Tumia Maisha Yako kwa Njia Ifaayo Kabisa
BABA alikuwa nyumbani, kitandani, akiwa mahututi kwa ugonjwa wa kansa. Mwana wake alikuwa katika karakana, akipanga vifaa vya useremala vya babake. Alipokuwa akivishikashika, alifikiria vitu vizuri ajabu ambavyo babake alikuwa amevitengeneza akitumia vifaa hivyo. Ingawa karakana hiyo ilikuwa karibu na nyumba, alijua kwamba babake hangeweza kamwe kuingia humo, hangeshika kamwe vifaa hivyo alivyovitumia kwa ustadi mkubwa. Wakati wa kufanya hivyo ulikuwa umepita.
Huyo mwana alifikiria andiko hili kwenye Mhubiri 9:10: “Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburi] uendako wewe.” Alijua andiko hilo vizuri. Alikuwa amelitumia nyakati nyingi alipowafundisha wengine ile kweli ya Biblia kwamba kifo ni hali ya kutotenda. Sasa kilichomaanishwa na hoja hiyo ya Solomoni kilimgusa moyo—yatupasa tuishi kikamili na kufurahia siku zetu wakati tuwezapo kufanya hivyo, kwa sababu wakati utafika ambapo hatutaweza kamwe kufanya hivyo.
Furahia Maisha
Kotekote katika kitabu cha Mhubiri, Mfalme Solomoni mwenye hekima awahimiza wasomaji wake watafute furaha maishani. Kwa kielelezo, sura ya 3 yasema: ‘Mimi najua ya kwamba hakuna jema kwa watu kupita kufurahi, na kufanya mema maadamu wanaishi. Tena ni karama ya Mungu kila mtu apate kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote.’—Mhubiri 3:12, 13.
Solomoni alipuliziwa na Mungu kurudia wazo hilo: “Tazama, mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote anayoifanya chini ya jua, siku zote za maisha yake alizopewa na Mungu; maana hilo ndilo fungu lake.”—Mhubiri 5:18.
Vivyo hivyo, yeye awahimiza vijana hivi: “Wewe kijana, uufurahie ujana wako, na moyo wako ukuchangamshe siku za ujana wako, ukaziendee njia za moyo wako, na katika maono ya macho yako.” (Mhubiri 11:9a) Ni jambo zuri kama nini kufurahia kikamili nguvu za ujana!—Mithali 20:29.
‘Mkumbuke Muumba Wako’
Bila shaka, Solomoni hamaanishi kwamba ni hekima kufuatia kila kitu ambacho huvutia mioyo na macho yetu. (Linganisha 1 Yohana 2:16.) Jambo hilo ni wazi kutokana na yale afuatayo kuandika: “Lakini ujue wewe ya kwamba kwa ajili ya hayo yote [ufuatiaji unaoweza kutosheleza tamaa zako] Mungu atakuleta hukumuni.” (Mhubiri 11:9b) Hata tuwe na umri gani, twapaswa kukumbuka kwamba Mungu huona yale tufanyayo maishani mwetu na atatuhukumu kulingana nayo.
Ni jambo la upumbavu kama nini kusababu kwamba twaweza kuishi maisha ya ubinafsi na kuahirisha ujitoaji wetu kwa Mungu hadi tutakapokuwa wazee! Twaweza kufa wakati wowote. Hata tusipokufa, kumtumikia Mungu wakati wa uzee si jambo rahisi sana. Kwa kutambua uhakika huo, Solomoni aandika hivi: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 12:1.
Kuzeeka kuna maafa yake. Kwa maneno ya ufananisho Solomoni afuatia kufafanua matokeo ya uzee. Mikono hutetemeka, miguu hudhoofika, na meno huwa machache. Nywele hugeuka kuwa nyeupe na kuanguka. Usingizi ni mwepesi hivi kwamba mtu huamshwa tu na sauti ya ndege. Hisi za kuona, kusikia, kugusa, kunusa, na kuonja—zote hufifia. Mwili uliodhoofika hufanya mtu ahofu kuanguka na kuhofu “vitisho” vinginevyo barabarani. Mwishowe mtu hufa.—Mhubiri 12:2-7.
Uzee ni wenye maafa hasa kwa wale ambao wameshindwa ‘kumkumbuka Muumba wao’ wakati wa ujana wao. Kwa sababu ya kutumia maisha yake vibaya, mtu kama huyo huwa ‘hana furaha’ katika miaka ya baadaye. Huenda mtindo-maisha wa kutomcha Mungu pia ukazidisha matatizo na maumivu ya uzee. (Mithali 5:3-11) Kwa kusikitisha, watazamapo maisha yao ya baadaye, watu kama hao hawaoni wakati ujao ila kaburi tu.
Kufurahi Wakati wa Uzee
Jambo hilo halimaanishi kwamba wazee-wazee hawawezi kufurahia maisha. Katika Biblia, ‘wingi wa siku na miaka ya uzima’ hushirikishwa na baraka za Mungu. (Mithali 3:1, 2) Yehova alimwambia Abrahamu rafiki yake hivi: “Lakini wewe . . . utazikwa katika uzee mwema.” (Mwanzo 15:15) Licha ya kusumbuliwa na uzee, Abrahamu alipata amani na utulivu uzeeni mwake, akikumbuka kwa uradhi maisha ya ujitoaji wake kwa Yehova. Pia alitazamia kwa imani Ufalme wa Mungu, “jiji lililo na misingi halisi.” (Waebrania 11:10) Hivyo, alikufa akiwa “mzee sana, ameshiba siku.”—Mwanzo 25:8.
Kwa hiyo Solomoni alihimiza hivi: “Mtu akiishi miaka mingi, na aifurahie yote.” (Mhubiri 11:8) Tuwe vijana au wazee, furaha ya kweli hutokana na uhusiano wetu na Mungu.
Yule mwanamume kijana katika karakana alikuwa akifikiria mambo hayo alipokuwa akiondoa kifaa cha mwisho kati ya vifaa vya babake. Alikumbuka watu wote aliowajua ambao walijaribu kutumia maisha yao kwa njia ifaayo kabisa lakini hawakupata furaha kwa sababu hawakuwa na uhusiano na Muumba wao. Ni jambo linalofaa kama nini kwamba, baada ya kumtia mtu moyo afurahi wakati wa maisha yake, Solomoni amalizia mambo kwa maneno haya: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu”!—Mhubiri 12:13.