Hatimaye—Haki kwa Wote
“Sisi tutajitahidi kusikiliza katika njia mpya . . . sauti za watu walioumia, sauti za watu wenye mahangaiko, sauti za watu waliokata tumaini la kusikiwa. . . . Linalobaki ni kutenda kulingana na yaliyo katika sheria; kuhakikisha hatimaye kwamba kwa kuwa watu wote wanazaliwa wakiwa sawa katika adhama mbele za Mungu, wote wanazaliwa wakiwa sawa katika adhama mbele za mwanadamu.”—Hotuba ya kuzindua ya Rais wa Marekani, Richard Milhous Nixon, katika Januari 20, 1969.
WAFALME, marais, na wabunge wapatapo cheo, huelekea kuongea juu ya haki. Richard Nixon, aliyekuwa rais wa Marekani, alikuwa mmoja wao. Lakini maneno yake yenye ufasaha hupoteza ubora yalinganishwapo na historia isiyopendelea. Ijapokuwa aliapa ‘kutenda kulingana na yaliyo katika sheria,’ Nixon baadaye alipatikana na hatia ya kuvunja sheria naye akalazimishwa kuacha cheo chake. Miongo mitatu baadaye, ‘sauti za watu walioumia, wenye mahangaiko, na waliokata tumaini’ bado zapiga kelele zisikiwe.
Kusikia sauti hizo na kushughulikia malalamiko yao si kazi rahisi, kama vile ambavyo viongozi wengi wenye nia nzuri wamevumbua. ‘Haki kwa wote’ imethibitika kuwa mradi ambao si rahisi kuufikia. Hata hivyo, karne nyingi zilizopita, ahadi inayostahili uangalifu wetu ilifanywa—ahadi isiyo na kifani kuhusu haki.
Mungu, kupitia nabii wake Isaya, alihakikishia watu Wake kwamba angewatumia “mtumishi” ambaye yeye mwenyewe angemchagua. “Nimeiweka roho yangu juu yake,” Yehova akawaambia. “Naye atayaletea mataifa haki.” (Isaya 42:1-3, Biblia Habari Njema) Hakuna mtawala wa kibinadamu ambaye angethubutu kufanya tangazo lenye nguvu hivyo, tangazo ambalo lingemaanisha haki yenye kudumu kwa kila taifa. Je, ahadi hiyo yaweza kutumainiwa? Je, inawezekana kufikia mafanikio kama hayo yasiyo ya kawaida?
Ahadi Tuwezayo Kutumaini
Ahadi yaweza kutegemeka sawa tu na yule aitoaye. Katika kisa hiki, si mwingine ila Mungu Mweza Yote atangazaye kwamba “mtumishi” wake atathibitisha haki ulimwenguni pote. Tofauti na wanasiasa, Yehova hatoi ahadi kijuujuu tu. ‘Haiwezekani kwake kusema uwongo,’ Biblia yatuhakikishia. (Waebrania 6:18) “Kile ambacho nimeazimia kufanya kitafanyika,” Mungu atangaza kwa mkazo.—Isaya 14:24, Today’s English Version.
Uhakika wetu katika ahadi hiyo pia watiwa nguvu na rekodi ya “mtumishi” ambaye Mungu alimchagua, Yesu Kristo. Yeye ambaye angeishi kupatana na haki. Yesu aliacha rekodi isiyo na waa akiwa mwanamume ‘aliyependa uadilifu, na kuchukia uasi-sheria.’ (Waebrania 1:9) Aliyosema, alivyoishi, na hata alivyokufa, yote hayo yathibitisha kwamba kwa kweli alikuwa mtu wa haki. Wakati wa kifo cha Yesu, ofisa wa jeshi Mroma, ambaye yaonekana alishuhudia kesi ya Yesu na kuhukumiwa kwake, alichochewa kusema hivi: “Kwa kweli mtu huyu alikuwa mwadilifu.”—Luka 23:47.
Yesu mwenyewe aliishi maisha ya uadilifu na kukinza ukosefu wa uadilifu ambao ulikuwa umeenea pote katika siku yake. Alifanya hivyo, si kwa mapinduzi, bali kwa kumfundisha haki ya kweli kila mtu ambaye angesikiliza. Mahubiri [yake] ya Mlimani ni masimulizi stadi ya jinsi ambavyo haki na uadilifu wa kweli wapaswa kuwekwa katika matendo.—Mathayo, sura ya 5-7.
Yesu alitenda aliyofundisha. Hakudharau wenye ukoma walio maskini, watu “wasioguswa” wa jamii ya Kiyahudi. Badala yake, alisema nao, akawagusa, na hata kuwaponya. (Marko 1:40-42) Watu wote aliokutana nao, kutia na maskini na wenye kuonewa, walikuwa watu wa maana kwake. (Mathayo 9:36) “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi,” akawaambia.—Mathayo 11:28.
Zaidi ya yote, Yesu alikataa kuruhusu ukosefu wa haki uliomzunguka umfisidi au umtie uchungu. Hakulipiza ovu kwa ovu kamwe. (1 Petro 2:22, 23) Hata alipokuwa katika maumivu makali sana, alisali kwa Baba yake wa kimbingu kwa niaba ya askari walewale waliomtundika. “Baba, wasamehe,” akaomba, “kwa maana hawajui wanalofanya.” (Luka 23:34) Hakika, Yesu ‘alifanya lililo haki kuwa wazi kwa mataifa.’ (Mathayo 12:18) Ni uthibitisho gani mkubwa zaidi tulio nao wa tamaa ya Mungu ya kuanzisha ulimwengu wa haki kuliko kielelezo kilicho hai cha Mwana wake mwenyewe?
Ukosefu wa Haki Waweza Kushindwa
Uthibitisho halisi kwamba ukosefu wa haki waweza kushindwa pia wapatikana katika ulimwengu wa leo. Wakiwa watu mmoja-mmoja, na wakiwa tengenezo, Mashahidi wa Yehova hujitahidi kushinda ubaguzi, upendeleo, ubaguzi wa kijamii, na ujeuri. Fikiria kielelezo kinachofuata.
Pedroa aliamini kwamba kitendo cha mapinduzi ndicho kingekuwa njia pekee ya kuletea haki Basque Country, mkoa wa Hispania ambako aliishi. Kuhusu jambo hilo akawa mwanachama wa shirika la utekaji-nyara ambalo lilimpa mazoezi ya kijeshi katika Ufaransa. Mazoezi yake yalipomalizika, aliamriwa aunde kikosi cha magaidi na alipue kambi ya polisi. Kikundi chake kilikuwa tayari kinatayarisha vilipuaji alipokamatwa na polisi. Alikaa gerezani miezi 18, lakini hata alipokuwa gerezani aliendeleza shughuli zake za kisiasa, akigomea chakula na kukata vifundo vya mikono yake wakati mmoja.
Pedro aliamini kwamba alikuwa akipigania haki. Kisha akaja kumjua Yehova na makusudi yake. Pedro alipokuwa gerezani, mke wake alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na alipoachiliwa, mkeye alimwalika ahudhurie mojawapo ya mikutano yao. Alifurahia pindi hiyo sana hivi kwamba aliomba funzo la Biblia, funzo lililomwongoza kufanya mabadiliko makubwa katika mtazamo wake na njia yake ya maisha. Mwishowe, katika 1989, Pedro na mke wake walibatizwa.
“Namshukuru Yehova kwamba kwa kweli sikuua mtu yeyote wakati wa miaka yangu ya utekaji-nyara,” Pedro asema. “Sasa natumia upanga wa roho ya Mungu, Biblia, kuwapa watu ujumbe wa amani na haki ya kweli—habari njema za Ufalme wa Mungu.” Muda usio mrefu sana, Pedro, ambaye sasa hutumikia akiwa mzee wa Mashahidi wa Yehova, alitembelea kambi aliyokusudia kuiangamiza. Wakati huu alikwenda kwa kusudi la kuhubiri ujumbe wa amani kwa familia zinazoishi huko.
Mashahidi wa Yehova hufanya mabadiliko hayo kwa sababu wanatamani ulimwengu mwadilifu. (2 Petro 3:13) Ijapokuwa wao hutumaini ahadi za Mungu kabisa, wanatambua kwamba pia ni wajibu wao kuishi kupatana na haki. Biblia yatuonyesha waziwazi kwamba Mungu hututazamia tufanye sehemu yetu.
Kupanda Mbegu za Uadilifu
Ni kweli, tukabiliwapo na ukosefu wa haki, huenda tukahisi tukitaka kulia hivi: “Yuko wapi yule Mungu mwenye haki?” Hicho ndicho kilichokuwa kilio cha Wayahudi katika siku za Malaki. (Malaki 2:17, BHN) Je, Mungu alifikiria kwa uzito lalamiko lao? Hata kidogo, lilimfanya ahisi ‘amechoka’ kwa sababu, pamoja na mambo mengine, wao wenyewe walikuwa wanawatendea wake zao ambao walikuwa wamezeeka mambo ya hiana, wakiwataliki kwa visingizio visivyo na maana. Yehova alionyesha hangaiko lake kwa ‘wake wa ujana wao, ambao walikuwa wamewatendea mambo ya hiana, ingawa walikuwa wenzao na wake wa agano lao.’—Malaki 2:14.
Je, twaweza kulalamika kisheria kuhusu ukosefu wa haki ikiwa sisi wenyewe twatenda kwa ukosefu wa haki? Kwa upande ule mwingine, tukijaribu kumwiga Yesu kwa kung’oa ubaguzi wa jamii kutoka mioyoni, kwa kuwa wasio na upendeleo na wenye upendo kwa wote, na kwa kutorudisha ovu kwa ovu, twaonyesha kwamba kwa kweli twapenda haki.
Ikiwa tutavuna haki, Biblia hutusihi ‘tupande katika uadilifu.’ (Hosea 10:12) Hata uonekane kuwa mdogo kadiri gani, kila ushindi wa kibinafsi dhidi ya ukosefu wa haki ni wa muhimu sana. Kama alivyoandika Martin Luther King, Jr., katika Letter From Birmingham Jail, “ukosefu wa haki mahali popote ni tisho la haki kila mahali.” Wale ‘wanaotafuta uadilifu’ ndio watu ambao Mungu atawachagua waurithi ulimwengu mwadilifu utakaokuja hivi karibuni.—Sefania 2:3, BHN.
Hatuwezi kujenga tumaini letu katika haki juu ya msingi usio imara wa ahadi za binadamu, lakini twaweza kutumaini neno la Muumba wetu mwenye upendo. Hiyo ndiyo sababu Yesu aliwaambia wafuasi wake waendelee kusali Ufalme wa Mungu uje. (Mathayo 6:9, 10) Yesu, Mfalme aliyewekwa wa Ufalme huo, “atamkomboa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:12, 13.
Kwa wazi, ukosefu wa haki hautadumu. Utawala wa Kristo kwa dunia yote utashinda ukosefu wa haki milele, kama Mungu atuhakikishiavyo kupitia nabii wake Yeremia: “Wakati unakuja nitakapotimiza ahadi niliyotoa . . . Wakati huo nitachagua mzao wa Daudi awe mfalme wa uadilifu. Mfalme huyo atafanya yaliyo sawa na haki nchini mwote.”—Yeremia 33:14, 15, TEV.
[Maelezo ya Chini]
a Jina limebadilishwa.