Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w98 11/1 kur. 24-28
  • “Mungu Hupenda Mpaji Mchangamfu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mungu Hupenda Mpaji Mchangamfu”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mchango kwa Ajili ya Wenye Uhitaji
  • Wasihiwa Wawe Wakarimu
  • Wapaji Wachangamfu Leo
  • Ukarimu Mwingi Huleta Shangwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • “Mheshimu Yehova kwa Vitu Vyako Vyenye Thamani” —Jinsi Gani?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Jinsi Ambavyo Wengine Hutoa Upaji kwa Ajili ya Kazi ya Kuhubiri Ufalme
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Kwa Nini Tumtolee Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
w98 11/1 kur. 24-28

“Mungu Hupenda Mpaji Mchangamfu”

YEHOVA ndiye wonyesho halisi wa ukarimu. Kwa kweli, Biblia husema kwamba yeye ni Mpaji wa “kila zawadi njema.” (Yakobo 1:17) Kwa kielelezo, fikiria vitu alivyoumba Mungu. Alitokeza chakula chenye ladha nzuri, wala si kisicho na ladha; maua yenye rangi zenye kupendeza; wala si zenye kuchujuka; machweo yenye kustaajabisha, wala si yenye utusiutusi. Naam, kila sehemu ya uumbaji wa Yehova hutoa uthibitisho wa upendo na ukarimu wake. (Zaburi 19:1, 2; 139:14) Zaidi ya hayo, Yehova ni Mpaji mchangamfu. Yeye hufurahia kufanya yaliyo mema kwa niaba ya watumishi wake.—Zaburi 84:11; 149:4.

Waisraeli waliamuriwa waonyeshe ukarimu wa Mungu katika kushughulika kwao mmoja na mwenzake. “Usifanye moyo wako kuwa mgumu, wala usimfumbie mkono wako nduguyo maskini,” Musa akawaambia. “Mpe kwa kweli, wala moyo wako usisikitike.” (Kumbukumbu la Torati 15:7, 10) Kwa kuwa upaji ulipaswa utoke moyoni, Waisraeli walipaswa kufurahia kuonyesha ukarimu.

Wakristo walipewa shauri lililo sawa na hilo. Kwa kweli, Yesu alisema kwamba kuna ‘furaha katika kutoa.’ (Matendo 20:35) Wanafunzi wa Yesu walikuwa kielelezo chema katika kutoa kwa uchangamfu. Kwa kielelezo, Biblia yaripoti kwamba, waliokuwa waamini katika Yerusalemu “wa[li]anza kuuza miliki na mali zao na kugawia wote hayo mapato, kama vile yeyote angekuwa na uhitaji.”—Matendo 2:44, 45.

Lakini baadaye Wayudea hao wakarimu walipatwa na umaskini. Biblia haisemi kihususa ni kitu gani hasa kilichosababisha hiyo hali yao. Wasomi fulani husema kwamba huenda ikawa njaa kubwa irejezewayo kwenye Matendo 11:28, 29 ndiyo iliyokuwa kisababishi. Kwa vyovyote vile, Wakristo hao Wayudea walikuwa katika hali yenye kukatisha tumaini, naye Paulo alitaka kuhakikisha kwamba mahitaji yao yangeshughulikiwa. Angefanyaje hivyo?

Mchango kwa Ajili ya Wenye Uhitaji

Paulo alipata msaada kutoka kwa makutaniko yaliyokuwa mbali sana kama vile Makedonia, naye alipanga mchango utolewe kwa niaba ya Wakristo wa Yudea waliokumbwa na umaskini. Kwa Wakorintho, Paulo aliandika: “Kama vile nilivyoyapa maagizo makutaniko ya Galatia, nyinyi wenyewe pia fanyeni kwa njia hiyohiyo. Kila siku ya kwanza ya juma acheni kila mmoja wenu kwenye nyumba yake mwenyewe aweke kando kitu fulani katika akiba kama aelekeavyo kuwa anafanikiwa.”a—1 Wakorintho 16:1, 2.

Paulo alikusudia kwamba fedha hizo zipelekwe upesi kwa ndugu waliokuwa Yerusalemu, lakini Wakorintho hawakuitikia kwa uharaka maagizo ya Paulo. Kwa nini? Je, walikuwa bila hisia yoyote kuelekea hali mbaya ya ndugu zao Wayudea? La, kwa maana Paulo alijua kwamba Wakorintho “[wali]zidi katika kila jambo, katika imani na neno na ujuzi na hali yote ya bidii.” (2 Wakorintho 8:7) Yaelekea, walikuwa na shughuli nyingi kuhusiana na mambo mengine muhimu ambayo Paulo alitaja katika barua yake ya kwanza kwao. Lakini sasa hali katika Yerusalemu ilikuwa yenye uharaka. Kwa hiyo, Paulo alitaja suala hilo katika barua yake ya pili kwa Wakorintho.

Wasihiwa Wawe Wakarimu

Kwanza, Paulo aliwaambia Wakorintho juu ya Wamakedonia, ambao itikio lao kwa jitihada ya kutoa msaada lilikuwa kielelezo chema. “Wakati wa jaribu kubwa chini ya taabu kubwa,” Paulo aliandika, “wingi wao wa shangwe na umaskini wa kina kirefu ulifanya utajiri wa ukarimu wao kuzidi.” Wamakedonia hawakuhitaji kusihiwa kutoa. Kinyume cha hilo, Paulo alisema kwamba “wa[li]fuliza kwa hiari yao wenyewe kutuomba kwa kusihi sana wapate pendeleo la kutoa kwa fadhili.” Ukarimu mchangamfu wa Wamakedonia ni wenye kutokeza zaidi tufikiriapo kwamba wao wenyewe walikuwa katika hali ya “umaskini wa kina kirefu.”—2 Wakorintho 8:2-4.

Je, Paulo alikuwa akijaribu kuchochea roho ya mashindano miongoni mwa Wakorintho kwa kuwasifu Wamakedonia? Sivyo kabisa, kwa maana alijua kwamba hiyo haikuwa njia ifaayo ya kuwachochea. (Wagalatia 6:4) Zaidi ya hayo, alijua kwamba Wakorintho hawakuhitaji kuaibishwa ili kufanya lililofaa. Badala yake, alikuwa na uhakika kwamba Wakorintho waliwapenda kikweli ndugu zao Wayudea na walitamani kuchangia jitihada hiyo ya kutoa msaada. “Tayari mwaka mmoja uliopita,” akawaambia, “nyinyi mlianzisha si kule kufanya tu bali pia kule kutaka kufanya.” (2 Wakorintho 8:10) Kwa kweli, kwa njia fulani Wakorintho walikuwa kielelezo chema katika jitihada hiyo ya kutoa msaada. “Najua utayari wenu wa akili ambao juu ya huo najisifu kwa Wamakedonia juu yenu,” Paulo akawaambia, akiongeza kusema hivi: “Bidii yenu imechochea walio wengi kati yao.” (2 Wakorintho 9:2) Ingawa hivyo, sasa Wakorintho walihitaji kubadili bidii yao na utayari wao wa akili uwe matendo.

Kwa sababu hiyo, Paulo aliwaambia: “Acheni kila mmoja afanye kama vile ameazimia moyoni mwake, si kwa kinyongo au kwa shurutisho, kwa maana Mungu hupenda mpaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kusudi la Paulo wakati huo halikuwa kuwashurutisha Wakorintho, kwa maana mtu hawezi kuwa mpaji mchangamfu akishurutishwa. Kwa wazi, Paulo alidhani kwamba nia ifaayo ilikuwepo tayari, kwamba kila mtu alikuwa tayari ameazimia kutoa. Kwa kuongezea, Paulo aliwaambia: “Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika hasa kulingana na alicho nacho mtu, si kulingana na kile ambacho mtu hana.” (2 Wakorintho 8:12) Naam, utayari ukiwepo—mtu anapochochewa na upendo—anachotoa kitakubaliwa na Mungu, hata kiwe chaonekana kidogo kadiri gani.—Linganisha Luka 21:1-4.

Wapaji Wachangamfu Leo

Jitihada ya kutoa msaada kwa niaba ya Wakristo Wayudea hutoa kielelezo bora kabisa kwa siku yetu. Mashahidi wa Yehova wamejiandaa kufanya kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote, wakipeleka lishe kwa mamilioni ya watu ambao wana njaa kubwa ya kiroho. (Isaya 65:13, 14) Wao hufanya hivyo kwa kutii amri ya Yesu: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20.

Kutimiza utume huo si kazi rahisi. Kwahusisha kutunza makao ya wamishonari na majengo ya ofisi za tawi zaidi ya mia moja ulimwenguni pote. Kwahusisha pia ujenzi wa Majumba ya Ufalme na Majumba ya Kusanyiko ili waabudu wa Yehova wawe na mahali pafaapo pa kukutania na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Nyakati nyingine, Mashahidi wa Yehova pia hutoa misaada ya kusaidia katika maeneo ambayo yameharibiwa na misiba ya asili.

Fikiria pia, ile gharama kubwa mno ya uchapaji. Kwa wastani, nakala zaidi ya 22,000,000 za Mnara wa Mlinzi au nakala 20,000,000 za Amkeni! huchapwa kila juma. Kuongezea ugavi huo wa kawaida wa chakula cha kiroho, kuna mamilioni ya vitabu, broshua, kaseti, na vidiokaseti ambazo hutolewa kila mwaka.

Kazi hiyo yote hutegemezwaje? Kwa upaji wa hiari. Upaji huo haufanywi kwa sababu ya kuvutia watu wala kwa kusudi lenye ubinafsi, bali hufanywa kwa sababu ya kuendeleza ibada ya kweli. Kwa sababu hiyo, upaji huo humletea mpaji furaha, pamoja na baraka ya Mungu. (Malaki 3:10; Mathayo 6:1-4) Hata watoto miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hujionyesha kuwa wakarimu, wapaji wachangamfu. Kwa kielelezo, baada ya kusikia uharibifu uliosababishwa na kimbunga katika sehemu fulani ya Marekani, Allison mwenye umri wa miaka minne alichanga dola 2. “Hizi ndizo fedha zote katika benki yangu ya sarafu,” akaandika. “Ninajua kwamba watoto walipoteza vichezeo vyao vyote na vitabu na watoto-bandia. Labda mwaweza kutumia fedha hizo kumnunulia kitabu msichana mdogo aliye na umri sawa na wangu.” Maclean, mwenye umri wa miaka minane, aliandika kwamba alifurahi kwamba hakuna ndugu wowote waliokufa katika dhoruba hiyo. Aliongezea: “Nilichuma dola 17 kwa kuuza vitovu vya magurudumu pamoja na baba yangu. Ningenunua kitu fulani kwa fedha hizo zangu, lakini nikawafikiria ndugu hao.”—Ona pia sanduku liliko juu.

Kwa kweli, moyo wa Yehova hushangilia kuona wachanga kwa wazee wakiweka masilahi ya Ufalme kwanza kwa ‘kumheshimu BWANA kwa mali yao.’ (Mithali 3:9, 10) Bila shaka, hakuna yeyote awezaye kumtajirisha Yehova, kwa maana yeye humiliki vitu vyote. (1 Mambo ya Nyakati 29:14-17) Lakini kutegemeza kazi hiyo ni pendeleo ambalo humtolea mwabudu fursa ya kuonyesha upendo wake kwa Yehova. Twamshukuru yeyote ambaye moyo wake umemsukuma kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

a Ingawa Paulo ‘alitoa maagizo,’ hilo halimaanishi kwamba alitoa madai ya lazima, yasiyo na msingi maalumu. Badala yake, Paulo alikuwa tu akisimamia mchango, uliohusisha makutaniko kadhaa. Kwa kuongezea, Paulo alisema kwamba kila mmoja “kwenye nyumba yake” angetoa “kama aelekeavyo kuwa anafanikiwa.” Yaani, kila mchango ungetolewa faraghani na kwa hiari. Hakuna aliyelazimishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 26, 27]

Njia Ambazo Watu Fulani Huchagua Kutoa Michango kwa Kazi ya Ulimwenguni Pote

Wengi huweka kando, au hupangia kiasi cha fedha ambazo wao hutia katika masanduku ya michango yaliyo na kibandiko hiki: “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi makutaniko hupeleka kiasi hicho ama kwenye makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn, New York, ama kwenye ofisi ya tawi ya kwao.

Upaji wa hiari wa fedha waweza kupelekwa pia moja kwa moja kwenye Treasurer’s Office, Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti inayotumikia nchi yako. Vito au mali nyingine zenye thamani zaweza kutolewa pia. Barua fupi yenye kutaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja yapaswa iambatane na michango hiyo.

Mpango wa upaji wenye masharti

Fedha zaweza kupewa kwa Watch Tower Society kukiwa na uandalizi maalumu kwamba kukiwa na uhitaji wa kibinafsi, zitarudishwa kwa mpaji. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Treasurer’s Office kwenye anwani iliyoonyeshwa juu.

Utoaji uliofanyiwa mpango

Kuongezea zawadi za fedha za moja kwa moja na upaji wa fedha wenye masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa ili kufaidi utumishi wa Ufalme wa ulimwenguni pote. Hizo zatia ndani:

Bima: Watch Tower Society yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa sera ya bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi/malipo ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akiba za benki, hati za amana, au akiba za fedha za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama zikiwa zawadi ya moja kwa moja ama zikiwa chini ya mpango ambao mapato yaendelea kulipwa kwa mpaji.

Mashamba na Nyumba: Mashamba na nyumba ziwezazo kuuzwa zaweza kupewa kwa Watch Tower Society ama kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja ama kwa kuweka shamba au nyumba ya maisha kwa ajili ya mpaji, ambaye aweza kuendelea kuishi humo muda wa maisha yake. Mtu apaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kuipa Sosaiti hati yoyote ya mashamba na nyumba.

Wasia na Amana: Watch Tower Society yaweza kurithishwa mali au fedha kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini yaweza kuandaa faida fulani za kodi.

Kama vile mtajo “utoaji uliopangwa” udokezavyo, upaji wa aina hii hutaka mpaji afanye mipango fulani hasa. Ili kuwasaidia watu mmoja-mmoja wanaotamani kunufaisha Sosaiti kupitia aina fulani ya utoaji uliofanyiwa mpango, Sosaiti imetayarisha broshua ya Kiingereza yenye kichwa Planned Giving to Benefit Kingdom Service Worldwide. Broshua hiyo iliandikwa kufuatia maswali mengi ambayo Sosaiti imepokea kuhusu zawadi, wasia, na amana. Pia ina habari ya ziada yenye mafaa juu ya mipango ya mashamba, ya kifedha, na kodi. Nayo imekusudiwa kuwasaidia watu mmoja-mmoja walio Marekani wanaopanga kuipa Sosaiti zawadi ya kipekee sasa au kuacha wasia wafapo wateue njia zenye matokeo na zenye kufaa zaidi kwa kufikiria hali za familia na za kibinafsi.

Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na walio kwenye Dawati la Utoaji Uliopangwa, watu wengi wameweza kusaidia Sosaiti na wakati uleule kupata faida kubwa zaidi ya manufaa ya kodi ya kufanya hivyo. Walio kwenye Dawati la Utoaji Uliopangwa kujulishwa na kupokea hati yoyote ile yenye kuhusiana na wowote wa mipango hiyo. Wale wanaopendezwa na broshua au wowote wa mipango hiyo ya utoaji uliofanyiwa mpango wanapaswa wawasiliane na walio kwenye Dawati la Utoaji Uliopangwa ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu kwenye anwani iliyoonyeshwa hapa chini au kwenye ofisi ya tawi inayotumikia nchi yako.

Dawati la Utoaji Uliopangwa

International Bible Students Association

P. O. Box 47788, Nairobi, Kenya

Simu: 573211/20

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

Watoto Ni Wapaji Wachangamfu Pia!

Nataka kuwapa fedha hizi ili mfanyize vitabu zaidi kwa ajili yetu. Niliziweka akiba kutokana na malipo niliyopata kwa kumsaidia baba yangu. Asanteni sana kwa jitihada zenu zote.—Pamela, mwenye umri wa miaka saba.

Ninawapelekea dola 6.85 za kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme. Nilizichuma kiangazi hiki nilipouza maji ya limau kwenye kibanda.—Selena, mwenye umri wa miaka sita.

Kutokana na kuku mmoja niliyekuwa nikifuga, nilipata jogoo na kuku mwingine. Kuku huyu mwingine nilimweka wakfu kwa Yehova. Hatimaye alipata kuku wengine watatu, ambao niliwauza. Natia fedha hizo ndani ya bahasha kwa ajili ya kazi ya Yehova.—Thierry, mwenye umri wa miaka minane.

Hizi ndizo fedha zangu zote! Tafadhali zitumieni kwa hekima. Haikuwa rahisi kuziweka akiba. Hapa kunazo dola 21.—Sarah, mwenye umri wa miaka kumi.

Nilishinda zawadi ya kwanza katika mgawo fulani wa shule, kwa hiyo ilinibidi nishiriki katika mashindano ya wilaya. Nilishinda zawadi ya kwanza pia, kisha nikashinda zawadi ya pili katika mashindano ya mwisho ya jimbo. Katika mashindano hayo yote, nilipata zawadi za fedha. Nilitaka kugawia Sosaiti nyingine za fedha hizo. Nahisi kwamba niliweza kushinda zawadi hizo kwa sababu ya mazoezi ambayo nimepokea katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Nilijihisi mwenye uhakika nilipotoa ripoti yangu mbele ya waamuzi.—Amber, aliye katika darasa la sita.

Ningependa kuwapatia fedha hizi kwa ajili ya Yehova. Mwulizeni kile mtakachozifanyia. Anajua kila kitu.—Karen, mwenye umri wa miaka sita.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Shughuli za Mashahidi wa Yehova hutegemezwa kwa upaji wa hiari

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki