Hakikisha Unatanguliza Mambo Yanayopasa Kutangulizwa!
Ni siku ya mkutano, lakini una kazi ya kufanya. Utatanguliza nini?
WEWE ni mume na baba. Siku ndefu, yenye kuchosha ikaribiapo kwisha, mawazo yako yarudi kwenye ratiba ya mkutano wa kutaniko wa siku hiyo. Ukiondoka kazini mara moja, utakuwa na wakati wa kutosha tu kuoga, kubadili mavazi yako, na kula haraka kabla hujaondoka kwenda mkutanoni. Kwa ghafula, mwajiri wako akufikia na kukuomba ufanye kazi saa za ziada. Anakuahidi kukulipa fedha nyingi. Wahitaji fedha hizo.
Au wewe ni mke na mama. Unapotayarisha chakula cha jioni, macho yako yanaona rundo la nguo ambazo hazijapigwa pasi, nyinginezo zitahitajiwa kesho yake. Wajiuliza mwenyewe, ‘Nikihudhuria mkutano leo, nitapata wapi nafasi ya kupiga pasi?’ Ukiwa umepata kazi ya wakati wote hivi majuzi, watambua jinsi ilivyo vigumu kushughulikia kazi za nyumbani unapotafuta riziki.
Au wewe ni mwanafunzi. Chumbani mwako, dawati lako limejaa migawo ya masomo ya nyumbani. Mingi yake ulipewa muda fulani uliopita, lakini umekuwa ukiahirisha, sasa migawo kadhaa imefika mara moja. Unashawishiwa kuuliza wazazi wako ruhusa ukose mkutano ili umalize migawo yako ya masomo ya nyumbani.
Ni nini ambacho ungetanguliza: kazi ya ziada ya kuajiriwa, kupiga pasi, migawo ya masomo ya nyumbani, au mkutano wa kutaniko? Kusema kwa namna ya kiroho, kutanguliza mambo yanayopasa kutangulizwa kwamaanisha nini? Maoni ya Yehova ni nini?
Ni Nini Kinachopasa Kutangulizwa?
Muda mfupi baada ya Waisraeli kupokea zile Amri Kumi, mwanamume mmoja alipatikana akikusanya kuni siku ya Sabato. Hilo lilikatazwa kabisa na Sheria. (Hesabu 15:32-34; Kumbukumbu la Torati 5:12-15) Ungeamuaje kisa hicho? Je, ungemsamehe mwanamume huyo, ukitoa hoja kwamba, hata hivyo, hakuwa anafanya kazi ili adumishe mtindo-maisha ulio wa kustarehesha bali kuandaa mahitaji ya lazima ya familia yake? Je, ungesababu kwamba kungekuwa na fursa nyingi mwaka mzima za kusherehekea Sabato na kwamba kukosa moja tu, labda kwa sababu ya mwanamume huyo kukosa kupanga mapema, angeweza kusamehewa kwa urahisi?
Yehova aliona kisa hicho kwa uzito. Biblia yasema, “BWANA akamwambia Musa, Mtu huyo lazima atauawa.” (Hesabu 15:35) Kwa nini Yehova aliona jambo ambalo mwanamume huyo alifanya kuwa zito sana?
Watu walikuwa na siku sita za kukusanya kuni na vilevile kushughulikia mahitaji yao ya chakula, mavazi, na makao. Siku ya saba ilikuwa itengwe kwa ajili ya mahitaji yao ya kiroho. Ingawa kukusanya kuni hakukuwa makosa, ilikuwa makosa kutumia wakati ambao ulipaswa kutengwa kwa ajili ya kumwabudu Yehova kufanya hivyo. Ijapokuwa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Kimusa, je, kisa hiki hakitufundishi somo la kutanguliza mambo tunayopasa kutanguliza leo?—Wafilipi 1:10.
Baada ya kukaa nyikani kwa miaka 40, Waisraeli walikuwa tayari kuingia Bara Lililoahidiwa. Wengine walikuwa wamechoka kula mana iliyoandaliwa na Mungu nyikani nao bila shaka walikuwa wakitazamia lishe tofauti. Ili kuwasaidia wawe na maoni yafaayo walipokuwa wakiingia bara ‘lijaalo maziwa na asali,’ Yehova aliwakumbusha hivi: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA.”—Kutoka 3:8; Kumbukumbu la Torati 8:3.
Iliwabidi Waisraeli wafanye kazi kwa bidii ili wapate “maziwa na asali.” Kulikuwa na majeshi ya kuangamiza, nyumba za kujenga, mashamba ya kupanda. Hata hivyo, Yehova aliamuru watu watenge wakati kila siku kutafakari juu ya mambo ya kiroho. Pia walipaswa kuwa na wakati wa kufundisha watoto wao njia za Mungu. Yehova alisema: “Nayo wafunzeni vijana [wenu amri zangu] kwa kuyazungumza uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo.”—Kumbukumbu la Torati 11:19.
Mara tatu kwa mwaka mtu wa kiume Mwisraeli na mgeuzwa-imani aliyekuwa katika bara hilo aliamriwa atokee mbele za Yehova. Wengi waliokuwa vichwa vya familia, wakitambua kwamba familia nzima ingenufaika kiroho na pindi kama hizo, walipanga wake zao na watoto waandamane nao. Lakini ni nani ambaye angelinda makao yao na mashamba yao dhidi ya shambulizi la adui familia ilipokuwa imekwenda? Yehova aliahidi hivi: “Hapana mtu ye yote atakayeitamani nchi yako, hapo utakapokwea kwenda kuhudhuria mbele za BWANA Mungu wako mara tatu kila mwaka.” (Kutoka 34:24) Ilihitaji imani kwa Waisraeli kuamini kwamba ikiwa wangetanguliza masilahi ya kiroho, hawangepoteza vitu vya kimwili. Je, Yehova alithibitika kuwa wa kweli kuhusu neno lake? Bila shaka ndiyo!
Fuliza Kutafuta Kwanza Ufalme
Yesu alifundisha wafuasi wake watangulize masilahi ya kiroho mbele ya kitu kingine chochote. Katika Mahubiri ya Mlimani, alishauri wasikilizaji wake hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tule nini?’ au, ‘Tunywe nini?’ au, ‘Tuvae nini?’ . . . Fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mathayo 6:31, 33) Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, Wakristo waliokuwa wamebatizwa karibuni walifuata shauri hilo. Wengi wao walikuwa Wayahudi au Wayahudi wageuzwa-imani ambao walikuwa wamesafiri hadi Yerusalemu kuadhimisha msherehekeo wa Pentekoste katika 33 W.K. Walipokuwa huko, jambo lisilotazamiwa lilitukia. Walisikia na kukubali habari njema juu ya Yesu Kristo. Wakiwa na tamaa ya kujifunza mengi zaidi kuhusu imani yao mpya, walibaki Yerusalemu. Maandalizi yao yalianza kupungua, lakini starehe za kimwili zilichukua mahali pa pili. Walikuwa wamempata Mesiya! Ndugu zao Wakristo walishiriki vitu vya kimwili walivyokuwa navyo ili wote waendelee “kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume . . . na katika sala.”—Matendo 2:42.
Baada ya muda, baadhi ya Wakristo walipuuza uhitaji wao wa kawaida wa kushirikiana kwenye mikutano. (Waebrania 10:23-25) Labda walikuja kuwa wafuatiaji wa vitu vya kimwili, wakipuuza mambo ya kiroho huku wakijaribu kujihakikishia wenyewe usalama wa kifedha na wa familia zao. Baada ya kusihi ndugu zake wasiache mikutano, mtume Paulo aliandika hivi: “Acheni namna yenu ya maisha iwe bila upendo wa fedha, huku nyinyi mkiridhika na vitu vilivyopo. Kwa maana yeye amesema: ‘Hakika sitakuacha kwa vyovyote wala kukuachilia mbali kwa vyovyote.’”—Waebrania 13:5.
Shauri la Paulo lilipata kuwa lenye kutumika sana. Miaka mitano hivi, baada ya Paulo kuandikia Waebrania barua yake, jeshi la Kiroma la Sesho Galo lilizingira Yerusalemu. Wakristo waaminifu walikumbuka onyo la Yesu: “Mwonapo mara hiyo kile kitu . . . mwacheni mtu aliye juu ya paa ya nyumba asiteremke, wala asiingie ndani kuchukua kitu chochote kutoka nyumbani mwake; na mwacheni mtu aliye katika shamba asirudi kwa mambo yaliyo nyuma kuchukua vazi lake la nje.” (Marko 13:14-16) Walijua kwamba wokovu wao ulitegemea utii wao kwa maagizo ya Yesu, bali si uthabiti wa kazi yao ya kuajiriwa au thamani ya mali zao za kimwili. Wale waliochukua hatua kuhusu shauri la Paulo na kutanguliza masilahi ya kiroho waliona ikiwa rahisi zaidi kuacha makao yao, kazi, mavazi, na vitu walivyovipenda na kuponyoka hadi milimani kuliko wowote ambao hawakuwa wameacha kupenda fedha.
Jinsi Ambavyo Watu Fulani Hutanguliza Mambo Yanayopasa Kutangulizwa Leo
Wakristo waaminifu leo huthamini ushirika wa kawaida pamoja na ndugu zao, na wengi hujidhabihu ili kuhudhuria mikutano. Katika maeneo mengine, kazi pekee ya kuajiriwa iwezayo kupatikana ni ile ya kufanya kwa zamu. Ndugu mmoja hujitolea kufanya mahali pa wafanyakazi wenzake Jumamosi usiku, ambazo wengi katika jumuiya yake hupendelea kutumia kwa ajili ya tafrija, ikiwa nao watafanya zamu yake ya usiku wa mikutano. Ndugu wengine ambao ni wafanyakazi wa zamu huhudhuria mikutano katika kutaniko la karibu ikiwa kazi yao huwazuia kuhudhuria mkutano wa kwao. Kwa njia hii, huwa hawakosi mkutano. Mtu aliyekuwa ameanza kupendezwa karibuni huko Kanada alitambua upesi umaana wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, lakini ratiba yake ya kazini iliingilia kuhudhuria kwake mkutano. Kwa sababu hiyo, alimlipa mfanyakazi mwenzake afanye kazi zamu yake ili aweze kuhudhuria mikutano hii ya maana.
Wengi ambao huwa na ugonjwa wa kudumu hawakosi mikutano. Wao husikiliza programu kupitia simu iliyounganishwa au utepe uliorekodiwa wanaposhindwa kufika kwenye Jumba la Ufalme. Wao huonyesha uthamini unaostahili pongezi kwa maandalizi ya Yehova ya kiroho kupitia “mtumwa [wake] mwaminifu na mwenye busara”! (Mathayo 24:45) Wakristo wanaotumika wakiwa watunzaji wa wazazi wao wazee-wazee kwa kweli huthamini ndugu au dada anapojitolea kukaa na mzazi ili mtunzaji aweze kuhudhuria mkutano wa kutaniko.
Panga Kimbele!
Wazazi ambao wanahangaikia mahitaji yao wenyewe ya kiroho watakuwa waangalifu kuwasaidia watoto wao wathamini mikutano ya Kikristo. Kwa kawaida, wanatazamia watoto wao wafanye migawo yao ya masomo ya nyumbani wanapogawiwa badala ya kuruhusu migawo irundamane. Siku za mkutano, watoto wanafanya migawo yao ya masomo ya nyumbani mara wanaporudi nyumbani kutoka shuleni. Hobi na shughuli nyinginezo haziruhusiwi kuingilia mikutano ya kutaniko.
Ukiwa mume na baba, je, wewe hutanguliza uhudhuriaji wa mikutano? Ukiwa mke na mama, je, wewe hujaribu kupanga madaraka yako ili uhudhurie mikutano? Ukiwa tineja, je, wewe huona migawo yako ya masomo ya nyumbani kuwa ya maana kuliko mikutano au mikutano kuwa ya maana kuliko migawo yako ya masomo ya nyumbani?
Mkutano wa kutaniko ni uandalizi wenye upendo wa Yehova. Kila jitihada yapasa kufanywa ili kushiriki katika mpango huo. Yehova atakubariki sasa ukitanguliza mambo yanayopasa kutangulizwa!