani “kwa moyo.” Imani hiyo huonyesha jinsi mtu ahisivyo kwa kweli ndani yake, nayo itadhihirishwa wazi pia katika mwendo wake wa maisha.

Noa Alitenda kwa Imani Yenye Msingi Mzuri

5, 6. Imani ya Noa ilitegemea nini?

5 Noa alikuwa mtu aliyekuwa na imani yenye msingi mzuri. (Waebrania 11:7) Alikuwa na msingi gani wa imani? Noa alikuwa na neno la Mungu, si kwa namna ya maandishi, bali kama alivyoambiwa. Mwanzo 6:13 lasema hivi: ‘Mungu akamwambia Noa, Mwisho wa kila mwenye mwili umekuja mbele zangu; kwa sababu wameijaza dunia dhuluma.’ Yehova alimwelekeza Noa ajenge safina na aliandaa mambo yote kuhusu ujenzi wake. Kisha Mungu akaongeza kusema hivi: “Na tazama, nitaleta gharika ya maji juu ya nchi, niharibu kila kitu chenye mwili na pumzi ya uhai, kisiwepo chini ya mbingu; kila kilichoko duniani kitakufa.”—Mwanzo 6:14-17.

6 Je, kulikuwa kumekuwa na mvua wakati uliotangulia huo? Biblia haisemi. Andiko la Mwanzo 2:5 lasema hivi: “BWANA Mungu hajainyeshea nchi mvua.” Lakini hivyo ndivyo Musa, aliyeishi karne kadhaa baadaye, alivyoeleza mambo akizungumza juu ya kipindi cha wakati mapema sana kabla ya siku ya Noa. Kama ionyeshwavyo kwenye Mwanzo 7:4, Yehova alirejezea mvua aliposema na Noa, na kwa wazi Noa alielewa alilomaanisha Mungu. Hata hivyo, Noa hakuwa na imani katika yale aliyoweza kuona. Mtume Paulo aliandika kwamba Noa “[ali]pewa onyo la kimungu la mambo yasiyoonwa bado.” Mungu alimwambia Noa kwamba Yeye angeleta juu ya dunia “gharika ya maji,” au “bahari ya kimbingu,” kama kisemavyo kielezi-chini cha New World Translation of the Holy Scriptures With References katika Mwanzo 6:17. Hadi wakati huo, jambo la namna hiyo halikuwa limepata kutukia kamwe. Lakini uumbaji wote aliouona Noa ulikuwa wonyesho dhahiri wa kwamba Mungu angeweza kwa kweli kuleta gharika hiyo yenye kusababisha uharibifu. Kwa kusukumwa na imani, Noa alijenga safina.

7. (a) Noa hakuhitaji nini ili kutimiza yale ambayo Mungu alikuwa amemwamuru? (b) Twanufaikaje kwa kuchunguza imani ya Noa, na imani yetu yaweza kuwaje baraka kwa wengine?

7 Mungu hakuwa amempa Noa tarehe ambayo Gharika ingeanza. Lakini Noa hakutumia hilo kuwa udhuru wa kuwa na mtazamo wa kungoja aone jinsi ambavyo mambo yangekuwa, akiweka ujenzi wa safina na kuhubiri mahali pa pili maishani mwake. Mungu alimwambia Noa mapema vya kutosha wakati wa kuingia ndani ya safina. Wakati uleule, ‘ndivyo alivyofanya Noa sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.’ (Mwanzo 6:22) Noa alitembea kwa imani, si kwa kuona. Twashukuru kama nini kwamba alifanya hivyo! Kwa sababu ya imani yake, sisi tuko hai leo. Kwa habari yetu pia, imani tuonyeshayo yaweza kuathiri sana wakati wetu ujao na pia wakati ujao wa watoto wetu na wa watu wengine walio kandokando yetu.

Imani ya Abrahamu

8, 9. (a) Abrahamu alitegemeza imani yake juu ya nini? (b) Yehova ‘alimtokeaje’ Abrahamu?

8 Fikiria kielelezo kingine—kielelezo cha Abrahamu. (Waebrania 11:8-10) Abrahamu aliweka imani yake juu ya msingi upi? Mazingira ya Uru ya Wakaldayo alimokulia yalikuwa yenye ibada ya sanamu na ufuatiaji wa vitu vya kimwili. Lakini uvutano mwingine mbalimbali ulielekeza mtazamo wa Abrahamu. Bila shaka angeweza kushirikiana na Shemu, mwana wa Noa, waliyeishi naye wakati uleule kwa miaka 150. Abrahamu alipata kusadikishwa kwamba Yehova ndiye “Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 14:22.

9 Jambo jingine lilimwathiri sana Abrahamu. Yehova “alimtokea . . . Abrahamu alipokuwa katika Mesopotamia, kabla ya yeye kuanza kukaa katika Harani, naye akamwambia, ‘Nenda utoke katika nchi yako na kutoka katika jamaa zako na uje hadi kuingia katika nchi ambayo nitakuonyesha wewe.’” (Matendo 7:2, 3) Yehova “alimtokea” Abrahamu kwa njia gani? Abrahamu hakumwona Mungu moja kwa moja. (Kutoka 33:20) Hata hivyo, yawezekana kwamba Yehova alimtokea Abrahamu katika ndoto, kupitia wonyesho wa utukufu wenye nguvu zizidizo zile za kibinadamu, au kupitia mjumbe, au mwakilishi wa kimalaika. (Linganisha Mwanzo 18:1-3; 28:10-15; Mambo ya Walawi 9:4, 6, 23, 24.) Njia iwayo yote ambayo Yehova alimtokea Abrahamu, mwanamume huyo mwaminifu alikuwa na uhakika kwamba Mungu alikuwa akiweka mbele yake pendeleo lenye thamani. Abrahamu aliitikia kwa imani.

10. Yehova aliitiaje nguvu imani ya Abrahamu?

10 Imani ya Abrahamu haikutegemea kupata kwake mambo yote juu ya nchi ambayo Mungu alikuwa akimwelekeza aende. Haikutegemea kujua kwake wakati ambapo angepewa nchi hiyo. Alikuwa na imani kwa sababu alimjua Yehova kuwa Mungu Mweza-Yote. (Kutoka 6:3) Yehova alimwambia Abrahamu kwamba angekuwa na wazao, lakini nyakati nyingine Abrahamu alijiuliza jinsi ambavyo hilo lingewezekana. Alikuwa akizeeka. (Mwanzo 15:3, 4) Yehova aliitia nguvu imani ya Abrahamu kwa kumwambia atazame nyota juu na kuzihesabu ikiwa angeweza. “Ndivyo utakavyokuwa uzao wako,” akasema Mungu. Abrahamu alichochewa sana. Ilikuwa wazi kwamba Muumba wa magimba hayo ya kimbingu yenye kutia kicho angeweza kutimiza yale aliyokuwa ameahidi. Abrahamu “akaweka imani katika Yehova.” (Mwanzo 15:5, 6, linganisha NW.) Abrahamu hakuamini kwa sababu tu alipenda yale aliyokuwa akisikia; alikuwa na imani yenye msingi mzuri.

11. (a) Alipokaribia umri wa miaka 100, Abrahamu aliitikiaje ahadi ya Mungu kwamba Sara mzee angezaa mwana? (b) Abrahamu alikuwa na imani ya aina gani alipokabili mtihani uliohusisha kumpeleka mwana wake Mlima Moria ili amtoe akiwa dhabihu?

11 Abrahamu alipokaribia umri wa miaka 100 na mkeye Sara, akikaribia umri wa miaka 90, Yehova alitaarifu tena ahadi yake kwamba Abrahamu angekuwa na mwana, na kwamba Sara angekuwa mama yake. Abrahamu alifikiria hali yao kihalisi. “Lakini kwa sababu ya ahadi ya Mungu yeye hakusitasita kwa ukosefu wa imani, bali akawa mwenye nguvu nyingi kwa imani yake, akimpa Mungu utukufu na akisadikishwa kikamili kwamba alilokuwa ameahidi alikuwa na uwezo pia wa kufanya.” (Waroma 4:19-21) Abrahamu alijua kwamba ahadi ya Mungu isingeweza kushindwa. Baadaye, kwa sababu ya imani yake, Abrahamu alitii wakati Mungu alipomwambia amchukue mwanaye Isaka hadi nchi ya Moria na kumtoa akiwa dhabihu. (Mwanzo 22:1-12) Abrahamu alikuwa na uhakika kamili kwamba Mungu ambaye alikuwa amemfanya mwana huyo azaliwe kimuujiza angeweza pia kumrudisha kwenye uhai ili kutimiza zile ahadi nyingine ambazo Yeye alikuwa ametoa kuhusiana naye.—Waebrania 11:17-19.

12. Abrahamu aliendelea kutembea kwa imani kwa muda gani, na ni thawabu gani imngojeayo yeye na washiriki wa familia yake ambao walionyesha imani yenye nguvu?

12 Abrahamu alionyesha kwamba hakuongozwa na imani katika pindi fulani-fulani tu bali muda wote wa maisha yake. Katika maisha yake yote Abrahamu hakupokea kutoka kwa Mungu sehemu yoyote ya Bara Lililoahidiwa ikiwa urithi. (Matendo 7:5) Hata hivyo, Abrahamu hakuchoka na kurudi Uru ya Wakaldayo. Kwa miaka 100, hadi kifo chake, aliishi mahemani katika nchi ambayo Mungu alikuwa amemwelekeza aende. (Mwanzo 25:7) Kuhusu yeye na mkeye Sara, mwana wao Isaka, na Yakobo mjukuu wao wa kiume, andiko la Waebrania 11:16 lasema hivi: “Mungu haaibiki juu yao, kuitwa akiwa Mungu wao, kwa maana amefanya jiji liwe tayari kwa ajili yao.” Ndiyo, Yehova amewawekea mahali katika makao ya kidunia ya Ufalme wake wa Kimesiya.

13. Ni nani miongoni mwa watumishi wa Yehova leo waonyeshao uthibitisho wa kuwa na imani kama ile ya Abrahamu?

13 Kuna wale miongoni mwa watumishi wa Yehova leo walio kama Abrahamu. Wametembea kwa imani kwa miaka mingi. Kwa nguvu atoazo Mungu, wameshinda vizuizi vilivyo kama mlima. (Mathayo 17:20) Hawasitisiti katika imani kwa sababu hawajui ni lini hasa ambapo Mungu atawapa urithi ambao ameahidi. Wao wajua kwamba neno la Yehova haliwezi kushindwa, na waona ni pendeleo lenye thamani sana kuwa miongoni mwa Mashahidi wake. Je, ndivyo uhisivyo?

Imani Iliyomchochea Musa

14. Msingi wa imani ya Musa uliwekwaje?

14 Kielelezo kingine cha imani ni Musa. Msingi wa imani yake ulikuwa nini? Msingi uliwekwa wakati wa utoto sana. Ingawa binti Farao alimpata Musa katika kisanduku cha mafunjo katika Mto Naili akamchukua kuwa mwanaye, Yokebedi, mama ya Musa mwenyewe aliye Mwebrania, alimnyonyesha huyo mvulana naye akamtunza katika miaka yake ya mapema. Kwa wazi Yokebedi alimfundisha vizuri, akikaza kikiki ndani yake kumpenda Yehova na kuthamini ahadi Zake kwa Abrahamu. Baadaye, akiwa mshiriki wa nyumba ya Farao, Musa “[ali]funzwa katika hekima yote ya Wamisri.” (Matendo 7:20-22; Kutoka 2:1-10; 6:20; Waebrania 11:23) Hata hivyo, ujapokuwa wadhifa wa Musa wenye upendeleo, moyo wake ulikuwa pamoja na watu wa Mungu waliofanywa watumwa.

15. Kujitambulisha mwenyewe na watu wa Yehova kulimaanisha nini kwa Musa?

15 Katika mwaka wake wa 40, Musa alimpiga Mmisri hata chini ili kumkomboa Mwisraeli aliyekuwa akitendwa isivyo haki. Tukio hilo lilionyesha jinsi Musa alivyowaona watu wa Mungu. Kwa kweli, “kwa imani Musa, alipokuwa amekua akawa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao.” Badala ya kushikamana na “mfurahio wa muda wa dhambi” akiwa mshiriki wa nyumba ya mfalme wa Misri, alikuwa amesukumwa na imani kujitambulisha pamoja na watu wa Mungu waliotendwa vibaya.—Waebrania 11:24, 25; Matendo 7:23-25.

16. (a) Yehova alimpa Musa utume gani, na Mungu alimsaidiaje? (b) Musa alionyeshaje imani katika kuutimiza utume wake?

16 Musa alikuwa na hamu ya kuchukua hatua ili kuwaletea watu wake kitulizo, lakini wakati wa Mungu wa kuwaletea ukombozi haukuwa umekuja bado. Musa alilazimika kukimbia kutoka Misri. Ni baada ya miaka 40 tu kwamba Yehova kupitia malaika alimpa Musa utume wa kurudi Misri ili kuwaongoza Waisraeli watoke nchi hiyo. (Kutoka 3:2-10) Musa aliitikiaje? Hakuonyesha shaka kuhusu uwezo wa Yehova wa kukomboa Israeli, lakini alijihisi kuwa mwenye upungufu kwa daraka ambalo Mungu aliweka mbele yake. Kwa upendo, Yehova aliandaa kitia-moyo alichohitaji Musa. (Kutoka 3:11–4:17) Imani ya Musa iliongezeka nguvu. Alirudi Misri akamwonya Farao uso kwa uso mara nyingi juu ya mapigo ambayo yangeipata Misri kwa sababu ya kukataa kwa mtawala huyo kuruhusu Israeli waende kumwabudu Yehova. Musa hakuwa na nguvu za kibinafsi za kusababisha mapigo hayo. Alitembea kwa imani, si kwa kuona. Imani yake ilikuwa katika Yehova na neno lake. Farao alimtisha Musa. Lakini Musa alistahimili. “Kwa imani aliondoka Misri, lakini bila kuihofu hasira ya mfalme, kwa maana aliendelea akiwa imara kama ambaye anaona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:27) Musa hakuwa mkamilifu. Alifanya makosa. (Hesabu 20:7-12) Hata hivyo, baada ya Mungu kumpa utume, mwendo wake wa maisha kwa ujumla uliongozwa na imani.

17. Kutembea kwa imani kulikuwa na matokeo gani kwa Noa, Abrahamu, na Musa, hata ingawa hawakuishi wapate kuona ulimwengu mpya wa Mungu?

17 Imani yako na ithibitike kuwa kama ile ya Noa, Abrahamu, na Musa. Ni kweli kwamba hawakuona ulimwengu mpya wa Mungu katika siku yao. (Waebrania 11:39) Huo bado haukuwa wakati uliowekwa rasmi na Mungu; kulikuwa na sehemu nyingine za kusudi lake zilizohitaji kutimizwa bado. Hata hivyo imani yao katika neno la Mungu haikusitasita, na majina yao yamo katika kitabu cha uhai cha Mungu.

18. Kwa wale walioitiwa uhai wa kimbingu, kwa nini imekuwa lazima kutembea kwa imani?

18 “Mungu aliona kimbele kitu fulani bora kwa ajili yetu sisi,” akaandika mtume Paulo. Yaani, Mungu aliona kimbele kitu fulani bora zaidi kwa ajili ya wale ambao, kama vile Paulo, wameitwa kwenye uhai wa kimbingu pamoja na Kristo. (Waebrania 11:40) Ndio wale ambao Paulo alikuwa akifikiria hasa alipoandika maneno yaliyorekodiwa kwenye 2 Wakorintho 5:7: “Tunatembea kwa imani, si kwa kuona.” Wakati hilo lilipoandikwa, bado hakukuwa yeyote kati yao aliyekuwa amepata thawabu yake ya kimbingu. Hawakuweza kuiona kwa macho yao ya kimwili, lakini imani yao katika hiyo ilikuwa na msingi mzuri. Kristo alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu, akiwa matunda ya kwanza ya wale watakaobarikiwa kwa uhai wa kimbingu. Na mashahidi zaidi ya 500 walikuwa wamemwona kabla ya kupaa kwake mbinguni. (1 Wakorintho 15:3-8) Walikuwa na sababu za kutosha za kuongoza mwendo wao wote wa maisha kwa imani hiyo. Sisi pia tuna sababu nzuri ya kutembea kwa imani.

19. Kama ionyeshwavyo kwenye Waebrania 1:1, 2, Mungu amesema nasi kupitia nani?

19 Leo, Yehova hasemi na watu wake kupitia malaika, kama alivyosema na Musa kwenye kichaka chenye kuwaka moto. Mungu amesema kupitia Mwanaye. (Waebrania 1:1, 2) Yale aliyosema Mungu kupitia Yesu, Yeye alielekeza yarekodiwe katika Biblia, ambayo imetafsiriwa katika lugha za watu kotekote ulimwenguni.

20. Hali yetu ikoje afadhali kuliko ile ya Noa, Abrahamu, na Musa?

20 Tuna mengi zaidi ya yale waliyokuwa nayo Noa, Abrahamu, na Musa. Tuna Neno la Mungu lililo kamili—sehemu kubwa yake tayari imetimizwa. Baada ya kuchunguza yale yote ambayo Biblia husema juu ya wanaume na wanawake waliojithibitisha kuwa mashahidi waaminifu wa Yehova walipokabili majaribu ya kila aina, andiko la Waebrania 12:1 lasihi sana hivi: “Acheni sisi pia tuondoe kila uzito na dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi, na acheni tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” Imani yetu si kitu cha kupuuzwa. “Dhambi ambayo hututatanisha kwa urahisi” ni ukosefu wa imani. Pigano kali lahitajiwa ikiwa tutaendelea ‘kutembea kwa imani.’

[Maelezo ya Chini]

a Ona kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

Elezo Lako Ni Nini?

◻ Ni nini kihusishwacho katika ‘kutembea kwa imani’?

◻ Twaweza kunufaishwaje na jinsi Noa alivyoonyesha imani?

◻ Njia ambayo Abrahamu alionyesha imani yatusaidiaje?

◻ Biblia yamrejezeaje Musa kuwa kielelezo cha imani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Abrahamu alitembea kwa imani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Musa na Aroni walionyesha imani walipokuwa mbele ya Farao

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki