Kuifikia Mioyo kwa Ufundi wa Ushawishi
WATU wengi hulishuku neno “ushawishi.” Huenda neno hilo likamfanya mtu awazie, mwuzaji mwenye hima au tangazo la biashara lililobuniwa ili kudanganya au kuongoza mnunuzi kwa hila. Hata katika Biblia, nyakati nyingine wazo linalohusu ushawishi hutoa vidokezo visivyofaa, vikimaanisha kufisidiwa kiadili au kuongozwa vibaya. Kwa mfano, mtume Mkristo Paulo aliwaandikia Wagalatia hivi: “Mlikuwa mkikimbia vema. Ni nani aliyewazuia msifulize kuitii kweli? Namna hii ya kushawisha si kutoka kwa Yule anayewaita nyinyi.” (Wagalatia 5:7, 8) Pia Paulo alionya Wakolosai wasiache mtu yeyote ‘apate kuwapotosha kwa hoja zenye kushawishi.’ (Wakolosai 2:4) Ushawishi huo wategemea hoja za ujanja ambazo msingi wake si wa kweli.
Hata hivyo, katika barua yake ya pili kwa Timotheo, mtume Paulo alitumia wazo linalohusu ushawishi katika maana tofauti. Yeye aliandika hivi: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishwa kuamini, ukijua ni kutoka kwa watu gani ulijifunza hayo.” (2 Timotheo 3:14) Katika ‘kushawishwa kuamini,’ Timotheo hakuwa anaongozwa kwa hila na mama yake na nyanya yake, ambao kupitia kwao alijifunza kweli za Kimaandiko.—2 Timotheo 1:5.a
Alipokuwa katika kifungo cha nyumbani kule Roma, Paulo alitoa ushahidi kamili kwa watu wengi, “[aki]tumia ushawishi kwao kuhusu Yesu kutoka katika sheria ya Musa na pia Manabii, tangu asubuhi hadi jioni.” (Matendo 28:23) Je, Paulo alikuwa akidanganya wasikilizaji wake? La hasha! Ni dhahiri basi, ushawishi si mbaya sikuzote.
Likitumiwa kwa njia ifaayo, neno la Kigiriki la msingi litafsiriwalo “shawishi” humaanisha kusadikisha, kubadilisha nia kupitia kusababu timamu, kwenye mantiki. Hivyo, mwalimu aweza kujenga juu ya msingi wa Kimaandiko, akitumia ushawishi kutia ndani ya wengine usadikisho wa kweli ya Biblia. (2 Timotheo 2:15) Kwa kweli, hiyo ilikuwa alama ya huduma ya Paulo. Hata Demetrio yule mfua-fedha, aliyeyafikiria mafundisho ya Kikristo kuwa ya uwongo, alisema hivi: “Si katika Efeso tu bali pia katika karibu wilaya yote ya Asia Paulo huyu ameshawishi umati mkubwa na kuwageuza kwenye kauli nyingine, akisema kwamba wale waliofanywa kwa mikono si miungu.”—Matendo 19:26.
Kutumia Ushawishi Katika Huduma
Yesu Kristo aliwaagiza wafuasi wake hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi. Na, tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20) Katika nchi zaidi ya 230, Mashahidi wa Yehova wanatii amri hiyo. Kila mwezi wakati wa mwaka wao wa utumishi wa 1997, waliongoza wastani wa mafunzo ya Biblia nyumbani 4,552,589 ulimwenguni pote.
Ikiwa umependelewa kuongoza funzo la Biblia nyumbani, huenda ukaweza kutazamia magumu yatakayotaka utumie ufundi wa ushawishi. Kwa mfano, tuseme kwamba katika kipindi chako kinachofuata cha funzo, swali litatokezwa juu ya Utatu. Vipi ukijua kwamba mwanafunzi wako huamini fundisho hili? Unaweza kumpa kichapo kinachozungumzia habari hiyo. Baada ya kukisoma, huenda ukaona kwamba ameshawishwa kwamba Mungu na Yesu si mtu yuleyule. Lakini akibaki na maswali kadhaa, waweza kufanyaje?
Sikiliza kwa uangalifu. Hilo litakusaidia kuamua yale ambayo mwanafunzi wako tayari anaamini juu ya habari fulani mahususi. Kwa mfano, mwanafunzi wako akisema, “Naamini Utatu,” ungeweza kufanya mazungumzo ya Kimaandiko kukanusha fundisho hilo haraka. Lakini kuna aina mbalimbali za itikadi zinazohusu Utatu. Huenda mwanafunzi wako akaamini jambo tofauti kabisa na lile ambalo ungelifafanua kuwa fundisho la Utatu. Inaweza kusemwa hivyo pia kuhusu itikadi nyinginezo, kama vile kuzaliwa upya katika umbo jingine, hali ya kutoweza kufa kwa nafsi, na wokovu. Kwa hiyo sikiliza vizuri kabla ya kusema. Usiwazie yale ambayo mwanafunzi huamini.—Mithali 18:13.
Uliza maswali. Hayo yaweza kutia ndani: ‘Je, umeamini Utatu sikuzote? Ulipata kuchunguza kikamili uone kile ambacho Biblia husema kuhusu somo hili? Ikiwa Mungu angekuwa sehemu ya utatu, je, Neno lake Biblia, halingetuambia hivyo waziwazi na moja kwa moja?’ Unapomfundisha mwanafunzi, pindi kwa pindi tua uulize maswali kama: ‘Yale ambayo tumejifunza kufikia sasa je, yanakuelea?’ ‘Je, wakubaliana na ufafanuzi huu?’ Kwa ustadi wako wa kutumia maswali, wamhusisha mwanafunzi katika utaratibu wa kujifunza. Hapaswi tu kuwa akikusikiliza ukifafanua habari hiyo.
Tumia kusababu timamu. Kwa mfano, mnapozungumzia fundisho la Utatu, unaweza kumwambia mwanafunzi wako hivi: ‘Yesu alipobatizwa, sauti kutoka mbinguni, ilisema: “Wewe ni Mwana wangu, mpendwa.” Ikiwa kwa kweli Mungu alikuwako duniani akibatizwa, je, angefanya sauti yake ipande hadi mbinguni kisha kuirudisha ili maneno hayo yaweze kusikiwa duniani? Je, jambo hilo halingepotosha? Je, Mungu “asiyeweza kusema uwongo,” angefanya jambo kama hilo lenye kudanganya?’—Luka 3:21, 22; Tito 1:1, 2.
Kusababu timamu kunakofanywa kwa njia ya busara mara nyingi kwaweza kuwa na matokeo. Fikiria kielelezo cha mwanamke tutakayemwita Barbara. Katika maisha yake yote, alikuwa ameamini kwamba Yesu alikuwa Mungu na sehemu ya utatu ambao ulitia ndani roho takatifu. Kisha mmoja wa Mashahidi wa Yehova akamwambia kwamba Mungu na Yesu ni watu wawili walio tofauti, na kumwonyesha maandiko ya kuunga mkono jambo hilo.b Barbara hangeweza kuikanusha Biblia. Na wakati uleule, alikuwa amevunjwa moyo. Kwa vyovyote, alikuwa amelipenda sana fundisho la Utatu.
Huyo Shahidi alisababu na Barbara kwa subira. “Ikiwa ulikuwa unajaribu kunifundisha kwamba watu wawili wako sawa,” yeye akamwuliza, “ungetumia uhusiano gani wa familia ili kutoa kielezi cha jambo hilo?” Alifikiria kwa muda mfupi kisha akajibu: “Naweza kutumia ndugu wawili.” “Haswa,” huyo Shahidi akajibu. “Labda hata mapacha wanaofanana. Lakini katika kutufundisha kumwona Mungu kuwa Baba na yeye mwenyewe kuwa Mwana, Yesu alikuwa akiwasilisha ujumbe gani?” “Naelewa sasa,” Barbara akajibu, macho yake yakiwa yanafunguka zaidi. “Anamweleza mmoja kuwa wa zamani zaidi na mwenye mamlaka zaidi.”
“Ndiyo,” yule Shahidi akajibu, “na huo ndio uamuzi ambao Wayahudi, wasikilizaji wa Yesu walioishi katika jamii ya kiukoo wangefikia.” Akikazia hoja yake, huyo Shahidi alimalizia kwa kusema: “Ikiwa tulipata kielelezo kama hicho kinachofaa ili kufundisha usawa, yaani, ule wa ndugu au mapacha wenye kufanana, kwa hakika Yesu, yule Mfundishaji Mkuu, angefanya hivyo pia. Badala yake, alitumia maneno ‘baba’ na ‘mwana’ kufafanua uhusiano kati yake na Mungu.”
Hatimaye Barbara alielewa hoja hiyo, na kuikubali. Moyo wake ulikuwa umefikiwa kwa ufundi wa ushawishi.
Kushughulika na Hisia-Moyo
Itikadi za kidini zilizotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki mara nyingi huhusisha hisia-moyo. Fikiria kisa cha Edna, Mkatoliki mstahifu. Wajukuu wake walio matineja walimtolea uthibitisho wa Kimaandiko ulio wazi kwamba Mungu na Yesu si mtu yuleyule. Edna alielewa aliyosikia. Hata hivyo, alisema hivi kwa fadhili lakini kwa uthabiti: “Naamini Utatu mtakatifu.”
Labda wewe pia umepatwa na jambo kama hilo. Wengi huona mafundisho ya dini yao kana kwamba ni sehemu ya utambulisho wao. Ili kuwashawishi wanafunzi hao wa Biblia, mengi yahitajiwa kuliko mantiki isiyo na hisia au hata mfululizo wa maandiko kuthibitisha kwamba maoni ya mtu huyo ni yenye kosa. Hali kama hizo zaweza kushughulikiwa vizuri kwa kusawazisha ustadi wa kushawishi pamoja na huruma. (Linganisha Waroma 12:15; Wakolosai 3:12.) Inakubalika kwamba, mwalimu mwenye matokeo apaswa kuwa na masadikisho yenye nguvu. Kwa mfano, Paulo alitumia misemo kama “Nasadiki” na “Najua nami nashawishwa katika Bwana Yesu.” (Waroma 8:38; 14:14) Hata hivyo, katika kuelezea masadikisho yetu, hatupaswi kuwa na aina ya sauti yenye kulazimisha kauli, ya kujiona kuwa waadilifu, wala hatupaswi kuwa wenye dhihaka au wenye kushusha heshima tunapotoa kweli za Biblia. Kwa hakika hatutaki kumwudhi au hata kumtukana mwanafunzi.—Mithali 12:18.
Kunakuwa na matokeo zaidi tukiheshimu itikadi za mwanafunzi na kutambua haki yake ya kuwa nazo. Unyenyekevu ndio ufunguo. Mwalimu mwenye hali ya akili ya kujishusha chini hahisi kwamba yeye ni bora kiasili kuliko mwanafunzi wake. (Luka 18:9-14; Wafilipi 2:3, 4) Ushawishi wa kimungu hutia ndani unyenyekevu ambao, kwa kweli, husema: ‘Kwa rehema, Yehova amenisaidia nione jambo hili. Acha nilishiriki nawe.’
Kwa Wakristo wenzake waliokuwa Korintho, Paulo aliandika hivi: “Silaha za shughuli yetu ya vita si za kimwili, bali zenye nguvu kupitia Mungu kwa ajili ya kupindua mambo yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki. Kwa maana sisi tunapindua mawazowazo na kila jambo lililoinuka sana lililoinuliwa dhidi ya ujuzi wa Mungu; nasi tunaingiza kila fikira katika utekwa ili kuifanya iwe tiifu kwa Kristo.” (2 Wakorintho 10:4, 5) Leo, Mashahidi wa Yehova wanatumia Neno la Mungu kugeuza mafundisho yasiyo ya kweli yaliyotiwa kwa nguvu sana katika mahandaki na vilevile mazoea yaliyotiwa ndani sana na tabia zisizompendeza. (1 Wakorintho 6:9-11) Katika kufanya hivyo, Mashahidi hukumbuka kwamba, kwa upendo Yehova amekuwa mwenye subira kuwaelekea. Wao wana furaha kama nini kuwa na Neno lake, Biblia, na kuitumia ikiwa chombo chenye nguvu kung’oa mafundisho yasiyo ya kweli na kufikia mioyo kwa ufundi wa ushawishi!
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala “Eunike na Loisi—Waelimishaji Walio Vielelezo Bora,” kwenye ukurasa wa 7-9 wa toleo hili la Mnara wa Mlinzi.
b Ona Yohana 14:28; Wafilipi 2:5, 6; Wakolosai 1:13-15. Kwa habari zaidi, ona broshua Je! Uamini Utatu?, iliyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Kuufikia Moyo wa Mwanafunzi Wako
◻ Sali ili kupata mwelekezo wa Yehova katika kuufikia moyo wa mwanafunzi wa Biblia.—Nehemia 2:4, 5; Isaya 50:4.
◻ Fahamu itikadi za mwanafunzi na sababu ambayo huenda ikamfanya apendezwe na itikadi isiyo ya kweli.—Matendo 17:22, 23.
◻ Katika njia yenye fadhili, yenye subira, jenga hoja yenye mantiki ya Kimaandiko huku ukidumisha makubaliano.—Matendo 17:24-34.
◻ Ikiwezekana, imarisha kweli za Biblia kwa vielezi vyenye matokeo.—Marko 4:33, 34.
◻ Mwonyeshe mwanafunzi manufaa za kukubali ujuzi sahihi kutoka katika Biblia.—1 Timotheo 2:3, 4; 2 Timotheo 3:14, 15.