Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 1/15 kur. 23-28
  • Kuitia Nguvu Imani Yetu Katika Neno la Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuitia Nguvu Imani Yetu Katika Neno la Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Neno la Mungu Ni Kweli —Msingi wa Imani Yetu
  • Igeni “Mkamilishaji wa Imani Yetu”
  • Ishini kwa Sababu ya Imani
  • Onyesha Imani Yako Katika Ahadi za Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2016
  • Je, Kweli Una Imani Katika Habari Njema?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Zoea Imani Yenye Msingi Wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • “Tupe Imani Zaidi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 1/15 kur. 23-28

Kuitia Nguvu Imani Yetu Katika Neno la Mungu

WATU wengi zaidi wameisoma Biblia kuliko kitabu kingine chochote. Lakini ni wangapi ambao wamedhihirisha imani yao katika ujumbe wake? Biblia yenyewe yaeleza kwamba “imani si miliki ya watu wote.” (2 Wathesalonike 3:2) Kwa wazi, hatuzaliwi tukiwa na imani. Lazima isitawishwe. Hata wale walio na kiasi fulani cha imani hawapaswi kuipuuza. Imani yaweza kudhoofika na kufa. Kwa sababu hiyo, jitihada yahitajiwa ili kuendelea kuwa “wenye afya katika imani.”—Tito 2:2.

Likiwa na sababu nzuri, basi, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilichagua kichwa “Imani Katika Neno la Mungu” kwa ajili ya mfululizo wa Mikusanyiko ya Wilaya ya mwaka wa 1997/1998. Hivyo mamilioni ya Mashahidi na watu wengine wamekuwa na pendeleo la kukusanyika pamoja ili kuitia nguvu imani yao katika Neno la Mungu.

Neno la Mungu Ni Kweli —Msingi wa Imani Yetu

Hicho ndicho kilichokuwa kichwa cha siku ya kwanza ya mkusanyiko. Ilianza kwa maneno ya kuwapongeza wahudhuriaji wote. Kuwapo kwenye mkusanyiko kulikuwa uthibitisho wa kuistahi Biblia. Lakini, maswali yenye kufanya mtu afikiri yalizushwa kuhusu ubora wa imani yetu: ‘Je, twaweza kuzitetea itikadi zetu, tukitumia Neno la Mungu likiwa mamlaka? Je, twakithamini chakula cha kiroho, bila kupuuza kamwe Biblia, mikutano ya kutaniko, na vichapo vyenye kuitegemea Biblia? Je, tunakua katika upendo, ujuzi sahihi, na ufahamu?’ Msemaji aliwatia moyo wote wasikilize kwa makini, akitaja kwamba “Mkusanyiko huu wa Wilaya ‘Imani Katika Neno la Mungu’ umetayarishwa ili kutusaidia tujichunguze sana na kuchunguza kiasi na ubora wa imani tuliyo nayo sisi mmoja-mmoja.”

Hotuba ya msingi ilikuwa na kichwa “Kutembea kwa Imani, Si kwa Kuona.” (2 Wakorintho 5:7) “Imani ya wale wanaopata kuwa Mashahidi wa Yehova si wepesi tu wa kuamini bila ushuhuda,” msemaji akasema. Jambo hilo ni kweli kama nini! Imani ya kweli yaweza kutambua mambo. Yategemezwa juu ya mambo halisi. Waebrania 11:1 husema hivi: “Imani ni taraja lililohakikishwa la mambo yatumainiwayo, wonyesho dhahiri wa mambo halisi ingawa hayaonwi.” Msemaji aliendelea kusema hivi: “Ikiwa kwa kweli tutatembea kwa imani, twahitaji imani yenye msingi mzuri.” Kwa sababu twatembea kwa imani, si kwa kuona hatuhitaji kujulishwa kila kitu juu ya jinsi gani na wakati gani Yehova atakapotimiza kila sehemu ya kusudi lake. Kile ambacho tayari twajua juu yake hutupa uhakika kamili katika nguvu zake za kutimiza ahadi zake kwa upendo na kwa uadilifu.

Hotuba “Vijana Wakristo—Sehemu Muhimu ya Kutaniko” iliwakumbusha vijana jinsi walivyo wenye thamani kwa Yehova. Walitiwa moyo kukua kiroho kwa kufuatia miradi ya kiroho kama vile kusoma Biblia nzima na kutimiza matakwa ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Kufuatia elimu ya ziada ni jambo la kibinafsi lipaswalo kuamuliwa mtu akiwa na wazazi wake, lakini ikiwa elimu ya ziada itafuatiwa, lengo sikuzote lapaswa kuwa kutayarishwa ili kumtumikia Mungu kwa matokeo zaidi. Elimu ya kilimwengu yaweza kuwa yenye manufaa ‘tuhakikishapo mambo yaliyo ya maana zaidi’ ambayo yahusu imani yetu.—Wafilipi 1:9, 10.

Kisha ukafuata mfululizo wa hotuba tatu juu ya kichwa “Wewe Hufuata Viwango vya Nani?” Imani katika Neno la Mungu hutuchochea kushikamana sana na viwango vya Biblia. Wakristo hutii sheria na kanuni za Yehova. Kwa mfano, Maandiko yatuonya kwa upole tusitumie usemi wa aibu na wenye kuudhi. (Waefeso 4:31, 32) Msemaji aliuliza hivi: “Ukasirishwapo au kusumbuliwa, je, wewe hupiga kelele ukitoa usemi wenye kuudhi kwa mwenzi wako au watoto wako?” Bila shaka, jambo hilo lingekuwa lisilo la Kikristo. Mungu pia ana viwango kuhusu sura yetu ya kibinafsi. Wakristo wapaswa kujivika “mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi.” (1 Timotheo 2:9, 10) Neno “kiasi” huonyesha wazo la kujistahi, heshima, utulivu, na kiasi. Twachochewa na kuwapenda wengine na twaongozwa na kanuni za Biblia na hisi ya yale yafaayo.

Hotuba mbili zilizofuata zilitia ndani mazungumzo ya mstari kwa mstari ya Waebrania 3:7-15 na 4:1-16. Vifungu hivyo vya Biblia vyatuonya dhidi ya hatari ya kuwa “[wa]gumu kwa nguvu ya udanganyifu ya dhambi.” (Waebrania 3:13) Twaweza kufanikiwaje katika vita vyetu dhidi ya dhambi? Yehova hutusaidia kupitia Neno lake. Kwa kweli, “neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na . . . ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12.

Hotuba ya mwisho katika siku ya kwanza ya mkusanyiko ilikuwa yenye kichwa “Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote.” Ilikazia uasilia, usahihi, na thamani yenye kutumika ya Biblia. Inasisimua kama nini kumsikia msemaji akitangaza kutolewa kwa broshua yenye kurasa 32 yenye kichwa Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote! Kichapo hicho kipya kilitayarishwa hasa kwa ajili ya watu ambao, ingawa wana elimu ya juu, wajua machache juu ya Biblia. Hiyo hotuba ilimalizika kwa maneno haya: “Watu wanahitaji kujichunguzia Neno la Mungu. Tuna hakika kwamba wakijifanyia wenyewe uchunguzi huo, watapata kutambua kwamba, kitabu hiki cha pekee, Biblia, kwa kweli ni kitabu kwa ajili ya watu wote!”

Igeni “Mkamilishaji wa Imani Yetu”

Kichwa hiki cha siku ya pili ya mkusanyiko kilielekeza uangalifu kwa Yesu Kristo, “Mkamilishaji wa imani yetu.” Twahitaji ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’ (Waebrania 12:2; 1 Petro 2:21) Wengi katika Jumuiya ya Wakristo huambiwa hivi: ‘Mwamini Bwana Yesu, na utaokoka!’ Lakini kusema hayo tu kwatosha ili kuwa na imani? Biblia hujulisha wazi kwamba “imani bila kuwa na kazi imekufa.” (Yakobo 2:26) Kwa hiyo, mbali na kumwamini Yesu, lazima tufanye kazi alizofanya, hasa kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.

Programu ya asubuhi ilimakinikia kazi ya kueneza evanjeli. Kama Paulo, twapaswa kuwa wenye hamu ya kutangaza habari njema ya wokovu. (Waroma 1:14-16) Yesu alihubiri watu kila mahali. Ingawa huduma yetu ya kawaida ya nyumba hadi nyumba ni yenye matokeo, watu zaidi na zaidi hawako nyumbani tunapozuru. (Matendo 20:20) Wengi wako shuleni, kazini, madukani, au safarini. Kwa sababu hiyo, twahitaji pia kuhubiri katika mahali pa watu wote na popote pale ambapo watu waweza kupatikana.

Hotuba “Pateni Kutia Mizizi na Kuimarishwa Katika Kweli” ilitukumbusha juu ya idadi kubwa ya wanafunzi wapya wanaobatizwa—wastani wa wanafunzi zaidi ya 1,000 kila siku! Ni muhimu kwamba hawa wanafunzi wapya wapate kutia mizizi na kuimarishwa katika imani. (Wakolosai 2:6, 7) Msemaji alieleza kwamba mizizi halisi hufyonza maji na virutubishi huku pia ikiandalia mti nanga au tegemezo. Hivyohivyo, kupitia mazoea mazuri ya kujifunza na mashirika yenye kujenga, wanafunzi wapya waweza kuimarishwa katika kweli.

Shauri hilo hasa liliwafaa wataka kubatizwa. Ndiyo, katika siku ya pili ya mkusanyiko, umati wa wanafunzi wapya ulibatizwa, ukifuata kielelezo cha Yesu. Hotuba “Imani Katika Neno la Mungu Huongoza Kwenye Ubatizo” iliwakumbusha wataka kubatizwa kwamba kuzamishwa kabisa katika maji ni ishara ifaayo ya kufa kwao kuhusu mwendo wao wa maisha wa zamani wenye ubinafsi. Kule kuinuliwa kwao kutoka majini huwakilisha kufanywa kwao hai ili kufanya mapenzi ya Mungu.

Hotuba “Fanya Pigano Kali kwa Ajili ya Imani” ilitegemea kitabu cha Biblia cha Yuda. Tulitiwa moyo kuhami imani yetu kwa kukinza mavutano yenye madhara, kama vile ukosefu wa adili, uasi, na uasi-imani. Halafu, wazazi—hasa akina baba—walipokea uangalifu wa pekee katika hotuba “Andalia Watu wa Nyumbani Mwako.” Kuandalia familia mahitaji ya kiroho, ya kimwili, na ya kihisia-moyo ni wajibu wa Kimaandiko. (1 Timotheo 5:8) Jambo hilo lahitaji wakati, uwasiliano, na ukaribu. Hakika Yehova Mungu apendezwa na ile kazi ngumu yote ambayo wazazi Wakristo hufanya ili kulea watoto wao katika kweli.

Mfululizo uliofuata, “Na Twende Nyumbani kwa Yehova,” ulijenga uthamini kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Hiyo huandaa pumziko kutokana na mahangaiko ya ulimwengu huu. Kwenye mikutano tuna fursa ya kuwa na badilishano la kitia-moyo, na twaweza kuonyesha upendo wetu kwa waamini wenzetu. (Waebrania 10:24, 25) Mikutano pia hutusaidia kunoa stadi zetu tukiwa walimu, na huongeza kina cha uelewevu wetu wa kusudi la Mungu. (Mithali 27:17) Na tusijitenge na kutaniko kamwe, na acheni tukumbuke maneno ya Yesu: “Palipo na wawili au watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.”—Mathayo 18:20.

Hotuba ya mwisho ya hiyo siku ilikuwa “Ubora wa Imani Yako—Watahiniwa Sasa.” Imani ambayo haijatahiniwa yakosa thamani iliyothibitishwa, na ubora wake hubaki bila kujulikana. Ni kama hundi ambayo fedha zake bado hazijalipwa. Je, kwa kweli hundi hiyo ni yenye thamani ilinganayo na kiasi cha fedha kionekanacho juu yake? Vivyo hivyo, imani yetu lazima itahiniwe ili kuthibitisha kwamba ni yenye maana na ubora halisi. (1 Petro 1:6, 7) Msemaji alisema hivi: “Nyakati nyingine, vyombo vya habari na pia wenye mamlaka hudanganywa na makasisi na waasi-imani watulaumu isivyo kweli, wakieleza isivyo kweli imani na maisha yetu ya Kikristo. . . . Je, tutaruhusu wanaopofushwa na Shetani watutishe na kutuvunja moyo na kutufanya tuaibikie habari njema? Je, tutaruhusu uwongo mbalimbali juu ya kweli uathiri kuhudhuria kwetu mikutano kwa ukawaida na utendaji wetu wa kuhubiri? Au tutasimama imara na kuwa wenye moyo mkuu na wenye kuazimia zaidi kuliko wakati mwingine wowote ili kuendelea kutangaza kweli juu ya Yehova na Ufalme wake?”

Ishini kwa Sababu ya Imani

Kichwa cha siku ya tatu ya mkusanyiko kilitegemea maneno ya Paulo: “Kwamba kwa sheria hakuna yeyote ambaye hutangazwa kuwa mwadilifu kwa Mungu ni dhahiri, kwa sababu ‘mwadilifu ataishi kwa sababu ya imani.’” (Wagalatia 3:11) Mfululizo, “Maneno ya Kiunabii ya Yoeli kwa Ajili ya Siku Yetu,” ulikuwa mojawapo ya mambo makuu ya asubuhi. Kitabu cha Yoeli hutaja siku yetu na kusema hivi kwa hisi ya uharaka: “Ole wake siku hii! Kwa maana siku ya BWANA inakaribia, nayo itakuja kama uangamivu utokao kwake aliye Mwenyezi.” (Yoeli 1:15) Kwa namna ifananayo na ile ya nzige wasiochoka, Wakristo watiwa-mafuta wamekataa kuruhusu chochote kizuie utangazaji wa Ufalme katika wakati huu wa mwisho.

Kitabu cha Yoeli pia chatoa tumaini, kikisema hivi: “Mtu awaye yote atakayeliita jina la BWANA [“Yehova,” NW] ataponywa.” (Yoeli 2:32) Hilo lamaanisha mengi zaidi ya kulitumia tu jina la Yehova. Toba ya kuhisiwa moyoni yahitajiwa, na hiyo yatia ndani kukataa utendaji wenye kosa. (Yoeli 2:12, 13) Hakuna wakati wa kukawia kwa sababu Yehova karibuni atatekeleza hukumu juu ya mataifa, kama vile alivyofanya juu ya Moabu, Amoni, na nchi yenye milima-milima ya Seiri katika siku za Mfalme Yehoshafati wa Yuda.—2 Mambo ya Nyakati 20:1-30; Yoeli 3:2, 12.

Wote walitiwa moyo na hotuba “Onyesheni Imani kwa Kumngojea Yehova.” Sasa tukiwa ndani kabisa katika wakati wa mwisho, twaweza kukumbuka utimizo wa ahadi nyingi za Yehova, na twapendezwa kwa makini na mambo ambayo bado yatakuja kutimia. Watu wa Yehova lazima waendelee kuwa na subira, wakikumbuka kwamba kila kitu ambacho Mungu ameahidi kitatokea.—Tito 2:13; 2 Petro 3:9, 10.

Programu ya asubuhi ilimalizika kwa drama “Weka Jicho Lako Likiwa Sahili.” Mchezo huo wa kuigiza ulio halisi ulitutia moyo tuchunguze mtazamo wetu kuhusiana na kufuatia vitu vya kimwili. Hata iwe twaishi wapi, tukitaka maisha yetu yasiwe na hangaiko, lazima tufuate shauri la Yesu la kuweka jicho letu likiwa sahili, limekazwa kabisa juu ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 6:22.

Hotuba ya watu wote ilikuwa na kichwa chenye kuvutia sana “Imani na Wakati Ujao Wako.” Ilitoa ithibati juu ya kushindwa kwa viongozi wa kibinadamu kutatua matatizo ya ulimwengu. (Yeremia 10:23) Historia ya mwanadamu yafuliza kujirudia—kwa kiwango kikubwa zaidi na chenye madhara zaidi. Mashahidi wa Yehova huhisije juu ya wakati ujao? Twaamini kwamba wanadamu waaminifu wana wakati ujao ulio mwangavu chini ya Ufalme wa Mungu. (Mathayo 5:5) Mungu atatimiza ahadi zake kwa manufaa ya wote walio na imani katika Neno lake, ambalo lahimiza hivi: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu.”—Isaya 55:6.

Yesu alizusha swali muhimu kwa kufikiria siku yetu. Aliuliza hivi: “Mwana wa binadamu awasilipo, je, kwa kweli ataipata hiyo imani duniani?” (Luka 18:8) Hotuba ya mwisho ilipitia programu ya mkusanyiko na kuonyesha jinsi ilivyoandaa uthibitisho mkubwa kwamba imani katika Neno la Mungu iko, hata ingawa twaishi katika ulimwengu usio na imani na usio wa kidini.

Hata hivyo, twaweza kujiuliza sisi mmoja-mmoja, ‘Je, nimo miongoni mwa walio na imani isiyositasita katika Mungu na Neno lake?’ Mkusanyiko wa Wilaya “Imani Katika Neno la Mungu” wapaswa kutusaidia kujibu ndiyo kwa swali hilo. Na twamshukuru Yehova kama nini kwa kuimarisha imani yetu katika yeye na katika Neno lake lililopuliziwa, Biblia!

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wajitoleaji wengi walifanya kazi kwa uchangamfu ili kuhudumia maelfu ya wajumbe

[Picha katika ukurasa wa 25]

Stediamu kubwa kama hii zilitumiwa ulimwenguni pote

[Picha katika ukurasa wa 25]

L. A. Swingle wa Baraza Linaloongoza akitoa ile broshua mpya

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wengi walibatizwa katika ufananisho wa wakfu wao kwa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wakusanyikaji waliimba nyimbo za Ufalme kwa shangwe. Picha ya ndani: ile drama “Weka Jicho Lako Likiwa Sahili”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki